Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Jinsi Inavyotamanika Imani Isiyofifia”!

“Jinsi Inavyotamanika Imani Isiyofifia”!

Simulizi la Maisha

“Jinsi Inavyotamanika Imani Isiyofifia”!

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA HERBERT MÜLLER

Miezi michache baada ya jeshi la Hitler kuvamia Uholanzi, Mashahidi wa Yehova walipigwa marufuku. Punde si punde, jina langu lilikuwa katika orodha ya watu waliokuwa wakitafutwa zaidi, nami niliwindwa kama mnyama.

WAKATI mmoja, nilikuwa nimechoka sana kutokana na kujificha na kukimbia, hivi kwamba nilimwambia mke wangu kuwa ingekuwa afadhali kukamatwa na jeshi. Ndipo nikakumbuka maneno ya wimbo fulani: “Jinsi inavyotamanika imani isiyofifia, ijaposhambuliwa na adui za kila aina.” * Kutafakari wimbo huo kulinitia nguvu na kunikumbusha wazazi wangu huko Ujerumani na ile siku ambayo rafiki zangu waliimba wimbo huo ili kuniaga. Je, unataka kujua baadhi ya mambo niliyoyakumbuka?

Mfano wa Wazazi Wangu

Nilipozaliwa mwaka wa 1913 mjini Copitz, Ujerumani, wazazi wangu walikuwa washiriki wa kanisa la Evangelical Church. * Miaka saba baadaye, mwaka wa 1920, baba aliacha hilo kanisa. Mnamo Aprili 6, aliomba Kirchenaustrittsbescheinigung (Hati ya Kujiuzulu Kutoka Kanisani). Ofisa wa kuandikisha raia wa mji alijaza hati moja. Juma moja baadaye Baba alirudi ofisini na kueleza kwamba hati hiyo haikuwa na jina la binti yake. Ofisa huyo alijaza hati ya pili iliyotaarifu kwamba hati ya kujiuzulu kanisani ilipaswa kutia ndani Martha Margaretha Müller. Wakati huo, dada yangu, Margaretha, alikuwa na umri wa mwaka mmoja na nusu. Baba alitaka mambo yanayohusu kumtumikia Yehova yafanywe kikamili!

Mwaka uo huo, wazazi wangu walibatizwa na Wanafunzi wa Biblia, kama walivyoitwa Mashahidi wa Yehova wakati huo. Baba alitulea kwa nidhamu kali, lakini uaminifu-mshikamanifu wake kwa Yehova ulifanya iwe rahisi kwetu kukubali mwongozo wake. Uaminifu-mshikamanifu uliwachochea wazazi wangu kufanya marekebisho pia. Kwa mfano, katika kipindi fulani hatukuruhusiwa kucheza nje siku za Jumapili. Hata hivyo, Jumapili moja mwaka 1925, wazazi wetu walituambia kuwa tungekwenda matembezi. Tulibeba vyakula vyepesi na tulifurahia siku hiyo—ilikuwa tofauti kama nini na kufungiwa nyumbani siku nzima! Baba alisema kwamba alikuwa amejifunza mambo mapya katika mkusanyiko wa karibuni yaliyorekebisha maoni yake juu ya utendaji wa Jumapili. Nyakati nyingine pia alionyesha utayari uleule wa kujirekebisha.

Hata ingawa wazazi wangu hawakuwa na afya nzuri, hawakuacha kuhubiri. Kwa mfano, ili kugawa trakti ya Ecclesiastics Indicted (Viongozi wa Kanisa Washtakiwa) tulipanda garimoshi jioni moja pamoja na ndugu wengine wa kutaniko na kusafiri hadi mji wa Regensburg, ulio umbali wa kilometa 300 kutoka Dresden. Siku iliyofuata, tuligawa trakti hizo kote kote mjini, na tulipomaliza, tukarudi nyumbani kwa garimoshi. Safari hiyo yote ilichukua karibu muda wa saa 24.

