Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni ya Mungu Juu ya Usafi wa Kiadili

Maoni ya Mungu Juu ya Usafi wa Kiadili

Maoni ya Mungu Juu ya Usafi wa Kiadili

“Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.”—ISAYA 48:17.

1, 2. (a) Kwa ujumla watu huonaje maadili ya ngono? (b) Wakristo wana maoni gani kuhusu maadili ya ngono?

KATIKA sehemu nyingi za dunia leo, mwenendo wa kiadili unaonwa kuwa suala la kibinafsi. Watu huona kufanya ngono kuwa njia ya kawaida ya kuonyesha upendo na kwamba watu waweza kufanya hivyo wakati wowote wanapotaka, wala si wenzi wa ndoa peke yao walio na haki ya kufanya ngono. Wanahisi kwamba ikiwa hakuna anayeumizwa, basi si vibaya mtu kujiamulia atakavyojiendesha. Kwa maoni yao, watu hawapaswi kuamuliwa mambo ya kiadili, hasa ngono.

2 Wale ambao wamemjua Yehova wana maoni tofauti. Wanafurahia kufuata miongozo ya Maandiko kwa sababu wanampenda Yehova na wanataka kumpendeza. Wanatambua kwamba Yehova anawapenda na huwapa mwongozo wenye kuwafaidi, mwongozo ambao utawanufaisha kikweli na kuwafurahisha. (Isaya 48:17) Kwa kuwa Mungu ndiye Chanzo cha uhai, inafaa wamtegemee ili wapate mwongozo wa jinsi ya kutumia miili yao, hasa katika suala hili linalohusiana sana na kupitisha uhai.

Zawadi Kutoka kwa Muumba Mwenye Upendo

3. Wengi katika Jumuiya ya Wakristo wamefundishwa nini kuhusu kufanya ngono, na maoni hayo yanatofautianaje na yale ambayo Biblia hufundisha?

3 Tofauti na ulimwengu wa sasa, baadhi ya watu katika Jumuiya ya Wakristo wamefundisha kwamba ni aibu na ni dhambi kufanya ngono, na kwamba “dhambi ya awali” katika bustani ya Edeni ilitokea baada ya Hawa kumtongoza Adamu wafanye ngono. Maoni hayo yanapingana na Maandiko yaliyopuliziwa. Biblia hurejezea wanadamu wawili wa kwanza kuwa “mwanamume na mkewe.” (Mwanzo 2:25, Biblia Habari Njema) Mungu aliwaambia wazae watoto, kwa kusema hivi: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi.” (Mwanzo 1:28) Ni jambo ambalo halingepatana na akili Mungu kuwaamuru Adamu na Hawa wazae watoto kisha awaadhibu kwa kutekeleza maagizo hayo.—Zaburi 19:8.

4. Kwa nini Mungu aliwapa wanadamu uwezo wa kufanya ngono?

4 Katika amri hiyo iliyotolewa kwa wazazi wetu wa kwanza, na kurudiwa kwa Noa na watoto wake, twaona kusudi kuu la uhusiano wa ngono: kuzaa watoto. (Mwanzo 9:1) Hata hivyo, Neno la Mungu laonyesha kwamba watumishi wake waliofunga ndoa wanaweza kufanya ngono hata wasipotaka kuzaa watoto. Uhusiano huo waweza kutimiza ifaavyo mahitaji ya kihisia-moyo na ya kimwili na waweza kuwafurahisha wenzi waliooana. Ni njia moja ya kuonyeshana upendo wenye kina.—Mwanzo 26:8, 9; Mithali 5:18, 19; 1 Wakorintho 7:3-5.

Vizuizi Vilivyowekwa na Mungu

5. Ni vizuizi gani ambavyo Mungu amewekea wanadamu kuhusu ngono?

5 Ingawa ngono ni zawadi kutoka kwa Mungu, yapasa kuwa na mipaka. Kanuni hiyo yatumika hata katika ndoa. (Waefeso 5:28-30; 1 Petro 3:1, 7) Kufanya ngono kumekatazwa nje ya ndoa. Biblia husema mambo wazi kuhusu suala hili. Katika Sheria ambayo Mungu alilipa taifa la Israeli, ilisemwa hivi: “Usizini.” (Kutoka 20:14) Baadaye, Yesu alitia ndani “uasherati” na “uzinzi” pamoja na “mawazowazo mabaya” ambayo hutoka moyoni na kumchafua mtu. (Marko 7:21, 22) Mtume Paulo alipuliziwa kuwashauri Wakristo katika Korintho hivi: “Ukimbieni uasherati.” (1 Wakorintho 6:18) Na katika barua yake kwa Waebrania, Paulo aliandika hivi: “Acheni ndoa iwe yenye kuheshimika miongoni mwa wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila kutiwa unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.”—Waebrania 13:4.

