Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kudumisha Usafi wa Kiadili

Unaweza Kudumisha Usafi wa Kiadili

Unaweza Kudumisha Usafi wa Kiadili

“Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake.”—1 YOHANA 5:3.

1. Kuna tofauti gani ya mwenendo kati ya watu leo?

ZAMANI za kale, nabii Malaki alipuliziwa kutabiri juu ya wakati ambapo mwenendo wa watu wa Mungu ungetofautiana kabisa na wa watu wasiomtumikia Mungu. Nabii huyo aliandika hivi: “Ndipo mtakaporudi, nanyi mtapambanua kati ya wenye haki na waovu, na kati ya yeye amtumikiaye Mungu na yeye asiyemtumikia.” (Malaki 3:18) Unabii huo unatimizwa leo. Kushika amri za Mungu, kutia ndani zile zinazodai usafi wa kiadili, ndio mwendo unaofaa na wa busara maishani. Hata hivyo, kwa kawaida huo si mwendo rahisi. Yesu alikuwa na sababu nzuri aliposema kwamba lazima Wakristo wajikakamue wenyewe kisulubu ili kupata wokovu.—Luka 13:23, 24.

2. Kuna msongo gani kutoka nje unaofanya iwe vigumu kwa wengine kudumisha usafi wa kiadili?

2 Kwa nini ni vigumu kudumisha usafi wa kiadili? Sababu moja ni kwamba kuna mkazo kutoka nje. Biashara ya vitumbuizo huonyesha ngono haramu kuwa yenye kusisimua, yenye kupendeza, inayofanya mmoja aonekane kuwa mtu mzima, huku ikipuuza kabisa matokeo yake yenye kudhuru. (Waefeso 4:17-19) Uhusiano wa kingono unaoonyeshwa mara nyingi huwa kati ya wenzi wasiofunga ndoa. Mara nyingi sinema na vipindi vya televisheni huonyesha uhusiano wa kingono katika hali ambayo watu hawawajibiki. Kwa kawaida hakuna uchangamfu na kustahiana. Wengi wameona vipindi hivyo tangu utotoni. Isitoshe, kuna mkazo mkubwa sana wa marika wa kujipatanisha na maadili malegevu ya kisasa, na wale wasiofanya hivyo nyakati nyingine hudhihakiwa au hata kutukanwa.—1 Petro 4:4.

3. Ni zipi baadhi ya sababu zinazofanya wengi ulimwenguni wajihusishe na ukosefu wa adili?

3 Mkazo kutoka ndani pia hufanya iwe vigumu kudumisha usafi wa kiadili. Yehova aliwaumba wanadamu wakiwa na tamaa ya ngono, na tamaa hiyo yaweza kuwa kubwa. Tamaa inahusiana na yale tunayofikiri, na ukosefu wa adili unahusiana na kufikiri juu ya mambo yasiyopatana na mawazo ya Yehova. (Yakobo 1:14, 15) Kwa mfano, kulingana na uchunguzi wa hivi majuzi uliochapishwa katika British Medical Journal, watu wengi waliofanya ngono mara ya kwanza walitaka tu kujua mtu huhisije. Wengine waliamini kwamba wengi wa marika wao walikuwa wakifanya ngono, kwa hiyo wao pia wakataka kuanza. Na bado wengine walisema kwamba walishindwa kudhibiti hisia zao au walikuwa “wamelewa kidogo wakati huo.” Tukitaka kumpendeza Mungu, lazima tufikiri kwa njia tofauti. Ni kufikiri kwa aina gani ambako kutatusaidia kudumisha usafi wa kiadili?

Sitawisha Msimamo Thabiti

4. Yatupasa kufanya nini ili tudumishe usafi wa kiadili?

4 Ili tudumishe usafi wa kiadili, lazima tutambue kwamba inafaa kuishi maisha ya kiadili. Hiyo yapatana na yale ambayo mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wa Roma: “[Jithibitishieni] wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Kutambua kwamba usafi wa kiadili unafaa kwahusisha mengi zaidi kuliko kujua tu ukosefu wa adili unakatazwa katika Neno la Mungu. Kwahusisha kuelewa sababu zinazofanya ukosefu wa adili ukatazwe na jinsi tunavyonufaika kwa kuuepuka. Baadhi ya sababu hizo zilizungumziwa katika makala iliyotangulia.

