Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Humpa Nguvu Aliyechoka

Yehova Humpa Nguvu Aliyechoka

Yehova Humpa Nguvu Aliyechoka

“[Yehova] anampa aliyechoka nguvu; na yule asiye na nishati yenye msukumo humfanya awe na uwezo tele.”—ISAYA 40:29, NW.

1. Eleza nguvu zilizo katika vitu ambavyo Mungu ameumba.

YEHOVA ana nguvu zisizo na kikomo. Navyo vitu alivyoumba vina nishati yenye msukumo iliyoje! Atomu iliyo ndogo sana—ambayo hutumiwa kutengeneza vitu vyote—ni ndogo mno hivi kwamba tone moja tu la maji lina atomu bilioni mia moja bilioni. * Viumbe wote katika dunia yetu hutegemea nishati inayotokana na utendanaji wa atomu katika jua. Ni kiasi gani cha nishati kutoka kwa jua kinachohitajika ili kuendeleza uhai duniani? Dunia hupokea kiasi kidogo sana cha nishati inayotokezwa na jua. Hata hivyo, sehemu iliyo ndogo zaidi ya nishati ya jua inayofika duniani ni kubwa sana kuliko nishati yote inayotumiwa viwandani ulimwenguni pote.

2. Kwa ufupi, Isaya 40:26 husema nini juu ya nguvu za Yehova?

2 Tuwe tunafikiri juu ya atomu, au tunafikiri juu ya ulimwengu wote ulio mkubwa sana, tunavutiwa na nguvu za ajabu za Yehova. Haishangazi kwamba angeweza kusema: “Inueni macho yenu juu, mkaone; ni nani aliyeziumba hizi; aletaye nje jeshi lao kwa hesabu; aziita zote kwa majina; kwa ukuu wa uweza [“nishati yenye msukumo,” NW] wake, na kwa kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake; hapana moja isiyokuwapo mahali pake”! (Isaya 40:26) Naam, Yehova ni “hodari kwa nguvu,” naye ndiye Chanzo cha “nishati yenye msukumo” iliyotumiwa kuumba ulimwengu wote mzima.

Nguvu Zinazozidi za Kawaida Zahitajiwa

3, 4. (a) Ni nini baadhi ya mambo yawezayo kutuchosha? (b) Ni swali gani tunalohitaji kufikiria?

3 Hata ingawa nguvu za Mungu hazina kikomo, wanadamu huchoka. Kila tuendapo, twaona watu waliochoka. Wanaamka wakiwa wamechoka, wanaenda kazini au shuleni wakiwa wamechoka, wanarudi nyumbani wakiwa wamechoka, na kwenda kulala wakiwa wameishiwa nguvu kabisa. Wengine hutamani kwenda mahali fulani ili angalau wapate pumziko wanalohitaji sana. Tukiwa watumishi wa Yehova, sisi pia huchoka, kwa kuwa maisha yetu ya ujitoaji-kimungu hutaka tujikakamue kisulubu. (Marko 6:30, 31; Luka 13:24; 1 Timotheo 4:8) Na kuna mambo mengine mengi ambayo hutufanya tuchoke.

4 Tujapokuwa Wakristo, tunapatwa na matatizo yanayowapata watu kwa ujumla. (Ayubu 14:1) Magonjwa, magumu ya fedha, au magumu mengineyo yaliyo ya kawaida maishani yaweza kuvunja moyo, hali ambayo hutufanya tuwe wanyonge. Mbali na magumu hayo, kuna majaribu yanayowapata hasa wale wanaonyanyaswa kwa ajili ya uadilifu. (2 Timotheo 3:12; 1 Petro 3:14) Kwa sababu ya mikazo ya kila siku kutoka kwa ulimwengu na pia upinzani dhidi ya kazi yetu ya kuhubiri Ufalme, baadhi yetu twaweza kuchoka sana na kutaka kupunguza bidii katika utumishi wa Yehova. Zaidi ya hayo, katika jitihada ya kuvunja uaminifu wetu wa maadili kwa Mungu, Shetani Ibilisi anatumia kila njia aliyo nayo. Basi, tunaweza kupataje nguvu za kiroho zinazohitajiwa ili kuendelea badala ya kuchoka na kuacha?

