Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakristo Hupata Furaha Kutumikia

Wakristo Hupata Furaha Kutumikia

Wakristo Hupata Furaha Kutumikia

“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—MATENDO 20:35.

1. Ni mtazamo gani mbaya ambao umeenea leo, na ni kwa nini una madhara?

KATIKA miongo ya mwisho ya miaka ya 1900, neno “me-ism” lilisikika sana. Neno hilo la Kiingereza lamaanisha “mimi kwanza” na laonyesha mtazamo wa ubinafsi, pupa, na kutojali wengine. Tunaweza kuwa na hakika kwamba katika mwaka wa 2000 mtazamo huo wa mimi kwanza bado upo. Ni mara ngapi unaposikia maswali kama, “Nitanufaikaje?” au, “Nitapata faida gani?” Mtazamo huo wa ubinafsi hauleti furaha. Ni kinyume kabisa cha kanuni hii aliyotaja Yesu: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

2. Inaonyeshwaje kwamba kutoa huleta furaha?

2 Je, ni kweli kwamba kutoa huleta furaha nyingi kuliko kupokea? Ndiyo. Hebu fikiria Yehova Mungu. Yeye ndiye “chemchemi ya uzima.” (Zaburi 36:9) Yeye hutuandalia kila kitu tunachohitaji ili tuwe wenye furaha na wenye mafanikio. Naam, yeye ndiye Chanzo cha “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu.” (Yakobo 1:17) Yehova, “Mungu mwenye furaha,” hutoa daima. (1 Timotheo 1:11) Yeye anapenda viumbe wake wa kibinadamu na huwapa vitu vingi sana. (Yohana 3:16) Fikiria pia familia ya kibinadamu. Ikiwa wewe ni mzazi, unajua jinsi unavyojidhabihu na kujitoa ili kulea mtoto. Na kwa miaka mingi mtoto huyo hafahamu jinsi unavyojidhabihu. Hata hajali kujidhabihu kwako. Hata hivyo, bado unafurahi kuona mtoto wako akikua kwa sababu unajitoa bila ubinafsi. Kwa nini? Kwa sababu unampenda.

3. Kwa nini inafurahisha kumtumikia Yehova na kuwatumikia waamini wenzetu?

3 Vivyo hivyo, ibada ya kweli hubainishwa na kutoa kunakotegemea upendo. Kwa kuwa tunampenda Yehova na tunawapenda waamini wenzetu, tunafurahia kuwatumikia na kujitoa kwao. (Mathayo 22:37-39) Yeyote anayeabudu kwa sababu za ubinafsi mwishowe hukosa furaha. Lakini wale wanaotumikia pasipo ubinafsi, wakihangaikia zaidi yale wawezayo kutoa kuliko yale watarajiayo kupokea, hupata furaha kwelikweli. Ukweli huo unafahamika kwa kuchunguza jinsi maneno fulani ya Biblia yanayohusiana na ibada yetu yanavyotumiwa katika Maandiko. Katika makala haya na yale yafuatayo, tutazungumzia maneno matatu kati ya hayo.

Utumishi wa Watu Wote wa Yesu

4. “Utumishi wa watu wote” katika Jumuiya ya Wakristo ni wa aina gani?

4 Katika Kigiriki cha awali, neno moja muhimu linalohusiana na ibada ni lei·tour·giʹa, linalotafsiriwa “utumishi wa watu wote” katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Katika Jumuiya ya Wakristo neno hilo lei·tour·giʹa limetokeza neno “liturujia.” * Lakini liturujia za kidesturi za ibada ya Jumuiya ya Wakristo si utumishi wa watu wote wenye manufaa kikweli.

5, 6. (a) Ni utumishi gani wa watu wote uliotolewa Israeli, kukiwa na manufaa gani? (b) Ni utumishi gani wa watu wote ulio mtukufu zaidi ambao ulichukua mahali pa ule uliotolewa Israeli, na kwa nini?

5 Mtume Paulo alitumia neno la Kigiriki linalohusiana na neno lei·tour·giʹa aliporejezea makuhani wa Israeli. Alisema: “Kila kuhani huenda mahali pa kazi kutoka siku hadi siku kutoa utumishi wa watu wote [aina fulani ya lei·tour·giʹa] na kutoa dhabihu zilezile mara nyingi.” (Waebrania 10:11) Makuhani Walawi walitoa utumishi wa watu wote wenye manufaa sana nchini Israeli. Walifundisha Sheria ya Mungu na kutoa dhabihu zilizofunika dhambi za watu. (2 Mambo ya Nyakati 15:3; Malaki 2:7) Wakati makuhani na watu walipofuata Sheria ya Yehova, taifa lilikuwa na sababu za kufurahi.—Kumbukumbu la Torati 16:15.

