Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Imependwa na Kukandamizwa Pia

Biblia Imependwa na Kukandamizwa Pia

Biblia Imependwa na Kukandamizwa Pia

“Ningetaka sana vitabu vitakatifu vitafsiriwe katika lugha zote,” akaandika Desiderius Erasmus, msomi Mholanzi mwenye kusifiwa wa karne ya 16.

ERASMUS alitumaini sana kwamba kila mtu angeweza kusoma na kuelewa Maandiko. Lakini wapinzani wa Biblia wakakataa katakata wazo hilo. Kwa kweli, wakati huo lilikuwa jambo hatari sana barani Ulaya kwa mtu yeyote hata kutaka kujua yaliyomo katika Biblia. Nchini Uingereza, bunge lilitunga sheria iliyoagiza kwamba “Yeyote anayesoma Maandiko katika Kiingereza apasa kupoteza shamba, mali, na uhai . . . na kwamba kama anaendelea kuwa mkaidi, au kurudia kosa baada ya kusamehewa, apasa kwanza kunyongwa kwa kosa la uhaini dhidi ya mfalme, kisha achomwe kwa uzushi dhidi ya Mungu.”

Katika bara la Ulaya, Baraza la Wakatoliki la Kuhukumu Wazushi lilisaka kikatili madhehebu ya “wazushi,” kama lile la French Waldenses, na kuwatenga ili kuwanyanyasa kwa sababu ya zoea lao la kuhubiri “kutoka kwa gospeli, nyaraka za mitume, na maandiko mengine matakatifu, . . . kwa kuwa watu wa kawaida walikatazwa kabisa kuhubiri na kufafanua maandiko.” Wanaume na wanawake wengi waliteswa vikali sana na kuuawa kwa sababu ya kuipenda Biblia. Wengine walikariri Sala ya Bwana au zile Amri Kumi na kuwafundisha watoto wao japo walijua wangepata adhabu kali sana kwa kufanya hivyo.

Upendo huo wa Neno la Mungu ulidumu katika mioyo ya wasafiri wengi waliokwenda kuanzisha koloni huko Amerika ya Kaskazini. Katika Amerika ya kale, “kusoma na dini zilihusiana sana, hali iliyoonyesha utamaduni ambao kwa jumla ulitegemea ufahamu wa Biblia,” chasema kitabu A History of Private Life—Passions of the Renaissance. Hata hotuba moja iliyotolewa huko Boston mwaka wa 1767 ilipendekeza hivi: “Tieni bidii kusoma maandiko matakatifu. Mwapaswa kusoma sura moja katika Biblia zenu kila asubuhi na kila jioni.”

Kulingana na kikundi cha utafiti kiitwacho Barna Research Group cha Ventura, California, zaidi ya asilimia 90 ya Wamarekani wana wastani wa Biblia tatu. Hata hivyo, uchunguzi wa hivi majuzi waonyesha kwamba ingawa Biblia inaheshimiwa sana huko, ‘watu hawachukui wakati kuisoma wala kuichunguza wala kutumia yaliyomo.’ Wengi wanajua machache sana kuhusu yaliyomo katika Biblia. Mwandishi mmoja wa gazeti alisema: “Wazo la kwamba [Biblia] bado ni muhimu katika kutatua matatizo na mahangaiko ya sasa ni nadra.”

Kufikiri kwa Ulimwengu Kunakobadilika-Badilika

Kuna itikadi inayopendwa sana kwamba tunaweza kufanikiwa maishani kupitia tu uwezo wa kufikiri na ushirikiano wa kibinadamu. Biblia huonwa kuwa kimojawapo tu cha vitabu vingi juu ya itikadi za dini na mambo yaliyopata watu kibinafsi, wala si kitabu cha mambo hakika na ya kweli.

Kwa hiyo, watu wengi hushughulikaje na masuala yanayozidi kuwa tata na yanayosumbua maishani? Wao hushughulika nayo katika hali isiyo ya kiroho, bila mwongozo au mwelekezo thabiti wa kiadili na kidini. Wamekuwa kama meli zisizo na usukani, ‘wakitupwa na kupeperushwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja.’—Waefeso 4:14, Union Version.

Basi, ni lazima tuulize, Je, Biblia ni kitabu kingine tu cha dini? Au je, kweli Biblia ni Neno la Mungu, lenye habari muhimu iwezayo kutumika? (2 Timotheo 3:16, 17) Je, twastahili kuichunguza Biblia? Makala yafuatayo yatajibu maswali hayo.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Desiderius Erasmus

[Hisani]

From the book Deutsche Kulturgeschichte

[Picha katika ukurasa wa 4]

“Waldenses” walitengwa ili kunyanyaswa kwa sababu ya kuhubiri kutoka katika Maandiko

[Hisani]

Stichting Atlas van Stolk, Rotterdam