Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Walio Wahudumu wa Mungu Leo?

Ni Nani Walio Wahudumu wa Mungu Leo?

Ni Nani Walio Wahudumu wa Mungu Leo?

“Kuwa kwetu na sifa za ustahili wa kutosha kwatoka kwa Mungu, ambaye kwa kweli ametustahilisha vya kutosha kuwa wahudumu wa agano jipya.” —2 WAKORINTHO 3:5, 6.

1, 2. Wakristo wote wa karne ya kwanza walikuwa na jukumu gani, lakini hali zilibadilikaje?

KATIKA karne ya kwanza ya Wakati Wetu wa Kawaida, Wakristo wote walishiriki jukumu muhimu—wajibu wa kuhubiri habari njema. Wote walikuwa watiwa-mafuta na walikuwa wahudumu wa agano jipya. Baadhi yao walikuwa na majukumu zaidi, kama vile kufundisha kutanikoni. (1 Wakorintho 12:27-29; Waefeso 4:11) Wazazi walikuwa na majukumu mazito katika familia. (Wakolosai 3:18-21) Lakini wote walishiriki kazi ya msingi na muhimu ya kuhubiri. Katika Kigiriki cha awali cha Maandiko ya Kikristo, jukumu hilo lilikuwa di·a·ko·niʹa—utumishi, au huduma.—Wakolosai 4:17.

2 Hali zilibadilika kadiri wakati ulivyopita. Kulitokea jamii, iliyoitwa makasisi, ambayo ilichukulia pendeleo la kuhubiri kuwa lao wenyewe. (Matendo 20:30) Makasisi walikuwa idadi ndogo tu ya wale wenye kujiita Wakristo. Walio wengi wa Wakristo hao wakaanza kuitwa watu wa kawaida. Ingawa Wakristo hao wa kawaida wamefundishwa kwamba wana majukumu fulani, kutia ndani kuchanga kwa ajili ya kuwatunza makasisi, wengi wao wamekuwa wasikilizaji tu wasiofanya lolote kwa habari ya kuhubiri.

3, 4. (a) Watu katika Jumuiya ya Wakristo hupataje kuwa wahudumu? (b) Ni nani anayeonwa kuwa mhudumu katika Jumuiya ya Wakristo, na kwa nini hali ni tofauti miongoni mwa Mashahidi wa Yehova?

3 Makasisi hudai kuwa wahudumu (kutokana na neno mhudumu, ambalo ni tafsiri ya neno la Kilatini, di·aʹko·nos, “mtumishi”). * Ili kuwa wahudumu, wanahitimu katika vyuo au seminari kisha wanawekwa rasmi kuwa makasisi. Kichapo The International Standard Bible Encyclopedia chasema: “‘Kuwekwa rasmi kuwa kasisi’ kwa kawaida hurejezea cheo cha pekee kinachopewa wahudumu au makasisi kupitia taratibu zilizoidhinishwa rasmi, zinazokazia mamlaka ya kutangaza Neno au kusimamia ushirika mtakatifu wa Kikristo, au kufanya yote mawili.” Wahudumu huwekwa rasmi na nani? Kichapo The New Encyclopædia Britannica chasema: “Katika makanisa ambayo yamehifadhi cheo muhimu cha uaskofu, kwa kawaida askofu ndiye huweka watu rasmi kuwa makasisi. Katika makanisa ya Kiprotestanti yasiyo na cheo cha uaskofu, wahudumu wa mabaraza ya mkoa ndio huweka watu rasmi kuwa makasisi.”

4 Hivyo, katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, ni watu wachache sana wanaopewa pendeleo la kuwa wahudumu. Hata hivyo, hali ni tofauti miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Kwa nini? Kwa kuwa hali haikuwa hivyo katika kutaniko la Wakristo wa karne ya kwanza.

Wahudumu wa Mungu Ni Nani Hasa?