6. Katika Biblia, neno “uasherati” latia ndani nini?

6 Neno “uasherati” lamaanisha nini? Latokana na neno la Kigiriki por·neiʹa, ambalo nyakati nyingine hutumiwa kurejezea ngono kati ya watu wasiofunga ndoa. (1 Wakorintho 6:9) Kwingineko, kama vile katika Mathayo 5:32 na Mathayo 19:9, neno hilo lina maana zaidi na hurejezea uzinzi, ngono ya maharimu, na ngono na mnyama. Mazoea mengine ya ngono kati ya watu wasiofunga ndoa, kama vile ngono inayohusisha mdomo na mkundu, na kushika-shika viungo vya uzazi vya mtu mwingine, yaweza kuitwa por·neiʹa pia. Mazoea hayo yote hulaumiwa—ama waziwazi ama kwa kugusiwa tu—katika Neno la Mungu.—Mambo ya Walawi 20:10, 13, 15, 16; Waroma 1:24, 26, 27, 32. *

Kunufaika na Sheria za Mungu za Kiadili

7. Tunanufaikaje kwa kudumisha usafi wa kiadili?

7 Linaweza kuwa jambo gumu kwa wanadamu wasiokamilika kutii mwongozo wa Yehova kuhusu mwenendo wa kingono. Maimonides, mwanafalsafa mashuhuri Myahudi wa karne ya 12, aliandika hivi: “Hakuna katazo katika Torati [Sheria ya Kimusa] nzima lililo gumu kutii kama lile la ngono ya maharimu na ngono haramu.” Lakini iwapo tunatii mwongozo wa Mungu tunanufaika sana. (Isaya 48:18) Kwa mfano, kuonyesha utii katika mambo hayo hutulinda na maradhi ya kuambukizwa kingono, ambayo baadhi yake hayana dawa na yanaweza kuua. * Tunalindwa tusipate mimba nje ya ndoa. Kutumia hekima ya Mungu pia huchangia dhamiri safi. Kufanya hivyo huchangia kujistahi na kufanya tuheshimiwe na wengine, kutia ndani watu wetu wa jamaa, wenzi wetu, watoto wetu, na ndugu na dada zetu Wakristo. Pia hutufanya tuwe na mtazamo unaofaa kuhusu ngono ambao utatokeza furaha katika ndoa. Mwanamke mmoja Mkristo aliandika hivi: “Kweli ya Neno la Mungu ndiyo ulinzi bora kabisa. Ninangoja kuolewa, na nitakapoolewa, nitafurahi sana kumwambia mwanamume Mkristo atakayenioa kwamba nimedumisha usafi wa kiadili.”

8. Ni katika njia zipi mwenendo wetu wa kiadili huchangia ibada safi?

8 Kwa kudumisha mwenendo safi wa kiadili, twaweza pia kuvutia watu kwa Mungu tunayeabudu na kufanya wengi wasiielewe vibaya ibada safi. Mtume Petro aliandika hivi: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa bora miongoni mwa mataifa, ili, katika jambo ambalo katika hilo wao wanasema dhidi yenu kuwa watenda-maovu, likiwa tokeo la kazi zenu bora ambazo wamekuwa mashahidi wa kujionea wapate kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.” (1 Petro 2:12) Hata ikiwa wale wasiomtumikia Yehova hawatambui wala hawaungi mkono mwenendo wetu safi kiadili, twaweza kuwa na hakika kwamba Baba yetu wa kimbingu, anaona, anapendezwa nasi, na hata anafurahia jitihada zetu za kufuata mwongozo wake.—Mithali 27:11; Waebrania 4:13.

9. Kwa nini twapaswa kuwa na uhakika katika mwongozo wa Mungu, hata ingawa huenda tusielewe kabisa sababu za kutoa mwongozo huo? Fafanua.

