Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Huwaandalia Watu Wake Mahali pa Kupumzikia

Yehova Huwaandalia Watu Wake Mahali pa Kupumzikia

Wapiga-mbiu wa Ufalme Waripoti

Yehova Huwaandalia Watu Wake Mahali pa Kupumzikia

MSAFIRI mchovu hupendezwa sana na mahali pa kupumzikia penye kivuli kwenye njia ya mlimani. Nchini Nepal, mahali kama hapo pa kupumzikia huitwa chautara. Chautara ya kawaida yaweza kujengwa karibu na mbaniani wenye majani mengi, mahali penye kivuli pa kuketi na kupumzikia. Kujengea watu chautara ni tendo la fadhili, na wengi wa wafadhili hao hawajulikani.

Mambo yaliyoonwa kutoka Nepal yanaonyesha jinsi ambavyo Yehova Mungu amekuwa Chanzo cha shangwe na burudisho la kiroho kwa “wasafiri” wengi wachovu katika mfumo huu wa mambo.—Zaburi 23:2.

• Lil Kumari anaishi katika jiji maridadi la Pokhara, ambapo anaweza kuona Milima maridadi ya Himalaya yenye vilele vilivyofunikwa na theluji. Lakini kwa sababu ya kuhangaikia hali ya kifedha ya familia, Lil Kumari alikosa tumaini. Alipotembelewa na mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alivutiwa na tumaini zuri la Biblia na mara moja akaomba funzo la Biblia nyumbani.

Ingawa Lil Kumari alifurahia funzo hilo, haikuwa rahisi kuendelea kwa sababu ya upinzani mkali wa familia. Lakini hakuacha kujifunza. Alihudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na kutumia yale aliyojifunza, hasa kuhusiana na ujitiisho wa mke. Matokeo yakawa kwamba, mume wake na mama yake wakaja kutambua kwamba funzo la Biblia la Lil Kumari lilikuwa likinufaisha familia nzima.

Mume wake na watu kadhaa wa jamaa sasa wanajifunza Neno la Mungu. Kwenye kusanyiko la karibuni lililofanywa huko Pokhara, Lil Kumari alifurahia programu pamoja na watu 15 wa jamaa yake. Yeye asema: “Nyumba yangu imekuwa mahali pa kupumzikia kwa sababu familia yetu sasa imeungana katika ibada ya kweli, na nimepata amani ya kweli ya akili.”

• Ingawa ubaguzi wa kitabaka ni kinyume cha sheria nchini Nepal, ungali unaathiri sana jinsi watu wanavyoishi. Hivyo, wengi wanapenda kujua yale Biblia isemayo kuhusu usawa na kutobagua. Kujua kwamba “Mungu si mwenye ubaguzi” kulibadili sana maisha ya Surya Maya na familia yake.—Matendo 10:34.

Surya Maya alihuzunishwa sana na ukosefu wa haki unaotokana na ubaguzi wa kitabaka na tatizo linalotokana na mapokeo na tamaduni zilizokolea sana. Surya Maya, aliyejitoa sana kwa mambo ya dini, aliomba miungu yake ya sanamu kwa miaka mingi ili imsaidie. Lakini sala zake hazikujibiwa. Siku moja alipokuwa akililia msaada, Babita, mjukuu wake wa kike mwenye umri wa miaka sita alimkaribia na kumwuliza: “Kwa nini unaziomba sanamu zisizoweza kufanya chochote zikusaidie?”

Kumbe mamake Babita alikuwa anajifunza Biblia na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Babita alimwalika nyanyake kwa shauku kwenye mikutano ya Kikristo. Alipohudhuria, Surya Maya alishangaa kuona watu wa tabaka mbalimbali wakifurahia kuwa pamoja bila ubaguzi wowote. Aliomba funzo la Biblia nyumbani mara moja. Ingawa jambo hilo lilifanya atengwe na majirani wake, hakuvunjika moyo; wala kutojua kusoma na kuandika vizuri hakukumzuia asifanye maendeleo ya kiroho.

Miaka minane imepita, na watu sita wa familia yake, kutia ndani mume wake na watoto watatu, wamekuwa Mashahidi wa Yehova. Surya Maya sasa ni mhudumu wa wakati wote, painia wa kawaida, ambaye kwa shangwe husaidia wengine wenye mizigo mizito wapate pumziko kwenye mahali pa pumziko la kweli ambapo Yehova pekee ndiye awezaye kuandaa.