Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukarimu Mwingi Huleta Shangwe

Ukarimu Mwingi Huleta Shangwe

Ukarimu Mwingi Huleta Shangwe

AKIWA mwangalizi Mkristo mwenye upendo, mtume Paulo aliwajali kikweli waamini wenzake na alitaka kuwasaidia. (2 Wakorintho 11:28) Hivyo, katikati ya miaka ya 50 ya karne ya kwanza ya Wakati Wetu wa Kawaida alipopanga michango ya kifedha itolewe kwa ajili ya Wakristo wenye uhitaji huko Yudea, alitumia fursa hiyo kufundisha jambo fulani lenye manufaa kuhusu ukarimu. Paulo alikazia kwamba michango inayotolewa kwa uchangamfu inathaminiwa sana na Yehova: “Acheni kila mmoja afanye kama vile ameazimia moyoni mwake, si kwa kinyongo au kwa shurutisho, kwa maana Mungu hupenda mpaji mchangamfu.”—2 Wakorintho 9:7.

Wenye Umaskini Mwingi, Bali Wakarimu

Wakristo wengi wa karne ya kwanza hawakuwa watu mashuhuri. Paulo alisema kwamba miongoni mwao ‘wengi hawakuwa wenye nguvu.’ Walikuwa “vitu dhaifu vya ulimwengu,” “vitu vinyonge vya ulimwengu.” (1 Wakorintho 1:26-28) Kwa mfano, Wakristo walioishi Makedonia walikuwa na “umaskini wa kina kirefu” na “chini ya taabu kubwa.” Hata hivyo, waamini hao wa hali ya chini wa Makedonia waliomba wapate pendeleo la kuchangia kifedha “huduma waliyokusudiwa watakatifu”; na Paulo alishuhudia kwamba walichanga “kupita uwezo wao”!—2 Wakorintho 8:1-4.

Lakini, utoaji huo mkarimu haukupimwa kulingana na kiasi walichochanga. Badala yake, kichocheo, utayari wa kushiriki vitu na wengine, na hali ya moyoni yalikuwa mambo muhimu. Paulo liwaonyesha Wakristo Wakorintho kwamba akili na moyo zinahusika katika kutoa michango. Alisema: “Najua utayari wenu wa akili ambao juu ya huo najisifu kwa Wamakedonia juu yenu, . . . na bidii yenu imechochea walio wengi kati yao.” Wakristo Wakorintho ‘waliazimia moyoni mwao’ kuchanga kwa ukarimu.—2 Wakorintho 9:2, 7.

‘Roho Yao Iliwahimiza’

Huenda mtume Paulo alikuwa anafikiria kielelezo fulani cha mapema kuhusu mchango wa ukarimu, ambao ulitokea nyikani zaidi ya karne 15 kabla ya wakati wake. Makabila 12 ya Israeli yalikuwa yamewekwa huru kutoka utumwani Misri. Walikuwa chini ya Mlima Sinai, na Yehova aliwaamuru wajenge tabenakulo kwa ajili ya ibada na kuweka humo vifaa vya ibada. Kwa kuwa kazi hiyo ilihitaji mali nyingi, taifa lilialikwa kuchanga.

Waisraeli hao waliitikiaje? “Wakaja kila mtu ambaye moyo wake ulimhimiza, na kila mtu ambaye roho yake ilimfanya kuwa apenda, nao wakaleta sadaka [“michango,” NW] za kumpa BWANA, kwa kazi ya hema ya kukutania.” (Kutoka 35:21) Je, taifa hilo lilitoa kwa ukarimu? Bila shaka! Musa alipokea ripoti ifuatayo: “Watu waleta vitu vingi sana zaidi ya hivyo vitoshavyo kwa ajili ya utumishi wa hiyo kazi, ambayo BWANA aliagiza ifanywe.”—Kutoka 36:5.