Kuondoka Nyumbani

Kushirikiana na Jugendgruppe (Kikundi cha Vijana) wa kutaniko letu, pia kulinisaidia kukua kiroho. Kila juma, vijana wenye umri unaozidi miaka 14 walikutana na baadhi ya ndugu wa kutaniko wenye umri mkubwa zaidi. Tulicheza michezo na kupiga ala za muziki, tukajifunza Biblia, na kuzungumza juu ya uumbaji na sayansi. Hata hivyo, mwaka 1932, nilipokuwa na umri wa miaka 19, sikushirikiana na kikundi hicho tena.

Mnamo Aprili mwaka huo, Baba alipokea barua kutoka ofisi ya Watch Tower Society huko Magdeburg. Sosaiti ilikuwa ikitafuta mtu aliyejua kuendesha gari na aliyetaka kuwa painia. Nilijua kuwa wazazi wangu walitaka niwe painia, lakini nilihisi kwamba singeweza. Kwa kuwa wazazi wangu walikuwa maskini, nilikuwa nimeanza kurekebisha baiskeli na cherehani, na vilevile taipureta na mashine nyingine za ofisi, nilipokuwa na umri wa miaka 14. Ningewezaje kuacha familia yangu? Walihitaji usaidizi wangu. Na zaidi ya hayo, hata sikuwa nimebatizwa bado. Baba alikaa nami, akaniuliza maswali kadhaa kuona ikiwa nilielewa maana ya ubatizo. Majibu yangu yalipomhakikishia kuwa nimefanya maendeleo ya kiroho vya kutosha ili kustahili kubatizwa, alisema hivi: “Wapaswa kujitolea kwa mgawo huu.” Ndivyo nilivyofanya.

Juma moja baadaye nilialikwa Magdeburg. Nilipowaeleza rafiki zangu wa Kikundi cha Vijana, walitaka kuniaga kwa kuniimbia wimbo mchangamfu. Walishangaa kuona kwamba nilichagua wimbo uliokuwa na ujumbe mzito sana. Hata hivyo, wengine walichukua zeze, gambusi, na gitaa zao na wote wakaimba: “Jinsi inavyotamanika imani isiyofifia, ijaposhambuliwa na adui za kila aina; ambayo haitayumba-yumba kwa sababu ya ole wowote wa dunia hii.” Siku hiyo, sikujua kwamba maneno hayo yangenitia nguvu mara nyingi miaka iliyofuata.

Mwanzo Wenye Msukosuko

Baada ya kutahini ustadi wangu wa kuendesha gari, akina ndugu huko Magdeburg walitukabidhi mimi na mapainia wengine wanne gari, nasi tukaelekea eneo la Schneifel lililoko karibu na Ubelgiji. Mara tulitambua kwamba gari lilikuwa la lazima. Watu wa Kanisa Katoliki la eneo hilo walichukia kuwapo kwetu, na mara nyingi watu wa vijiji waliochochewa na makasisi walitungojea ili watufukuze. Mara nyingi gari lilitusaidia kuepa walipotushambulia kwa majembe na nyuma za kuzoa nyasi.

Baada ya Ukumbusho mwaka wa 1933, mwangalizi wa eneo, Paul Grossmann, alituambia kuwa kazi ya Sosaiti huko Ujerumani ilikuwa imepigwa marufuku. Punde si punde, ndugu wa ofisi ya tawi waliniomba nije na gari hadi Magdeburg, nichukue vichapo na kuvisafirisha hadi jimbo la Saxony, lililo umbali wa kilometa 100 hivi kutoka Magdeburg. Hata hivyo, nilipofika Magdeburg, tayari Gestapo (polisi wa siri wa Nazi) walikuwa wamefunga ofisi ya Sosaiti. Niliacha gari kwa ndugu mmoja huko Leipzig, nikarudi nyumbani—lakini sikukaa kwa muda mrefu.

