Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wavipenda Mno Vikumbusha vya Yehova?

Je, Wavipenda Mno Vikumbusha vya Yehova?

Je, Wavipenda Mno Vikumbusha vya Yehova?

“Nafsi yangu imezishika shuhuda [“vikumbusha,” “NW”] zako, nami nazipenda mno.”—ZABURI 119:167.

1. Ni wapi hasa tunapopata vikumbusha vya Yehova vikiwa vimerudiwa-rudiwa?

YEHOVA anataka watu wake wawe na furaha. Bila shaka, ili tuwe na furaha ya kweli, ni lazima tutembee katika sheria ya Mungu na kushika maagizo yake. Ili tuweze kutimiza hilo, anatupa vikumbusha. Vikumbusha hivyo vinatajwa kwa kurudiwa-rudiwa katika Maandiko hasa katika Zaburi 119, ambayo labda ilitungwa na Hezekia, Mwana-mfalme mchanga wa Yuda. Wimbo huo mzuri huanza kwa maneno haya: “Heri walio kamili njia zao, waendao katika sheria ya BWANA. Heri wazitiio shuhuda [“vikumbusha,” NW] zake, wamtafutao kwa moyo wote.”—Zaburi 119:1, 2.

2. Vikumbusha vya Mungu vinahusianaje na furaha?

2 ‘Tunatembea katika sheria ya Yehova’ kwa kutwaa ujuzi sahihi wa Neno lake na kwa kuutumia maishani. Hata hivyo, kwa kuwa sisi sio wakamilifu, twahitaji vikumbusha. Neno la Kiebrania lililotafsiriwa “vikumbusha” laonyesha kwamba Mungu hutukumbusha sheria, maagizo, kanuni, na amri zake. (Mathayo 10:18-20) Tutabaki wenye furaha tukiendelea tu kushika vikumbusha hivyo, kwa kuwa hivyo hutusaidia kuepuka mitego ya kiroho ambayo hutokeza maafa na majonzi.

Shikamana na Vikumbusha vya Yehova

3. Kwa kutegemea Zaburi 119:60, 61, tuna uhakika gani?

3 Mtunga-zaburi alithamini sana vikumbusha vya Mungu na kuimba hivi: “Nalifanya haraka wala sikukawia, kuyatii maagizo yako. Kamba za wasio haki zimenifunga, sikuisahau sheria yako.” (Zaburi 119:60, 61) Vikumbusha vya Yehova hutusaidia kuvumilia mnyanyaso kwa sababu tuna hakika kwamba Baba yetu wa kimbingu anaweza kukata kamba tunazofungwa na maadui wetu ili kutuzuia kutenda. Katika wakati ufaao, yeye hutufungua kutoka kwenye vizuizi hivyo ili tuendelee kuhubiri Ufalme.—Marko 13:10.

4. Tuitikieje vikumbusha vya Mungu?

4 Nyakati nyingine tunarekebishwa na vikumbusha vya Yehova. Sikuzote na tuthamini marekebisho hayo kama alivyofanya mtunga-zaburi. Alimwambia Mungu hivi kupitia sala: “Shuhuda zako nazo ndizo furaha yangu . . . nimezipenda shuhuda [“vikumbusha,” NW] zako.” (Zaburi 119:24, 119) Sisi tuna vikumbusha vingi vya Mungu kuliko mtunga-zaburi. Mamia ya Maandiko ya Kigiriki ambayo yamenukuliwa kutoka katika Maandiko ya Kiebrania hutukumbusha juu ya maagizo ya Yehova kwa watu wake waliokuwa chini ya Sheria na pia makusudi yake kuhusu kutaniko la Kikristo. Mungu aonapo inafaa kutukumbusha mambo yanayohusu sheria zake, tunathamini mwelekezo huo. Na kwa ‘kushikamana na vikumbusha vya Yehova,’ tunaepuka kushawishiwa kufanya dhambi, jambo ambalo humchukiza Muumba wetu na kutukosesha furaha.—Zaburi 119:31.

