Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Lazima Uamini?

Je, Ni Lazima Uamini?

Je, Ni Lazima Uamini?

MWANAFUNZI mwenye umri wa miaka 12 alikuwa anang’ang’ana kuelewa kanuni za msingi za aljebra. Mwalimu wake alionyesha darasa hesabu rahisi ya aljebra.

“Acheni x=y na acheni zote mbili ziwe sawa na 1,” akaanza.

‘Mambo yanaonekana kuwa sawa,’ mwanafunzi huyo akawaza.

Hata hivyo, baada ya mistari minne ya ule ulioonekana kuwa upigaji hesabu unaopatana na akili, mwalimu alipata matokeo yenye kushtua: “Hivyo, 2=1!”

“Pingeni matokeo hayo,” akawatolea mwito wa ushindani wanafunzi wake waliotatanika.

Kwa kuwa alikuwa na ujuzi kidogo sana wa aljebra, mwanafunzi huyo mchanga hakuona jinsi angeweza kupinga matokeo hayo. Kila hatua katika upigaji hesabu ilionekana sawa kabisa. Basi, je, yampasa kuamini matokeo hayo ya ajabu? Mwalimu wake alijua hesabu zaidi kuliko yeye. Bila shaka, haimpasi kuamini! ‘Si lazima nipinge matokeo haya,’ akawaza. ‘Maarifa ya kawaida yanionyesha kwamba huu ni upumbavu.’ (Mithali 14:15, 18) Alijua kwamba wala mwalimu wake wala wanadarasa wenzake hawangeweza kubadilisha dola mbili kwa moja!

Baadaye mwanafunzi huyo wa aljebra alipata kasoro ya hesabu hiyo. Wakati huohuo, jambo hilo lilimfundisha somo la maana. Hata wakati mtu mwenye ujuzi mwingi wa hali ya juu anapoleta hoja iliyotungwa kwa hila sana, ambayo yaonekana ngumu, haimpasi yule anayemsikiliza kuamini uamuzi wa kipumbavu kwa sababu tu hawezi kuipinga hoja hiyo wakati huo. Kwa kweli mwanafunzi huyo alikuwa akifuata kanuni ya Biblia yenye kutumika ipatikanayo kwenye 1 Yohana 4:1—inayosema kwamba usiamini haraka mno kila jambo usikialo, hata linapoonekana kuwa latoka kwa mtu mwenye mamlaka.

Hiyo haimaanishi kwamba ni lazima ushikilie kwa ushupavu maoni yako ya awali. Ni kosa kupuuza habari ambazo zaweza kurekebisha maoni yenye makosa. Lakini haikupasi ‘kutikiswa upesi kutoka kwenye kufikiri kwako’ unapokabiliwa na mkazo kutoka kwa mtu anayedai kuwa na ujuzi mkubwa au mamlaka. (2 Wathesalonike 2:2) Bila shaka mwalimu huyo alikuwa tu anawatania wanafunzi wake. Ingawa hivyo, mara nyingine hali zinakuwa zenye madhara. Watu wanaweza kuwa ‘wajanja sana katika kutunga kosa.’—Waefeso 4:14; 2 Timotheo 2:14, 23, 24.

Je, Wataalamu Huwa Sahihi Sikuzote?

Hata wawe na ujuzi kadiri gani, wataalamu katika uwanja wowote ule wanaweza kuwa na mawazo yenye kutofautiana na maoni yenye kubadilika-badilika. Kwa mfano, fikiria majadiliano yanayoendelea katika sayansi ya kitiba juu ya jambo la msingi kama vile visababishi vya magonjwa. “Umuhimu wa maumbile yanapolinganishwa na malezi ndiyo mambo yanayosababisha majadiliano makali kati ya wanasayansi kwa habari ya ugonjwa,” aandika profesa wa kitiba wa Chuo Kikuu cha Harvard. Wanasayansi wa kikundi cha determinist (wanaoshikilia dhana kwamba matukio na matendo yote ya wanadamu husababishwa na mambo yasiyoweza kudhibitiwa), wanaamini kwa dhati kwamba chembe zetu za urithi zinahusika sana katika kushikwa na magonjwa mbalimbali. Hata hivyo, wengine wanabisha kwamba mazingira na mtindo wa maisha ndizo sababu kuu za kushikwa na magonjwa. Vikundi vyote viwili hutetea hoja zao kwa kurejezea uchunguzi na takwimu. Hata hivyo, majadiliano hayo yanaendelea.