5. Kulingana na Biblia, wanaotumikia wakiwa wahudumu hutia ndani nani?

5 Kulingana na Biblia, waabudu wote wa Yehova—wa mbinguni na wa duniani—ni wahudumu. Malaika walimhudumia Yesu. (Mathayo 4:11; 26:53; Luka 22:43) Malaika pia ‘huwahudumia wale watakaorithi wokovu.’ (Waebrania 1:14; Mathayo 18:10) Yesu alikuwa mhudumu. Yeye alisema: “Mwana wa binadamu [alikuja], si kuhudumiwa, bali kuhudumu.” (Mathayo 20:28; Waroma 15:8) Kwa hiyo, kwa kuwa wafuasi wa Yesu ‘wangefuata hatua zake kwa ukaribu,’ si ajabu kwamba wao pia lazima wawe wahudumu.—1 Petro 2:21.

6. Yesu alionyeshaje kwamba wanafunzi wake wapaswa kuwa wahudumu?

6 Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi muda mfupi kabla ya kupaa mbinguni: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Wanafunzi wa Yesu wangekuwa wafanya-wanafunzi—wahudumu. Wanafunzi wapya ambao hao walifanya wangejifunza kushika mambo yote aliyoamuru Yesu, kutia ndani amri ya kwenda na kufanya wanafunzi. Mwanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo angekuwa mhudumu, awe mwanamume au mwanamke, mtu mzima au mtoto.—Yoeli 2:28, 29.

7, 8. (a) Ni maandiko gani yaonyeshayo kwamba Wakristo wote wa kweli ni wahudumu? (b) Ni maswali gani yanayoulizwa kuhusiana na kuwekwa rasmi kwa wahudumu?

7 Kwa kupatana na hayo, siku ya Pentekoste 33 W.K., wanafunzi wote wa Yesu waliokuwepo, wanaume kwa wanawake, waliungana kutangaza “mambo yenye fahari ya Mungu.” (Matendo 2:1-11) Isitoshe mtume Paulo aliandika: “Kwa moyo mtu hudhihirisha imani kwa ajili ya uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.” (Waroma 10:10) Paulo hakusema maneno hayo kwa makasisi wachache tu, bali “kwa wale wote [waliokuwa] katika Roma wakiwa wapendwa wa Mungu.” (Waroma 1:1, 7) Vivyo hivyo, ‘watakatifu wote walioko Efeso na waaminifu katika muungano na Kristo Yesu’ walipaswa ‘kuvika miguu yao kama viatu vifaa vya habari njema ya amani.’ (Waefeso 1:1; 6:15) Na wote waliosoma barua iliyoandikiwa Waebrania walipaswa “kushika sana tangazo la hadharani la tumaini lao bila kuyumbayumba.”—Waebrania 10:23.

8 Hivyo basi, mtu anakuwa mhudumu lini? Yaani, ni lini anawekwa rasmi kuwa mhudumu? Na ni nani anayemweka rasmi kuwa mhudumu?

Kuwekwa Rasmi Kuwa Mhudumu—Lini?

9. Yesu aliwekwa rasmi kuwa mhudumu lini, na nani?

9 Kwa habari ya ni lini na ni kupitia nani mtu huwekwa rasmi kuwa mhudumu, hebu fikiria kielelezo cha Yesu Kristo. Yeye hakuwa na cheti cha kuwekwa rasmi kuwa mhudumu au digrii kutoka seminari ili kuthibitisha kwamba alikuwa mhudumu, naye hakuwekwa rasmi na mtu yeyote kuwa mhudumu. Basi, kwa nini tunaweza kusema kwamba alikuwa mhudumu? Kwa sababu maneno haya ya Isaya yaliyopuliziwa yalitimizwa kuhusiana naye: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kutangaza habari njema.” (Luka 4:17-19; Isaya 61:1) Maneno hayo yanatuhakikishia kwamba Yesu aliidhinishwa kutangaza habari njema. Na nani? Kwa kuwa roho ya Yehova ilimtia mafuta kwa ajili ya kazi hiyo, ni wazi kwamba Yesu aliwekwa rasmi kuwa mhudumu na Yehova Mungu. Aliwekwa rasmi lini? Roho ya Yehova ilimjia Yesu alipobatizwa. (Luka 3:21, 22) Kwa hiyo, aliwekwa rasmi kuwa mhudumu wakati wa ubatizo wake.