6 Lilikuwa pendeleo kwelikweli kwa makuhani Waisraeli kutoa utumishi wa watu wote chini ya Sheria, lakini utumishi wao ulikosa thamani kabisa wakati Israeli lilipokataliwa kwa sababu ya kukosa uaminifu. (Mathayo 21:43) Yehova alipanga kuwe na utumishi mtukufu zaidi—utumishi wa watu wote uliotolewa na Yesu, Kuhani wa Cheo cha Juu aliye mkuu. Twasoma hivi kumhusu: “Yeye kwa sababu ya kuendelea kuwa hai milele ana ukuhani wake bila kuwa na wafuataji wowote. Kwa sababu hiyo aweza pia kuokoa kikamili wale wanaomkaribia Mungu kupitia yeye, kwa sababu yeye yuko hai sikuzote ili kuwaombea.”—Waebrania 7:24, 25.

7. Kwa nini utumishi wa watu wote wa Yesu unaleta manufaa zisizo na kifani?

7 Yesu anaendelea akiwa kuhani milele, bila kuwa na wafuatiaji. Hivyo, ni yeye tu awezaye kuokoa watu kabisa. Yeye hutoa utumishi huo wa watu wote usio na kifani, si katika hekalu lililotengenezwa na mwanadamu, bali katika hekalu lililofananishwa kimbele, yaani mpango mkuu wa Yehova wa ibada ulioanza kufanya kazi mwaka wa 29 W.K. Yesu sasa anatumikia katika Patakatifu Zaidi pa hekalu hilo, mbinguni. Yeye ni “mtumishi wa watu wote [lei·tour·gosʹ] wa mahali patakatifu na wa hema la kweli, ambalo Yehova alisimamisha, wala si mwanadamu.” (Waebrania 8:2; 9:11, 12) Ingawa ana cheo cha juu sana, Yesu bado ni “mtumishi wa watu wote.” Yeye hutumia mamlaka yake ya juu kutoa wala si kupokea. Na utoaji huo humletea shangwe. Ni sehemu ya “shangwe iliyowekwa mbele yake” iliyomtia nguvu kuvumilia katika maisha yake yote duniani.—Waebrania 12:2.

8. Yesu alitoaje utumishi wa watu wote kuwa badala ya agano la Sheria?

8 Kuna jambo jingine analofanya Yesu katika utumishi wa watu wote. Paulo aliandika: “Yesu amepata utumishi wa watu wote ulio bora kabisa zaidi, hivi kwamba kwa kulingana yeye ni mpatanishi pia wa agano lililo bora, ambalo limethibitishwa kisheria juu ya ahadi zilizo bora.” (Waebrania 8:6) Musa alikuwa mpatanishi wa agano lililokuwa msingi wa uhusiano wa Israeli na Yehova. (Kutoka 19:4, 5) Yesu alikuwa mpatanishi wa agano jipya, lililowezesha kuzaliwa kwa taifa jipya, “Israeli wa Mungu,” linalofanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta kwa roho kutoka mataifa mengi. (Wagalatia 6:16; Waebrania 8:8, 13; Ufunuo 5:9, 10) Huo ulikuwa utumishi wa watu wote bora kama nini! Tunafurahi kama nini kumjua Yesu, mtumishi wa watu wote ambaye kupitia kwake tunaweza kutoa ibada yenye kukubalika kwa Yehova!—Yohana 14:6.

Wakristo Pia Hutoa Utumishi wa Watu Wote

9, 10. Wakristo hutoa aina zipi za utumishi wa watu wote?

9 Hakuna mwanadamu ambaye hutoa utumishi wa watu wote uliotukuka kama ule wa Yesu. Hata hivyo, Wakristo watiwa-mafuta wanapopokea thawabu yao ya kimbingu, wao hujiunga na Yesu na kushiriki katika utumishi wake wa watu wote wakiwa wafalme na makuhani wa kimbingu. (Ufunuo 20:6; 22:1-5) Lakini Wakristo walio duniani hutoa utumishi wa watu wote, nao hufurahi kufanya hivyo. Kwa mfano, kulipokuwa na upungufu wa chakula Palestina, mtume Paulo alichukua michango kutoka kwa ndugu wa Ulaya ili kusaidia kutuliza dhiki ya Wakristo Wayahudi huko Yudea. Huo ulikuwa utumishi wa watu wote. (Waroma 15:27; 2 Wakorintho 9:12) Leo, Wakristo wanafurahi kutoa utumishi kama huo, wakitoa msaada haraka wakati ndugu zao wanapopatwa na dhiki, maafa ya kiasili, au misiba mingineyo.—Mithali 14:21.