5. Tutapataje kuvipenda mno vikumbusha vya Yehova?

5 Twapaswa kuvipenda vikumbusha vya Yehova kadiri gani? “Nafsi yangu imezishika shuhuda [“vikumbusha,” NW] zako, nami nazipenda mno,” akaimba mtunga-zaburi. (Zaburi 119:167, italiki ni zetu.) Tutapata kuvipenda mno vikumbusha vya Yehova tukiviona na kuvikubali kama shauri kutoka kwa Baba anayetujali kwelikweli. (1 Petro 5:6, 7) Twahitaji vikumbusha vyake, na tutazidi kuvipenda tunapoona jinsi ambavyo vinatunufaisha.

Kwa Nini Tunahitaji Vikumbusha vya Mungu?

6. Ni ipi mojawapo ya sababu ifanyayo tuhitaji vikumbusha vya Yehova, na ni nini kitakachotusaidia kuvikumbuka?

6 Sababu moja inayofanya tuhitaji vikumbusha vya Yehova ni kwamba sisi ni wasahaulifu. Kichapo The World Book Encyclopedia chasema hivi: “Kwa ujumla, watu husahau zaidi na zaidi kadiri wakati unavyopita. . . . Labda umewahi kujikuta katika hali ambayo umesahau jina au habari fulani ambayo ungeweza kuikumbuka mara moja. . . . Kusahau huko kwa muda mfupi, ambako hutukia mara nyingi, ni kushindwa kukumbuka jambo. Wanasayansi hulinganisha hali hiyo na kule kujaribu kutafuta kitu kilichopotea katika chumba chenye vitu vilivyoachwa ovyoovyo. . . . Njia nzuri ya kuhakikisha unakumbuka habari fulani ni kujifunza juu ya habari hiyo muda mrefu hata baada ya kufikiri kuwa unaifahamu kikamili.” Kujifunza kwa bidii na kurudia kutatusaidia kukumbuka vikumbusha vya Mungu na kuvitii kwa faida yetu wenyewe.

7. Kwa nini vikumbusha vya Mungu vyahitajika leo kuliko wakati mwingine wowote?

7 Tunahitaji vikumbusha vya Yehova leo kuliko wakati mwingine wowote kwa sababu uovu umeongezeka pasipo kifani katika historia ya binadamu. Tukisikiliza vikumbusha vya Mungu, tunapata ufahamu wenye kina tunaohitaji ili kuepuka kushawishiwa katika njia mbovu za ulimwengu. “Ninazo akili kuliko wakufunzi wangu wote,” akasema mtunga-zaburi, “maana shuhuda [“vikumbusha,” NW] zako ndizo nizifikirizo. Ninao ufahamu kuliko wazee, kwa kuwa nimeyashika mausia yako. Nimeiepusha miguu yangu na kila njia mbaya, ili nilitii neno lako.” (Zaburi 119:99-101) Kwa kushika vikumbusha vya Mungu, tutaepuka “kila njia mbaya” na kuepuka kuwa kama wanadamu wengi, ambao wako “katika giza kiakili, na kufanywa wageni kwa uhai ambao ni wa Mungu.”—Waefeso 4:17-19.

8. Tunawezaje kujiandaa vema zaidi ili kukabiliana na majaribu ya imani kwa mafanikio?

8 Vikumbusha vya Mungu vinahitajika pia kwa sababu vinatuimarisha kuvumilia majaribu mengi katika “wakati [huu] wa mwisho.” (Danieli 12:4) Bila vikumbusha hivyo tungekuwa ‘wasikiaji wasahaulifu.’ (Yakobo 1:25) Lakini kujifunza kwa bidii Maandiko kibinafsi na kutanikoni kupitia msaada wa vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” kutatusaidia kukabiliana na majaribu ya imani kwa mafanikio. (Mathayo 24:45-47) Maandalizi hayo ya kiroho hutusaidia kuona yale tunayohitaji kufanya ili kumpendeza Yehova tunapojikuta katika hali zenye majaribu.