5. Ni kwa nini hasa Wakristo wanapaswa kudumisha usafi wa kiadili?

5 Hata hivyo, kwa kweli sababu kubwa zinazofanya Wakristo waepuke ukosefu wa adili katika ngono zategemea uhusiano wetu na Mungu. Tumejifunza kwamba anajua yale yanayotufaa zaidi. Kumpenda kutatusaidia tuchukie lililo baya. (Zaburi 97:10) Mungu ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu.” (Yakobo 1:17) Anatupenda. Kwa kumtii, twaonyesha kwamba twampenda na kuthamini yote ambayo ametufanyia. (1 Yohana 5:3) Hatutaki kamwe kumtamausha wala kumwumiza Yehova kwa kuvunja amri zake za uadilifu. (Zaburi 78:41) Hatungependa kujiendesha kwa njia ambayo itafanya ibada yake takatifu na adilifu itukanwe. (Tito 2:5; 2 Petro 2:2) Kwa kudumisha usafi wa kiadili, tunamfurahisha Aliye Mkuu Kabisa.—Mithali 27:11.

6. Kujulisha wengine viwango vyetu vya kiadili kunasaidiaje?

6 Tuazimiapo kudumisha usafi wa kiadili, tutapata ulinzi zaidi kwa kuwaeleza wengine msimamo huo. Wajulishe watu kwamba wewe ni mtumishi wa Yehova Mungu na kwamba umeazimia kudumisha viwango vyake vya juu. Ni maisha yako, mwili wako, uchaguzi wako. Ni nini kimo hatarini? Uhusiano wako wenye thamani pamoja na Baba yako wa kimbingu. Kwa hiyo onyesha waziwazi kwamba huwezi kamwe kubadili msimamo wako wa uaminifu-maadili. Jivunie kumwakilisha Mungu kwa kutegemeza kanuni zake. (Zaburi 64:10) Usiaibike kamwe kuzungumza juu ya msimamo wako wa maadili na wengine. Kusema waziwazi kwaweza kukuimarisha, kukulinda, na kuwatia moyo wengine wafuate kielelezo chako.—1 Timotheo 4:12.

7. Tunaweza kudumishaje azimio letu la kubaki safi kiadili?

7 Kisha, baada ya kuazimia kudumisha viwango vya juu vya adili na kujulisha msimamo wetu, lazima tuchukue hatua za kushikamana na azimio letu. Njia moja ya kufanya hivyo ni kuwa waangalifu tunapochagua marafiki. “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima,” yasema Biblia. Shirikiana na wale wanaofuata kanuni sawa na wewe; watakuimarisha. Pia andiko hilo lasema hivi: “Bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Kwa kadiri uwezavyo, epuka watu wanaoweza kudhoofisha azimio lako.—1 Wakorintho 15:33.

8. (a) Kwa nini twapaswa kulisha akili zetu mambo yanayofaa? (b) Twapaswa kuepuka nini?

8 Zaidi ya hayo, twahitaji kulisha akili zetu mambo yaliyo ya kweli, mazito, ya uadilifu, yaliyo safi kiadili, ya kupendeka, yanayosemwa vema, yenye wema wa adili, na yanayostahili sifa. (Wafilipi 4:8) Tunafanya hivyo kwa kuteua yale tunayotazama na kusoma na muziki tunaosikiliza. Kusema kwamba vichapo visivyo vya adili havipotoshi mtu ni sawa na kusema kwamba vichapo vyenye mambo ya adili haviathiri mtu ifaavyo. Kumbuka kwamba wanadamu wasiokamilika wanaweza kutumbukia kwa urahisi katika ukosefu wa adili. Kwa hiyo, vitabu, magazeti, sinema, na muziki unaochochea nyege utaongoza kwenye tamaa mbaya ambazo hatimaye zaweza kuongoza kwenye dhambi. Ili tudumishe usafi wa kiadili lazima tujaze akili zetu hekima ya Mungu.—Yakobo 3:17.

Hatua Zinazoongoza Kwenye Ukosefu wa Adili

9-11. Kama ilivyosimuliwa na Solomoni, ni hatua zipi zilizomwongoza kijana fulani kutumbukia katika ukosefu wa adili?