10 Paulo alirejezea utumishi mwingine wa watu wote alipoandika: “Hata ikiwa ninamwagwa kama toleo la kinywaji juu ya dhabihu na utumishi wa watu wote ambako imani imewaongoza nyinyi, mimi naterema nami nashangilia pamoja nanyi nyote.” (Wafilipi 2:17) Jitihada za Paulo kwa ajili ya Wafilipi zilikuwa utumishi wa watu wote uliotolewa kwa upendo na kwa bidii. Utumishi wa watu wote wa aina hiyo unatolewa leo, hasa na Wakristo watiwa-mafuta, wanaotumikia wakiwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” wakiandaa chakula cha kiroho kwa wakati ufaao. (Mathayo 24:45-47) Isitoshe, wakiwa kikundi, wao ni “ukuhani mtakatifu,” waliopewa wajibu wa “kutoa dhabihu za kiroho zenye kukubalika kwa Mungu kupitia Yesu Kristo” na ‘kutangaza kotekote sifa bora kabisa za yeye aliyewaita kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.’ (1 Petro 2:5, 9) Kama Paulo, wanafurahia mapendeleo hayo hata ‘wanapojimwaga’ katika kutimiza wajibu wao mbalimbali. Na wenzao “kondoo wengine” hujiunga nao na huwaunga mkono katika kazi ya kuwajulisha wanadamu kuhusu Yehova na makusudi yake. * (Yohana 10:16; Mathayo 24:14) Ni utumishi wa watu wote mtukufu na wenye kufurahisha kama nini!—Zaburi 107:21, 22.

Toa Utumishi Mtakatifu

11. Nabii wa kike Ana aliwawekeaje Wakristo wote kielelezo bora?

11 Neno lingine la Kigiriki linalohusiana na ibada yetu ni la·treiʹa, linalotafsiriwa “utumishi mtakatifu” katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Utumishi mtakatifu unatia ndani matendo ya ibada. Kwa mfano, inaelezwa kwamba nabii wa kike Ana, aliyekuwa mjane mwenye umri wa miaka 84, “alikuwa hakosi kamwe kuwa katika hekalu, akitoa utumishi mtakatifu [neno la Kigiriki linalohusiana na la·treiʹa] usiku na mchana kwa mifungo na dua.” (Luka 2:36, 37) Ana alimwabudu Yehova kwa uaminifu. Yeye ni mfano mzuri kwetu sote—vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake. Kama vile Ana alivyosali kwa Yehova kwa bidii na kumwabudu kwa ukawaida kwenye hekalu, hali kadhalika utumishi wetu mtakatifu watia ndani sala na kuhudhuria mikutano.—Waroma 12:12; Waebrania 10:24, 25.

12. Ni ipi sehemu muhimu ya utumishi wetu mtakatifu, na hiyo pia inakuwaje utumishi wa watu wote?

12 Mtume Paulo alitaja sehemu muhimu ya utumishi wetu mtakatifu alipoandika: “Mungu, nitoleaye utumishi mtakatifu kwa roho yangu kuhusiana na ile habari njema juu ya Mwana wake, ni shahidi wangu wa jinsi niwatajavyo sikuzote katika sala zangu bila kukoma.” (Waroma 1:9) Naam, kuhubiriwa kwa habari njema ni utumishi wa watu wote kwa wale wanaosikiliza na pia ni tendo la ibada kwa Yehova Mungu. Hata kama watu wanatusikiliza au la, kazi ya kuhubiri ni utumishi mtakatifu tunaomtolea Yehova. Jitihada zetu za kuwaambia wengine sifa bora na makusudi yenye manufaa ya Baba yetu mpendwa wa mbinguni bila shaka hutuletea furaha kubwa.—Zaburi 71:23.

Tunatolea Wapi Utumishi Mtakatifu?

13. Wale watoao utumishi mtakatifu katika ua wa ndani wa hekalu la Yehova la kiroho wana tumaini gani, na ni nani hushangilia pamoja nao?