Fungu Muhimu Linalotimizwa na Mikutano Yetu

9. Ni nani walio “zawadi zikiwa wanadamu,” nao husaidiaje waamini wenzao?

9 Uhitaji wetu wa vikumbusha vya Mungu hutimizwa kwa njia fulani kwenye mikutano ya Kikristo, ambapo mafundisho hutolewa na akina ndugu waliowekwa rasmi. Mtume Paulo aliandika kwamba wakati Yesu “alipopaa juu alichukua mateka; a[ka]toa zawadi zikiwa wanadamu.” Paulo aliongezea hivi: “[Kristo] alitoa wengine kuwa mitume, wengine kuwa manabii, wengine kuwa waeneza-evanjeli, wengine kuwa wachungaji na walimu, kwa kusudi la kuwarekebisha upya watakatifu, kwa ajili ya kazi ya huduma, kwa ajili ya kuujenga mwili wa Kristo.” (Waefeso 4:8, 11, 12) Twaweza kuwa wenye shukrani kama nini kwamba “zawadi [hizi] zikiwa wanadamu”—wazee waliowekwa rasmi—huelekeza fikira zetu kwenye vikumbusha vya Yehova tunapokutana pamoja ili kuabudu!

10. Jambo kuu katika Waebrania 10:24, 25 ni gani?

10 Kuonyesha shukrani kwa maandalizi haya ya Mungu kutatuchochea kuhudhuria mikutano mitano ya kutaniko kila juma. Paulo alikazia uhitaji wa kukutanika pamoja kwa ukawaida. Aliandika hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali kutiana moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri mwonavyo siku ikikaribia.”—Waebrania 10:24, 25.

11. Tunanufaikaje na kila mmojawapo wa mikutano yetu ya kila juma?

11 Je, unathamini yale ambayo mikutano yetu hutufanyia? Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma huimarisha imani yetu, hutusaidia kuishi kupatana na vikumbusha vya Yehova, na kutuimarisha dhidi ya “roho ya ulimwengu.” (1 Wakorintho 2:12; Matendo 15:31) Kwenye Mkutano wa Watu Wote, wasemaji hufundisha kutoka katika Neno la Mungu, kutia ndani vikumbusha vya Yehova na “semi [nzuri za Yesu] za uhai udumuo milele.” (Yohana 6:68; 7:46; Mathayo 5:1–7:29) Ustadi wetu wa kufundisha huboreshwa kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mkutano wa Utumishi ni wenye manufaa sana katika kutusaidia kuboresha njia ya kuhubiri habari njema nyumba hadi nyumba, kwenye ziara za kurudia, kwenye mafunzo ya Biblia ya nyumbani, na katika njia nyinginezo za huduma yetu. Kwenye kikundi kidogo zaidi cha Funzo la Kitabu la Kutaniko sisi hupata fursa ya kutoa maelezo ambayo mara nyingi huhusisha vikumbusha vya Mungu.

12, 13. Watu wa Mungu katika nchi fulani ya Asia wamedhihirishaje kwamba wanathamini mikutano ya Kikristo?

12 Kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida hutukumbusha amri za Mungu na kutusaidia kuendelea kuwa imara kiroho tunapokabili vita, magumu ya kiuchumi, na majaribu mengine ya imani yetu. Wakristo wapatao 70 katika nchi fulani ya Asia waliona umuhimu wa mikutano wakati walipolazimika kuhama makao yao na kwenda kuishi ndani ya msitu. Wakiwa wameazimia kukutanika pamoja kwa ukawaida, walirudi kwenye mji wao ulioathiriwa na vita, wakabomoa mabaki ya Jumba la Ufalme, na kulijenga upya msituni.

13 Baada ya kuvumilia vita kwa miaka mingi katika eneo jingine la nchi hiyohiyo, watu wa Yehova wangali wanatumikia kwa bidii. Mmoja wa wazee katika eneo hilo aliulizwa hivi: “Ni nini ambacho kimewasaidia sana akina ndugu wakae pamoja?” Alijibuje? “Katika muda wa miaka 19, hatujawahi kukosa mkutano hata mmoja. Nyakati nyingine kwa sababu ya kuangushwa kwa mabomu au magumu mengineyo, baadhi ya akina ndugu hawangeweza kufika mahali pa kufanyia mikutano, lakini hatukutangua hata mkutano mmoja kamwe.” Bila shaka, akina ndugu na dada hawa wapendwa huthamini umuhimu wa ‘kutoachilia mbali kukusanyika pamoja wao wenyewe.’

