Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Kitabu cha Kuongoza Watu Maishani

Biblia Kitabu cha Kuongoza Watu Maishani

Biblia Kitabu cha Kuongoza Watu Maishani

“NENO la Mungu liko hai na hukazia nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili . . . na ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.” (Waebrania 4:12) Bila shaka, maelezo hayo kuhusu yale ambayo Neno la Mungu laweza kutimiza yathibitisha kwamba Biblia ni zaidi ya kitabu kizuri tu.

“Ujumbe wake ni muhimu kwa maisha yetu kama kulivyo kupumua,” mwandishi mmoja wa dini akaandika kwa maneno mafupi na dhahiri. Kisha akaongeza: “Unapofikiria jinsi tunavyotamani na kuhitaji kuponywa leo, kisha usome Biblia kwa kuzingatia hayo, unapata matokeo yenye kushangaza.” Kama taa ing’aayo kwa uangavu, Biblia hufafanua masuala mengi tata na matatizo ya maisha ya siku hizi.—Zaburi 119:105.

Kwa kweli, hekima inayoelezwa katika Biblia ina uwezo wa kuongoza kufikiri kwetu, kutusaidia kutatua matatizo, kuboresha hali ya maisha yetu, na kutuandalia ujuzi wa kukabiliana na hali ambazo hatuwezi kubadili. La muhimu zaidi ni kwamba Biblia hutuwezesha kupata kumjua Mungu na kumpenda.

Kitabu Kinachotoa Kusudi

Mtungaji wa Biblia, Yehova Mungu, ‘anaelewa njia zetu zote.’ Yeye anajua mahitaji yetu ya kimwili, ya kihisia-moyo, na ya kiroho kuliko hata vile tuyajuavyo sisi wenyewe. (Zaburi 139:1-3) Yeye huweka kwa uangalifu mipaka dhahiri kuhusiana na mwenendo wa wanadamu. (Mika 6:8) Ni jambo linalopatana na akili kujitahidi kujua mipaka na mielekezo hiyo na kujifunza kuishi kulingana nayo. Mwenye furaha ni yule ambaye “sheria ya BWANA ndiyo impendezayo,” asema mtunga-zaburi. “Kila alitendalo litafanikiwa.” (Zaburi 1:1-3) Bila shaka twastahili kuyachunguza matazamio hayo.

Maurice, ambaye ni mwalimu aliyestaafu, aliamini sikuzote kwamba Biblia ina thamani kihistoria na kifasihi. Lakini, alitia shaka kama imepuliziwa na Mungu. Baada ya kusikiliza maelezo juu ya ni kwa nini Mungu aliwapa wanadamu Neno lake lililopuliziwa, Maurice alichunguza unabii mbalimbali wa Biblia. Alipokuwa kijana, alisoma historia ya mambo ya kale, fasihi, sayansi, na jiografia. Anakiri kwamba alijiona mwenye akili sana asiweze kukubali mifano mingi inayounga mkono uasilia wa Biblia. “Nilikuwa ninafuatia starehe, mali, na raha za maisha bila kufikiri. Kwa kusikitisha, sikuwa na habari wala sikufahamu ubora na ukweli wa kitabu muhimu zaidi kupata kuandikwa.”

Maurice, ambaye sasa ana umri wa miaka 70 na kitu, asema hivi kwa shukrani, akirejezea pindi ambapo Yesu alimtokea mtume Tomasi: “Mkono wangu umeelekezwa kwenye ‘jeraha linalovuja damu’ litakalonisadikisha milele kwamba Biblia ni ya kweli kabisa.” (Yohana 20:24-29) Kama mtume Paulo alivyosema kwa usahihi, Biblia hufichua makusudi ya moyoni, na huyapa maisha kusudi. Kwa kweli ni kitabu kinachotuongoza maishani.

Kuyaimarisha Maisha Yenye Matatizo

Biblia pia inatoa ushauri ambao husaidia watu waache mazoea mabaya. Daniel aliweza kuacha zoea chafu la kuvuta sigareti, na vilevile akaachana na karamu zenye kelele na ulevi. (Waroma 13:13; 2 Wakorintho 7:1; Wagalatia 5:19-21) Ni kweli kwamba kuacha mazoea hayo na kuvaa “utu mpya” kwahitaji jitihada nyingi sana. (Waefeso 4:22-24) “Ilikuwa vigumu,” asema Daniel, “kwa sababu sisi si wakamilifu.” Lakini alifaulu. Sasa Daniel husoma Neno la Mungu kila siku, na hilo hufanya awe na ukaribu na Yehova.

Alipokuwa akikua, sikuzote Daniel aliiheshimu Biblia—ingawa hakuisoma kamwe—na alisali kwa Mungu kila usiku. Lakini kuna kitu fulani alichokosa. Alikosa furaha. Alifanya badiliko kubwa pale alipoona jina la Mungu katika Biblia kwa mara ya kwanza. (Kutoka 6:3; Zaburi 83:18) Baadaye, alitumia jina Yehova aliposali, na sala zake zikawa za kutoka moyoni. “Yehova akawa mtu wa karibu zaidi kwangu, na bado yeye ni rafiki yangu wa karibu zaidi.”

