Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unakadiriaje Mafanikio?

Unakadiriaje Mafanikio?

Unakadiriaje Mafanikio?

KAMUSI moja yafafanua mafanikio kuwa “kupata mali, kibali, au umashuhuri.” Je, huo ni ufafanuzi kamili? Je, mafanikio yaweza tu kukadiriwa kupitia mali, kibali, au umashuhuri? Kabla ya kujibu, fikiria jambo hili: Yesu Kristo hakupata mali za kimwili alipoishi duniani. Hakupata kibali cha watu walio wengi; wala hakuhesabiwa kuwa mtu wa maana na waasisi wa wakati wake. Lakini, Yesu alikuwa mtu mwenye mafanikio. Kwa nini?

Alipokuwa duniani, Yesu alikuwa “tajiri kuelekea Mungu.” (Luka 12:21) Baada ya kufufuliwa, Mungu alimthawabisha kwa kumvika “taji la utukufu na heshima.” Yehova alimtukuza Mwana wake “kwenye cheo cha juu zaidi akampa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina jingine.” (Waebrania 2:9; Wafilipi 2:9) Maisha ya Yesu yalimfurahisha Yehova. (Mithali 27:11) Maisha yake duniani yalifanikiwa kwa sababu yalitimiza kusudi lake. Yesu alifanya mapenzi ya Mungu na kulitukuza jina Lake. Mungu naye akamtukuza Yesu kwa utajiri, kibali na umashuhuri wa aina ambayo hata wale walio hodari katika elimu, siasa, au michezo, hawatapata kamwe. Kwa kweli Yesu ndiye mtu mwenye kufanikiwa zaidi aliyepata kuishi duniani.

Wazazi Wakristo wanatambua kwamba watoto wao wakifuata hatua za Kristo na kuwa matajiri mbele ya Mungu kama Yesu alivyokuwa, watapata baraka nyingi sasa na kufurahia thawabu zisizowazika katika mfumo wa mambo unaokuja. Kijana anaweza kufuata hatua za Kristo vyema zaidi kwa kufanya kazi ambayo Yesu alifanya—kwa kushiriki katika huduma ya wakati wote ikiwezekana.

Hata hivyo, katika tamaduni fulani si jambo la kawaida kwa vijana kujiunga na huduma ya wakati wote. Mwanamume kijana anapomaliza shule, huenda watu wakatazamia aajiriwe kazi ya wakati wote, aoe, na kuishi maisha ya kawaida. Mara kwa mara, vijana waliokulia katika tamaduni kama hizo husita kimakosa kujiunga na huduma ya wakati wote. (Mithali 3:27) Kwa nini? Kwa sababu ya kushinikizwa, wao hutenda kulingana na viwango vya kitamaduni vyenye kuenea. Robert * alifanya hivyo.

Wakati Utamaduni na Dhamiri Zinapopingana

Robert alilelewa akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ujanani, mwenendo wake na mashirika yake yakawa mabaya. Mama yake akaanza kuwa na wasiwasi kumhusu. Kwa hiyo, akamwomba painia mmoja, mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, amtie moyo. Robert aeleza yaliyotukia baadaye.

“Nilithamini sana jinsi ndugu huyo painia alivyonijali. Kielelezo chake bora kilinifanya nitake kuufanya upainia uwe kazi-maisha mara tu nilipomaliza shule. Ndipo mama akawa na wasiwasi tena—lakini kwa sababu tofauti. Katika utamaduni wetu ni sawa kwa msichana kuanza upainia mara tu amalizapo shule, lakini mvulana hutazamiwa afanye kazi na kupata fedha kwanza kisha anaweza kufikiria kupainia.

“Nilijifunza kazi fulani ya ufundi na kuanzisha biashara yangu. Upesi nilijiingiza sana katika biashara hiyo na nilikuwa ninahudhuria mikutano na kuhubiri kama desturi tu. Dhamiri yangu ilinisumbua—nilijua ningeweza kumtumikia Yehova kikamili zaidi. Hata hivyo, nilijikakamua kwelikweli kutofanya yale ambayo wengine walitazamia nifanye, na ninafurahi nilifanya hivyo. Sasa nimeoa, na mimi na mke wangu tumekuwa mapainia kwa muda wa miaka miwili iliyopita. Hivi karibuni, niliwekwa kuwa mtumishi wa huduma kutanikoni. Ninaweza kusema kwa unyofu kwamba sasa ninahisi nimeridhika kikweli kwa kumtumikia Yehova kwa moyo wangu wote, kadiri niwezavyo.”

Mara nyingi gazeti hili limewatia moyo vijana wajifunze kazi fulani au wasitawishe stadi mbalimbali zenye manufaa—wakiwa bado shuleni iwapo yawezekana. Kwa kusudi gani? Ili wawe matajiri? La. Sababu kuu ni ili waweze kujitegemeza ifaavyo wakiwa watu wazima na kumtumikia Yehova kwa kadiri wawezavyo, hasa katika huduma ya wakati wote. Hata hivyo, mara kwa mara imetokea kwamba vijana wanaume na wanawake hujishughulisha sana na kazi-maisha ya ulimwengu hivi kwamba huduma inakuwa si muhimu sana. Baadhi yao hawafikirii utumishi wa wakati wote hata kidogo. Kwa nini?