5. Kwa nini nguvu inayozidi ile ya wanadamu inahitajika ili kutekeleza huduma ya Kikristo?

5 Ili kupata nguvu za kiroho, lazima tumtegemee Yehova, Muumba mwenye nguvu zote. Mtume Paulo alisema kwamba huduma ya Kikristo ingehitaji nguvu inayozidi ile ya kawaida, ya wanadamu wasiokamilika. Aliandika hivi: “Sisi tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili nguvu ipitayo iliyo ya kawaida ipate kuwa ya Mungu na si ile ya kutoka katika sisi wenyewe.” (2 Wakorintho 4:7) Wakristo watiwa-mafuta wanatekeleza “huduma ya upatanisho” wakiungwa mkono na waandamani wao walio na tumaini la kidunia. (2 Wakorintho 5:18; Yohana 10:16; Ufunuo 7:9) Kwa kuwa sisi wanadamu wasio wakamilifu tunafanya kazi ya Mungu huku tukikabili mnyanyaso, hatuwezi kuifanya kwa nguvu zetu wenyewe tu. Yehova hutusaidia kupitia roho yake takatifu, na hivyo udhaifu wetu hutukuza nguvu zake. Jinsi tunavyofarijiwa na uhakikisho kwamba ‘Yehova atategemeza wenye haki’!—Zaburi 37:17.

‘Yehova Ni Nguvu Yetu’

6. Maandiko hutuhakikishiaje kwamba Yehova ndiye Chanzo cha nguvu yetu?

6 Baba yetu wa kimbingu ni “hodari kwa nguvu” na anaweza kututia nguvu kwa urahisi. Kwa kweli tunaambiwa hivi: “[Yehova] huwapa nguvu wazimiao [“humpa nguvu aliyechoka,” NW], humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo [“nishati yenye msukumo,” NW]. Hata vijana watazimia na kuchoka, na wanaume vijana wataanguka; bali wao wamngojeao BWANA watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka.” (Isaya 40:29-31) Kwa sababu ya kuongezeka kwa mikazo, huenda nyakati fulani tukahisi kama mkimbiaji aliyechoka ambaye miguu yake haiwezi kumtegemeza tena. Lakini sehemu ya kumalizia mbio za uhai iko karibu, na hatupaswi kufa moyo. (2 Mambo ya Nyakati 29:11) Mpinzani wetu Ibilisi, anazunguka-zunguka “kama simba anayenguruma,” na anataka kutuzuia tusiendelee katika mbio. (1 Petro 5:8) Acheni tukumbuke kwamba ‘Yehova ni nguvu na ngao yetu,’ na amefanya maandalizi ya kutosha ‘kumpa nguvu aliyechoka.’—Zaburi 28:7.

7, 8. Kuna uthibitisho gani kwamba Yehova alimwimarisha Daudi, Habakuki, na Paulo?

7 Yehova alimpa Daudi nguvu alizohitaji ili kuendelea licha ya vizuizi vikubwa. Kwa hiyo, akiwa na imani na uhakika kamili, Daudi aliandika hivi: “Kwa msaada wa Mungu tutatenda makuu, maana Yeye atawakanyaga watesi wetu.” (Zaburi 60:12) Yehova pia alimpa Habakuki nguvu ili akamilishe mgawo wake akiwa nabii. Andiko la Habakuki 3:19 lasema hivi: “YEHOVA, aliye BWANA, ni nguvu [“nishati hai,” NW] zangu, yeye huifanya miguu yangu kuwa kama ya kulungu, naye ataniendesha katika mahali pangu palipoinuka.” Twapaswa pia kuangalia kielelezo cha Paulo, aliyeandika hivi: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye [Mungu] anipaye nguvu.”—Wafilipi 4:13.

8 Kama Daudi, Habakuki na Paulo, yatupasa kudhihirisha imani katika uwezo wa Mungu wa kutuimarisha na katika nguvu zake za kutuokoa. Tukiwa tunatambua kwamba Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova ndiye Chanzo chetu cha “nishati hai,” acheni sasa tuchunguze baadhi ya njia ambazo twaweza kupata nguvu za kiroho kutokana na maandalizi ambayo Mungu hutoa kwa wingi.