9 Kumwamini Mungu kwatia ndani kuwa na uhakika kwamba anajua yale yanayotufaa zaidi, hata kama hatuelewi kabisa sababu zote za kutuongoza kama afanyavyo. Fikiria kielelezo kimoja katika Sheria ya Kimusa. Kanuni moja kuhusu kambi za kijeshi ilisema kwamba kinyesi chapasa kufukiwa nje ya kambi. (Kumbukumbu la Torati 23:13, 14) Labda Waisraeli walijiuliza ni kwa nini mwongozo huo ulitolewa; labda wengine walifikiri haukuwa wa lazima. Hata hivyo, tangu wakati huo, sayansi ya kitiba imegundua kwamba sheria hiyo ilisaidia kuzuia maji yasichafuliwe na kuzuia maradhi mengi yanayopitishwa na wadudu. Vivyo hivyo, kuna sababu za kiroho, kijamii, kihisia-moyo, kimwili, na kiakili zinazofanya Mungu akataze kufanya ngono nje ya ndoa. Acheni sasa tuchunguze mifano michache ya Biblia ya watu waliodumisha usafi wa kiadili.

Yosefu—Alibarikiwa kwa Sababu ya Mwenendo Wake wa Kiadili

10. Ni nani aliyejaribu kumtongoza Yosefu, naye alijibuje?

10 Yaelekea unafahamu mfano unaotajwa katika Biblia wa Yosefu, mwana wa Yakobo. Akiwa na umri wa miaka 17, alijikuta akiwa mtumwa wa Potifa, mkuu wa walinzi wa Farao wa Misri. Yehova alimbariki Yosefu, na baada ya muda akawekwa kuwa msimamizi wa nyumba ya Potifa. Alipofikisha umri wa miaka 20, Yosefu alikuwa “mtu mzuri, na mwenye uso mzuri.” Mke wa Potifa alivutiwa naye na kujaribu kumtongoza. Yosefu alitangaza waziwazi msimamo wake, akisema kwamba kukubali ombi hilo hakungekuwa kumsaliti tu bwana wake bali pia kungekuwa ni “kumkosea Mungu.” Kwa nini Yosefu alisababu hivyo?—Mwanzo 39:1-9, BHN.

11, 12. Ingawa hakukuwa na sheria yoyote ya Mungu iliyoandikwa ambayo ilikataza uasherati na uzinzi, kwa nini Yosefu alisababu jinsi hiyo?

11 Kwa wazi, Yosefu hakufikia uamuzi huo kwa sababu ya kuogopa kugunduliwa na watu. Familia ya Yosefu iliishi mbali sana, na baba yake alifikiri kwamba alikuwa amekufa. Ikiwa Yosefu angejihusisha na ukosefu wa adili katika ngono, familia yao haingejua kamwe. Labda Potifa na watumishi wake wa kiume wangeweza kufichwa dhambi hiyo, kwa kuwa kuna nyakati ambazo hawakuwa nyumbani. (Mwanzo 39:11) Lakini Yosefu alijua kwamba hangeweza kumficha Mungu mwenendo huo.

12 Lazima Yosefu awe alitafakari juu ya mambo aliyojua kuhusu Yehova. Bila shaka alijua yale aliyosema Yehova katika bustani ya Edeni: “Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Zaidi ya hayo, yaelekea Yosefu alijua yale ambayo Yehova alimwambia mfalme Mfilisti aliyejaribu sana kumtongoza Sara mama ya nyanya ya Yosefu. Yehova alimwambia hivi mfalme huyo: “Umekuwa mfu wewe kwa sababu ya mwanamke huyu uliyemtwaa, maana ni mkewe mtu. . . . Nami nikakuzuia usinitendee dhambi, kwa hiyo sikukuacha umguse.” (Mwanzo 20:3, 6, Italiki ni zetu.) Kwa hiyo ingawa Yehova hakuwa ameandika sheria yoyote kufikia wakati huo, Yosefu alifahamu waziwazi maoni ya Yehova kuhusu ndoa. Uwezo wa Yosefu wa kupambanua mema na mabaya pamoja na tamaa ya kumpendeza Yehova, vilimfanya akatae ukosefu wa adili.

