Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Unavyoweza Kupata Marafiki

Jinsi Unavyoweza Kupata Marafiki

Jinsi Unavyoweza Kupata Marafiki

“KUWA NA RAFIKI MMOJA MAISHANI NI JAMBO LINALOVUTIA; WAWILI NI WENGI; WATATU NI NADRA SANA.”—Henry Brooks Adams.

MANENO hayo yanadokeza kwamba ni nadra kuwa na marafiki wa kweli. Mara nyingi watu walio wapweke sana na wanaotafuta urafiki, wamesikika wakisema “sina mtu wa kumkimbilia,” “siwezi kumwamini yeyote,” au “mbwa wangu ndiye rafiki yangu aliye bora zaidi.”

Ni vigumu kuanzisha na kudumisha urafiki. Uchunguzi uliofanyiwa wanunuzi fulani ulifunua kwamba “nchini Marekani, asilimia 25 ya watu wazima wana ‘upweke wa kudumu’ na . . . katika Ufaransa nusu ya watu wamewahi kupatwa na upweke mwingi sana.” Kuenea kwa vikundi vya watu wanaotafuta urafiki na watu wa jinsia tofauti na vituo vya kupiga gumzo katika kompyuta na matangazo mengi sana magazetini ya watu wanaotafuta marafiki kwaonyesha kwamba watu wanatamani sana kupata marafiki.

Upweke huathiri akili ya mtu na pia afya yake ya kimwili, adai Dakt. David Weeks, mtaalamu wa mfumo wa neva na ubongo. “Nina wagonjwa wengi sana walioshuka moyo na walio na woga unaosababishwa na wasiwasi, ambao yaweza kusemwa ni wapweke. Kuna uhusiano kati ya kushuka moyo sana na kuwa mpweke sana.”

Talaka na kuvunjika kwa familia hufanya watu wengi zaidi waishi peke yao. Uchunguzi uliofanywa nchini Uingereza ulifikia mkataa kwamba mwanzoni mwa karne ya 21, angalau asilimia 30 ya watu nchini humo watakuwa wakiishi peke yao.

Maandiko yaliyopuliziwa yalitabiri kwamba mtazamo wa ubinafsi ungeenea sana katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Inaonekana kwamba watu wengi wanapendezwa zaidi na vitu vya kimwili, kama vile nyumba au gari, au kazi zao kuliko kusitawisha urafiki na wanadamu wenzao. Mwandishi Anthony Storr asema hivi: “Badala ya kupendezwa na mwenzi wa ndoa na watoto, wanapendezwa na mahali wanapofanyia kazi.”

MARAFIKI WA KWELI NI WENYE THAMANI SANA

Ubora wa maisha yako wategemea sana ubora wa marafiki wako. Mara nyingi watu wasiojali wengine hawana furaha kwa sababu hawana rafiki wanayeweza kumweleza mambo yao au fikira zao. Maneno haya ya Yesu Kristo ni ya kweli: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Akirudia ukweli wa maneno hayo, mtunga-mashairi Mwingereza George Byron aliandika hivi: “Wote watakaopata shangwe, lazima waishiriki na wengine.”

Rafiki ni nani? Kamusi moja hufasiri rafiki kuwa “mtu anayeambatana na mwingine kwa sababu ya kumpenda au kumthamini.” Rafiki wa kweli anaweza kukusaidia ufikirie mambo yanayonufaisha. Anaweza kukutia moyo na kukujenga wakati wa uhitaji. Hata anaweza kuhuzunika pamoja nawe. Mfalme Solomoni alisema hivi: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” (Mithali 17:17) Ingawa vitu vya kimwili hupoteza thamani baada ya muda, urafiki wa kweli hukua na kusitawi kadiri muda unavyopita.

Maandiko huwahimiza Wakristo ‘wapanuke’ katika upendo wao. (2 Wakorintho 6:13) Ni jambo la hekima kuwa na ukaribu na wengine. Katika Mhubiri 11:1, 2 twasoma hivi: “Tupa chakula chako usoni pa maji; maana utakiona baada ya siku nyingi. Uwagawie sehemu watu saba, hata wanane; maana hujui baa gani litakalokuwa juu ya nchi.” Kanuni hii inatumikaje kuhusiana na urafiki? Ikiwa umefanya urafiki na watu wengi, baadhi yao waweza kukusaidia wakati wa magumu.

Marafiki wa kweli ni ulinzi kwako katika njia nyingine. “Jeraha utiwazo na rafiki ni amini,” yasema Mithali 27:6. Ingawa watu wengi wanaweza kukusifu, ni marafiki wa kweli peke yao watakaokuthamini vya kutosha kukuonyesha kasoro kubwa na kukushauri ifaavyo kwa upendo.—Mithali 28:23.