Maandalizi ya Kiroho ya Kututia Nguvu

9. Vichapo vya Kikristo hutimiza fungu gani katika kututia nguvu?

9 Tunaweza kutiwa nguvu na kutegemezwa kwa kujifunza Maandiko kwa bidii pamoja na msaada tupatao kutoka kwa vichapo vya Kikristo. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Heri mtu yule . . . [ambaye] sheria ya BWANA ndiyo impendezayo, na sheria yake huitafakari mchana na usiku. Naye atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki; na kila alitendalo litafanikiwa.” (Zaburi 1:1-3) Kama vile ni lazima tule ili kudumisha nguvu za kimwili, twahitaji pia kula chakula cha kiroho kinachoandaliwa na Mungu kupitia Neno lake na vichapo vya Kikristo ili tudumishe nguvu zetu za kiroho. Kwa hiyo, ni muhimu kuwa na funzo lenye maana na kutafakari.

10. Ni lini tunapoweza kupata wakati wa kujifunza na kutafakari?

10 Kwa kweli ni jambo linalothawabisha kutafakari “mambo yenye kina kirefu ya Mungu.” (1 Wakorintho 2:10) Lakini ni lini tuwezapo kupata wakati wa kutafakari? Mwana wa Abrahamu, Isaka “[ali]toka ili kutafakari kondeni wakati wa jioni.” (Mwanzo 24:63-67) Mtunga-zaburi Daudi ‘alitafakari juu ya Mungu makesha yote ya usiku.’ (Zaburi 63:6) Twaweza kujifunza Neno la Mungu na kulitafakari asubuhi, jioni, usiku—naam, wakati wowote. Funzo la namna hiyo pamoja na kutafakari huongoza kwenye uandalizi mwingine wa Yehova wenye kutuimarisha kiroho—sala.

11. Kwa nini twapaswa kutilia maanani sana sala ya ukawaida?

11 Tunatiwa nguvu tunaposali kwa Mungu kwa ukawaida. Kwa hiyo, na ‘tudumu katika sala.’ (Waroma 12:12) Nyakati nyingine, twahitaji kutoa ombi hususa ili kupata hekima na nguvu tunayohitaji ili kukabiliana na jaribu fulani. (Yakobo 1:5-8) Acheni pia tumshukuru na kumsifu Mungu tuonapo makusudi yake yakitimizwa au tuonapo kwamba ametuimarisha ili kuendelea katika utumishi wake. (Wafilipi 4:6, 7) Tukiendelea kuwa karibu na Yehova kupitia sala, hatatuacha kamwe. “Tazama Mungu ndiye anayenisaidia,” akaimba Daudi.—Zaburi 54:4.

12. Kwa nini tumwombe Mungu roho yake takatifu?

12 Baba yetu wa kimbingu hututia nguvu na kutuimarisha kupitia roho yake takatifu, au kani ya utendaji. Paulo aliandika hivi: “Namkunjia Baba magoti yangu . . . kwa kusudi la kwamba apate kuwaruhusu nyinyi kulingana na utajiri wa utukufu wake ili mfanywe wenye uweza katika mtu mliye kwa ndani mkiwa na nguvu kupitia roho yake.” (Waefeso 3:14-16) Twapaswa kusali ili kupata roho takatifu, tukiwa na uhakika kwamba Yehova atatupatia roho hiyo. Yesu alisababu hivi: Ikiwa mtoto aomba samaki, je, baba mwenye upendo atampa nyoka? Bila shaka la. Hivyo, akakata kauli hivi: “Ikiwa nyinyi, mjapokuwa [wenye dhambi na hivyo kwa kadiri fulani] waovu, mwajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, si zaidi sana yule Baba aliye mbinguni atawapa roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:11-13) Acheni tusali tukiwa na uhakika huo na kukumbuka sikuzote kwamba watumishi waaminifu wa Mungu waweza ‘kufanywa kuwa wenye uweza’ kwa nguvu za roho yake.

Kutaniko—Msaada Wenye Kutia Nguvu

13. Twapaswa kuionaje mikutano ya Kikristo?

13 Yehova hututia nguvu kupitia mikutano ya kutaniko la Kikristo. Yesu alisema hivi: “Palipo na wawili au watatu wakiwa wamekusanyika pamoja katika jina langu, hapo mimi nipo katikati yao.” (Mathayo 18:20) Alipotoa ahadi hiyo, Yesu alikuwa akizungumzia mambo yaliyohitaji kushughulikiwa na wale wanaoongoza kutanikoni. (Mathayo 18:15-19) Hata hivyo, kwa jumla maneno yake yahusu mikutano yetu yote, makusanyiko na mikusanyiko, ambayo hufunguliwa na kufungwa kwa sala katika jina lake. (Yohana 14:14) Kwa hiyo, ni pendeleo kuhudhuria mikutano hiyo ya Kikristo iwe imehudhuriwa na watu wachache au maelfu ya watu. Kwa hiyo, acheni tuonyeshe shukrani kwa pindi hizi zinazokusudiwa kutuimarisha kiroho na kutuchochea katika upendo na kazi zilizo bora.—Waebrania 10:24, 25.

