Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Hamjui Uhai Wenu Utakuwa Nini Kesho”

“Hamjui Uhai Wenu Utakuwa Nini Kesho”

Simulizi la Maisha

“Hamjui Uhai Wenu Utakuwa Nini Kesho”

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA HERBERT JENNINGS

“Nilikuwa ninarudi kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower Society huko Ghana nikitoka katika mji wenye bandari wa Tema niliposimamisha gari kumbeba kijana mmoja aliyekuwa anaomba lifti kwenda mjini. Nilitumia nafasi hiyo kumhubiria. Nilidhani nilikuwa ninamtolea ushahidi mzuri! Lakini tulipofika mahali huyo kijana alikuwa anaenda, aliruka kutoka garini na kukimbia.”

TUKIO ambalo nimetaja lilinidokezea kwamba nilikuwa nimeanza kupatwa na hali fulani isiyo ya kawaida. Kabla ya kusimulia yaliyotokea, acheni niwaambie jinsi mimi, Mkanada, nilivyokuja kuwa nchini Ghana.

Ilikuwa katikati ya Desemba 1949 katika kitongoji kimoja cha kaskazini mwa Toronto, Kanada. Tulikuwa tu tumemaliza kuchimba urefu upatao meta moja kwenye ardhi iliyoganda ili kupeleka maji katika nyumba mpya. Tukiwa tumechoka na tunahisi baridi, mimi na wafanyakazi wenzangu tuliketi tumesongamana kuzunguka moto wa kuni, tukingojea gari la kutubeba. Mara, Arnold Lorton, mmoja wa wafanyakazi, akaanza kusema jambo fulani kuhusu “vita na uvumi wa vita,” “mwisho wa dunia hii,” na kutumia semi nyingine ambazo sikuzifahamu kabisa. Watu wote wakanyamaza, wakaaibika, na hata wengine wakawa na uhasama kumwelekea. Ninakumbuka nikiwaza, ‘Mtu huyu ana ujasiri mwingi! Hakuna anayetaka kusikiliza, na bado anaendelea kuzungumza.’ Lakini nilivutiwa na yale aliyokuwa anasema. Ilikuwa miaka michache tu baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, na sikuwa nimewahi kusikia mambo kama hayo katika dini ya Christadelphia ambayo familia yetu ilikuwa imeshirikiana nayo kwa vizazi kadhaa. Nilisikiliza kwa makini sana maelezo yake.

Baada ya muda mfupi nilimwendea Arnold ili kupata habari zaidi. Nikumbukapo wakati huo, ninatambua jinsi yeye na mke wake, Jean, walivyonivumilia na kunionyesha fadhili, nikiwa kijana mwenye umri wa miaka 19 asiye na ujuzi. Mara nyingi nilienda nyumbani kwao kuongea nao bila kuwajulisha mapema na bila kualikwa. Walirekebisha mawazo yangu na kunisaidia kupambanua maoni yenye kutatanisha niliyokuwa nayo katika akili yangu changa kuhusu viwango na maadili. Miezi kumi baada ya mazungumzo hayo tuliyokuwa nayo tulipokuwa tunaota moto kando ya barabara Oktoba 22, 1950, nilibatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na kuanza kushirikiana na Kutaniko la Willowdale, North York, ambayo sasa ni sehemu ya Toronto.

Kusonga Mbele na Waabudu Wenzangu

Maisha nyumbani yalizidi kuwa yenye mgogoro baba alipofahamu kwamba nilikuwa nimeazimia kushikilia imani yangu mpya. Baba alikuwa mhasiriwa wa aksidenti ya karibuni ya uso kwa uso iliyosababishwa na dereva mlevi, na hivyo mara nyingi ilikuwa vigumu kushughulika naye. Maisha yalikuwa magumu kwa Mama, ndugu zangu wawili, na dada zangu wawili. Upinzani dhidi ya kweli ya Biblia uliongezeka. Kwa hiyo nikaona ni jambo la busara kuondoka nyumbani ili niwe na amani na wazazi wangu na kujiimarisha katika “njia ya kweli.”—2 Petro 2:2.