10. Ni kupitia nani mhudumu Mkristo anapata kuwa “na sifa za ustahili wa kutosha”?

10 Namna gani wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza? Yehova pia ndiye aliyewaweka rasmi kuwa wahudumu. Paulo alisema: “Kuwa kwetu na sifa za ustahili wa kutosha kwatoka kwa Mungu, ambaye kwa kweli ametustahilisha vya kutosha kuwa wahudumu wa agano jipya.” (2 Wakorintho 3:5, 6) Yehova anawastahilishaje waabudu wake kuwa wahudumu? Fikiria mfano wa Timotheo, ambaye Paulo alimwita “mhudumu wa Mungu katika habari njema juu ya Kristo.”—1 Wathesalonike 3:2.

11, 12. Timotheo alifanyaje maendeleo ili kuwa mhudumu?

11 Maneno yafuatayo yaliyoandikiwa Timotheo yanatusaidia kuelewa jinsi alivyopata kuwa mhudumu: “Hata hivyo, wewe endelea katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishwa kuamini, ukijua ni kutoka kwa watu gani ulijifunza hayo na kwamba tangu utoto sana umeyajua maandishi matakatifu, yawezayo kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia imani kuhusiana na Kristo Yesu.” (2 Timotheo 3:14, 15) Imani ya Timotheo, iliyomchochea kufanya tangazo la hadharani, ilitegemea ujuzi wa Maandiko. Je, alihitaji kusoma tu kibinafsi? La. Timotheo alihitaji msaada ili kupata ujuzi sahihi na uelewevu wa kiroho wa mambo aliyosoma. (Wakolosai 1:9) Hivyo Timotheo “alishawishwa kuamini.” Kwa kuwa alijua Maandiko “tangu utoto sana,” bila shaka wafunzi wake wa kwanza walikuwa mama na nyanya yake, kwa kuwa yaonekana babake hakuwa mwamini.—2 Timotheo 1:5.

12 Hata hivyo, ili Timotheo apate kuwa mhudumu, mengi yalihusika. Kwanza, imani yake iliimarika kwa kushirikiana na Wakristo wa makutaniko ya karibu. Tunajuaje? Kwa sababu Paulo alipokutana na Timotheo mara ya kwanza, kijana huyo “aliripotiwa vema na akina ndugu katika Listra na Ikoniamu.” (Matendo 16:2) Isitoshe, wakati huo ndugu fulani waliyaandikia barua makutaniko ili kuyaimarisha. Nao waangalizi wakayatembelea makutaniko ili kuyatia moyo. Maandalizi hayo yaliwasaidia Wakristo kama Timotheo kufanya maendeleo ya kiroho.—Matendo 15:22-32; 1 Petro 1:1.

13. Timotheo aliwekwa rasmi lini kuwa mhudumu, na ni kwa nini waweza kusema kwamba maendeleo yake ya kiroho hayakukoma hapo?

13 Kwa kuzingatia amri ya Yesu kwenye Mathayo 28:19, 20, tunaweza kuwa na hakika kwamba wakati fulani imani ya Timotheo ilimchochea kumwiga Yesu na kubatizwa. (Mathayo 3:15-17; Waebrania 10:5-9) Kwa kufanya hivyo, Timotheo alionyesha ujitoaji wa nafsi yote kwa Mungu. Timotheo alipata kuwa mhudumu alipobatizwa. Tangu wakati huo na kuendelea, uhai wake, nguvu zake na chochote alichokuwa nacho kikawa cha Mungu. Hiyo ilikuwa sehemu muhimu ya ibada yake, “utumishi mtakatifu.” Hata hivyo, Timotheo hakutosheka tu na kuwa mhudumu. Aliendelea kukua kiroho, akawa mhudumu Mkristo aliyekomaa. Hilo lilitokea kwa sababu Timotheo alishirikiana kwa ukaribu na Wakristo wakomavu kama Paulo, akajifunza mwenyewe kibinafsi, na kuhubiri kwa bidii.—1 Timotheo 4:14; 2 Timotheo 2:2; Waebrania 6:1.