14. Tunanufaikaje na jitihada za wazee Wakristo?

14 Wazee Wakristo hutoa msaada na kitia-moyo cha kiroho. (1 Petro 5:2, 3) Paulo alisaidia na kutia moyo makutaniko aliyotumikia, kama wafanyavyo waangalizi wasafirio leo. Kwa kweli, alitamani sana kuwa pamoja na waamini wenzake ili kuwe na badilishano la kitia-moyo chenye kujenga. (Matendo 14:19-22; Waroma 1:11, 12) Acheni sikuzote tuonyeshe uthamini kwa wazee wa kwetu na waangalizi wengine Wakristo, wanaotimiza fungu kubwa katika kutuimarisha kiroho.

15. Ni jinsi gani waamini wenzetu katika kutaniko wanakuwa “msaada wenye kutia nguvu”?

15 Waamini wenzetu ambao hufanyiza kutaniko letu waweza kuwa “msaada wenye kutia nguvu.” (Wakolosai 4:10, 11) Wakiwa ‘rafiki za kweli’ wanaweza kutusaidia wakati wa taabu. (Mithali 17:17, Biblia Habari Njema) Mathalani, wakati watumishi wa Mungu 220 walipoachiliwa mwaka wa 1945 kutoka katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen iliyokuwa ikilindwa na Nazi, walihitaji kusafiri umbali wa kilometa 200. Walisafiri wakiwa kikundi, na wale waliokuwa na nguvu zaidi waliwavuta waliokuwa dhaifu zaidi kwa mikokoteni midogo michache. Matokeo yakawaje? Katika msafara wa kifo ambapo wafungwa 10,000 wa kambi za mateso walikufa, hakuna hata mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyekufa. Masimulizi kama hayo yaliyo katika vichapo vya Watch Tower, kutia ndani Yearbook of Jehovah’s Witnesses na Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, yathibitisha kwamba Mungu huwapa watu wake nguvu, ili wasikate tamaa.—Wagalatia 6:9. *

Twaimarishwa na Huduma Yetu ya Shambani

16. Kushiriki kwa ukawaida katika huduma hutuimarishaje kiroho?

16 Kushiriki kwa ukawaida kazi ya kuhubiri Ufalme hutuimarisha kiroho. Utendaji huo hutusaidia tukazie fikira Ufalme wa Mungu na kufikiria umilele pamoja na matazamio yake yenye baraka. (Yuda 20, 21) Ahadi za Kimaandiko tunazoongea juu yake katika huduma yetu hutupa tumaini na zaweza kutufanya tuwe na azimio kama la nabii Mika aliyesema hivi: “Sisi tutakwenda kwa jina la BWANA, Mungu wetu, milele na milele.”—Mika 4:5.

17. Ni madokezo gani ambayo yametolewa kuhusu mafunzo ya Biblia ya nyumbani?

17 Uhusiano wetu pamoja na Yehova huimarishwa tunapotumia sana Maandiko kufundisha wengine. Kwa mfano, tunapoongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani tukitumia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, ni jambo la hekima kusoma na kuzungumzia maandiko kadhaa yaliyotajwa. Kufanya hivyo humsaidia mwanafunzi na kuimarisha ufahamu wetu wa kiroho. Ikiwa mwanafunzi haelewi wazo au kielezi fulani katika Biblia, si lazima sura moja ya kitabu Ujuzi isomwe katika pindi moja. Tunafurahi kama nini kutayarisha vizuri na kufanya jitihada ya ziada kusaidia wengine wawe na ukaribu na Mungu!