Mwishoni mwa kiangazi cha 1951, nilijiunga na kutaniko dogo la Coleman, Alberta. Katika kutaniko hilo kulikuwa na vijana wawili, Ross Hunt na Keith Robbins, ambao walikuwa na kazi nyingi ya kuhubiri hadharani wakati wote, iitwayo upainia wa kawaida. Walinisaidia kujiunga na huduma hiyohiyo ya kujitolea. Machi 1, 1952 nikawa mhudumu painia wa kawaida.

Ninakumbuka kwa shauku kitia-moyo nilichopokea. Nilikuwa na mengi sana ya kujifunza na hapa ndipo ningethibitisha uwezo wangu. Baadaye, baada ya kufanya utumishi wa painia kwa muda wa mwaka mmoja pamoja na Kutaniko la Lethbridge, Alberta, nilipokea mwaliko nisiotazamia wa kutumikia nikiwa mwangalizi asafiriye. Nilikuwa nitumikie makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yaliyotawanyika kandokando ya pwani ya mashariki ya Kanada toka Moncton, New Brunswick, hadi Gaspé, Quebec.

Nilikuwa na umri wa miaka 24 tu na mpya katika kweli, hivyo nikahisi sifai, hasa nikilinganishwa na Mashahidi wakomavu ambao ningetumikia. Nilijitahidi vilivyo katika miezi kadhaa iliyofuata. Kisha nikapokea mwaliko mwingine nisiotazamia.

Shule ya Gileadi na Kwenda Gold Coast

Mnamo Septemba 1955, nilialikwa kujiunga na wanafunzi wengine wapatao mia moja katika darasa la 26 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower huko South Lansing, New York. Mazoezi na mafunzo mazito ya miezi mitano yangenifaa sana. Shauku yangu iliimarishwa kwa kuwa pamoja na kikundi hicho chenye bidii nyingi. Wakati huo, kuna jambo jingine lililotokea ambalo limeboresha maisha yangu hadi leo.

Kulikuwa na dada fulani kijana, Aileen Stubbs, miongoni mwa wanafunzi waliokuwa wakijitayarisha kwa ajili ya kazi ya mishonari. Nilimwona Aileen kuwa mtu thabiti, asiyependa upuuzi, mwenye busara, kiasi, na furaha. Nadhani nilimshtua nilipomjulisha kwa haya kwamba nilitaka kumwoa. Lakini hakukataa! Mimi na Aileen tuliafikiana kwamba yeye aende kwa mgawo wake wa mishonari huko Kosta Rika nami niende Gold Coast (ambayo sasa ni Ghana), Afrika Magharibi.

Asubuhi moja mnamo Mei 1956, nilijikuta katika ofisi ya Ndugu Nathan Knorr kwenye orofa ya kumi huko Brooklyn, New York. Wakati huo alikuwa msimamizi wa Watch Tower Society. Nilikuwa ninapewa mgawo wa kuwa mtumishi wa ofisi ya tawi ili kusimamia kazi ya kuhubiri huko Gold Coast, Togoland (ambayo sasa ni Togo), Ivory Coast (ambayo sasa ni Côte d’Ivoire), Upper Volta (ambayo sasa ni Burkina Faso), na Gambia.

Ninakumbuka maneno ya Ndugu Knorr kana kwamba yalisemwa jana tu. “Si lazima uanze kazi mara moja,” akasema. “Usiwe na haraka; jifunze kutokana na ndugu wa huko wenye ujuzi. Kisha ukiwa tayari, unapaswa kuanza kutumikia ukiwa mtumishi wa ofisi ya tawi. . . . Barua ya kukuweka rasmi kuwa mtumishi ndiyo hii. Unapaswa kuchukua usimamizi siku saba baada ya kufika huko.”

‘Siku saba tu,’ nikawaza. ‘Namna gani ule ushauri“usiwe na haraka”?’ Nilitoka kwenye mahojiano hayo nikiwa nimeduwaa.

Siku zilizofuata zilipita haraka sana. Muda si muda nilikuwa nimesimama kwenye kitalu cha meli, nikisafiri kwenye Mto wa East huku nikiacha nyuma ofisi za Society za Brooklyn na kuanza safari ya baharini ya siku 21 kwenda Gold Coast.