14. Leo, mtu ‘aliye na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele’ hufanyaje maendeleo ili awe mhudumu?

14 Leo, watu huwekwa rasmi vivyo hivyo kuwa wahudumu katika huduma ya Kikristo. Mtu ‘aliye na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele’ anasaidiwa kujifunza juu ya Mungu na makusudi yake kupitia funzo la Biblia. (Matendo 13:48) Mtu huyo hujifunza kutumia kanuni za Biblia maishani mwake na kutoa sala zenye maana kwa Mungu. (Zaburi 1:1-3; Mithali 2:1-9; 1 Wathesalonike 5:17, 18) Hushirikiana na waamini wengine na hujinufaisha na maandalizi na mipango ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47; Mithali 13:20; Waebrania 10:23-25) Hivyo yeye hufanya maendeleo akifuata utaratibu fulani wa kujifunza.

15. Ni nini hutukia mtu anapobatizwa? (Ona kielezi-chini pia.)

15 Baada ya kusitawisha upendo kwa Yehova Mungu na imani yenye nguvu katika dhabihu ya fidia, mwanafunzi wa Biblia hutamani kujiweka wakfu kabisa kwa Baba yake wa mbinguni. (Yohana 14:1) Yeye hujiweka wakfu kupitia sala ya kibinafsi, kisha anabatizwa kama wonyesho wa hadharani wa kitendo hicho kilichofanywa faraghani. Ubatizo wake ndiyo sherehe ya kuwekwa rasmi kwake kuwa mhudumu kwa sababu wakati huo ndipo anapotambuliwa kuwa mtumishi, di·aʹko·nos, wa Mungu aliyejiweka wakfu kabisa. Ni lazima ajitenge na ulimwengu. (Yohana 17:16; Yakobo 4:4) Amejitoa kabisa kuwa “dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu” bila vizuizi wala masharti. (Waroma 12:1) * Yeye ni mhudumu wa Mungu, anayemwiga Kristo.

Huduma ya Kikristo Ni Nini?

16. Timotheo alikuwa na wajibu gani mbalimbali akiwa mhudumu?

16 Huduma ya Timotheo ilitia ndani nini? Alikuwa na wajibu mbalimbali wa pekee alipoandamana na Paulo katika safari zake. Na alipopata kuwa mzee, Timotheo alijitahidi sana kuwafundisha na kuwaimarisha Wakristo wenzake. Lakini sehemu muhimu ya huduma yake, kama vile Yesu na Paulo, ilikuwa kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. (Mathayo 4:23; 1 Wakorintho 3:5) Paulo alimwambia Timotheo: “Ingawa hivyo, wewe tunza akili zako katika mambo yote, vumilia uovu, fanya kazi ya mweneza-evanjeli, timiza kikamili huduma yako.”—2 Timotheo 4:5.

17, 18. (a) Wakristo hushiriki katika huduma gani? (b) Kazi ya kuhubiri ni muhimu kadiri gani kwa mhudumu Mkristo?

17 Ndivyo ilivyo na wahudumu Wakristo leo. Wao hufanya huduma ya watu wote, kazi ya kueneza evanjeli, wakiwaelekeza wengine kwenye wokovu unaotegemea dhabihu ya Yesu na kuwafundisha wapole kuliitia jina la Yehova. (Matendo 2:21; 4:10-12; Waroma 10:13) Wanathibitisha kwa Biblia kwamba Ufalme ndio tumaini la pekee kwa wanadamu wenye kuteseka na kuonyesha kwamba hata sasa hali zinakuwa nzuri zaidi tukiishi kupatana na kanuni za Mungu. (Zaburi 15:1-5; Marko 13:10) Lakini mhudumu Mkristo hahubiri gospeli ya kijamii. Badala yake, yeye hufundisha kwamba ‘ujitoaji-kimungu una ahadi ya uhai wa sasa na ule utakaokuja.’—1 Timotheo 4:8.