13 Paulo aliwaandikia hivi Wakristo watiwa-mafuta: “Kwa kuwa tutapokea ufalme usioweza kutikiswa, acheni sisi tuendelee kuwa na fadhili isiyostahiliwa, ambayo kupitia hiyo twaweza kumtolea Mungu katika njia ya kukubalika utumishi mtakatifu kwa hofu ya kimungu na kicho.” (Waebrania 12:28) Wakiwa na matazamio yenye uhakika ya kurithi Ufalme, watiwa-mafuta hawayumbiyumbi katika imani wanapomwabudu Aliye Juu Zaidi Sana. Ni wao tu wanaoweza kumtolea Yehova utumishi mtakatifu katika sehemu ya Patakatifu na ua wa ndani wa hekalu la Yehova la kiroho, nao wanatazamia kwa hamu nyingi sana kutumikia pamoja na Yesu katika Patakatifu Zaidi Sana, mbinguni kwenyewe. Wenzao, jamii ya kondoo wengine, hushangilia pamoja nao katika tumaini lao la ajabu.—Waebrania 6:19, 20; 10:19-22.

14. Umati mkubwa unanufaikaje na utumishi wa watu wote wa Yesu?

14 Basi, namna gani kondoo wengine? Kama mtume Yohana alivyoona kimbele, umati mkubwa wa kondoo hao umetokea siku hizi za mwisho, “nao wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 7:14) Hilo lamaanisha kwamba, kama waabudu wenzao watiwa-mafuta, wao wana imani katika utumishi wa watu wote wa Yesu na pia katika kutoa kwake uhai mkamilifu wa kibinadamu kwa ajili ya wanadamu. Kondoo wengine pia hunufaika na utumishi wa watu wote wa Yesu kwa sababu ‘wanashika sana agano la Yehova.’ (Isaya 56:6) La, wao si washiriki wa agano jipya, lakini wanalishika sana kwa sababu mbali na kutii sheria zinazohusiana na agano hilo wanaunga mkono mipango inayofanywa kupitia hilo. Wao hushirikiana na Israeli wa Mungu na kula kwenye meza moja ya kiroho na kufanya kazi pamoja nao, wakimsifu Mungu hadharani na kutoa dhabihu za kiroho zinazompendeza.—Waebrania 13:15.

15. Umati mkubwa wanatolea wapi utumishi wao mtakatifu, na baraka hiyo ina matokeo gani kwao?

15 Hivyo, umati mkubwa wanaonekana “wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo, wamevaa kanzu nyeupe.” Isitoshe, “wako mbele ya hicho kiti cha ufalme cha Mungu; nao wanamtolea utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake; na Yeye aketiye juu ya kiti cha ufalme atatandaza hema lake juu yao.” (Ufunuo 7:9, 15) Katika Israeli, wageuzwa-imani waliabudu katika ua wa nje wa hekalu la Solomoni. Vivyo hivyo, umati mkubwa humwabudu Yehova katika ua wa nje wa hekalu lake la kiroho. Kutumikia hapo huwafurahisha sana. (Zaburi 122:1) Hata baada ya yule wa mwisho kati ya wenzao watiwa-mafuta kupokea urithi wake wa mbinguni, umati mkubwa wataendelea kumtolea Yehova utumishi mtakatifu wakiwa watu wake.—Ufunuo 21:3.

Utumishi Mtakatifu Usiokubalika

16. Ni maonyo gani yanayotolewa kuhusu utumishi mtakatifu?

16 Wakati wa Israeli la kale, utumishi mtakatifu ulipasa kutolewa kulingana na sheria za Yehova. (Kutoka 30:9; Mambo ya Walawi 10:1, 2) Hali kadhalika leo, kuna matakwa ya kufuatwa ikiwa utumishi wetu mtakatifu utakubalika kwa Yehova. Hiyo ndiyo sababu Paulo aliwaandikia Wakolosai hivi: “Sisi . . . hatujaacha kusali kwa ajili yenu na kuomba ili nyinyi mpate kujazwa ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na ufahamivu wa kiroho, kusudi mtembee kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili mnapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.” (Wakolosai 1:9, 10) Si juu yetu kuamua njia inayofaa ya kumwabudu Mungu. Ujuzi sahihi wa Maandiko, uelewevu wa kiroho, na hekima ya kimungu ni muhimu. Bila mambo hayo, matokeo yanaweza kuwa mabaya sana.

17. (a) Utumishi mtakatifu ulipotoshwaje wakati wa Musa? (b) Utumishi mtakatifu unaweza kupotoshwaje leo?