Mimi na Aileen tuliandikiana barua nyingi sana. Tulikutana tena mwaka wa 1958 na tukaoana Agosti 23 mwaka huo. Ninamshukuru Yehova sikuzote kwa ajili ya mwenzi mzuri kama Aileen.

Kwa miaka 19 nilithamini pendeleo la kutumikia pamoja na mishonari wenzangu na ndugu na dada zangu Waafrika kwenye ofisi ya tawi ya Society. Familia ya Betheli ilikua kutoka watu wachache tu hadi kufikia watu 25 wakati huo. Hizo zilikuwa siku zenye magumu, zenye matukio mengi, na zenye manufaa kwetu. Ingawa hivyo, ni lazima niseme mambo wazi. Tabia ya nchi yenye joto na unyevunyevu ilinitatiza sana. Nilikuwa natokwa na jasho wakati wote, mwenye kunata daima, na nyakati nyingine, mwenye kuudhika upesi. Hata hivyo, nilifurahia sana kutumikia, kwa kuwa idadi yetu nchini Ghana ilikua kutoka wahubiri wa Ufalme 6,000 tu mwaka 1956 hadi 21,000 mwaka wa 1975. Na inafurahisha sana kuona Mashahidi zaidi ya 60,000 wenye shughuli nyingi huko leo.

“Kesho” Ambayo Hatukuitazamia

Wapata mwaka wa 1970, nilipatwa na tatizo la kiafya lililokuwa gumu kujulikana. Nilifanyiwa uchunguzi kamili wa kitiba na kuambiwa kwamba nilikuwa “na afya nzuri.” Lakini ni kwa nini nilihisi kuwa mgonjwa hivyo, mwenye kuchoka, na nisiyetulia? Maswali hayo yalijibiwa kupitia mambo mawili yenye kushtua. Kwa kweli, kama Yakobo alivyoandika: ‘Hujui uhai wako utakuwa nini kesho.’—Yakobo 4:14.

Dalili ya kwanza niliitambua wakati nilipomtolea ushahidi yule kijana niliyempa lifti kwenda mjini. Sikujua kwamba nilikuwa ninapayuka-payuka, nikiongea haraka sana na kwa mkazo mwingi. Tulipofika mahali kijana huyo alipokuwa anaenda, nilishtuka aliporuka kutoka garini na kukimbia. Kiasili, Waghana wengi ni watulivu, watu ambao hawaudhiki upesi. Alitenda kinyume cha ilivyo kawaida. Niliketi hapo nikitafakari. Nilitambua nilikuwa na tatizo. Sikujua hasa nilikuwa na tatizo la aina gani. Lakini kwa hakika nilikuwa na tatizo.

Pili, baada ya kufikiria mambo kwa uzito, Aileen alipendekeza: “Ikiwa tatizo hili si la kimwili, basi ni la kiakili.” Kwa hiyo niliandika dalili zote na kwenda kwa daktari wa magonjwa ya akili. Nilipomsomea orodha yangu, alijibu: “Dalili hizo zaonyesha wazi ugonjwa wako. Una ugonjwa wa manic-depressive (ugonjwa wa akili wa kushuka moyo na kusisimka-sisimka ghafula).”

Niliduwaa! Hali yangu ilizidi kudhoofika huku nikipambana na hali hii miaka kadhaa iliyofuata. Niliendelea kutafuta suluhisho la tatizo hilo. Lakini hakuna aliyejua la kufanya. Ilikuwa jitihada yenye kuvunja moyo kama nini!

Sikuzote tulinuia kuendelea na pendeleo la utumishi wa wakati wote ukiwa kazi yetu maishani, na kulikuwa na mengi yaliyohitaji kufanywa. Nilisali kwa moyo na kwa bidii hivi: “Yehova ukipenda, ‘nitaishi na pia kufanya hili au lile.’” (Yakobo 4:15) Lakini haikuwezekana. Kwa hiyo, kwa kukubali hali ilivyokuwa, tulipanga kuondoka Ghana na kuacha rafiki zetu wengi wa karibu na kurudi Kanada mnamo Juni mwaka wa 1975.