18 Ni kweli kwamba wahudumu wengi wana njia zaidi za kutumikia, ambazo huenda zikatofautiana kati ya Wakristo. Wengi wana majukumu ya familia. (Waefeso 5:21–6:4) Wazee na watumishi wa huduma wana wajibu mbalimbali kutanikoni. (1 Timotheo 3:1, 12, 13; Tito 1:5; Waebrania 13:7) Wakristo wengi husaidia kujenga Majumba ya Ufalme. Wengine wana pendeleo zuri la kutumikia wakiwa wajitoleaji katika mojawapo ya makao ya Betheli ya Watch Tower Society. Hata hivyo, wahudumu wote Wakristo hushiriki kuhubiri habari njema. Hakuna wasiofanya hivyo. Kushiriki katika kazi hii ndiko humtambulisha mtu kuwa mhudumu Mkristo wa kweli.

Mtazamo wa Mhudumu Mkristo

19, 20. Wahudumu Wakristo wapaswa kusitawisha mtazamo gani?

19 Wahudumu wengi wa Jumuiya ya Wakristo hutazamia kupewa heshima ya pekee, nao hujiita majina ya cheo kama “padri” na “baba.” Lakini mhudumu Mkristo anajua kwamba Yehova pekee ndiye astahiliye heshima. (1 Timotheo 2:9, 10) Hakuna mhudumu Mkristo ambaye hudai heshima hiyo ya juu au kutamani majina ya pekee ya cheo. (Mathayo 23:8-12) Anajua kwamba maana ya msingi ya neno di·a·ko·niʹa ni “utumishi.” Wakati mwingine kitenzi kinachohusianishwa na neno hilo hutumiwa katika Biblia kuhusiana na utumishi wa kibinafsi, kama vile kuhudumu mezani. (Luka 4:39; 17:8; Yohana 2:5) Hata ingawa matumizi yake kuhusiana na huduma ya Kikristo yana maana kubwa zaidi, di·aʹko·nos bado ni mtumishi.

20 Kwa hiyo, hakuna mhudumu Mkristo aliye na sababu ya kujikweza. Wahudumu Wakristo wa kweli—hata wale walio na majukumu ya pekee kutanikoni—ni watumwa wanyenyekevu. Yesu alisema: “Yeyote yule atakaye kuwa mkubwa miongoni mwenu lazima awe mhudumu wenu, na yeyote yule atakaye kuwa wa kwanza miongoni mwenu lazima awe mtumwa wenu.” (Mathayo 20:26, 27) Alipowaonyesha wanafunzi wake mtazamo ufaao kusitawisha, Yesu aliwaosha miguu, akifanya kazi ya mtumwa aliye wa cheo cha chini zaidi. (Yohana 13:1-15) Ni utumishi wa unyenyekevu kama nini! Hivyo, wahudumu Wakristo humtumikia Yehova Mungu na Yesu Kristo kwa unyenyekevu. (2 Wakorintho 6:4; 11:23) Wao huonyesha mtazamo wa kujishusha chini wanapotumikiana. Na wanapohubiri habari njema, wanawatumikia bila ubinafsi majirani wao wasioamini.—Waroma 1:14, 15; Waefeso 3:1-7.

Vumilia Katika Huduma

21. Paulo alithawabishwaje kwa kuvumilia katika huduma?

21 Paulo alihitaji uvumilivu ili kuwa mhudumu. Aliwaambia Wakolosai kwamba alivumilia mambo mengi ili kuwahubiria habari njema. (Wakolosai 1:24, 25) Hata hivyo, kwa sababu alivumilia, wengi walikubali habari njema kisha wakawa wahudumu. Walizaliwa kuwa wana wa Mungu na ndugu za Yesu Kristo, wakiwa na matazamio ya kuwa viumbe wa roho pamoja naye mbinguni. Ni thawabu tukufu kama nini kwa uvumilivu!

