Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kusali Kuna Manufaa Yoyote?

Je, Kusali Kuna Manufaa Yoyote?

Je, Kusali Kuna Manufaa Yoyote?

NYAKATI fulani karibu kila mtu huona uhitaji wa kusali. Kwa kweli, karibu watu wa kila dini husali kwa bidii. Mathalani, huenda Mbudha akasali akirudia-rudia mara elfu nyingi kwa siku ile sala “mimi naamini Amida Buddha.”

Kwa sababu ya matatizo yaliyoko ulimwenguni kote inafaa kujiuliza hivi: Watu hutarajia kupata nini kwa kusali? Je, sala hizo zote zina manufaa yoyote?

Kwa Nini Watu Husali?

Watu wengi wa Mashariki husali kwa wazazi wao wa kale na kwa miungu ya Shinto au Tao. Hufanya hivyo wakitumaini kupita mitihani shuleni, kuvuna mazao mazuri, au kuzuia maradhi. Kupitia jitihada zao, Wabudha hutumaini kuelimishwa zaidi. Wahindu husali kwa bidii kwa miungu ya kiume na ya kike wanayoipenda ili kupata ujuzi, mali, na ulinzi.

Wakatoliki wengine hutumaini kunufaisha wanadamu kwa kujitoa watumikie kama watawa wa kiume au wa kike kwenye nyumba za watawa, wakisali daima. Mamilioni ya Wakatoliki hutafuta kibali cha Maria kwa kutoa sala zilizokaririwa, labda kwa kutumia shanga za tasbihi. Katika nchi za Mashariki, watu wengi hutumia magurudumu ya sala. Waprotestanti hurudia maneno ya Sala ya Bwana, ijapokuwa pia huenda wakadhihirisha hisia zao kwa Mungu kupitia sala zao wenyewe. Wayahudi wengi husafiri mbali ili kusali kwenye Ukuta wa Magharibi wa Yerusalemu, wakitumaini kurudishwa kwa hekalu na kizazi kipya chenye ufanisi na amani.

Ingawa mamilioni hujikakamua kusali, jamii ya wanadamu inazidi kukumbwa na matatizo ya umaskini, uraibu, familia zilizovunjika, uhalifu, na vita. Je, inaweza kuwa kwamba watu hawa wote hawasali kwa njia inayofaa? Zaidi ya hayo, je, kweli kuna yeyote anayesikia sala?

Je, Kuna Yeyote Anayesikia Sala?

Sala haziwezi kuwa na manufaa yoyote zisiposikiwa. Mtu anaposali, kwa wazi anaamini kwamba mtu fulani katika makao ya roho anasikia. Hata hivyo, sala hazipitishwi na mawimbi ya sauti tu. Watu wengi wanaamini kwamba mtu fulani anaweza kusoma mawazo ya mwenye kusali. Huyo anaweza kuwa nani?

Watafiti wanatatanishwa na jinsi ambavyo mawazo hutoka katika mabilioni ya nyuroni ambazo hufanyiza tabaka la nje la ubongo wetu. Hata hivyo, ni jambo linalopatana na akili kwamba Yule aliyeumba ubongo anaweza kusoma mawazo hayo. Huyo si mwingine ila Muumba wetu, Yehova Mungu. (Zaburi 83:18; Ufunuo 4:11) Sala zapasa kuelekezwa kwake. Lakini je, Yehova husikia sala zote za namna hiyo?

Je, Sala Zote Husikiwa?

Mfalme Daudi wa Israeli la kale, alikuwa mtu wa kusali. Akiwa mtunga-zaburi aliyepuliziwa, aliimba hivi: “Wewe usikiaye kuomba, wote wenye mwili watakujia.” (Zaburi 65:2) Yehova anaweza kuelewa sala zinazotolewa katika yoyote ya maelfu ya lugha zinazosemwa na wanadamu. Ingawa ni kweli kwamba hakuna akili ya mwanadamu iwezayo kushughulika na habari nyingi kadiri hiyo, hiyo haimaanishi kwamba Mungu hawezi kusikia wote wanaosali kwake kwa njia inayokubalika.

Lakini, Yesu Kristo—ambaye pia alikuwa mtu wa sala alifunua kwamba Mungu hapendezwi na sala zote. Ona yale ambayo Yesu alisema kuhusu zoea lililopendwa sana wakati huo la kurudia-rudia sala zilizokaririwa. Kulingana na Biblia Habari Njema, alisema hivi: “Mnaposali, msipayuke maneno kama watu wasiomjua Mungu. Wao hudhani kwamba Mungu atawasikiliza ati kwa sababu ya maneno mengi.” (Mathayo 6:7) Hatuwezi kutazamia Yehova asikize sala ambazo hazielezi hisia zetu za kweli.

Ikionyesha kwa nini sala fulani hazimpendezi Mungu, mithali moja ya Biblia husema hivi: “Yeye aligeuzaye sikio lake asiisikie sheria, hata sala yake ni chukizo.” (Mithali 28:9) Mithali nyingine husema hivi: “BWANA yu mbali na wasio haki; bali huisikia sala ya mwenye haki.” (Mithali 15:29) Wakati viongozi wa Yuda la kale walipokuwa na hatia nzito, Yehova alisema hivi: “Nanyi mkunjuapo mikono yenu, nitaficha macho yangu nisiwaone; naam, mwombapo maombi mengi, sitasikia; mikono yenu imejaa damu.”—Isaya 1:1, 15.

Mtume Petro alitaja jambo jingine ambalo laweza kufanya Mungu asikubali sala. Petro aliandika hivi: “Nyinyi waume, endeleeni kukaa pamoja na [wake zenu] kwa namna kama hiyo kulingana na ujuzi, mkiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi, kile cha kike, kwa kuwa nyinyi pia ni warithi pamoja nao wa pendeleo lisilostahiliwa la uhai, kusudi sala zenu zisizuiwe.” (1 Petro 3:7) Sala za mtu anayepuuza shauri hilo hazifiki popote!

Kwa wazi, ni lazima tutimize matakwa fulani ili sala zisikiwe. Hata hivyo, wengi wanaosali hawajali yale ambayo Mungu anataka tufanye. Ndiyo sababu kusali kwa bidii hakujatokeza ulimwengu bora.

Kwa hiyo basi, Mungu hutaka nini ili asikie sala zetu? Jibu linahusu sababu yenyewe inayotufanya tusali. Kwa kweli, tukitaka kujua ikiwa sala ina na manufaa yoyote, lazima tuelewe kusudi lake. Kwa nini Yehova amefanya iwezekane tuzungumze naye?

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

G.P.O., Jerusalem