Ndugu katika ofisi ya Sosaiti nchini Uswisi walinialika nianze kufanya upainia nchini Uholanzi. Nikapanga kuondoka baada ya juma moja au mawili. Hata hivyo, Baba alinishauri nianze safari mara moja. Nikafuata ushauri wake, na baada ya saa chache nikaondoka nyumbani. Siku iliyofuata, polisi walikuja nyumbani kwa baba ili kunikamata kwa shtaka la kutoroka. Walichelewa.

Naanza Upainia Huko Uholanzi

Agosti 15, 1933, niliwasili kwenye nyumba ya mapainia huko Heemstede, mji ulio umbali wa kilometa 25 kutoka Amsterdam. Kesho yake nilianza kuhubiri bila kujua hata neno moja la Kiholanzi. Nikiwa na kadi yenye ushahidi ulioandikwa, nikaanza kufanya kazi. Nilitiwa moyo sana mwanamke mmoja Mkatoliki alipokubali kupokea kitabu cha Reconciliation! Siku hiyohiyo, pia niligawa vijitabu 27. Mwishoni mwa siku hiyo ya kwanza nilifurahi sana kuweza kuhubiri kwa uhuru tena.

Siku hizo, mapainia hawakuwa na mapato mengine isipokuwa michango waliyopata walipogawia watu vichapo. Fedha hizo zilitumiwa kununua chakula na kwa mahitaji mengine. Iwapo kiasi kidogo cha fedha kilibaki mwishoni mwa mwezi, mapainia walikigawanya miongoni mwao kwa matumizi ya binafsi. Hatukuwa na vitu vingi vya kimwili, lakini Yehova alituandalia vya kutosha hivi kwamba mwaka wa 1934, niliweza kuhudhuria mkusanyiko Uswisi.

Mwenzi Mwaminifu

Mkusanyikoni, nilikutana na Erika Finke mwenye umri wa miaka 18. Nilimjua tangu nilipokuwa nikiishi nyumbani. Erika alikuwa rafiki ya dada yangu, Margaretha, na sikuzote nilivutiwa na msimamo wake imara kwa ile kweli. Punde tu baada ya kubatizwa mwaka wa 1932, mtu fulani aliwajulisha Gestapo kwamba Erika alikuwa amekataa kusema “Heil Hitler!” Gestapo walimtafuta, wakataka kujua sababu ya kukataa. Erika alimsomea ofisa aliyekuwa kwenye kituo cha polisi Matendo 17:3 na kueleza kuwa Mungu ameweka mtu mmoja tu kuwa Mwokozi, Yesu Kristo. “Kuna wengine wanaoshikilia imani kama yako?” ofisa huyo akataka kujua. Erika akakataa kutaja majina yoyote. Polisi huyo alipotisha kumfunga, Erika alimwambia kwamba afadhali afe kuliko kutaja majina. Alimkodolea macho na kupaaza sauti: “Toka hapa. Nenda nyumbani. Heil Hitler!”

Baada ya mkusanyiko, nilirudi Uholanzi na Erika akabaki Uswisi. Hata hivyo, sisi wote tulihisi kwamba urafiki wetu umekua. Alipokuwa bado Uswisi, Erika alipata habari kwamba alikuwa akitafutwa na Gestapo huko nyumbani. Akaamua kubaki Uswisi na kutumikia akiwa painia. Miezi michache baadaye Sosaiti ilimwomba aende Hispania. Alipainia Madrid, baadaye Bilbao, na hatimaye San Sebastián, ambapo mnyanyaso uliochochewa na makasisi ulisababisha yeye na painia mwenzake kufungwa gerezani. Mwaka 1935 walifukuzwa Hispania. Erika akaja Uholanzi, na mwaka uohuo tukaoana.