Hali ya kifedha ya Waisraeli ilikuwaje wakati huo? Muda mfupi kabla ya kutoa mchango huo, Waisraeli walikuwa watumwa maskini, ‘walioteseka kwa mizigo yao,’ wakiishi ‘maisha yenye uchungu,’ maisha ‘ya kuteseka.’ (Kutoka 1:11, 14; 3:7; 5:10-18) Basi, haielekei kwamba walikuwa na ufanisi wa kimwili. Ni kweli kwamba Waisraeli waliondoka katika nchi ya utumwa wakiwa na kondoo na ng’ombe. (Kutoka 12:32) Lakini huenda mifugo hiyo haikuwa mingi, kwa kuwa muda mfupi baada ya kuondoka Misri, walilalamika kwamba hawakuwa na nyama wala mikate ya kula.—Kutoka 16:3.

Basi, Waisraeli walitoa wapi vitu vya thamani walivyochanga kwa ajili ya ujenzi wa tabenakulo? Walivitoa kwa Wamisri, mabwana wao wa zamani. Biblia yasema: “Wana wa Israeli . . . wakataka kwa Wamisri vyombo vya fedha na vyombo vya dhahabu, na mavazi. . . . [Wamisri] wakawapa kila walichokitaka.” Matendo hayo ya ukarimu ya Wamisri yalikuwa baraka kutoka kwa Yehova, si kutoka kwa Farao. Maandiko ya Mungu yasema: “BWANA akawajalia kupendelewa na Wamisri hata wakawapa kila walichokitaka.”—Kutoka 12:35, 36.

Hebu fikiria jinsi Waisraeli walivyohisi. Vizazi vingi vilikuwa vimeteseka kwa sababu ya utumwa mbaya na ufukara. Sasa walikuwa huru na walikuwa na mali nyingi. Wangehisije kutoa baadhi ya mali hiyo? Huenda wangehisi kwamba walikuwa wanastahili kuwa na mali hiyo na kwamba walikuwa na haki ya kubaki nayo. Hata hivyo, walipoombwa watoe mchango ili kutegemeza ibada safi, walifanya hivyo—si kwa kulazimishwa wala kwa kukosa ukarimu! Hawakusahau kwamba Yehova ndiye aliyewawezesha kupata mali hizo. Hivyo, walichanga kwa wingi fedha na dhahabu na mifugo yao. Walikuwa na “moyo wa kupenda.” ‘Mioyo yao iliwahimiza.’ ‘Roho yao ikawafanya kuwa wapenda.’ Zilikuwa kwa kweli “sadaka za kumpa BWANA kwa moyo wa kupenda.”—Kutoka 25:1-9; 35:4-9, 20-29; 36:3-7.

Utayari wa Kutoa

Si lazima ukarimu wa mwenye kuchanga udhihirishwe na kadiri anavyoweza kuchanga. Wakati mmoja Yesu Kristo alitazama watu walipokuwa wakitumbukiza pesa katika masanduku ya hazina ya hekalu. Matajiri walitumbukiza sarafu nyingi, lakini Yesu alivutiwa alipoona mjane mmoja mwenye uhitaji akitumbukiza sarafu ndogo mbili za thamani ndogo sana. Alisema: “Mjane huyu, ijapokuwa ni maskini, alitumbukiza nyingi kuliko wao wote. . . . Kutokana na uhitaji wake alitumbukiza ndani njia yote ya kujipatia riziki aliyokuwa nayo.”—Luka 21:1-4; Marko 12:41-44.

Maneno ya Paulo kwa Wakorintho yanapatana na maoni hayo ya Yesu. Kwa habari ya kuchanga ili kuwasaidia waamini wenzetu wenye uhitaji, Paulo alisema: “Ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika hasa kulingana na alicho nacho mtu, si kulingana na kile ambacho mtu hana.” (2 Wakorintho 8:12) Naam, hatupaswi kuchanga kwa kusudi la kushindana au kujilinganisha na wengine. Mtu huchanga kulingana na uwezo wake, na Yehova hupendezwa na roho ya ukarimu.

