Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yatakayofanywa na Ufalme wa Mungu

Yatakayofanywa na Ufalme wa Mungu

Yatakayofanywa na Ufalme wa Mungu

“Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—MATHAYO 6:10.

1. Kuja kwa Ufalme wa Mungu kutamaanisha nini?

YESU alipowafundisha wafuasi wake wasali kwa ajili ya Ufalme wa Mungu, alijua kwamba ufalme huo ukija utakomesha maelfu ya miaka ya utawala wa wanadamu pasipo kumtegemea Mungu. Wakati huo wote, mapenzi ya Mungu hayakufanywa duniani kwa jumla. (Zaburi 147:19, 20) Lakini baada ya Ufalme kusimamishwa mbinguni, mapenzi ya Mungu yatafanywa kila mahali. Wakati wa badiliko hilo lenye kutia kicho, kutoka utawala wa wanadamu kuingia utawala wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu, unazidi kukaribia.

2. Ni nini kitakachoashiria mabadiliko kutoka utawala wa wanadamu kuingia utawala wa Ufalme?

2 Badiliko hilo litaashiriwa na kipindi ambacho Yesu alikiita “dhiki kubwa ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu hadi sasa, la, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:21) Biblia haisemi kipindi hicho kitakuwa kirefu kadiri gani, lakini maafa ambayo yatatokea wakati huo yatakuwa mabaya kuliko chochote kile ambacho kimewahi kuupata ulimwengu. Mwanzoni mwa dhiki kubwa, jambo fulani litatokea ambalo litashtua sana watu wengi duniani: kuharibiwa kwa dini zote zisizo za kweli. Mashahidi wa Yehova hawatashtushwa na jambo hilo, kwa kuwa wamelitarajia kwa muda mrefu. (Ufunuo 17:1, 15-17; 18:1-24) Dhiki kubwa itamalizika kwenye Har–Magedoni wakati Ufalme wa Mungu utakapoponda-ponda mfumo wote wa Shetani.—Danieli 2:44; Ufunuo 16:14, 16.

3. Yeremia anaelezaje mwisho wa watu wasiotii?

3 Jambo hilo litamaanisha nini kwa watu “wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema” juu ya Ufalme wake wa mbinguni mikononi mwa Kristo? (2 Wathesalonike 1:6-9) Unabii wa Biblia watuambia: “Tazama, uovu utatokea toka taifa hata taifa, na tufani kuu itainuliwa toka pande za mwisho wa dunia. Na waliouawa na BWANA siku ile watakuwapo, toka upande mmoja wa dunia hata upande wa pili; hawataliliwa, wala kukusanywa, wala kuzikwa; watakuwa samadi juu ya uso wa nchi.”—Yeremia 25:32, 33.

Mwisho wa Uovu

4. Kwa nini Yehova ana haki ya kukomesha mfumo huu mwovu?

4 Yehova Mungu amevumilia uovu kwa miaka mingi sana. Amevumilia muda mrefu vya kutosha kwa watu wenye mioyo minyofu kuona kwamba utawala wa wanadamu huleta msiba mkuu. Kwa mfano, kichapo kimoja chasema kwamba katika karne ya 20 pekee, watu zaidi ya milioni 150 waliuawa katika vita, mapinduzi, na ghasia nyingine za raia. Ukatili wa mwanadamu hasa ulidhihirika wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili wakati watu milioni 50 walipouawa, wengi wao wakifa kifo cha kutisha katika kambi za mateso za Nazi. Kama Biblia ilivyotabiri, katika wakati wetu ‘watu waovu wataendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi.’ (2 Timotheo 3:1-5, 13) Leo, ukosefu wa maadili, uhalifu, jeuri, ufisadi, na kudharau kanuni za Mungu ni mambo yaliyoenea sana. Hivyo, Yehova ana haki ya kukomesha mfumo huu mwovu.

5, 6. Eleza uovu uliokuwako Kanaani ya kale.