22, 23. (a) Kwa nini wahudumu Wakristo leo wanahitaji uvumilivu? (b) Uvumilivu wa Kikristo una matokeo gani mazuri?

22 Uvumilivu ni muhimu leo kwa wale ambao kweli ni wahudumu wa Mungu. Wengi hupambana kila siku na magonjwa au maumivu ya uzee. Wazazi hujitahidi sana—wengi wao wakiwa bila mwenzi wa ndoa—kulea watoto wao. Kwa ujasiri, watoto shuleni hukinza uvutano mbaya unaowazunguka. Wakristo wengi hupambana na hali ngumu sana za kiuchumi. Nao wengi hunyanyaswa au hukabili magumu kwa sababu ya “nyakati za hatari [za leo] zilizo ngumu kushughulika nazo”! (2 Timotheo 3:1) Naam, wahudumu wa Yehova leo wapatao milioni sita wanaweza kuungana na mtume Paulo kusema: “Katika kila njia twajipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu, kwa uvumilivu wa mengi.” (2 Wakorintho 6:4) Wahudumu Wakristo hawakati tamaa. Kwa kweli wanastahili kusifiwa kwa uvumilivu wao.

23 Isitoshe, kama ilivyokuwa kuhusiana na Paulo, uvumilivu huleta matokeo mazuri. Kwa kuvumilia, sisi hudumisha uhusiano wetu wa karibu pamoja na Yehova na kumfurahisha moyo. (Mithali 27:11) Huimarisha imani yetu na kufanya wanafunzi, hivyo kuongeza idadi ya ndugu wa Kikristo. (1 Timotheo 4:16) Yehova amewategemeza wahudumu wake na kubariki huduma yao katika siku hizi za mwisho. Matokeo yamekuwa kwamba wa mwisho kati ya wale 144,000 wamekusanywa, na mamilioni zaidi wana matumaini hakika ya kufurahia uhai udumuo milele katika dunia paradiso. (Luka 23:43; Ufunuo 14:1) Ni kweli kwamba huduma ya Kikristo ni wonyesho wa rehema ya Yehova. (2 Wakorintho 4:1) Sote na tuithamini huduma na kushukuru kwamba matokeo yake yatadumu milele.—1 Yohana 2:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Neno “shemasi,” yaani ofisa wa kanisa, linatokana na neno la Kigiriki di·aʹko·nos. Katika makanisa ambapo wanawake wanaweza kuwa mashemasi, wanaweza kuitwa mashemasi wa kike.

^ fu. 15 Ingawa andiko la Waroma 12:1 lahusu hasa Wakristo watiwa-mafuta, kanuni ya andiko hilo yahusu pia “kondoo wengine.” (Yohana 10:16) Hao ‘huandamana na Yehova ili wamhudumu, na kulipenda jina la Yehova ili kuwa watumishi wake.’—Isaya 56:6.

Je, Unaweza Kueleza?

• Wakristo wote wa karne ya kwanza walikuwa na jukumu gani?

• Mhudumu Mkristo huwekwa rasmi na nani na lini?

• Mhudumu Mkristo apaswa kusitawisha mtazamo gani?

• Kwa nini yampasa mhudumu Mkristo kuvumilia anapokabili magumu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Timotheo alifunzwa Neno la Mungu tangu utotoni. Alipata kuwa mhudumu aliyewekwa rasmi wakati alipobatizwa

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ubatizo ni wonyesho wa kujiweka wakfu kwa Mungu na huonyesha kwamba mtu amewekwa rasmi kuwa mhudumu

[Picha katika ukurasa wa 20]

Wahudumu Wakristo wako tayari kutumikia