13. Yaelekea ni kwa nini Yosefu hangeweza kumkwepa mke wa Potifa?

13 Hata hivyo, mke wa Potifa aliendelea kumwomba “siku baada ya siku” alale naye. Kwa nini Yosefu hakumkwepa tu? Kwa kuwa alikuwa mtumwa, alikuwa na kazi za kufanya na hivyo hangeweza kubadili hali yake. Uthibitisho wa kiakiolojia wadokeza kwamba kwa sababu ya mtindo wa ujenzi wa nyumba za Wamisri ilikuwa lazima mtu apite katikati ya sehemu kuu ya nyumba ili kufika kwenye maghala. Kwa hiyo, labda Yosefu hangeweza kumwepuka mke wa Potifa.—Mwanzo 39:10.

14. (a) Ni nini kilichompata Yosefu alipomkimbia mke wa Potifa? (b) Yehova alimbarikije Yosefu kwa uaminifu wake?

14 Siku ikafika walipojikuta peke yao nyumbani. Mke wa Potifa akamshika Yosefu huku akisema kwa sauti: “Lala nami.” Yosefu akakimbia. Mke wa Potifa aliumia sana kihisia-moyo alipokataliwa na akamshtaki Yosefu kuwa alijaribu kumbaka. Matokeo yakawa nini? Je, Yehova alimthawabisha papo hapo kwa sababu ya mwendo wake wa kushika uaminifu-maadili? La. Yosefu alitupwa gerezani na kufungwa kwa pingu. (Mwanzo 39:12-20; Zaburi 105:18) Yehova aliona udhalimu aliotendewa Yosefu na hatimaye akamkweza kutoka gerezani hadi kwenye nyumba ya mfalme. Akawa mtu wa pili mwenye uwezo mkubwa zaidi nchini Misri na kubarikiwa kupata mke na watoto. (Mwanzo 41:14, 15, 39-45, 50-52) Zaidi ya hayo, masimulizi ya uaminifu-maadili wa Yosefu yaliandikwa miaka 3,500 iliyopita ili watumishi wa Mungu waendelee kuyasoma tangu wakati huo. Ni baraka zilizoje zinazopatikana kwa kufuata sheria za Mungu za uadilifu! Vivyo hivyo, huenda sisi leo tusione manufaa ya papo hapo ya kudumisha uaminifu-maadili, lakini twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaona na atatubariki kwa wakati wake.—2 Mambo ya Nyakati 16:9.

‘Agano [la Yobu] na Macho Yake’

15. ‘Agano la Yobu na macho yake’ lilikuwa gani?

15 Yobu pia alishika uaminifu-maadili. Wakati wa majaribu aliyoletewa na Ibilisi, Yobu alichunguza maisha yake na kusema kwamba alikuwa tayari kuadhibiwa vikali iwapo, miongoni mwa kanuni nyingine, alikuwa amekiuka kanuni ya Yehova ya adili za ngono. Yobu alisema hivi: “Nilifanya agano na macho yangu; basi nawezaje kumwangalia msichana?” (Ayubu 31:1) Kwa kusema hivyo, Yobu alimaanisha kwamba katika uamuzi wake wa kushika uaminifu-maadili kwa Mungu, alikuwa ameazimia kuepuka kumwangalia mwanamke kwa kumtamani. Bila shaka, angeona wanawake kila siku na labda kuwasaidia walipohitaji msaada. Lakini hakuwatazama akiwa na lengo la kutafuta mahaba. Kabla ya majaribu yake, alikuwa na mali mengi, “mkuu sana kuliko watu wote wa upande wa mashariki.” (Ayubu 1:3) Hata hivyo, hakutumia mali yake kuvutia wanawake wengi. Ni wazi kwamba hakucheza-cheza na wazo la kujihusisha katika ngono haramu na wasichana.

16. (a) Kwa nini Yobu ni kielelezo kizuri kwa Wakristo waliofunga ndoa? (b) Tabia ya wanaume walioishi siku za Malaki ilitofautianaje na ya Yobu, na hali ikoje leo?

16 Hivyo, katika nyakati zifaazo hali kadhalika nyakati ngumu, Yobu alidhihirisha uaminifu-maadili. Yehova aliona jambo hilo na kumbariki sana. (Ayubu 1:10; 42:12) Yobu ni kielelezo kizuri kama nini kwa wanaume na wanawake Wakristo waliofunga ndoa! Si ajabu kwamba Yehova alimpenda kadiri hiyo! Tofauti na Yobu, tabia ya watu wengi leo inafanana sana na ya watu wa siku za Malaki. Nabii huyo alilaumu jinsi waume wengi walivyoacha wake zao, na mara nyingi kuoa wasichana. Madhabahu ya Yehova ilifunikwa kwa machozi ya wake walioachwa, na Mungu alilaumu wale ‘waliotenda mambo ya hiana’ dhidi ya wake zao.—Malaki 2:13-16.