5 Hali sasa ni kama vile ilivyokuwa Kanaani miaka 3,500 hivi iliyopita. Biblia yasema: “Kila yaliyo machukizo kwa BWANA, ayachukiayo yeye, wameifanyia miungu yao; kwa maana hata wana wao na binti zao huiteketezea hiyo miungu yao ndani ya moto.” (Kumbukumbu la Torati 12:31) Yehova aliliambia taifa la Israeli hivi: “Ni kwa uovu wa mataifa haya BWANA, Mungu wako, awafukuza nje mbele yako.” (Kumbukumbu la Torati 9:5) Mwanahistoria wa Biblia, Henry H. Halley alisema: “Ibada ya Baali, Ashtorethi, na miungu ya Kanaani ilikuwa na sherehe zilizopotoka zaidi za ulafi, ulevi na uasherati; mahekalu yao yalikuwa vituo vya uovu.”

6 Halley alionyesha jinsi uovu wao ulivyokuwa mbaya, kwa kuwa katika kimojawapo cha vituo hivyo vingi; waakiolojia “walipata mitungi mingi sana iliyojaa maiti za watoto waliokuwa wametolewa dhabihu kwa Baali.” Yeye alisema: “Eneo lote lilikuwa makaburi ya vitoto vichanga. . . . Wakanaani waliabudu, kwa kujiingiza katika uasherati, ukiwa sherehe ya kidini, mbele ya miungu yao; kisha wakawaua watoto wao wa kwanza, na kuwatoa dhabihu kwa miungu hiyohiyo. Yaonekana kwamba, kwa kiwango kikubwa, nchi yote ya Kanaani ilikuwa kama Sodoma na Gomora. . . . Je, ustaarabu wenye uchafu na ukatili wa aina hiyo ulifaa kuendelea kuwako? . . . Waakiolojia wanaochimbua magofu ya majiji ya Kanaani hushangaa ni kwa nini Mungu hakuwaharibu mapema zaidi ya alivyofanya.”

Kuirithi Dunia

7, 8. Mungu atasafishaje dunia hii?

7 Kama Mungu alivyosafisha Kanaani, karibuni ataisafisha dunia, nayo itapewa wale wafanyao mapenzi yake. “Wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi.” (Mithali 2:21, 22) Naye mtunga-zaburi asema: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo . . . Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:10, 11) Shetani pia ataondolewa, ili “asipate kuongoza mataifa vibaya tena kamwe mpaka miaka elfu i[taka]pokuwa imekwisha.” (Ufunuo 20:1-3) Naam, “ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:17.

8 Akimaliza mazungumzo yake juu ya tumaini la wale wanaotaka kuishi milele duniani, Yesu alisema: “Wenye furaha ni wenye tabia-pole, kwa kuwa wao watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Yaelekea alikuwa anarejezea andiko la Zaburi 37:29, lililotabiri: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” Yesu alijua kwamba Yehova alikusudia wanyofu waishi milele katika dunia paradiso. Yehova asema: “Mimi nimeiumba dunia hii, wanadamu na wanyama walio juu ya uso wa nchi, kwa uweza wangu mkuu . . . , nami nawapa watu kama inipendezavyo.”—Yeremia 27:5.

Ulimwengu Mpya Bora

9. Ufalme wa Mungu utaleta ulimwengu wa aina gani?

9 Baada ya Har–Magedoni, Ufalme wa Mungu utaleta “dunia mpya” bora ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Kuondolewa kwa mfumo huu mwovu wa mambo wenye kukandamiza kutakuwa kitulizo kilichoje kwa waokokaji wa Har–Magedoni! Watafurahi kama nini kuingia katika ulimwengu mpya wenye uadilifu chini ya Ufalme wa mbinguni wa Mungu, wakitarajia baraka za ajabu na uhai udumuo milele!—Ufunuo 7:9-17.

10. Ni mambo gani mabaya ambayo hayatakuwapo katika utawala wa Ufalme?

10 Watu hawatatishwa tena na vita, uhalifu, njaa, au hata wanyama wawindaji. “Nitafanya agano la amani [na watu wangu], nami nitawakomesha wanyama wakali kati yao . . . Na mti wa kondeni utazaa matunda yake, nayo ardhi itatoa mazao yake, nao watakuwa salama katika nchi yao.” “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe. Bali wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.”—Ezekieli 34:25-28; Mika 4:3, 4.

11. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba magonjwa yataisha?

11 Ugonjwa, huzuni, na hata kifo zitaondolewa. “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa; watu wakaao humo watasamehewa uovu wao.” (Isaya 33:24) “[Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali. . . . ‘Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’” (Ufunuo 21:4, 5) Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha uwezo wake wa kufanya mambo hayo kwa nguvu alizopewa na Mungu. Kwa msaada wa roho takatifu, Yesu alitembea kotekote nchini akiwaponya vilema na wagonjwa pia.—Mathayo 15:30, 31.