9 Mara nyingi, kuna hatua dhahiri ambazo huongoza kwenye ukosefu wa adili. Hatua moja inapopigwa inakuwa vigumu sana kurudi nyuma. Ona jinsi jambo hilo linavyoelezwa katika Mithali 7:6-23. Solomoni aona “kijana asiyekuwa na akili,” au asiyekuwa na nia njema. Kijana huyo ‘anapita njiani karibu na pembe yake [ya kahaba], akiishika njia iendayo nyumbani kwake, wakati wa magharibi, wakati wa jioni.’ Anafanya kosa la kwanza. Wakati wa jioni, “moyo” wake umemwelekeza, si katika barabara yoyote ile, bali katika barabara ambayo anajua kwa kawaida inaweza kuwa na kahaba.

10 Kisha twasoma hivi: “Tazama, mwanamke akamkuta, ana mavazi ya kikahaba, mwerevu wa moyo.” Sasa kijana anamwona! Anaweza kugeuka na kurudi nyumbani, lakini sasa ni vigumu zaidi kuliko hapo awali, hasa kwa kuwa yeye ni dhaifu kiadili. Huyo mwanamke anamshika na kumbusu. Baada ya kukubali busu, sasa anasikiliza utongozi wake: “Kwangu ziko sadaka za amani,” asema. “Leo hivi nimeziondoa nadhiri zangu.” Sadaka za amani zilitia ndani nyama, unga, mafuta, na divai. (Mambo ya Walawi 19:5, 6; 22:21; Hesabu 15:8-10) Kwa kutaja vitu hivyo, labda alikuwa akimdokezea kwamba hali yake ya kiroho haikuwa mbaya, na wakati huohuo, labda alikuwa akimjulisha kwamba kulikuweko vyakula na vinywaji vingi tena vizuri nyumbani mwake. “Haya,” anamsihi “na tushibe upendo hata asubuhi, tujifurahishe nafsi zetu kwa mahaba.”

11 Si vigumu kujua matokeo yalikuwaje. “Kwa ubembelezi wa midomo yake akamshinda.” Kijana akamfuata kahaba nyumbani “kama vile ng’ombe aendavyo machinjoni” na “kama ndege aendaye haraka mtegoni.” Solomoni amalizia kwa maneno yenye kuamsha fikira: “Wala hajui ya kuwa ni hasara ya nafsi yake.” Nafsi, au uhai wake wahusika kwa sababu “Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Waebrania 13:4) Ni somo lenye maana kubwa kama nini kwa wanaume na wanawake! Twapaswa kuepuka kuchukua hatua za kwanzakwanza zitakazotuongoza kukosa kibali cha Mungu.

12. (a) Usemi “asiyekuwa na akili” wamaanisha nini? (b) Twaweza kuimarishaje nguvu za kiadili?

12 Ona kwamba kijana anayesimuliwa ‘hakuwa na akili.’ Usemi huo watuonyesha kwamba mawazo, tamaa, shauku, hisia-moyo, na miradi yake maishani haikupatana na yale ambayo Mungu hukubali. Udhaifu wake wa kiadili ulitokeza mambo yenye kuhuzunisha. Katika “siku [hizi] za mwisho” zenye hatari, jitihada inahitajiwa ili kusitawisha nguvu za kiadili. (2 Timotheo 3:1) Mungu ametuandalia misaada. Huandaa mikutano ya kutaniko la Kikristo ili kututia moyo tuendelee kufuata njia inayofaa na kuwa na ushirika na wale walio na miradi kama yetu. (Waebrania 10:24, 25) Kuna wazee wa kutaniko wanaotuchunga na kutufundisha njia za uadilifu. (Waefeso 4:11, 12) Tuna Neno la Mungu, Biblia, ili kutuongoza. (2 Timotheo 3:16) Na nyakati zote, tuna fursa ya kusali kupata roho ya Mungu ili itusaidie.—Mathayo 26:41.

Kujifunza Kutokana na Dhambi za Daudi

13, 14. Mfalme Daudi alihusikaje katika dhambi nzito?

13 Ingawa hivyo, inasikitisha kwamba watumishi wa Mungu wenye kutokeza wamehusika katika ukosefu wa adili katika ngono. Mmoja wa watumishi hao ni Mfalme Daudi, ambaye alikuwa amemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miongo mingi. Bila shaka alimpenda Mungu sana. Hata hivyo, alitumbukia hatua kwa hatua katika dhambi. Kama ilivyokuwa na yule kijana aliyesimuliwa na Solomoni, kuna hatua zilizomwongoza Daudi kwenye dhambi kisha zikafanya dhambi hiyo iwe mbaya hata zaidi.