Marafiki wazuri na wa karibu ni baadhi ya zawadi adimu zinazoweza kukuathiri ifaavyo. Katika Matendo sura ya 10, twasoma juu ya tukio fulani katika maisha ya Kornelio, ofisa wa kijeshi Mroma, aliyeelezwa na malaika kwamba sala zake zilikuwa zimesikiwa. Alipokuwa akitarajia kutembelewa na mtume Petro, Kornelio “[ali]waita pamoja jamaa zake na marafiki wa karibu sana.” Marafiki hao wa karibu wa Kornelio walikuwa miongoni mwa watu wa kwanza wa Mataifa wasiotahiriwa kukubali habari njema na kutiwa mafuta na roho takatifu, na hivyo kupata taraja la kutawala pamoja na Kristo katika Ufalme wa Mungu. Marafiki wa karibu wa Kornelio walipokea baraka iliyoje!—Matendo 10:24, 44.

Ingawa hivyo, unaweza kupataje marafiki? Biblia, ambayo ina mengi ya kusema kuhusu urafiki, hujibu swali hilo kwa kutoa shauri lenye kutumika. (Ona sanduku lililo chini.)

MAHALI UNAPOWEZA KUPATA MARAFIKI WA KWELI

Mahali bora zaidi kupata marafiki wa kweli ni kwenye kutaniko la Kikristo. Kwanza kabisa, unaweza kutwaa fursa ya kufanya urafiki na Yehova, Muumba wako na Baba yako wa kimbingu, na Yesu Kristo, Mwokozi wako. “Hakuna aliye na upendo mkubwa zaidi kuliko huu, kwamba mtu fulani aisalimishe nafsi yake kwa niaba ya marafiki wake,” akasema Yesu, anayekualika uwe rafiki yake. (Yohana 15:13, 15) Kwa kufanya urafiki pamoja na Yehova na Yesu Kristo, unaweza kuwa na hakika kwamba ‘watakupokea wewe ndani ya mahali pa kukaa padumupo milele.’ Naam, urafiki pamoja na Yehova na Yesu wamaanisha uhai udumuo milele.—Luka 16:9; Yohana 17:3.

Unaweza kupataje urafiki wao mchangamfu? Matakwa ya kuwa mgeni katika hema la Yehova kama mmoja wa wageni wake yanaonyeshwa katika Zaburi 15. Fungua Zaburi hiyo katika Biblia, kisha usome mistari yake mitano. Kwa kuongezea, Yesu Kristo alisema hivi: “Nyinyi ni marafiki wangu ikiwa mwafanya lile ninalowaamuru nyinyi.”—Yohana 15:14.

Naam, kwa kudhamiria kujifunza na kutumia mwelekezo kutoka kwa Neno la Mungu, Biblia, unaonyesha kwamba unataka kuwa rafiki ya Yehova na Yesu. Ili kutimiza hilo, ni lazima pia uhudhurie mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, ambapo ujuzi juu ya Yehova Mungu hutolewa. Jitahidi kumsikiliza Yehova kwa uaminifu, nawe utakuwa na ukaribu zaidi naye na Mwanaye.

Pia kwenye mikutano unaweza kujuana na watu wanaompenda Yehova na kudhihirisha matunda ya roho—upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujidhibiti—maishani mwao. (Wagalatia 5:22, 23) Ikiwa una bidii ya kutafuta marafiki na kuepuka upweke, hudhuria mikutano ya Kikristo kila juma. Kuihudhuria kutafanya uwe mahali panapofaa wakati unaofaa ili kusitawisha urafiki wenye kudumu pamoja na watu wa Mungu waliobarikiwa.

MARAFIKI MILELE

Urafiki wa kweli ni zawadi bora kutoka kwa Yehova Mungu. Unatokana na utu wake mwenyewe. Kwa sababu ya mtazamo wake wenye upendo na ukarimu, ameijaza dunia viumbe wenye akili ambao unaweza kufanya urafiki nao. Shirikiana na Wakristo wenzako. Watie moyo. Fanya kazi pamoja nao katika huduma. Sali pamoja nao na kwa ajili yao kwa ukawaida. Kwa kufanya hivyo utakuwa ukimwiga Yehova na Mwanaye, Yesu Kristo.

Urafiki ni zawadi ambayo kila mtu anaweza kutoa na kupokea. Utakuwa na fursa ya kuongeza idadi ya marafiki wako wakati ujao ulio karibu. Unaweza kufanya urafiki pamoja na mamilioni ya watu wanaoishi sasa, na vilevile wale wa vizazi vya zamani ambao wamelala katika kifo, wakingojea ufufuo wakati ambapo “kifo hakitakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4; Yohana 5:28, 29) Fanya jitihada sasa ya kuwa mwenye urafiki, na ufanye urafiki na wale wanaompenda Yehova. Fuatia urafiki pamoja na Yehova Mungu na Yesu Kristo kwa kusikiliza Neno la Mungu lililopuliziwa. Kisha, hutakuwa mpweke tena kamwe kwa umilele.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22, 23]