17 Kumbuka Waisraeli wa wakati wa Musa. Twasoma hivi: “Mungu akageuka na kuwakabidhi watoe utumishi mtakatifu kwa jeshi la mbinguni.” (Matendo 7:42) Waisraeli hao walikuwa wameona matendo yenye nguvu ya Yehova aliyofanya kwa niaba yao. Hata hivyo, waligeukia miungu mingine walipofikiri wangenufaika. Hawakuwa waaminifu-washikamanifu, na uaminifu-mshikamanifu ni wa lazima ikiwa utumishi wetu mtakatifu utampendeza Mungu. (Zaburi 18:25) Ni kweli kwamba ni watu wachache leo ambao wangemwacha Yehova ili kuabudu nyota au ndama za dhahabu, lakini kuna aina nyinginezo za ibada ya sanamu. Yesu alionya dhidi ya kutumikia “Mali,” naye Paulo akaiita tamaa ibada ya sanamu. (Mathayo 6:24; Wakolosai 3:5) Shetani hujikweza kuwa mungu. (2 Wakorintho 4:4) Aina hizo za ibada ya sanamu zimeenea sana na ni mtego. Fikiria kwa mfano, mtu ambaye anadai kumfuata Yesu lakini lengo lake maishani ni kuwa tajiri, au mtu ambaye hujitumaini mwenyewe na maoni yake. Yeye kweli anamtumikia nani? Yeye ana tofauti gani na Wayahudi wa wakati wa Isaya walioapa kwa jina la Yehova lakini wakazisifu sanamu zisizo safi eti ndizo zilizofanya matendo makuu ya Yehova?—Isaya 48:1, 5.

18. Utumishi mtakatifu umetolewaje kimakosa wakati uliopita na leo?

18 Yesu pia alionya: “Saa inakuja wakati kila mtu awauaye nyinyi atawazia amemtolea Mungu utumishi mtakatifu.” (Yohana 16:2) Hapana shaka Sauli, aliyekuja kuwa mtume Paulo, alifikiri kwamba alikuwa anamtumikia Mungu ‘alipokubali kuuawa kimakusudi kwa Stefano’ ‘na kupumua tisho na uuaji-kimakusudi dhidi ya wanafunzi wa Bwana.’ (Matendo 8:1; 9:1) Leo, baadhi ya watekelezaji wa vita na mauaji ya kikabila pia wanadai kumwabudu Mungu. Kuna watu wengi wanaodai kumwabudu Mungu, lakini wao kwa kweli huabudu miungu ya uzalendo, ukabila, utajiri, ubinafsi, na kadhalika.

19. (a) Tunauonaje utumishi wetu mtakatifu? (b) Ni utumishi mtakatifu wa aina gani utakaotuletea shangwe?

19 Yesu alisema: “Ni Yehova Mungu wako ambaye lazima uabudu, na ni kwake peke yake lazima utoe utumishi mtakatifu.” (Mathayo 4:10) Alikuwa anazungumza na Shetani, lakini ni muhimu jinsi gani kwetu sote kuyatilia maanani maneno yake! Kumtolea utumishi mtakatifu Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu ni pendeleo kubwa, lenye kutia kicho. Tusemeje kuhusu kutoa utumishi wa watu wote unaohusiana na ibada yetu? Kufanya hivyo kwa ajili ya wanadamu wenzetu ni kazi yenye shangwe ambayo huleta furaha kubwa. (Zaburi 41:1, 2; 59:16) Lakini utumishi huo huleta furaha ya kweli unapotolewa kwa moyo wote na kwa njia ifaayo. Ni nani hasa wanaomwabudu Mungu ifaavyo? Yehova anakubali utumishi mtakatifu wa nani? Tunaweza kujibu maswali hayo tukichunguza neno la tatu katika Biblia ambalo linahusiana na ibada yetu. Tutafanya hivyo katika makala yafuatayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kwa jumla liturujia za Jumuiya ya Wakristo ni taratibu za ibada au desturi maalum za ibada, kama vile Ushirika Mtakatifu wa Kikristo katika Kanisa Katoliki.

^ fu. 10 Katika Matendo 13:2, inasemwa kwamba manabii na walimu huko Antiokia walikuwa “wakimhudumia Yehova hadharani” (tafsiri ya neno la Kigiriki linalohusiana na lei·tour·giʹa). Yaelekea, huduma hiyo ya hadharani ilitia ndani kuhubiria watu.

Ungejibuje?

• Yesu alitoa utumishi gani mtukufu wa watu wote?

• Wakristo hutoa utumishi gani wa watu wote?

• Utumishi mtakatifu wa Wakristo ni nini, nao unatolewa wapi?

• Lazima tuwe na nini ili utumishi wetu mtakatifu umpendeze Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wazazi hupata shangwe kubwa kwa kutoa

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Wakristo hutoa utumishi wa watu wote wanapowasaidia wengine na wanapotangaza habari njema

[Picha katika ukurasa wa 14]

Tunahitaji ujuzi sahihi na uelewevu ili kuwa na hakika kwamba utumishi wetu mtakatifu unakubalika kwa Mungu