14 Wakati huo Daudi alikuwa na umri wa makamo, labda miaka 50 hivi. Akiwa juu ya paa lake, alimwona Bath-sheba mrembo akioga. Aliulizia habari zake na kupata kujua mwanamke huyo alikuwa nani. Akagundua kwamba mume wake, Uria, alikuwa katika kampeni ya kuzingira Raba, jiji la Waamoni. Daudi alifanya mpango mwanamke huyo aletwe kwenye jumba la mfalme na kulala naye. Baadaye, mambo yakatatanika—Bath-sheba akagundua kwamba ana mimba ya Daudi. Daudi alimwita Uria arudi kutoka vitani akitumaini kwamba angelala na mke wake usiku huo. Kwa njia hiyo, ingeonekana kwamba Uria ndiye baba ya mtoto wa Bath-sheba. Lakini Uria hakwenda nyumbani kwake. Akitaka sana kuficha dhambi yake, Daudi alimtuma Uria arudi Raba akiwa na barua ya mkuu wa jeshi iliyosema kwamba Uria awekwe mahali ambapo angeuawa. Hivyo Uria akauawa, na Daudi akamwoa mjane huyo kabla watu hawajajua kwamba alikuwa mjamzito.—2 Samweli 11:1-27.

15. (a) Dhambi ya Daudi ilifichuliwaje? (b) Daudi aliitikiaje karipio la Nathani lililotolewa kwa ustadi?

15 Ilionekana kana kwamba njama ya Daudi ya kuficha dhambi yake ilikuwa imefaulu. Miezi kadhaa ikapita. Mtoto wa kiume akazaliwa. Ikiwa Daudi alikuwa akikumbuka kisa hiki alipoandika Zaburi ya 32, basi ni wazi kwamba dhamiri yake ilimsumbua sana. (Zaburi 32:3-5) Hata hivyo, Mungu hakufichwa dhambi hiyo. Biblia husema: “Jambo lile alilolitenda Daudi likamchukiza BWANA.” (2 Samweli 11:27) Yehova alimtuma nabii Nathani, aliyemkabili Daudi kwa ustadi kuhusu yale aliyokuwa amefanya. Daudi aliungama mara moja na kumwomba Yehova msamaha. Toba yake ya kweli ilimpatanisha na Mungu. (2 Samweli 12:1-13) Daudi hakuchukia karipio. Badala yake, alionyesha mtazamo unaoelezwa katika Zaburi 141:5: “Mwenye haki na anipige, itakuwa fadhili; anikemee, itakuwa kama mafuta kichwani; kichwa changu kisikatae.”

16. Solomoni alitoa onyo na shauri gani kuhusu ukiukaji-sheria?

16 Huenda Solomoni, aliyekuwa mwana wa pili wa Daudi na Bath-sheba alikumbuka tukio hilo lenye kuhuzunisha katika maisha ya baba yake. Baadaye aliandika hivi: “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema.” (Mithali 28:13) Tukitumbukia katika dhambi nzito, twapaswa kutii shauri hilo lililopuliziwa, ambalo ni onyo na shauri pia. Twapaswa kuungama kwa Yehova na kuwafikia wazee wa kutaniko ili watusaidie. Daraka moja muhimu la wazee ni kusaidia kuwarekebisha upya wale ambao wametenda kosa.—Yakobo 5:14, 15.

Kuvumilia Matokeo ya Dhambi

17. Ingawa Yehova husamehe dhambi, yeye hatukingi na mambo gani?

17 Yehova alimsamehe Daudi. Kwa nini? Kwa sababu Daudi alishika uaminifu-maadili, aliwarehemu wengine, na alionyesha toba ya kweli. Hata hivyo, Daudi hakukingwa na matokeo yenye msiba. (2 Samweli 12:9-14) Ndivyo ilivyo leo. Ingawa Yehova hasababishi uovu kwa watu wanaotubu, hawakingi wasipatwe na mambo ambayo hutokea kwa sababu ya makosa yao. (Wagalatia 6:7) Ukosefu wa adili katika ngono waweza kutokeza talaka, mimba isiyotakiwa, maradhi yanayoambukizwa kingono, na kukosa kuaminiwa na kustahiwa.