Watu wenye akili walio maarufu wamethibitishwa tena na tena kuwa wenye makosa, hata ingawa waliyofundisha yalionekana kuwa yasiyoweza kupingwa wakati huo. Mwanafalsafa Bertrand Russell alimtaja Aristotle kuwa “mwanafalsafa mwenye uvutano mkubwa zaidi kuliko wengine wote.” Lakini Russell pia alitaja kwamba, kwa jumla mafundisho mengi ya Aristotle yalikuwa “uwongo mtupu.” “Katika kipindi chote cha wakati wa sasa,” akaandika, “imebidi kila hatua katika sayansi, katika mantiki, au katika falsafa ipigwe kukiwa na upinzani mkali kutoka kwa wanafunzi wa Aristotle.”—History of Western Philosophy.

‘Ule Wenye Kuitwa “Ujuzi” Isivyo Kweli’

Yaelekea Wakristo wa mapema waliwafahamu wengi wa wanafunzi wa wanafalsafa maarufu wa Kigiriki, kama vile Socrates, Plato, na Aristotle. Watu wenye elimu wa siku hizo walijiona kuwa wana akili nyingi kuliko Wakristo wengi. Ni wanafunzi wachache tu wa Yesu ambao walionwa kuwa “wenye hekima katika njia ya kimwili.” (1 Wakorintho 1:26) Kwa kweli, wale waliofundishwa falsafa za wakati huo walifikiri kwamba yale Wakristo waliyoamini yalikuwa “upumbavu” tu au “upuuzi mtupu.”—1 Wakorintho 1:23; Phillips.

Kama ungalikuwa miongoni mwa Wakristo hao wa mapema, je, ungalivutiwa na hoja za wasomi wa wakati huo au kutishwa na hekima yao? (Wakolosai 2:4) Kulingana na mtume Paulo, hakungalikuwa na sababu ya kufanya hivyo. Aliwakumbusha Wakristo kwamba Yehova huona “hekima ya watu wenye hekima” na “akili ya watu wenye akili” wa wakati wowote ule kuwa upumbavu. (1 Wakorintho 1:19) “Hebu wazia, ni nini ambacho mwanafalsafa, mwandishi na mchambuzi wa ulimwengu huu ametimiza kwa hekima yake yote?” Paulo akauliza. (1 Wakorintho 1:20, Phillips) Wanafalsafa, waandishi na wachambuzi wa wakati wa Paulo hawakuwa wametatua matatizo ya wanadamu licha ya akili yao nyingi.

Kwa hiyo Wakristo walijifunza kuepuka yale ambayo mtume Paulo alisema yalikuwa “mapinganisho yenye kuitwa ‘ujuzi’ isivyo kweli.” (1 Timotheo 6:20) Sababu iliyomfanya Paulo autaje ujuzi huo kuwa ‘usio wa kweli’ ni kwamba, ulikosa jambo moja muhimu—chanzo au marejezo kutoka kwa Mungu ambayo yangetumiwa kuthibitisha dhana zao. (Ayubu 28:12; Mithali 1:7) Kwa kukosa hilo, na wakati uleule kupofushwa na mdanganyi mkuu, Shetani, wale walioshikilia ujuzi huo hawangeweza kamwe kutumaini kupata kweli.—1 Wakorintho 2:6-8, 14; 3:18-20; 2 Wakorintho 4:4; 11:14; Ufunuo 12:9.

Biblia—Mwongozo Uliopuliziwa

Wakristo wa mapema hawakutia shaka kamwe kwamba Mungu alikuwa amefunua mapenzi, kusudi, na kanuni zake katika Maandiko. (2 Timotheo 3:16, 17) Jambo hilo liliwalinda ‘wasichukuliwe kama windo kupitia falsafa na udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu.’ (Wakolosai 2:8) Hali iko hivyo leo. Tofauti na maoni ya wanadamu yenye kutatanisha na yenye kutofautiana, Neno la Mungu lililopuliziwa huandaa msingi imara ambao tunaweza kutegemeza imani yetu. (Yohana 17:17; 1 Wathesalonike 2:13; 2 Petro 1:21) Bila Neno la Mungu tunakuwa katika hali ngumu ya kujaribu kujenga kitu imara juu ya dhana na falsafa za wanadamu zenye kubadilika-badilika.—Mathayo 7:24-27.