Hatua Sita za Kuwa na Urafiki wa Kudumu

1. UWE MWENYE URAFIKI. Abrahamu aliitwa “rafiki ya Yehova” kwa sababu ya imani yake isiyoyumbayumba. (Yakobo 2:23) Lakini kulikuwa na sababu nyingine. Biblia husema kwamba Abrahamu alionyesha kwamba anampenda Mungu. (2 Mambo ya Nyakati 20:7) Alichukua hatua ya kwanza na kumjulisha Yehova jinsi alivyohisi. (Mwanzo 18:20-33) Naam, unahitaji kuchukua hatua ya kwanza ili kuthibitisha urafiki wako. Yesu alisema: “Zoeeni upaji, na watu watawapa nyinyi.” (Luka 6:38) Kitia-moyo au kutoa msaada fulani kwaweza kuwa chanzo cha kusitawisha urafiki mkubwa. Ralph Waldo Emerson, mwandishi wa insha Mmarekani, alisema hivi wakati mmoja: “Njia pekee ya kupata rafiki ni kuwa rafiki.”

2. TAFUTA WAKATI WA KUSITAWISHA URAFIKI. Watu wengi hutaka sana kunufaika na urafiki. Hata hivyo, wana shughuli nyingi mno hivi kwamba hawapati wakati unaohitajika ili kufanya urafiki. Waroma 12:15, 16 hututia moyo tushiriki furaha na mafanikio, majonzi na matamauko ya wengine. Andiko hilo lasema hivi: “Shangilieni pamoja na watu washangiliao; toeni machozi pamoja na watu watoao machozi. Iweni na nia ya jinsi ileile kuelekea wengine kama ilivyo kwenu wenyewe.” Ingawa Yesu Kristo alikuwa mtu mwenye shughuli nyingi, sikuzote alitumia wakati pamoja na marafiki wake. (Marko 6:31-34) Kumbuka, urafiki, kama vile mmea unaochanua maua, wahitaji kumwagiliwa maji na kutunzwa ili ukue—na hilo huchukua muda.

3. SIKILIZA WENGINE WANAPOONGEA. Mara nyingi, wasikilizaji makini hupata marafiki kwa urahisi. “Kila mtu lazima awe mwepesi sana juu ya kusikia, wa polepole juu ya kusema,” asema mwanafunzi Yakobo. (Yakobo 1:19) Unapoongea na wengine pendezwa kibinafsi na hisia zao. Watie moyo wajieleze wenyewe. Uwe wa kwanza kuwaonyesha heshima. (Waroma 12:10) Kwa kufanya hivyo, watataka kuwa pamoja nawe. Kinyume cha hilo, ikiwa wewe tu ndiye unayetaka kuzungumza wakati wote, au kujitokeza daima, itakuwa vigumu kwako kupata mtu anayetaka kukusikiliza au anayejali hisia na mahitaji yako.

4. UWE MWENYE KUSAMEHE. Wakati mmoja Yesu alimwambia Petro awe tayari kusamehe “mpaka mara sabini na saba.” (Mathayo 18:21, 22) Rafiki wa kweli hupuuza kasoro ndogo-ndogo mara moja. Kwa kielelezo: Watu fulani hawapendi kula mapera kwa sababu ya mbegu zake ndogo. Hata hivyo, wale wanaopenda tunda hili, hupuuza mbegu hizo. Marafiki wa kweli hupendwa kwa sababu ya sifa zao nzuri; kasoro zao ndogo-ndogo hupuuzwa. Paulo alituhimiza hivi: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake.” (Wakolosai 3:13) Wale wanaojifunza kusamehe hudumisha marafiki wao.

5. HESHIMU WAKATI WA FARAGHA WA WENGINE. Kila mtu anahitaji wakati wa faragha, kutia ndani marafiki wako. Mithali 25:17 husema hivi kwa hekima: “Mguu wako usiingie katika nyumba ya juani yako ila kwa kiasi; asije akakukinai na kukuchukia.” Kwa hiyo, uwe mwenye kiasi kuhusu mara ambazo unatembelea marafiki wako na muda unaotumia unapowatembelea. Epuka kufanya rafiki yako awe wako tu, jambo ambalo laweza kusababisha wivu. Uwe mwenye busara unapoeleza mapendezi yako na maoni yako kuhusu mambo mbalimbali. Hiyo hutokeza urafiki wenye kuburudisha na wenye kupendeza.

6. UWE MKARIMU. Urafiki husitawishwa kupitia ukarimu. Mtume Paulo atushauri “kuwa wakarimu, tayari kushiriki.” (1 Timotheo 6:18) Kwa mfano, watie moyo wengine kwa maneno. (Mithali 11:25) Uwe huru kutoa pongezi kwa unyofu na pia kusema maneno yajengayo. Unapoonyesha unapendezwa kikweli na wengine, watavutiwa nawe. Fikiria mambo unayoweza kuwafanyia badala ya kufikiria mambo wanayoweza kukufanyia.