14. Twaweza kujifunza nini kutokana na desturi ya Ana aliyekuwa mzeemzee?

14 Ana, mjane mwenye umri wa miaka 84, “alikuwa hakosi kamwe kuwa katika hekalu.” Kwa sababu hiyo, Ana alikuwako wakati kitoto kichanga, Yesu, kilipoletwa huko muda mfupi baada ya kuzaliwa. (Luka 2:36-38) Je, umeazimia kutokosa mikutano? Je, unajitahidi kadiri uwezavyo kuhudhuria kila kipindi cha makusanyiko na mikusanyiko yetu? Mafundisho yanayonufaisha kiroho ambayo sisi hupokea kwenye mikutano hiyo hutupa uthibitisho dhahiri kwamba Baba yetu wa kimbingu huwajali watu wake. (Isaya 40:11) Pindi hizo pia huchangia shangwe, na tunapohudhuria twadhihirisha kwamba tunathamini vikumbusha vya Yehova.—Nehemia 8:5-8, 12.

Vikumbusha vya Yehova Hutufanya Tuwe Tofauti

15, 16. Kushika vikumbusha vya Yehova huathirije mwenendo wetu?

15 Kushika vikumbusha vya Mungu husaidia kutufanya tuwe tofauti na ulimwengu huu ulio mwovu. Mathalani, kutii vikumbusha vya Mungu hutuzuia tusijihusishe na ukosefu wa adili katika ngono. (Kumbukumbu la Torati 5:18; Mithali 6:29-35; Waebrania 13:4) Kishawishi cha kusema uwongo, kutokuwa mnyofu, au kuiba chaweza kushindwa kwa mafanikio kwa kujipatanisha na vikumbusha vya Mungu. (Kutoka 20:15, 16; Mambo ya Walawi 19:11; Mithali 30:7-9; Waefeso 4:25, 28; Waebrania 13:18) Kushika vikumbusha vya Yehova hutusaidia pia tusilipize kisasi, tusiwe na kinyongo, au kuchongea yeyote.—Mambo ya Walawi 19:16, 18; Zaburi 15:1, 3.

16 Tunapotii vikumbusha vya Mungu, tunabaki tukiwa tumetakaswa, au tukiwa tumetengwa kwa ajili ya utumishi wake. Na ni jambo muhimu kama nini kuwa tofauti na ulimwengu huu! Alipokuwa akisali kwa Yehova usiku wa mwisho wa maisha yake ya kidunia, Yesu aliomba hivi kwa ajili ya wafuasi wake: “Nimewapa wao neno lako, lakini ulimwengu umewachukia, kwa sababu wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu. Nakuomba wewe, si uwachukue kutoka ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu. Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu. Watakase kwa njia ya ile kweli; neno lako ni kweli.” (Yohana 17:14-17) Acheni tuendelee kuthamini Neno la Mungu, ambalo hututenga kwa ajili ya utumishi wake mtakatifu.

17. Ni nini kinachoweza kutukia tukipuuza vikumbusha vya Mungu, kwa hiyo twapaswa kufanya nini?

17 Tukiwa watumishi wa Yehova, twataka kuendelea kukubalika kwa ajili ya utumishi wake. Hata hivyo, tukipuuza vikumbusha vya Mungu, twaweza kushindwa na roho ya ulimwengu huu, ambayo huendelezwa kupitia usemi, vichapo, vitumbuizo, na maadili yake. Nasi bila shaka hatungependa kuwa wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, wakali, wenye vichwa vigumu, wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kumpenda-Mungu—kwa kutaja tabia chache tu ambazo zinadhihirishwa na wale waliotengwa na Mungu. (2 Timotheo 3:1-5) Kwa kuwa tunaishi katika umalizio wa siku za mwisho za mfumo huu mwovu wa mambo, acheni tuzidi kusali ili kupata msaada wa Yehova kusudi tuendelee kushika vikumbusha vyake na hivyo ‘kutii na kulifuata neno lake.’—Zaburi 119:9.

18. Kushika vikumbusha vya Mungu kutafanya tuchukue hatua gani zinazofaa?

18 Vikumbusha vya Yehova hutimiza mengi kuliko kututahadharisha tu kuhusu mambo tusiyopaswa kufanya. Kushika vikumbusha vyake kutafanya tuchukue hatua inayofaa, tukichochewa kumwitibari Yehova kabisa na kumpenda kwa moyo wetu wote, nafsi, akili, na nguvu. (Kumbukumbu la Torati 6:5; Zaburi 4:5; Mithali 3:5, 6; Mathayo 22:37; Marko 12:30) Vikumbusha vya Yehova hutuchochea pia tupende jirani yetu. (Mambo ya Walawi 19:18; Mathayo 22:39) Tunaonyesha kuwa twampenda Mungu na jirani hasa tunapofanya mapenzi ya Mungu na kushiriki na wengine “ujuzi juu ya Mungu” unaotoa uhai.—Mithali 2:1-5, NW.