‘Lakini kabla hujaendelea,’ huenda mtu fulani akasema. ‘Je, si kweli kwamba mambo ya hakika ya sayansi yameonyesha kwamba Biblia ina makosa na kwa hiyo haiwezi kutegemeka kama vile tu falsafa za wanadamu zenye kubadilika-badilika?’ Kwa mfano, Bertrand Russell alidai kwamba “Copernicus, Kepler, na Galileo walilazimika kukabiliana na Aristotle na vilevile Biblia ili kuthibitisha maoni ya kwamba dunia siyo kitovu cha ulimwengu.” (Italiki ni zetu.) Kwa mfano je, si kweli kwamba leo wale wanaoamini uumbaji husisitiza kwamba Biblia inafundisha kwamba dunia iliumbwa katika siku sita zenye urefu wa saa 24, ilhali mambo ya hakika yanaonyesha kwamba dunia yenyewe imekuwapo kwa mabilioni ya miaka?

Kwa kweli, Biblia haisemi kwamba dunia ndiyo kitovu cha ulimwengu. Hilo lilikuwa fundisho la viongozi wa kanisa ambao hawakushika Neno la Mungu. Simulizi la uumbaji la kitabu cha Mwanzo lakubali kwamba dunia imekuwapo kwa mabilioni ya miaka na halisemi kwamba kila siku ya uumbaji ilikuwa na urefu wa saa 24. (Mwanzo 1:1, 5, 8, 13, 19, 23, 31; 2:3, 4) Ukiichunguza Biblia kwa unyofu utaona kwamba ingawa si kitabu cha sayansi, hiyo bila shaka si “upuuzi mtupu.” Kwa kweli inapatana kabisa na sayansi iliyothibitishwa. *

Zile ‘Nguvu za Kufikiri’

Ingawa wengi wa wanafunzi wa Yesu walikuwa wanaume na wanawake wa kawaida, labda wasio na elimu nyingi, wao walikuwa na kipawa kingine kutoka kwa Mungu. Bila kujali malezi, wote walipewa nguvu na uwezo wa kufikiri. Mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo wenzake watumie kikamili ‘nguvu zao za kufikiri’ ili ‘wapate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.’—Waroma 12:1, 2.

Wakiwa na ‘nguvu za kufikiri’ kutoka kwa Mungu, Wakristo wa mapema walielewa vizuri kwamba falsafa au mafundisho yoyote yasiyopatana na Neno la Mungu lililofunuliwa yalikuwa bure. Hata nyakati nyingine watu wenye hekima wa wakati wao walikuwa ‘wakiikandamiza kweli’ na kupuuza uthibitisho uliokuweko kwamba kuna Mungu. “Ijapokuwa walisisitiza kuwa ni wenye hekima, wakawa wapumbavu,” akaandika mtume Paulo. Kwa sababu walikataa kweli kuhusu Mungu na kusudi lake, “wakawa wenye akili haba katika mawazowazo yao na moyo wao usio na akili ukawa wenye giza.”—Waroma 1:18-22; Yeremia 8:8, 9.

Mara nyingi wale wanaosisitiza kwamba wana hekima hufikia maamuzi kama vile “Hakuna Mungu” au “Biblia haipaswi kutumainiwa” au “Hizi si ‘siku za mwisho.’” Maoni hayo ni ya upumbavu machoni pa Mungu kama vile kuamua kwamba “2=1.” (1 Wakorintho 3:19) Hata watu wajitwike mamlaka ya aina gani, si lazima ukubali maamuzi yao ikiwa yanapingana na ya Mungu, yanapuuza Neno lake, au kupingana na maarifa ya kawaida. Mwishowe, njia ya hekima sikuzote ni ‘kuacha Mungu apate kuonekana kuwa wa kweli, lakini kila binadamu apate kuonekana kuwa mwongo.’—Waroma 3:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Kwa habari zaidi, ona vitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? na Je, Kuna Muumba Anayekujali?, vilivyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Tofauti na maoni ya wanadamu yenye kubadilika-badilika, Biblia huandaa msingi imara wa imani

[Hisani]

Kushoto, Epicurus: Photograph taken by courtesy of the British Museum; juu katikati, Plato: National Archaeological Museum, Athens, Greece; kulia, Socrates: Roma, Musei Capitolini