12. Wafu wana tumaini gani?

12 Yesu alifanya mambo mengi hata zaidi. Alifufua wafu. Wanyenyekevu waliitikiaje? Alipomfufua msichana mwenye umri wa miaka 12, wazazi wake “wa[li]pigwa na bumbuazi ya upeo wa shangwe kubwa.” (Marko 5:42) Huo ni mfano mwingine wa mambo ambayo Yesu atafanya duniani kote wakati wa utawala wa Ufalme, kwa kuwa wakati huo “kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Ebu wazia upeo wa shangwe wakati vikundi vya wafu watakapofufuka na kuungana na wapendwa wao! Yaelekea Ufalme utasimamia kazi nyingi sana ya kuelimisha hivi kwamba “dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

Enzi Kuu ya Yehova Yatetewa

13. Haki ya Mungu ya kutawala itadhihirishwaje?

13 Kufikia mwisho wa miaka elfu ya utawala wa Ufalme, familia ya kibinadamu itakuwa imerudishiwa ukamilifu wa akili na mwili. Dunia itakuwa bustani ya Edeni ya ulimwenguni pote, yaani paradiso. Kutakuweko amani, furaha, usalama, na jamii ya kibinadamu yenye upendo. Hali kama hiyo haijawahi kuonekana katika historia ya wanadamu kabla ya utawala wa Ufalme. Ni tofauti iliyoje ambayo itakuwa imedhihirishwa wakati huo kati ya miaka elfu nyingi iliyopita ya utawala wenye taabu wa wanadamu na utawala mtukufu wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu wa miaka elfu! Kwa jumla utawala wa Mungu kupitia Ufalme utakuwa umedhihirishwa kuwa bora kabisa. Haki ya Mungu ya kutawala, enzi yake kuu, zitakuwa zimetetewa kabisa.

14. Ni nini kitakachowapata waasi miaka ile elfu inapoisha?

14 Mwishoni mwa hiyo miaka elfu, Yehova atawaruhusu wanadamu wakamilifu kutumia uhuru wao wa kuchagua kwa habari ya wanayetaka kumtumikia. Biblia yaonyesha kwamba “Shetani atafunguliwa kutoka katika gereza lake.” Atajaribu tena kuwapotosha wanadamu na baadhi yao watachagua kutomtegemea Mungu. Ili kuzuia ‘mateso yasiinuke mara ya pili,’ Yehova atamwangamiza Shetani, roho wake waovu, na wote wanaoasi enzi kuu ya Yehova. Hakuna anayeweza kubisha kwamba wanadamu wowote wale watakaoharibiwa milele wakati huo hawakuwa na nafasi, au mwenendo wao mbaya ulitokana na kutokamilika. La, watakuwa kama Adamu na Hawa wakamilifu, ambao walichagua kwa hiari kuasi utawala mwadilifu wa Yehova.—Ufunuo 20:7-10; Nahumu 1:9.

15. Waaminifu-washikamanifu watakuwa na uhusiano gani na Yehova?

15 Kwa upande mwingine, yaelekea walio wengi watachagua kuunga mkono enzi kuu ya Yehova. Baada ya waasi wote kuangamizwa, waadilifu watasimama mbele za Yehova, wakiwa wamepita mtihani wa mwisho wa uaminifu-mshikamanifu. Kisha waaminifu-washikamanifu hao watakubaliwa na Yehova kuwa wana na binti zake. Kwa hiyo watakuwa na uhusiano ambao Adamu na Hawa walikuwa nao pamoja na Mungu kabla ya kuasi. Hivyo, andiko la Waroma 8:21 litatimizwa: “Viumbe vyenyewe [wanadamu] pia vitawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” Nabii Isaya anatabiri: “[Mungu] amemeza mauti hata milele; na Bwana MUNGU atafuta machozi katika nyuso zote.”—Isaya 25:8.