Ingawa hakuna awezaye kwa kweli kumtajirisha Yehova ambaye anamiliki vitu vyote, kuchanga ni pendeleo ambalo huwapa waabudu fursa ya kuonyesha upendo wao kwake. (1 Mambo ya Nyakati 29:14-17) Michango inayotolewa kwa mtazamo ufaao na kwa kusudi la kuendeleza ibada ya kweli, wala si kwa kusudi la kujionyesha au kwa sababu nyingine za ubinafsi, huleta shangwe na pia baraka za Mungu. (Mathayo 6:1-4) Yesu alisema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Tunaweza kupata furaha hiyo kwa kutumia nguvu zetu katika utumishi wa Yehova na kuweka kando kitu fulani kutoka kwa mali zetu za kimwili ili kutegemeza ibada ya kweli na kuwasaidia wanaostahili.—1 Wakorintho 16:1, 2.

Utayari wa Kutoa Leo

Leo, Mashahidi wa Yehova wanasisimuka kuona maendeleo ya ulimwenguni pote ya kuhubiriwa kwa “habari njema hii ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Wakati wa mwongo wa mwisho wa karne ya 20, watu zaidi ya 3,000,000 walibatizwa kuonyesha wakfu wao kwa Yehova Mungu, na makutaniko yapatayo 30,000 yakaanzishwa. Naam, theluthi moja ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yalianzishwa katika miaka kumi iliyopita! Ongezeko hilo linatokana na kazi ngumu ya wanaume na wanawake Wakristo ambao wanatumia wakati na nguvu zao ili kuwatembelea majirani wao na kuwajulisha makusudi ya Yehova. Sehemu ya ongezeko hilo limetokana na kazi ya wamishonari, ambao huacha nchi zao na kusafiri kwenda nchi za mbali ili kusaidia katika kazi ya kuhubiri Ufalme. Ongezeko hilo limesababisha kuanzishwa kwa mizunguko mipya, jambo ambalo limefanya iwe lazima kuweka waangalizi wapya wa mzunguko. Mbali na hayo, Biblia zaidi zimehitajika ili kutumiwa katika kuhubiri na katika funzo la kibinafsi. Vichapo zaidi vimehitajika pia. Na katika nchi nyingi, imekuwa lazima kupanua ofisi za tawi au kujenga nyingine kubwa zaidi. Mahitaji hayo yote yametimizwa kwa michango ya hiari ya watu wa Yehova.

Uhitaji wa Majumba ya Ufalme

Kuna uhitaji mkubwa sana wa majumba ya Ufalme kutokana na kuongezeka kwa idadi ya Mashahidi wa Yehova. Uchunguzi uliofanywa mapema mwaka wa 2000 ulionyesha kwamba kuna uhitaji wa Majumba ya Ufalme 11,000 katika mataifa yanayoendelea, ambayo yana upungufu wa fedha. Fikiria nchi ya Angola. Licha ya miaka mingi ya vita vya wenyewe kwa wenyewe, wahubiri wa Ufalme katika nchi hiyo wanaongezeka kwa asilimia 10 kila mwaka. Lakini mengi kati ya makutaniko 675 katika nchi hiyo kubwa ya Afrika yanafanya mikutano yao nje. Kuna Majumba ya Ufalme 22 tu katika nchi hiyo, na ni majumba 12 tu kati ya hayo ambayo yana paa.

Hivyo ndivyo ilivyo katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Ingawa kuna makutaniko yapatayo 300 katika jiji kuu la Kinshasa, kuna Majumba ya Ufalme kumi tu. Nchini kote, kuna uhitaji wa haraka wa Majumba ya Ufalme zaidi ya 1,500. Kutokana na ongezeko la haraka katika nchi za Ulaya Mashariki, Urusi na Ukrainia pia zinahitaji mamia ya Majumba ya Ufalme. Ongezeko kubwa sana huko Amerika ya Kusini limedhihirika zaidi nchini Brazili, ambako kuna Mashahidi zaidi ya nusu milioni na uhitaji mkubwa wa Majumba ya Ufalme.