Ishara za Vita

Baada ya arusi yetu, tulifanya utumishi wa painia Heemstede, na baadaye tukahamia jiji la Rotterdam. Huko mwana wetu Wolfgang, alizaliwa mwaka wa 1937. Mwaka mmoja baadaye tukahamia jiji la Groningen, sehemu ya kaskazini ya Uholanzi, tulipoishi pamoja na mapainia Wajerumani Ferdinand na Helga Holtorf na binti yao. Mnamo Julai 1938 Sosaiti ilituambia kuwa serikali ya Uholanzi imewakataza Mashahidi Wajerumani wasihubiri tena nchini. Pindi hiyo, niliwekwa kuwa mtumishi wa kanda (mwangalizi wa mzunguko), jamaa yetu ikahama kwenye Lichtdrager (Kimulikaji), mashua ya Sosaiti iliyokuwa makao ya mapainia waliokuwa wakihubiri sehemu ya kaskazini mwa Uholanzi. Niliona jamaa yangu mara chache, huku nikisafiri kwa baiskeli kutoka kutaniko moja hadi jingine kuwatia moyo akina ndugu waendelee kuhubiri. Na hivyo ndivyo ndugu walivyofanya. Baadhi yao hata waliongeza utendaji wao. Wim Kettelarij alikuwa mfano mzuri.

Nilipokutana na Wim, alikuwa kijana aliyejua kweli lakini alikuwa na kazi nyingi za kibarua wa shamba. “Ukitaka kuwa na wakati wa kumtumikia Yehova, lazima utafute kazi nyingine,” nikamshauri. Ndivyo alivyofanya. Baadaye, tulipokutana tena, nikamtia moyo kutumikia akiwa painia. “Lakini lazima nifanye kazi ili nile,” akajibu. “Utakula,” nikamhakikishia. “Yehova atakutunza.” Wim akawa painia. Baadaye, alitumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko, hata wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu. Leo, Wim ambaye ana umri unaozidi miaka 80, bado ni Shahidi mwenye bidii. Naam, Yehova alimtunza.

Chini ya Marufuku na Kutafutwa

Mnamo Mei 1940, mwaka mmoja hivi baada ya kuzaliwa kwa mtoto wetu wa pili Reina, jeshi la Uholanzi lilisalimu amri na Wanazi wakamiliki Uholanzi. Mnamo Julai, matbaa na ofisi ya Sosaiti zilitwaliwa na Gestapo. Mwaka uliofuata Mashahidi wengi walikamatwa, kutia ndani mimi. Kwa sababu nilikuwa Shahidi Mjerumani mwenye umri wa kuitwa jeshini, halikuwa jambo gumu kuwazia kile ambacho kingenipata. Nilijaribu kukubali wazo la kwamba singeona jamaa yangu tena kamwe.

Halafu mnamo Mei 1941, Gestapo waliniacha huru wakaniamuru niende nikaanze utumishi wa jeshi. Sikuamini. Tangu siku hiyo Gestapo hawakuniona tena, na mwezi uohuo nikarudia kazi ya kuzunguka. Jina langu liliwekwa kwenye orodha ya Gestapo ya watu waliokuwa wakitafutwa sana.

Jinsi Jamaa Yangu Ilivyoishi

Mke wangu na watoto walikuwa wamehamia kijiji cha Vorden sehemu ya mashariki mwa nchi. Hata hivyo, ili nisiwahatarishe, sikuwatembelea nyumbani mara nyingi. (Mathayo 10:16) Kwa sababu za usalama, ndugu hawakutumia jina langu halisi, walitumia jina langu bandia tu Duitse Jan (John Mjerumani). Hata mwana wangu mwenye umri wa miaka minne, Wolfgang, hakuruhusiwa kusema juu ya “Baba,” badala yake alisema juu ya “Ome Jan” (Mjomba John). Jambo hilo lilikuwa gumu kwake kihisia-moyo.

Huku nilipokuwa nikisafiri na kujaribu kuhepa Gestapo, Erika alitunza watoto na kuendelea kuhubiri. Reina alipokuwa na umri wa miaka miwili, Erika alimpandisha kwenye sehemu ya kuwekea mizigo ya baiskeli na kuandamana naye alipohubiri sehemu za mashambani. Hata ingawa chakula kilikuwa haba, Erika hakukosa kamwe chakula kwa jamaa. (Mathayo 6:33) Mkulima Mkatoliki, ambaye nilikuwa nimemrekebishia cherehani alimpa viazi. Pia alimpasha Erika habari kutoka kwangu. Wakati mmoja, Erika alilipa guldeni moja kwa kitu alichonunua katika duka la dawa. Mwenye duka aliyejua anaishi mafichoni na hangeweza kupata kadi ya posho, alimpa kile alichotaka kununua na pia guldeni mbili. Vitendo vya huruma vya namna hiyo vilimsaidia kuendelea kuishi.—Waebrania 13:5.