Yehova Hutoa Msaada Kupitia Watu Wake

Muda si muda nikajua kwamba kazi ingeendelea bila mimi kuwepo na kwamba tatizo langu halikuwa la pekee. Maneno ya 1 Petro 5:9 yakawa na maana kwangu: “[Jua] kwamba mambo yaleyale kwa njia ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zenu katika ulimwengu.” Nilipoelewa maana ya andiko hilo, nilianza kutambua hasa jinsi Yehova alivyotutegemeza sote wawili licha ya badiliko hilo lisilopendeza. ‘Ushirika wa ndugu’ ulitusaidia kwa njia nyingi nzuri kama nini!

Ingawa hatukuwa na vitu vingi vya kimwili, Yehova hakutuacha. Alichochea rafiki zetu huko Ghana watusaidie kimwili na vinginevyo. Tukiwa na shaka nyingi, tuliwaacha watu tuliopenda sana, tukaanza kushughulika na “kesho” hii ambayo haikutazamiwa.

Tulikaribishwa kwa fadhili na Lenora, dada yake Aileen, pamoja na mume wake Alvin Friesen, ambao kwa ukarimu walituruzuku kwa miezi kadhaa. Daktari maarufu wa magonjwa ya akili alibashiri kwa hakika hivi: “Utapona katika muda wa miezi sita.” Labda alisema hivyo ili kunitumainisha, lakini ubashiri huo haukutimia hata baada ya miaka sita. Hadi leo, ninavumilia kile ambacho huitwa kiheshima tu ugonjwa wa kubadilika-badilika kwa hisia. Bila shaka hilo ni jina la fadhili, lakini kama vile wale walio na ugonjwa huo wanavyojua, jina la fadhili halipunguzi hata kidogo hali mbaya ya ugonjwa huo.

Kufikia wakati huo, Ndugu Knorr alikuwa tayari anaugua ugonjwa ambao mwishowe ulisababisha kifo chake mnamo Juni mwaka wa 1977. Hata hivyo, alipata wakati na nguvu za kuniandikia barua ndefu, zenye kutia moyo, kufariji na kushauri. Bado ninazithamini sana barua hizo. Maneno yake yalisaidia sana kutuliza hali isiyofaa ya kuhisi kuwa nimeshindwa iliyokuwa ikinipata mara kwa mara.

Mwishoni mwa mwaka wa 1975, tulilazimika kuacha utumishi wetu wa wakati wote wenye thamani na kuzingatia kuboresha afya yangu. Nuru ya kawaida ya mchana iliniumiza macho. Sauti kali za ghafula zilivuma kama mlio wa bunduki. Mmiminiko wa watu ulinitia wasiwasi. Nilihitaji kujikakamua sana kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Hata hivyo, nilijua kabisa manufaa ya ushirika wa kiroho. Ili kukabiliana na hali hiyo, nilikuwa ninaingia katika Jumba la Ufalme baada ya watu kuketi na kutulia kisha kuondoka muda mfupi tu kabla hawajaanza kuondoka baada ya programu.

Ilikuwa vigumu sana kushiriki katika huduma ya hadharani. Mara nyingine, singeweza hata kupiga kengele ya mlango hata baada ya kufika kwenye nyumba. Hata hivyo, niliendelea kuhubiri kwa sababu niling’amua kwamba huduma yetu yamaanisha wokovu kwetu wenyewe na kwa yeyote anayeitikia ifaavyo. (1 Timotheo 4:16) Baada ya muda mfupi, ningeweza kudhibiti hisia zangu, kwenda kwenye mlango mwingine, na kujaribu tena kupiga kengele. Kwa kuendelea kushiriki katika huduma, nilidumisha afya ya kiroho ifaayo nayo ikaongeza uwezo wangu wa kuvumilia.

Kwa sababu ya hali ya kudumu ya kubadilika-badilika kwa hisia, nimekuja kung’amua kwamba ugonjwa huo yaelekea sana utaniathiri kwa maisha yangu yote katika mfumo huu wa mambo. Katika mwaka wa 1981 mfululizo wa makala bora ulitokea katika Amkeni! * Kupitia makala hayo, nilianza kuuelewa vema zaidi ugonjwa huu na kujifunza njia zenye matokeo zaidi za kukabiliana nao.