Kushika Vikumbusha vya Yehova Humaanisha Uhai!

19. Tunaweza kuonyeshaje wengine kwamba inafaa na inanufaisha kutii vikumbusha vya Yehova?

19 Tukishika vikumbusha vya Yehova na kusaidia wengine wafanye hivyo, tutajiokoa wenyewe na wale watusikilizao pia. (1 Timotheo 4:16) Tunaweza kuonyeshaje wengine kwamba kutii vikumbusha vya Yehova ni jambo lifaalo na linalonufaisha kwelikweli? Kwa kutumia kanuni za Biblia maishani mwetu. Wale walio na “mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele” wataona uthibitisho kwamba mwenendo unaoonyeshwa katika Neno la Mungu ndio bora kabisa kufuatia. (Matendo 13:48) Pia wataona kwamba ‘Mungu kwa kweli yumo miongoni mwetu’ na watachochewa kujiunga nasi kumwabudu Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.—1 Wakorintho 14:24, 25.

20, 21. Vikumbusha vya Mungu na roho yake itatuwezesha kufanya nini?

20 Kwa kuendelea kujifunza Maandiko, kutumia yale tunayojifunza, na kutumia kikamili maandalizi ya kiroho ya Yehova, tutapata kuvipenda mno vikumbusha vyake. Tukitii vikumbusha hivyo, vitatusaidia kuvaa “utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.” (Waefeso 4:20-24) Vikumbusha vya Yehova na roho yake takatifu itatuwezesha kudhihirisha upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti—sifa zinazotofautiana kabisa na tabia za ulimwengu unaotawaliwa na Shetani! (Wagalatia 5:22, 23; 1 Yohana 5:19) Kwa hiyo, tunaweza kushukuru tunapokumbushwa juu ya matakwa ya Yehova wakati wa funzo la kibinafsi la Biblia, na wazee waliowekwa rasmi, na kwenye mikutano, makusanyiko, na mikusanyiko yetu.

21 Kwa sababu tunashika vikumbusha vya Yehova, tunaweza kushangilia hata wakati tunapoteswa kwa ajili ya uadilifu. (Luka 6:22, 23) Tunamtegemea Mungu atuokoe kutoka katika hali zenye kutisha zaidi. Jambo hilo ni la maana sasa, hasa kwa sababu mataifa yote yanakusanywa kwa ajili ya “vita ya siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote” kwenye Har–Magedoni.—Ufunuo 16:14-16.

22. Azimio letu lapasa kuwa nini kuhusu vikumbusha vya Yehova?

22 Ikiwa tutapokea zawadi isiyostahiliwa ya uhai udumuo milele, lazima tuvipende mno vikumbusha vya Yehova na kuvishika kwa moyo wote. Kwa hiyo na tuwe na mtazamo kama wa mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Haki ya shuhuda [“vikumbusha,” NW] zako ni ya milele, unifahamishe, nami nitaishi.” (Zaburi 119:144) Na tuonyeshe azimio lililo wazi katika maneno ya mtunga-zaburi: “Nimekuita wewe, [Yehova] uniokoe, nami nitazishika shuhuda [“vikumbusha,” NW] zako.” (Zaburi 119:146) Naam, acheni tuonyeshe kwa maneno na kwa matendo kwamba kwa kweli tunavipenda mno vikumbusha vya Yehova.

Ungejibuje?

• Mtunga-zaburi alivionaje vikumbusha vya Yehova?

• Kwa nini tunahitaji vikumbusha vya Mungu?

• Mikutano yetu hutimiza fungu gani kuhusiana na vikumbusha vya Mungu?

• Vikumbusha vya Yehova hutufanya tuwe tofauti na ulimwengu huu jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mtunga-zaburi alivipenda mno vikumbusha vya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Kwa kufuata kielelezo cha Ana, je, umeazimia kutokosa mikutano?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kutii vikumbusha vya Yehova hututenga tukiwa watu safi na wanaokubalika kwa ajili ya utumishi wake