18. (a) Paulo aliambia kutaniko la Korintho lishughulikieje kisa cha mwenendo mbaya sana wa ngono? (b) Yehova huonyeshaje upendo na rehema kwa watenda-dhambi?

18 Ikiwa sisi wenyewe tumetenda kosa zito, ni rahisi kuvunjika moyo tunapopatwa na matokeo ya makosa ambayo tumefanya. Hata hivyo, tusiruhusu kitu chochote kituzuie kutubu na kupatanishwa na Mungu. Katika karne ya kwanza, Paulo aliandikia Wakorintho kwamba walipaswa kumwondoa kutoka kutanikoni mtu aliyekuwa amezoea kufanya ngono ya maharimu. (1 Wakorintho 5:1, 13) Mtu huyo alipotubu kikweli, Paulo aliagiza kutaniko hilo hivi: “[Msameheni] kwa fadhili na kumfariji [na] kumthibitishia upendo wenu.” (2 Wakorintho 2:5-8) Katika shauri hilo lililopuliziwa, twaona upendo wa Yehova na rehema yake kuelekea watenda-dhambi wanaotubu. Malaika mbinguni hufurahi mtenda-dhambi anapotubu.—Luka 15:10.

19. Twaweza kupata manufaa gani tukihuzunishwa ifaavyo na mwenendo usiofaa?

19 Ijapokuwa tunahuzunishwa na mwenendo usiofaa, majuto tunayohisi yaweza kutusaidia ‘tujitunze tusiutazame uovu.’ (Ayubu 36:21) Kwa kweli, matokeo mabaya ya dhambi yapasa kutuzuia tusirudie kosa. Isitoshe, Daudi alitumia jambo lenye kuhuzunisha lililompata kwa sababu ya mwenendo wake wa dhambi, kuwashauri wengine. Alisema hivi: “Nitawafundisha wakosaji njia zako, na wenye dhambi watarejea kwako.”—Zaburi 51:13.

Furaha Huja kwa Kumtumikia Yehova

20. Tunapata manufaa gani kwa kutii matakwa ya Mungu ya uadilifu?

20 “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!” akasema Yesu. (Luka 11:28) Kutii matakwa ya Mungu ya uadilifu hutokeza baraka sasa na wakati ujao usio na mwisho. Ikiwa tumedumisha usafi wa kiadili, na tuendelee vivyo hivyo kwa kutumia maandalizi yote ambayo Yehova ametupa ili kutusaidia. Ikiwa tumetumbukia katika ukosefu wa adili, na tutiwe moyo kujua kwamba Yehova yuko tayari kusamehe wale wanaotubu kikweli, na acheni tuazimie kutorudia dhambi hiyo kamwe.—Isaya 55:7.

21. Tunaweza kudumisha usafi wa kiadili kwa kutumia shauri gani la mtume Petro?

21 Karibuni ulimwengu huu usio mwadilifu utapitilia mbali, pamoja na mitazamo na mazoea yake yasiyo ya adili. Kwa kudumisha usafi wa kiadili tutanufaika sasa na milele. Mtume Petro aliandika hivi: “Wapendwa, kwa kuwa mnangojea mambo haya, fanyeni kabisa yote mwezayo ili mwishowe mpatikane naye mkiwa bila doa na bila waa na katika amani. . . . Mkiwa mnakuwa na ujuzi huu wa kimbele, iweni wenye kulinda ili msipate kuongozwa kando pamoja nao kwa kosa la watu wanaokaidi sheria na kuanguka kutoka kwenye uimara wenu wenyewe.”—2 Petro 3:14, 17.

Je, Waweza Kueleza?

• Kwa nini inaweza kuwa vigumu kudumisha usafi wa kiadili?

• Kuna njia gani za kutusaidia kuimarisha azimio letu la kufuata viwango vya juu vya adili?

• Twaweza kujifunza nini kutokana na dhambi za kijana aliyetajwa na Solomoni?

• Kielelezo cha Daudi chatufunza nini kuhusu toba?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Ni ulinzi kuwajulisha wengine msimamo wako kuhusu mambo ya kiadili

[Picha katika ukurasa wa 16. 17]

Kwa sababu Daudi alitubu kikweli, Yehova alimsamehe