Ili kutimiza mahitaji katika nchi kama hizo, Mashahidi wa Yehova wanatekeleza miradi ya ujenzi wa haraka wa Majumba ya Ufalme. Miradi hiyo inagharimiwa na michango ya ukarimu ya ndugu ulimwenguni pote ili kuyawezesha hata makutaniko yaliyo maskini zaidi kuwa na mahali pafaapo pa ibada.

Kama wakati wa Israeli la kale, mengi yanaweza kutimizwa kwa sababu Wakristo wanyofu ‘humheshimu BWANA kwa mali yao.’ (Mithali 3:9, 10) Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova linachukua fursa hii kutoa shukrani nyingi kwa yeyote ambaye moyo wake umemhimiza kutoa michango ya hiari. Na twaweza kuwa na hakika kwamba roho ya Yehova itaendelea kuchochea mioyo ya watu wake ili kutegemeza kazi ya Ufalme inayopanuka daima.

Upanuzi katika ulimwengu wote unapoendelea, na tuendelee kutafuta fursa za kuonyesha shangwe yetu na utayari wa kutumia nguvu zetu, wakati wetu, na mali zetu. Na tupate shangwe ya kweli itokanayo na roho hiyo ya kuchanga.

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

“ZITUMIENI KWA HEKIMA!”

“Mimi nina umri wa miaka kumi. Ninawatumia pesa hizi ili mweze kununua karatasi au kitu kingine chochote cha kutengenezea vitabu.”—Cindy.

“Ninapenda kuwatumia pesa hizi ili mtutengenezee vitabu zaidi. Niliziweka akiba kutokana na malipo niliyopata kwa kumsaidia baba yangu. Kwa hiyo zitumieni kwa hekima!”—Pam, mwenye umri wa miaka saba.

“Nilisikitika sana kuhusu kimbunga hicho. Natumaini nyinyi ni salama. Hizi [dola mbili za Marekani] ndizo pesa zote katika sanduku langu la kuhifadhia sarafu.”—Allison, mwenye umri wa miaka minne.

“Mimi naitwa Rudy, na nina umri wa miaka 11. Ndugu yangu Ralph ana umri wa miaka sita. Naye dada yangu Judith ana umri wa miaka miwili u nusu. Tumeweka akiba pesa zetu za matumizi ya kibinafsi kwa miezi mitatu ili kuwasaidia ndugu zetu katika [maeneo yaliyoathiriwa na vita]. Tuliweza kuweka akiba dola 20 ambazo tunawatumia sasa.”

“Ninawasikitikia ndugu [ambao walikumbwa na kimbunga]. Nilichuma dola 17 kwa kufanya kazi na babangu. Siwatumii pesa hizi kwa ajili ya jambo fulani hususa, kwa hiyo ni juu yenu kuamua.”—Maclean, mwenye umri wa miaka minane.

[Sanduku katika ukurasa wa 31]

Njia Ambazo Watu Fulani Huchagua Kutoa

MICHANGO KWA KAZI YA ULIMWENGUNI POTE

Wengi huweka kando, au hupangia kiasi cha pesa ambazo wao hutia katika masanduku ya michango yenye kibandiko “Michango kwa Kazi ya Sosaiti ya Ulimwenguni Pote—Mathayo 24:14.” Kila mwezi makutaniko hupeleka kiasi hicho kwenye makao makuu ya ulimwengu huko Brooklyn, New York, au kwenye ofisi ya tawi ya kwao.

Michango ya hiari ya pesa yaweza pia kupelekwa moja kwa moja kwenye Treasurer’s Office, Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, 25 Columbia Heights, Brooklyn, New York 11201-2483, au kwenye ofisi ya tawi ya Sosaiti ya nchi yako. Vito au mali nyingine zenye thamani zaweza kutolewa pia. Barua fupi inayotaarifu kwamba hiyo ni zawadi ya moja kwa moja yapasa kuambatana na michango hiyo.