Maelezo ya Robert yanafafanua jambo hili. Baada ya kujifunza kazi, Robert alianzisha biashara. Muda si muda akawa anafanya kazi yenye kuchosha isiyokuwa na matokeo. Alikusudia kupata fedha za kutosha. Lakini je, kuna yeyote ndani au nje ya kutaniko la Kikristo anayeweza kupata fedha za kutosha? Wakristo wanapaswa kujitahidi kuwa wenye kuwajibika kifedha, wakijitahidi sana kutimiza matakwa yao ya kifedha; lakini wanapaswa pia kutambua kwamba katika nyakati hizi zisizo na uhakika, ni wachache ambao hufikia hatua wanapoweza kwa kweli kuona kwamba wana fedha za kutosha. Hiyo ndiyo sababu ahadi ya Yesu kwenye Mathayo 6:33 inawafariji sana Wakristo.

Robert anafurahi kwamba aliamua kufuata tamaa za moyo wake badala ya kufanya vile utamaduni wa kwao ulivyotaka afanye. Leo, yeye anafurahia kazi-maisha ya utumishi wa wakati wote. Naam, huduma ya wakati wote ni kazi-maisha yenye kuheshimika. Robert ana amani kwa sababu anamtumikia Yehova, kama asemavyo, ‘kwa uwezo wake wote.’

Tumia Vipawa Vyako Kadiri Uwezavyo

Kuna watu wengi wenye vipawa miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Baadhi yao wana akili nyingi sana; wengine wana vipawa vya kufanya kazi ya mikono. Vipawa hivyo vyote hutoka kwa Yehova, ambaye huwapa “watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:25) Bila uhai, vipawa hivyo havingekuwa na maana yoyote.

Basi, inafaa kutumia maisha yetu tuliyoweka wakfu kwa Yehova katika utumishi wake. Hivyo ndivyo kijana mmoja mwenye kipawa alivyoamua kufanya. Aliishi katika karne ya kwanza W.K. Alikuwa wa familia mashuhuri naye aliishi katika jiji maarufu la Tarso huko Kilikia alipokuwa kijana. Ingawa alizaliwa Myahudi, alirithi uraia wa Roma kutoka kwa babake. Jambo hilo lilifanya astahili haki na mapendeleo mengi. Alipofikia umri mkubwa zaidi, alifunzwa Sheria na Gamalieli, mmojawapo wa “profesa” mashuhuri wakati huo. Ilionekana kwamba baada ya muda mfupi, angepata ‘mali, kibali, na umashuhuri.’—Matendo 21:39; 22:3, 27, 28.

Kijana huyo alikuwa nani? Aliitwa Sauli. Lakini Sauli alipata kuwa Mkristo na hatimaye akawa mtume Paulo. Aliachilia mbali tamaa yake ya awali, akajitoa kabisa kumtumikia Yehova akiwa Mkristo. Paulo alijulikana kuwa mhubiri wa habari njema mwenye bidii wala si mwanasheria maarufu. Baada ya kutumikia akiwa mishonari kwa muda wa miaka 30, Paulo aliwaandikia barua rafiki zake waliokuwa Filipi. Katika barua hiyo alitaja baadhi ya mambo aliyotimiza kabla ya kuwa Mkristo, kisha akasema: “Kwa sababu [ya Yesu Kristo] nimekubali hasara ya vitu vyote nami naviona kuwa takataka nyingi, ili niweze kupata Kristo.” (Wafilipi 3:8) La, Paulo hakujuta kwa jinsi alivyokuwa ametumia maisha yake!

Namna gani mazoezi ambayo Paulo alipata kutoka kwa Gamalieli? Je, yalipata kuwa na manufaa yoyote kwake? Ndiyo! Mara kadhaa alisaidia “kutetea na kuthibitisha kisheria habari njema.” Lakini kazi muhimu ya Paulo ilikuwa kuhubiri habari njema—kazi ambayo hangeweza kujifunza kutokana na elimu yake ya hapo awali.—Wafilipi 1:7; Matendo 26:24, 25.

Vivyo hivyo leo, wengine wametumia vipawa vyao na hata elimu yao ili kuendeleza masilahi ya Ufalme. Kwa mfano, Amy ana digrii ya chuo kikuu ya mambo ya biashara na nyingine ya uanasheria. Wakati mmoja alikuwa na kazi yenye mapato makubwa, lakini leo anatumikia akiwa mjitoleaji asiyelipwa mshahara katika mojawapo ya ofisi za tawi za Watch Tower Society. Amy anaeleza hivi kuhusu maisha yake ya sasa: “Ninaamini kwamba nimefanya uamuzi ufaao kabisa maishani. . . . Sitaki hata kufanya kazi wanazofanya wale niliosoma nao chuoni. Ninajivunia kazi niliyochagua kufanya. Nina kila kitu ninachohitaji na ninachotaka—maisha yenye kuridhisha na yenye furaha na kazi-maisha yenye kuridhisha pia.”