Kufanya Kazi Bega kwa Bega Pamoja na Ndugu Wajasiri

Wakati uleule, niliendelea kutembelea makutaniko—ijapokuwa niliwasiliana na ndugu wenye madaraka tu kutanikoni. Kwa sababu nilitafutwa na Gestapo, nilikaa mahali pamoja kwa muda wa saa chache tu. Ndugu na dada wengi hawakuruhusiwa kukutana nami. Walijuana na Mashahidi wa kikundi kidogo cha funzo lao la Biblia pekee. Kwa sababu hiyo, dada wawili wa kimwili walioishi sehemu tofauti-tofauti katika jiji lilelile walijua tu baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili kwamba wote wawili walipata kuwa Mashahidi wakati wa vita.

Pia, nilikuwa na daraka la kutafuta mahali pa kuficha vichapo vya Sosaiti. Pia, tulificha karatasi, mashine za bamba la kupigia chapa, na taipureta zilizotumiwa kufanyiza nakala za Mnara wa Mlinzi, iwapo zingehitajiwa. Mara kwa mara, tulilazimika kuhamisha vichapo vya Sosaiti kutoka mahali pa maficho pamoja hadi pengine. Nakumbuka pindi moja nilipohamisha masanduku 30 yaliyojaa vichapo, huku nikijificha—kazi yenye kutia wasiwasi mno!

Zaidi ya hayo, tulipanga kusafirisha chakula kutoka katika mashamba yaliyokuwa mashariki ya Uholanzi hadi majiji ya magharibi, ijapokuwa jambo hilo lilikatazwa. Tukapakia chakula kwenye gari lililovutwa na farasi na kuelekea magharibi. Tulipofika mtoni, hatukuweza kuvuka kwa kutumia madaraja yoyote kwa kuwa yalilindwa na wanajeshi. Badala yake, tulihamisha mizigo kwenye mashua ndogo, mashua hizo zikavuka mto mara kadhaa zikiwa na chakula, halafu tukapakia mizigo kwenye gari jingine la farasi. Tulipofika jiji la mwisho wa safari yetu, tulingoja hadi usiku, tukavisha farasi soksi kwenye kwato, na bila kufanya kelele tukaelekea mahali pa kutaniko pa kuficha chakula. Hapo chakula kiligawanywa na kupelekwa kwa akina ndugu wenye uhitaji.

Ikiwa jeshi la Ujerumani lingaligundua mahali kama hapo pa kuficha chakula, ingaliweza kusababisha mtu auawe. Hata hivyo, ndugu kadhaa walijitoa kusaidia kufanya kazi hiyo. Kwa mfano jamaa ya Bloemink katika mji wa Amersfoort, walitoa sebule yao itumiwe kama ghala ya chakula, ijapokuwa nyumba yao ilikuwa karibu sana na ngome ya jeshi la Ujerumani! Mashahidi wajasiri kama hao walihatarisha uhai wao kwa ajili ya ndugu zao.

Yehova alinisaidia pamoja na mke wangu kudumu waaminifu muda wote wa marufuku. Mnamo Mei 1945 jeshi la Ujerumani lilishindwa, na hatimaye nikaacha kuwa mkimbizi. Sosaiti iliniomba niendelee kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko hadi ndugu wengine wapatikane. Mwaka wa 1947, Bertus van der Bijl, alichukua nafasi yangu. * Wakati huo, mtoto wetu wa tatu alikuwa amezaliwa, na tukahamia sehemu ya mashariki mwa nchi.

