Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Maadili ya Biblia Ndiyo Bora Kabisa?

Je, Maadili ya Biblia Ndiyo Bora Kabisa?

Je, Maadili ya Biblia Ndiyo Bora Kabisa?

“JAMII yahitaji mfumo wa kanuni za msingi zinazowapa washiriki wake usalama na mwongozo.” Ndivyo alivyosema mwandishi na mtangazaji wa televisheni Mjerumani mwenye uzoefu. Kwa kweli hilo linaeleweka. Ili jamii ya binadamu iwe na utulivu na ifanikiwe, watu wapaswa kuwa na msingi imara wa viwango vinavyokubaliwa na wote, vinavyopambanua yanayofaa na yasiyofaa, mema na mabaya. Swali ni: Ni viwango gani vilivyo bora kabisa kwa jamii?

Maadili ya Biblia yanapotumika yakiwa viwango, yanapasa kusaidia watu waishi maisha yenye utulivu na furaha. Yakifuatwa na jamii nzima, jamii hiyo itakuwa na watu wenye furaha zaidi na watulivu zaidi. Je, ndivyo ilivyo? Acheni tuchunguze yale isemayo Biblia juu ya masuala mawili muhimu: uaminifu katika ndoa na unyofu katika maisha ya kila siku.

Usimwache Mwenzi Wako

Muumba wetu alimwumba Adamu kisha akamwumba Hawa kuwa mwenzi wake. Muungano wao ulikuwa ndoa ya kwanza katika historia na ulipasa kuwa uhusiano wa kudumu. Mungu alisema: “Mwanamume atamwacha mama yake na baba yake naye ataambatana na mkewe.” Miaka 4,000 hivi baadaye, Yesu Kristo alirudia kiwango hicho cha ndoa kwa wafuasi wake wote. Zaidi ya hayo, alishutumu uhusiano wa ngono nje ya ndoa.—Mwanzo 1:27, 28; 2:24; Mathayo 5:27-30; 19:5.

Kulingana na Biblia, funguo mbili muhimu za ndoa yenye furaha ni upendo na staha kutoka kwa wenzi wote wawili. Mume, ambaye ni kichwa cha familia, apaswa kuonyesha upendo usio na ubinafsi kwa kuzingatia masilahi ya mkewe. Anapaswa kuishi naye “kulingana na ujuzi” na hapaswi “[kumkasirikia] kwa uchungu.” Mke apaswa kumpa mume wake “staha yenye kina kirefu.” Wenzi wa ndoa wakifuata kanuni hizo, wanaweza kuepuka au kutatua magumu mengi ya ndoa. Mume atataka kushikamana na mkewe, na mke vivyo hivyo.—1 Petro 3:1-7; Wakolosai 3:18, 19; Waefeso 5:22-33.

Je, kiwango cha Biblia cha kushikamana kwa uaminifu na mwenzi wa ndoa hufanya ndoa iwe yenye furaha? Fikiria matokeo ya uchunguzi uliofanywa nchini Ujerumani. Watu waliulizwa ni mambo gani yaliyo muhimu kwa ndoa nzuri. Mojawapo ya mambo muhimu zaidi yaliyotajwa ni uaminifu wa wenzi wote wawili. Je, hukubali kwamba watu waliofunga ndoa huwa na furaha zaidi wanapojua kwamba wenzi wao ni waaminifu?

Vipi Matatizo Yakitokea?

Iweje mume na mke wanapokosa kuafikiana kabisa-kabisa? Vipi upendo wao ukipoa? Je, haingefaa kuvunja ndoa chini ya hali kama hizo? Au je, kiwango cha Biblia cha kushikamana kwa uaminifu na mwenzi wa ndoa bado ni chenye busara?

Waandishi wa Biblia walitambua kwamba wenzi wote waliofunga ndoa watakuwa na matatizo kwa sababu ya kutokamilika kwa binadamu. (1 Wakorintho 7:28) Hata hivyo, wenzi wa ndoa wanaofuata viwango vya maadili vya Biblia hujaribu kusamehe na kutatua magumu yao pamoja. Bila shaka, kuna hali fulani—kama vile uzinzi au kutendwa vibaya kimwili—ambazo kwa kufaa huenda zikamfanya Mkristo afikirie kutengana au kutalikiana. (Mathayo 5:32; 19:9) Lakini kuvunja ndoa harakaharaka bila sababu nzito au ili kupata mwenzi mwingine kwaonyesha ubinafsi na kutowajali wengine. Bila shaka hakutokezi maisha yenye utulivu au yenye furaha. Acheni tuchukue mfano mmoja.