Kujifunza Kuvumilia

Katika hayo yote, mke wangu amejidhabihu na kufanya marekebisho. Ikiwa unatunza mtu mwenye ugonjwa kama wangu, bila shaka utaelewa maoni yake:

“Hali ya kubadilika-badilika kwa hisia yaelekea huleta mabadiliko ya ghafula katika utu wa mtu. Katika muda wa saa chache, mgonjwa anaweza kubadilika akaacha kuwa mwenye msisimko, mwenye kutia moyo na mwenye mipango na mawazo mapya, akawa mchovu, mwenye mawazo yasiyofaa, hata mwenye hasira. Ikiwa hautambuliwi kuwa ugonjwa, unaweza kufanya wengine waudhike na kushangaa. Ni wazi kwamba mipango yapaswa kubadilishwa haraka, na pambano la kibinafsi dhidi ya hisia za kukata tamaa au kukataliwa huanza.”

Ninapohisi ni mzima isivyo kawaida, mimi huwa na wasiwasi. Hujua kisilika kwamba kipindi cha “msisimko” hufuatwa na kipindi cha “kushuka moyo.” Mimi napendelea kipindi cha “kushuka moyo” kwa sababu kipindi hiki hunifanya nisiweze kufanya lolote kwa siku kadhaa, na sielekei kujihusisha na lolote lisilofaa. Aileen hunisaidia sana kwa kunionya ninaposisimka kupita kiasi na kunitegemeza ninaposhuka moyo.

Ugonjwa unapofikia kilele, kuna hatari ya kuzama katika mawazo bila kujali wengine. Mtu anaweza kujitenga na wengine kabisa anaposhuka moyo au akashindwa kufahamu hisia na jinsi wengine wanavyotenda wakati wa kipindi cha msisimko. Wakati uliopita, ilikuwa vigumu kwangu kukubali uthibitisho kwamba nilikuwa na tatizo la kiakili na kihisia-moyo. Nimelazimika kupambana na mawazo kwamba mtu mwingine au mradi ambao haukufaulu, ndio kisababishi cha tatizo hilo wala si mimi mwenyewe. Mara kwa mara, nimelazimika kujikumbusha kwamba, ‘Hakuna chochote ambacho kimebadilika. Tatizo ni langu mwenyewe, halisababishwi na kitu kingine.’ Polepole, mawazo yangu yamerekebika.

Kwa miaka ambayo imepita, sote wawili tumejifunza kuwa wazi na wanyofu, kati yetu wenyewe na pia kwa wengine, kuhusu ugonjwa wangu. Sisi hujitahidi sana kudumisha mtazamo mwema na kutoruhusu ugonjwa utawale maisha yetu.

Kesho” Iliyo Bora

Kupitia sala za bidii na jitihada nyingi, tumenufaika na baraka na utegemezo wa Yehova. Sote wawili tumezeeka sasa. Ninaangaliwa daima na daktari na ninatumia dawa kwa kiasi na kwa ukawaida, na afya yangu si mbaya sana. Tunathamini mapendeleo yoyote ya utumishi tuwezayo kupata. Ninaendelea kutumikia nikiwa mzee wa kutaniko. Sikuzote sisi hujaribu kuwaunga wengine mkono katika imani.

Ni kweli vile andiko la Yakobo 4:14 lisemavyo: “Hamjui uhai wenu utakuwa nini kesho.” Hali hiyo itakuwa hivyo maadamu mfumo huu wa mambo unaendelea kuwako. Hata hivyo, maneno ya Yakobo 1:12 ni ya kweli: “Mwenye furaha ni mtu afulizaye kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uhai, ambalo [Yehova] aliahidi wale waendeleao kumpenda.” Sote na tusimame imara leo na kutambua baraka ambazo Yehova atatutolea kesho.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 35 Ona makala “Unaweza Kukabiliana na Maisha,” katika toleo la Amkeni! la Agosti 8, 1981, (la Kiingereza); “Jinsi Uwezavyo Kupambana na Mshuko-Moyo,” katika toleo la Septemba 8, 1981, (la Kiingereza); na “Kupambana na Mshuko-Moyo Mkubwa,” katika toleo la Oktoba 22, 1981, (la Kiingereza).

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikitafuta faragha katika chumba changu cha sanaa

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na mke wangu Aileen

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kwenye Kusanyiko la “Habari Njema za Milele,” lililofanywa huko Tema, Ghana, mwaka wa 1963