Huzuni na Shangwe

Baada ya vita, nilipata kujua kwamba mwaka mmoja baada ya kuondoka nyumbani na kuhamia Uholanzi, Baba alifungwa gerezani. Akaachiliwa mara mbili kwa sababu ya afya mbaya, lakini kila alipoachiliwa alifungwa tena. Mnamo Februari mwaka wa 1938 alipelekwa kwenye kambi ya mateso ya Buchenwald na hatimaye Dachau. Huko, tarehe 14 mwezi wa Mei, 1942, baba yangu akafa. Alisimama imara na kudumu mwaminifu-mshikamanifu hadi mwisho.

Mama pia alipelekwa kwenye kambi ya Dachau. Akabaki humo hadi alipoachiliwa mwaka wa 1945. Kwa kuwa kielelezo kizuri cha wazazi wangu kilinisaidia sana kupata baraka nyingi za kiroho, tuliona ni pendeleo kumwalika Mama aje kuishi nasi mwaka wa 1954. Dada yangu Margaretha, aliyekuwa amefanya utumishi wa painia Ujerumani-Mashariki ya Kikomunisti tangu 1945, akaja pamoja naye. Hata ingawa Mama alikuwa mgonjwa na hakusema Kiholanzi, aliendelea kushiriki utumishi wa shambani akiwa mwaminifu hadi mwisho wa maisha yake duniani mwezi wa Oktoba 1957.

Mkusanyiko wa mwaka wa 1955 mjini Nuremberg, Ujerumani, ulikuwa wa kipekee. Tulipowasili huko, ndugu wa mji wa Dresden walimwambia Erika kwamba mama yake alikuwa mkusanyikoni vilevile. Kwa kuwa Dresden ulikuwa chini ya utawala wa Ujerumani-Mashariki wakati huo, Erika hakuwa amemwona mama yake kwa muda wa miaka 21. Mipango ilifanywa wakutane, na mama na binti wakakumbatiana. Kulikuwa kukutana kwenye shangwe kama nini!

Hatimaye, tulikuwa na watoto wanane. Kwa kuhuzunisha, mwana wetu mmoja alikufa katika aksidenti ya gari. Hata hivyo, tunapata shangwe nyingi sana kuona watoto wetu wengine wote wakimtumikia Yehova. Tunafurahi kwamba mwana wetu Wolfgang na mke wake wanafanya kazi ya kuzunguka na mwana wao pia anatumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko.

Ninashukuru kwamba nimeona maendeleo ya kazi ya Yehova Uholanzi. Nilipoanza kutumikia nikiwa painia hapa mwaka wa 1933, kulikuwa na Mashahidi mia moja hivi. Leo, kuna Mashahidi zaidi ya 30,000. Hata ingawa nguvu zetu za mwili zinaendelea kupungua, bado mimi na Erika tumeazimia kuishi kwa kupatana na maneno ya wimbo ule wa siku zilizopita: “Jinsi inavyotamanika imani isiyofifia.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Wimbo 194.—Songs of Praise to Jehovah (1928).

^ fu. 7 Leo, mji wa Copitz, unaoitwa Pirna, uko kando ya Mto Elbe, ulio umbali wa kilometa 18 kutoka jiji la Dresden.

^ fu. 38 Ona Mnara wa Mlinzi, Januari 1, 1998, ukitaka kusoma simulizi la maisha la Ndugu Van der Bijl, “Hakuna Kitu Kilicho Bora Kuliko Kweli.”

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kikundi cha “Jugendgruppe” wakati wa mapumziko baada ya utumishi wa shambani

[Picha katika ukurasa wa 24]

Mimi na mapainia wenzangu tulihubiri eneo la Schneifel. Nilikuwa na umri wa miaka 20

[Picha katika ukurasa wa 25]

Mimi, Erika na Wolfgang mwaka wa 1940

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kushoto hadi kulia: Mjukuu wangu wa kiume Jonathan na mke wake, Mirjam; Erika, mimi, mwana wangu Wolfgang na mke wake, Julia

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ndugu aliyefungwa gerezani pamoja na baba alichora picha hii ya baba mwaka wa 1941