Tumaini la Uhai Udumuo Milele

16. Kwa nini inafaa kutazamia kwa hamu thawabu ya uhai udumuo milele?

16 Watu waaminifu wana matazamio mazuri kama nini, kujua kwamba Mungu atawafanikisha sana kiroho na kimwili milele! Kwa kufaa, mtunga-zaburi alisema hivi: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake [yafaayo].” (Zaburi 145:16) Yehova huwatia moyo wale wa jamii ya kidunia wawe na tumaini hili la uhai katika Paradiso likiwa sehemu ya imani yao kwake. Ingawa suala la enzi kuu ya Yehova ni muhimu zaidi, yeye haaliki watu wamtumikie bila kutazamia thawabu. Katika Biblia yote, uaminifu-mshikamanifu kwa Mungu na tumaini la uhai udumuo milele, mambo yasiyoweza kutenganishwa, ni sehemu muhimu za imani ya Mkristo katika Mungu. “Amkaribiaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Waebrania 11:6.

17. Yesu alionyeshaje kwamba inafaa kutegemezwa na tumaini letu?

17 Yesu alisema: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Hapa alihusisha kumjua Mungu na makusudi yake na ile thawabu itokanayo na kufanya hivyo. Kwa mfano, wakati mkosaji mmoja alipoomba akumbukwe baada ya Yesu kupokea Ufalme, Yesu alisema: “Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:43) Hakumwambia mtu huyo awe na imani hata ikiwa hatapata thawabu. Alijua kwamba Yehova hutaka watumishi wake wawe na tumaini la uhai udumuo milele katika dunia paradiso ili kuwategemeza wanapokabili majaribu mbalimbali katika ulimwengu huu. Hivyo, kutarajia kwa hamu thawabu hiyo ni msaada muhimu ili kuvumilia ukiwa Mkristo.

Wakati Ujao wa Ufalme

18, 19. Ni nini kitakachotukia kwa Mfalme na Ufalme mwishoni mwa Utawala wa Milenia?

18 Kwa kuwa Ufalme ni serikali saidizi ambayo Yehova atatumia kuleta ukamilifu kwa dunia na wakazi wake na pia kuwapatanisha naye, basi Mfalme Yesu Kristo na wale wafalme na makuhani 144,000 watakuwa na wajibu gani baada ya Milenia? “Halafu, mwisho, wakati amkabidhipo ufalme Mungu wake aliye Baba, wakati akiwa amefanya serikali yote na mamlaka yote na nguvu kuwa si kitu. Kwa maana ni lazima yeye atawale akiwa mfalme mpaka Mungu awe ameweka maadui wote chini ya miguu yake.”—1 Wakorintho 15:24, 25.

19 Kristo amkabidhipo Mungu Ufalme, yaelewekeje maandiko yanayosema kwamba ufalme huo utadumu milele? Mambo utakayotimiza yatadumu milele. Kristo atatukuzwa milele kwa sababu ya wajibu wake katika kutetewa kwa enzi kuu ya Mungu. Lakini kwa kuwa wakati huo dhambi na kifo zitakuwa zimeondolewa kabisa, na mwanadamu amekombolewa, Yesu hatahitajika akiwa Mkombozi. Utawala wa Milenia wa Ufalme utakuwa pia umekamilika kabisa; kwa hiyo, hakutahitajika tena kuweko serikali saidizi kati ya Yehova na wanadamu watiifu. Hivyo, “Mungu apate kuwa vitu vyote kwa kila mtu.”—1 Wakorintho 15:28.

20. Tunaweza kujuaje yale ambayo Kristo na wale 144,000 watafanya wakati ujao?

20 Kristo na watawala wenzake watakuwa na wajibu gani baada ya Utawala wa Milenia kukamilika? Biblia haisemi. Hata hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawapa mapendeleo mengine mengi ya utumishi katika uumbaji wake wote. Sote na tuunge mkono enzi kuu ya Yehova na kupewa uhai udumuo milele, ili wakati ujao, tuwe hai kujua ni nini Yehova amekusudia kwa Mfalme, hata kwa wafalme na makuhani wenzake, na vilevile ulimwengu wake wote wa ajabu!

Mambo ya Kupitia

• Tunakaribia badiliko gani la utawala?

• Mungu atahukumuje waovu na waadilifu?

• Ni hali gani zitakazokuwapo katika ulimwengu mpya?

• Enzi kuu ya Yehova itatetewaje kikamili?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

“Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia”

[Picha katika ukurasa wa 18]

Waaminifu-washikamanifu watakuwa tena na uhusiano ufaao pamoja na Yehova