Msichana Aliye Safi Kiadili

17. Mshulami alikuwaje kama “bustani iliyofungwa”?

17 Mtu wa tatu aliyeshika uaminifu-maadili ni msichana Mshulami. Alivutia mvulana mchungaji na pia Solomoni, mfalme tajiri wa Israeli, kwa kuwa alikuwa mchanga tena mrembo. Katika masimulizi yote yenye kuvutia yapatikanayo katika Wimbo Ulio Bora, Mshulami alidumisha usafi wa kiadili, na kuheshimiwa na watu walioishi karibu naye. Ingawa Solomoni alikataliwa naye, alipuliziwa kuandika simulizi juu yake. Mchungaji aliyempenda pia aliheshimu msimamo wake safi kiadili. Pindi moja aliwaza kwamba Mshulami alikuwa kama “bustani iliyofungwa.” (Wimbo Ulio Bora 4:12) Katika Israeli la kale, bustani nzuri zilikuwa na mboga zenye kupendeza za namna mbalimbali, maua yenye harufu nzuri, na miti ya fahari. Bustani hizo zilizingirwa ua au ukuta na mtu angeweza kuingia tu kupitia lango lililofungwa. (Isaya 5:5) Mchungaji aliona usafi wa kiadili na uzuri wa Mshulami huyo kuwa kama bustani hiyo yenye umaridadi adimu. Alikuwa safi kabisa kiadili. Angedhihirisha upendo mwororo tu kwa yule ambaye angekuja kumwoa.

18. Masimulizi ya Yosefu, Yobu na Mshulami yatukumbusha nini?

18 Mshulami aliwekea wanawake Wakristo leo kielelezo bora kabisa cha uaminifu-maadili. Yehova aliona na kuthamini wema wa adili wa msichana Mshulami na kumbariki kama alivyombariki Yosefu na Yobu. Matendo yao ya uaminifu-maadili yameandikwa katika Neno la Mungu ili kutuongoza. Ingawa jitihada zetu za kudumisha uaminifu-maadili leo haziandikwi katika Biblia, Yehova ana “kitabu cha ukumbusho” kwa wale wanaojitahidi kufanya mapenzi yake. Na tusisahau kamwe kwamba Yehova “anasikiliza” na kushangilia tunapojitahidi kwa uaminifu kudumisha usafi wa kiadili.—Malaki 3:16.

19. (a) Twapaswa kuuonaje usafi wa kiadili? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala ifuatayo?

19 Ijapokuwa wasio na imani huenda wakatudhihaki, tunafurahi kumtii Muumba wetu mwenye upendo. Tuna maadili ya kiwango cha juu zaidi, maadili ya Mungu. Tunajivunia hayo, tunayaona kuwa hazina. Kwa kudumisha msimamo safi wa kiadili, twaweza kufurahia baraka za Mungu na kudumisha tumaini hakika la baraka za wakati ujao zisizo na kikomo. Hata hivyo, twaweza kufanya nini ili kudumisha usafi wa kiadili? Makala ifuatayo itazungumzia swali hilo muhimu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona Mnara wa Mlinzi, Januari 1, 1984, ukurasa wa 5-8.

^ fu. 7 Kwa kusikitisha, kuna hali ambazo Mkristo asiye na hatia hupatwa na maradhi yanayoambukizwa kingono kutoka kwa mwenzi asiyeamini ambaye hafuati mwongozo wa Mungu.

Je, Unaweza Kueleza?

• Biblia inafundisha nini kuhusu kufanya ngono?

• Katika Biblia neno “uasherati” hutia ndani nini?

• Tunanufaikaje kwa kudumisha usafi wa kiadili?

• Kwa nini Yosefu, Yobu, na msichana Mshulami ni vielelezo bora kwa Wakristo leo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yosefu aliukimbia ukosefu wa adili

[Picha katika ukurasa wa 10]

Msichana Mshulami alikuwa kama “bustani iliyofungwa”

[Picha katika ukurasa wa 11]

Yobu alifanya ‘agano na macho yake’