MPANGO WA MICHANGO YENYE MASHARTI

Pesa zaweza kupewa Watch Tower Society kukiwa na mpango maalumu kwamba, kukiwa na uhitaji wa kibinafsi, zinaweza kurudishwa kwa mtoaji. Kwa habari zaidi, tafadhali wasiliana na Treasurer’s Office kwa kutumia anwani iliyoonyeshwa juu.

UTOAJI ULIOPANGWA

Mbali na zawadi za pesa za moja kwa moja na michango ya pesa yenye masharti, kuna njia nyinginezo za kutoa kwa ajili ya utumishi wa Ufalme wa ulimwenguni pote. Hizo zatia ndani:

Bima: Watch Tower Society yaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa sera ya bima ya maisha au katika mpango wa kustaafu kazi/malipo ya uzeeni.

Akiba za Benki: Akiba za benki, hati za amana, au akiba za pesa za kustaafu za mtu mmoja-mmoja zaweza kuwekwa zikiwa amana kwa ajili ya au kuweza kulipwa wakati wa kifo kwa Watch Tower Society, kulingana na matakwa ya benki ya hapo.

Hisa na Dhamana: Hisa na dhamana zaweza kupewa Watch Tower Society zikiwa zawadi ya moja kwa moja.

Mashamba na Nyumba: Mashamba na nyumba ziwezazo kuuzwa zaweza kupewa Watch Tower Society kwa kutoa zawadi ya moja kwa moja au kwa kuhifadhi shamba au nyumba ya maisha kwa ajili ya mtoaji, ambaye aweza kuendelea kuishi humo muda wa maisha yake. Mtu apaswa kuarifu Sosaiti kabla ya kuipa Sosaiti hati yoyote ya mashamba na nyumba.

Wasia na Amana: Watch Tower Society yaweza kurithishwa mali au pesa kwa njia ya wasia wenye kutekelezwa kisheria, au Sosaiti yaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mkataba wa amana. Amana inayofaidi tengenezo la kidini yaweza kuwa na faida fulani kwa habari ya ulipaji kodi.

Kama vile mtajo “utoaji uliopangwa” udokezavyo, michango ya aina hii kwa kawaida hutaka mtoaji afanye mipango fulani. Ili kuwasaidia watu wanaotamani kusaidia Sosaiti kupitia aina fulani ya utoaji uliopangwa, Sosaiti imetayarisha broshua ya Kiingereza na Kihispania yenye kichwa Charitable Planning to Benefit Kingdom Service Worldwide. Broshua hiyo iliandikwa kufuatia maswali mengi ambayo Sosaiti imepokea kuhusu zawadi, wasia, na amana. Pia ina habari za ziada zenye mafaa juu ya mipango ya mashamba, ya kifedha, na kodi. Nayo imekusudiwa kuwasaidia watu wa Marekani, wanaopanga kuipa Sosaiti zawadi ya kipekee sasa au kuacha wasia wafapo, wateue njia zenye matokeo na zenye kufaa zaidi kwa kufikiria hali za familia na za kibinafsi. Unaweza kupata broshua hii kwa kuiomba moja kwa moja kwenye Ofisi ya Utoaji Uliopangwa.

Baada ya kusoma broshua hiyo na kushauriana na Ofisi ya Utoaji Uliopangwa, watu wengi wameweza kuisaidia Sosaiti na wakati uleule kupata faida kubwa zaidi kwa habari ya ulipaji kodi. Ofisi ya Utoaji Uliopangwa yapasa kujulishwa na kupokea hati yoyote ile inayohusiana na yoyote ya mipango hiyo. Ikiwa unapendezwa na yoyote ya mipango hiyo ya utoaji unapaswa kuwasiliana na Ofisi ya Utoaji Uliopangwa kwa kuandika au kwa kupiga simu kwenye anwani iliyoonyeshwa hapa chini au kwenye ofisi ya tawi ya nchi yako.

International Bible Students Association

P.O. Box 47788

Nairobi, Kenya

Simu: (02)573211