Kabla ya kujifunza Biblia, Daniel hakuwa na tumaini lolote la wakati ujao. “Si lazima uwe na akili nyingi ili ujue jinsi hali ilivyo ulimwenguni,” yeye asema. “Niliogopa, nikajaribu kujishughulisha na mambo mengi ili nisifikirie hali hiyo.” Ndipo akajifunza kwamba Mungu ataleta haki kwa wote katika dunia iliyosafishwa, ambamo wanadamu watiifu wanaweza kuwa na amani na furaha ya milele. (Zaburi 37:10, 11; Danieli 2:44; Ufunuo 21:3, 4) Sasa Daniel ana tumaini hakika. Uvutano huo wa Biblia wenye kuimarisha unamwezesha kudumisha maoni yafaayo kuhusu maisha.

Msaada wa Kushinda Matatizo ya Kihisia-Moyo

George alikuwa na umri wa miaka saba alipofiwa na mama yake. Aliogopa sana kwenda kulala usiku, kwa kuwa hakujua kama angeamka siku iliyofuata. Ndipo akasoma yale Yesu aliyosema kuhusu kifo na ufufuo: “Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti [ya Yesu] na kutoka.” Pia aliguswa moyo na maneno haya ya Yesu: “Mimi ndio ufufuo na uhai. Yeye ambaye hudhihirisha imani katika mimi, hata ingawa afa, atakuja kwenye uhai.” (Yohana 5:28, 29; 11:25) Maneno hayo yanapatana na akili na ni yenye kufariji. “Kweli hii,” asema George, “haivutii akili tu bali hugusa moyo pia.”

Daniel aliyetajwa hapo awali aliogopa pia. Mama yake hangeweza kumlea akiwa peke yake, kwa hiyo alipelekwa katika makao kadha wa kadha ya wazazi walezi. Sikuzote alijihisi kama mgeni, akatamani hali ya usalama ambayo mtu huhisi anapoishi na familia yenye upendo. Hatimaye, alipata alichokuwa akitafuta kupitia funzo lake la Biblia. Daniel alianza kushirikiana na kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova, akawa sehemu ya familia ya kiroho, ambapo alihisi amekubaliwa na kupendwa na wengine. Kwa kweli, Biblia inanufaisha kwa njia yenye kutumika na yenye kuridhisha kihisia-moyo.

Kumbuka kwamba Yehova huona yaliyo moyoni mwetu na anajua tunachotafuta. Mungu “huipima mioyo,” naye ‘humpa kila mtu kiasi cha njia zake.’—Mithali 21:2; Yeremia 17:10.

Ushauri Wenye Kutumika Kuhusu Familia

Biblia hutoa ushauri wenye kutumika kwa habari ya mahusiano ya kibinadamu. George asema: “Migongano ya nyutu na kutoelewana ni baadhi ya hali zenye mkazo zaidi maishani.” Anakabilianaje na hali hizo? “Nikihisi kwamba mtu ana jambo fulani dhidi yangu, mimi hutumia ushauri huu ulio wazi wa Mathayo 5:23, 24: ‘Fanya amani yako na ndugu yako.’ Kuzungumzia mgongano huo huwa na matokeo. Ninaweza kuhisi amani ya Mungu ambayo Biblia huzungumzia. Ushauri wa Biblia hutokeza manufaa. Unatumika kwelikweli.”—Wafilipi 4:6, 7.

Mume na mke wanapokosana, wote wawili wanahitaji ‘kuwa wepesi sana juu ya kusikia, wa polepole juu ya kusema, wa polepole juu ya hasira ya kisasi.’ (Yakobo 1:19) Ushauri huo huboresha mawasiliano. George aongeza kusema: “Ninapotumia ushauri wa kumpenda na kumtendea mke wangu kama ninavyojitendea mwenyewe, ninapata matokeo papo hapo. Inakuwa rahisi zaidi kwake kuniheshimu.” (Waefeso 5:28-33) Naam, Biblia hutufundisha jinsi ya kukubali na kushughulika na hali yetu wenyewe ya kutokamilika na jinsi ya kukabiliana kwa mafanikio na hali ya wengine ya kutokamilika.

Ushauri Unaodumu

Mfalme Solomoni mwenye hekima alisema: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:5, 6) Ni maneno sahili, lakini yenye maana kubwa kama nini!

Biblia ni nguvu inayoleta mafanikio. Huwawezesha wanaompenda Mungu waishi kulingana na mapenzi yake na kufurahia ‘kwenda katika sheria ya BWANA.’ (Zaburi 119:1) Hata hali zetu ziweje, Biblia ina mwelekezo na ushauri tunaohitaji. (Isaya 48:17, 18) Isome kila siku, tafakari unayosoma, na kuyatumia. Itafanya akili yako iwe safi na iweze kufikiria mambo ambayo ni safi na yafaayo. (Wafilipi 4:8, 9) Utajifunza jinsi ya kuishi na kufurahia maisha na pia jinsi ya kumpenda Muumba wa uhai.

Kwa kufuata mwenendo huo, Biblia itakuwa kwako—kama ambavyo imekuwa kwa mamilioni wengine—zaidi ya kitabu kizuri tu. Kwa kweli itakuwa kitabu cha kukuongoza maishani!

[Picha katika ukurasa wa 6]

Biblia yaweza kuimarisha azimio lako la kushinda mazoea yenye kudhuru

[Picha katika ukurasa wa 7]

Biblia hukufunza jinsi ya kumkaribia Mungu