18. Toa mfano kuhusu jinsi ambavyo kitabu Ujuzi kinatumiwa kwa matokeo.

18 Kila mwaka, kitabu Ujuzi kinatumiwa kwa njia yenye matokeo kusaidia maelfu ya watu wawe watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu, na idadi hiyo yatia ndani watu wengi ambao wamelelewa bila kuijua Biblia. Mathalani, alipokuwa mtoto, mwanamume mmoja Mhindu wa Sri Lanka alisikia Shahidi mmoja akizungumza juu ya Paradiso. Miaka kadhaa baadaye, mwanamume huyo alimwendea yule dada, na punde si punde mume wake akaanzisha funzo la Biblia pamoja naye. Kwa kweli, kijana huyo alijifunza kila siku, na kitabu Ujuzi kikamalizika kwa muda mfupi. Akaanza kuhudhuria mikutano yote, akavunja ushirika na dini yake ya awali, na kuwa mhubiri wa Ufalme. Alipobatizwa, tayari alikuwa akiongoza funzo la Biblia la nyumbani pamoja na mtu fulani aliyemfahamu vizuri.

19. Tunapoutafuta Ufalme kwanza, twaweza kuwa na uhakika gani?

19 Kuutafuta Ufalme kwanza hutupa shangwe inayotuimarisha. (Mathayo 6:33) Ingawa tunapatwa na majaribu mbalimbali, tunaendelea kutangaza habari njema kwa furaha na kwa bidii. (Tito 2:14) Wengi wetu tunatimiza matakwa ya utumishi wa wakati wote wa upainia, na wengine wanatumikia mahali penye uhitaji mkubwa wa waeneza-evanjeli. Tuwe tunaendeleza masilahi ya Ufalme kwa furaha katika njia hizi au nyinginezo, tuna hakika kwamba Yehova hatasahau kazi yetu na upendo tunaoonyesha kwa ajili ya jina lake.—Waebrania 6:10-12.

Endelea kwa Kutegemea Nguvu za Yehova

20. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunamtegemea Yehova ili kupata nguvu?

20 Acheni tuonyeshe kwa moyo wote kwamba tunamtumaini Yehova na kumtegemea ili kupata nguvu. Twaweza kufanya hivyo kwa kutumia kikamili maandalizi ya kiroho anayotoa kupitia “mtumwa mwaminifu.” (Mathayo 24:45) Kujifunza Neno la Mungu kibinafsi na katika kutaniko kupitia msaada wa vichapo vya Kikristo, sala ya kutoka moyoni, msaada wa kiroho kutoka kwa wazee, vielelezo bora vya waamini wenzetu waaminifu, na kushiriki kwa ukawaida katika huduma ni baadhi ya maandalizi ambayo huimarisha uhusiano wetu na Yehova na kutupa nguvu za kuendelea katika utumishi wake mtakatifu.

21. Mtume Petro na mtume Paulo walionyeshaje kwamba walihitaji nguvu kutoka kwa Mungu?

21 Licha ya udhaifu wetu wa kibinadamu, Yehova atatuimarisha kufanya mapenzi yake tukimtegemea atusaidie. Akitambua kwamba alihitaji msaada huo, mtume Petro aliandika hivi: “Ikiwa yeyote ahudumu, acheni ahudumu kama ategemeaye nguvu ambazo Mungu hutoa.” (1 Petro 4:11) Paulo alionyesha kwamba alitegemea nguvu zinazotoka kwa Mungu aliposema hivi: “Napendezwa na udhaifu, katika matusi, katika visa vya uhitaji, katika minyanyaso na magumu, kwa ajili ya Kristo. Kwa maana niwapo dhaifu, ndipo niwapo mwenye nguvu.” (2 Wakorintho 12:10) Acheni tuonyeshe usadikisho huohuo na kumletea utukufu Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ambaye humpa nguvu aliyechoka.—Isaya 12:2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Idadi hii, kulingana na mfumo wa kuhesabia wa Marekani, ni nambari 1 inayofuatwa na sufuri 20.

^ fu. 15 Vilivyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

Ungejibuje?

• Kwa nini watu wa Yehova wanahitaji nguvu zinazozidi zile za kawaida?

• Kuna uthibitisho gani wa Kimaandiko kwamba Mungu huwapa nguvu watumishi wake?

• Ni nini baadhi ya maandalizi ya kiroho ambayo Yehova ametoa ili kutuimarisha?

• Twaweza kuonyeshaje kwamba tunamtegemea Mungu ili kupata nguvu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Uhusiano wetu pamoja na Yehova huimarishwa tunapotumia Biblia kufundisha wengine