Peter alihisi kwamba ndoa yake haikuwa na uchangamfu kama hapo mwanzoni. * Kwa hiyo, akaacha mke wake na kuanza kuishi na Monika aliyekuwa amemwacha mumewe. Mambo yakawaje? Baada ya miezi michache tu, Peter alikiri kwamba “haikuwa rahisi [kuishi na Monika] kama nilivyowazia.” Kwa nini? Mwenzi huyu mpya alikuwa na kasoro zilezile za kibinadamu alizokuwa nazo yule wa kwanza. Jambo lililokuwa baya zaidi ni kwamba uamuzi wake wa haraka na wa ubinafsi ulimletea matatizo makubwa sana ya kifedha. Isitoshe, watoto wa Monika waliathirika sana kihisia-moyo kwa sababu ya badiliko kubwa lililoikumba familia yao.

Kama ionyeshwavyo na jambo hili, ndoa inapokumbwa na matatizo, utatuzi si kuivunja. Kwa upande mwingine, wakati wa matatizo, kuishi kwa kupatana na kanuni za maadili za Neno la Mungu, Biblia, mara nyingi kwaweza kuokoa ndoa. Ilikuwa hivyo kwa Thomas na Doris.

Thomas na Doris walikuwa wameoana kwa zaidi ya miaka 30 wakati Thomas alipoanza kunywa vileo kupindukia. Doris alipatwa na mshuko-moyo, na wote wawili wakazungumza kuhusu kutalikiana. Doris alizungumza jambo hilo pamoja na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Shahidi huyo alimwonyesha Doris yale ambayo Biblia husema kuhusu ndoa, na kumtia moyo asifanye haraka kutengana na mume wake lakini kwanza ajaribu kutatua matatizo yake pamoja naye. Doris akafanya hivyo. Baada ya miezi michache, hawakuzungumza tena kuhusu talaka. Thomas na Doris walikuwa wakitatua matatizo yao pamoja. Kufuata shauri la Biblia kuliimarisha ndoa yao na kukawapa wakati wa kutatua matatizo yao.

Unyofu Katika Mambo Yote

Kushikamana kwa uaminifu na mwenzi wa ndoa hutaka nguvu za kiadili na kuazimia kufuata kanuni zifaazo. Sifa hizohizo zahitajika ili kuendelea kuwa mnyofu katika ulimwengu usio mnyofu. Biblia husema mengi kuhusu unyofu. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa karne ya kwanza katika Yudea: “Twataka kujiendesha wenyewe kwa kufuata haki katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Hiyo yamaanisha nini?

Mtu mnyofu husema kweli na hadanganyi. Hutendea wengine kwa haki—kwa njia ya waziwazi, kwa heshima, bila kuwadanganya au kuwapotosha. Isitoshe, mtu mnyofu ni mwenye uaminifu-maadili na halaghai wanadamu wenzake. Watu wanyofu huchangia hali ya kutumainiana, ambayo hutokeza mitazamo inayofaa na kuendeleza mahusiano thabiti kati ya watu.

Je, watu wanyofu ni wenye furaha? Naam, wana sababu ya kuwa na furaha. Licha ya kuenea kwa ufisadi na ulaghai—au kwa sababu ya kuwepo kwa mambo hayo—kwa ujumla watu wanyofu huvutia wengine. Kulingana na uchunguzi uliofanyiwa vijana, asilimia 70 ya waliohojiwa walisema kwamba unyofu ni sifa bora sana. Zaidi ya hayo, bila kujali tuna umri gani, unyofu ni sifa muhimu tunayotarajia kutoka kwa rafiki zetu.

Christine alifundishwa kuiba tangu alipokuwa na umri wa miaka 12. Baada ya miaka kadhaa akawa stadi wa kuiba kutoka mifukoni mwa watu. “Kuna siku ambazo nilirudi nyumbani na Maki 5,000 za Ujerumani [Dola 2,200 za Marekani] pesa taslimu,” yeye aeleza. Lakini Christine alikamatwa mara kadhaa, naye aliishi kwa hofu ya kufungwa gerezani. Mashahidi wa Yehova walipomweleza yale ambayo Biblia husema juu ya unyofu, Christine alivutiwa na viwango vya maadili vya Biblia. Akajifunza kutii shauri hili: “Mwibaji na asiibe tena.”—Waefeso 4:28.