Amy alichagua kazi inayomletea amani ya akili, uradhi, na baraka za Yehova. Kwa hakika, wazazi wangetaka watoto wao wapate hayo hayo!

Mafanikio Katika Huduma ya Kikristo

Bila shaka, ni muhimu kuwa na maoni yafaayo kuhusu mafanikio katika huduma ya Kikristo yenyewe. Si vigumu kuhisi kwamba tumefanikiwa tunapofurahia huduma kwa kuangusha vichapo vya Biblia na kuwa na mazungumzo ya Biblia yenye kusisimua pamoja na wenye nyumba. Lakini ikiwa mara nyingi hatukuti watu wenye kusikiliza, huenda tukashawishiwa kuona kwamba tunapoteza wakati. Hata hivyo, kumbuka kwamba ufafanuzi mmoja wa neno mafanikio ni ‘kupata kibali.’ Tunataka kupata kibali cha nani? Pasipo shaka tunataka kupata kibali cha Yehova. Tunaweza kukipata hata kama watu wanatusikiliza au hawatusikilizi. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake somo muhimu kuhusiana na hilo.

Yaelekea unakumbuka kwamba Yesu aliwatuma wahubiri wa Ufalme 70 “kuingia katika kila jiji na mahali ambako yeye mwenyewe alikuwa akitaka kwenda.” (Luka 10:1) Walipaswa kuhubiri katika majiji na vijiji bila kuandamana na Yesu. Hilo lilikuwa jambo jipya kwao. Kwa hiyo, Yesu aliwapa maagizo kamili kabla ya kuwatuma. Walipokutana na “rafiki wa amani,” wangemtolea ushahidi kamili kuhusu Ufalme. Lakini, walipokataliwa, wangeenda zao, bila wasiwasi. Yesu alieleza kwamba wale ambao wangekataa kuwasikiliza wangekuwa wakimkataa Yehova mwenyewe.—Luka 10:4-7, 16.

Wakati wale 70 walipomaliza mgawo wao wa kuhubiri, walimtolea Yesu ripoti kwa “shangwe, wakisema: ‘Bwana, hata roho waovu watiishwa kwetu kwa utumizi wa jina lako.’” (Luka 10:17) Lazima watu hao wasiokamilika wawe walisisimuka kufukuza viumbe wa roho wenye nguvu! Hata hivyo, Yesu aliwatahadharisha wanafunzi wake wenye shauku: “Msishangilie juu ya hili, kwamba roho watiishwa kwenu, bali shangilieni kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.” (Luka 10:20) Huenda si wakati wote ambapo hao 70 wangekuwa na nguvu za kuwafukuza roho waovu wala kupata matokeo mazuri katika huduma. Lakini kama wangedumisha uaminifu wao, wangekuwa na kibali cha Yehova sikuzote.

Je, Unawathamini Watumishi wa Wakati Wote?

Kijana mmoja mwanamume alimwambia mzee Mkristo hivi: “Nitakapomaliza shule ya upili, nitajitahidi kutafuta kazi. Lakini nikikosa kazi, basi nitafikiria kujiunga na aina fulani ya utumishi wa wakati wote.” Lakini wengi ambao wamejiunga na huduma ya wakati wote wana maoni tofauti. Ili kupainia, baadhi yao wameacha fursa za kufuatia kazi-maisha zenye mapato makubwa. Wengine wamekataa fursa nzuri za kupata elimu ya juu. Kama mtume Paulo wamejidhabihu, lakini kama Paulo, Robert, na Amy, hawajuti kwa sababu ya maamuzi waliyofanya. Wanathamini pendeleo lao la kutumia vipawa vyao kumsifu Yehova, anayestahili kupewa kilicho bora zaidi.

Kwa sababu mbalimbali, wengi wa Mashahidi wa Yehova waaminifu hawawezi kupainia. Labda wana matakwa ya Kimaandiko ya kutimiza. Hata hivyo, Yehova anapendezwa nao ikiwa wanamtumikia kwa ‘moyo wao wote na kwa nafsi yao yote na kwa akili yao yote.’ (Mathayo 22:37) Ingawa wao wenyewe hawawezi kupainia, wanatambua kwamba wale wanaopainia wamechagua kazi-maisha bora.

Mtume Paulo aliandika: “Komeni kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo.” (Waroma 12:2) Kulingana na ushauri wa Paulo, hatupaswi kuruhusu viwango vya utamaduni au vya kilimwengu vya mfumo huu vigeuze mawazo yetu. Iwe unaweza kupainia au la, ufanye utumishi wa Yehova kuwa jambo muhimu maishani mwako. Utafanikiwa maadamu unapata kibali cha Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Usiendelee kufanya kazi yenye kuchosha isiyo na matokeo