Wakati alipobatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, Christine alikuwa ameacha kuiba. Alikuwa akijitahidi kuwa mnyofu katika mambo yote, kwa kuwa Mashahidi hukazia sana unyofu na sifa nyingine za Kikristo. Gazeti Lausitzer Rundschau laripoti hivi: “Maadili kama vile unyofu, kiasi, na kupenda jirani yanaonwa kuwa ya maana sana katika imani ya Mashahidi.” Christine anahisije juu ya badiliko hilo katika maisha yake? “Sasa nina furaha zaidi kwa sababu nimeacha kuiba. Ninahisi kuwa mshiriki mwenye kuheshimika katika jamii.”

Jamii Nzima Hunufaika

Watu ambao ni waaminifu kwa wenzi wao wa ndoa na ni wanyofu wana furaha na pia hunufaisha jamii kwa ujumla. Waajiri hupendelea wafanyakazi wasiolaghai. Sote hupenda kuwa na majirani waaminifu, na twapenda kununua vitu kwenye maduka ya wafanyabiashara wanyofu. Je, hatuwaheshimu wanasiasa, polisi, na mahakimu wanaojiepusha na ufisadi? Jumuiya hunufaika sana watu wake wanapokuwa wanyofu kwa sababu ya kupenda kanuni, si wakati tu inapofaa kufanya hivyo.

Zaidi ya hayo, wenzi wa ndoa waaminifu ndio msingi wa familia thabiti. Watu wengi watakubaliana na mwanasiasa mmoja wa Ulaya aliyesema hivi: “Kufikia sasa familia [ya kawaida] bado ndiyo huandaa mahali panapofaa sana kwa ajili ya usalama na maisha yenye maana ya wanadamu.” Amani katika familia huwapa watu wazima na watoto fursa bora kabisa ya kupata usalama wa kihisia-moyo. Kwa hiyo wale ambao ni waaminifu katika ndoa wanasaidia kujenga jamii thabiti.

Fikiria jinsi ambavyo kila mtu angenufaika ikiwa hakungekuwa na wenzi walioachwa, kesi za talaka, au kesi zinazohusu malezi ya watoto. Vipi kama hakungekuwa na wezi wanaoibia watu mifukoni, wezi wanaoiba vitu madukani, watu wanaoiba fedha zilizowekwa amana, maofisa wafisadi, au wanasayansi wadanganyifu? Je, hayo yasikika kama ndoto tu? Wale wanaopendezwa kikweli na Biblia na yale isemayo kuhusu wakati wetu ujao hawaoni maneno hayo kuwa ndoto. Neno la Mungu laahidi kwamba hivi karibuni Ufalme wa Kimesiya wa Yehova utachukua mahali pa serikali zote za wanadamu zinazotawala duniani. Chini ya Ufalme huo raia wote watafundishwa kuishi kulingana na maadili ya Biblia. Wakati huo “wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29.

Maadili ya Biblia Ndiyo Maadili Bora Kabisa

Mamilioni ya watu ambao wamechunguza Maandiko Matakatifu wamepata kujua kwamba shauri la Biblia linategemea hekima ya Mungu, ambayo yapita kwa mbali kufikiri kwa wanadamu. Watu hao huiona Biblia kuwa yenye kutumainika na yenye kutumika katika maisha ya ulimwengu wetu wa kisasa. Wanajua kwamba watapata faida kwa kutii shauri la Neno la Mungu.

Kwa hiyo, watu hao huzingatia shauri la Biblia linalosema: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:5, 6) Kwa kufanya hivyo, wanaboresha sana maisha yao, na pia wananufaisha wale wanaoishi karibu nao. Nao wanasitawisha tumaini imara katika “uhai . . . utakaokuja,” wakati ambapo wanadamu wote watafuata maadili ya Biblia.—1 Timotheo 4:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Majina yamebadilishwa katika makala hii.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Wakati wa matatizo ya ndoa, mara nyingi kuishi kwa kupatana na viwango vya Biblia kwaweza kuokoa ndoa na kusaidia kuepuka matatizo

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Licha ya kuenea kwa ufisadi—au kwa sababu ya kuwepo kwa ufisadi—kwa ujumla watu wanyofu huvutia wengine