Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Unamtumikia Mungu?

Kwa Nini Unamtumikia Mungu?

Kwa Nini Unamtumikia Mungu?

Mfalme fulani mwenye kuhofu Mungu wakati mmoja alimshauri hivi mwanaye: “Mjue Mungu wa baba yako, ukamtumikie kwa moyo mkamilifu, na kwa nia ya kumkubali.” (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Ni wazi kwamba Yehova anataka watumishi wake wamtumikie kwa mioyo yenye shukrani na uthamini.

TUKIWA Mashahidi wa Yehova, twakiri kwa utayari kwamba tulipoelezwa ahadi za Biblia mara ya kwanza tulijawa na shukrani za kutoka moyoni. Tulijifunza jambo jipya kila siku kuhusu makusudi ya Mungu. Kadiri tulivyojifunza mengi kuhusu Yehova, ndivyo tamaa yetu ya kumtumikia “kwa moyo mkamilifu, na kwa nia ya kumkubali” ilivyoongezeka.

Wengi ambao wanakuwa Mashahidi wa Yehova huendelea kumtumikia Yehova kwa shangwe isiyo na kifani katika maisha yao yote. Hata hivyo, baadhi ya Wakristo huanza vizuri, lakini baada ya muda, wao husahau sababu ambazo hutuchochea kumtumikia Mungu. Je, umepatwa na jambo hilo? Ikiwa limekupata usikate tumaini. Unaweza kupata shangwe hata baada ya kuipoteza. Jinsi gani?

Fikiria Baraka Zako

Kwanza, tafakari baraka unazopokea kutoka kwa Mungu kila siku. Fikiria zawadi nzuri za Yehova: kazi zake mbalimbali za uumbaji—zinazoonekana na wote bila kujali hali yao ya kiuchumi au hadhi yao katika jamii—maandalizi yake ya asili kama chakula na kinywaji, afya unayofurahia kwa kiasi fulani, kuijua kweli ya Biblia, na zaidi ya yote, zawadi ya Mwana wake. Kifo chake kilikuandalia njia ya kumtumikia Mungu ukiwa na dhamiri safi. (Yohana 3:16; Yakobo 1:17) Kadiri unavyotafakari wema wa Mungu, ndivyo utakavyomthamini hata zaidi. Kisha moyo wako utakuchochea kumtumikia kwa kumshukuru kwa yote ambayo amefanya. Bila shaka, utaanza kuhisi tena kama mtunga-zaburi aliyeandika hivi: “Ee BWANA, Mungu wangu, umefanya kwa wingi miujiza yako na mawazo yako kwetu; hakuna awezaye kufananishwa nawe. . . . Ni mengi sana hayahesabiki.”—Zaburi 40:5.

Maneno hayo yaliandikwa na Daudi, mtu aliyekuwa na matatizo maishani. Akiwa kijana, Daudi alikuwa mkimbizi kwa muda mrefu kwa kuwa Mfalme Sauli mwovu na walinzi wake walimtafuta ili kumuua. (1 Samweli 23:7, 8, 19-23) Daudi alilazimika pia kushindana na udhaifu wa kibinafsi aliokuwa nao. Alikiri hayo katika Zaburi ya 40: “Mabaya yasiyohesabika yamenizunguka mimi. Maovu yangu yamenipata, wala siwezi kuona. Yamezidi kuliko nywele za kichwa changu.” (Zaburi 40:12) Naam, Daudi alikuwa na matatizo, lakini hayakumlemea kabisa. Licha ya matatizo yake alikazia fikira njia ambazo Yehova alikuwa anambariki, na kuona kwamba baraka hizo zilishinda kwa mbali taabu zake.

Unapohisi umelemewa na matatizo ya kibinafsi au na hisia za kutofaa, ni vizuri kutulia na kufikiria baraka zako, kama alivyofanya Daudi. Bila shaka, kuthamini baraka hizo kulikuchochea kujiweka wakfu kwa Yehova; mawazo hayo yaweza kukusaidia pia upate tena shangwe uliyopoteza na kukusaidia umtumikie Mungu kwa shukrani za kutoka moyoni.

Mikutano ya Kutaniko Yaweza Kusaidia

Mbali na kutafakari wema wa Yehova faraghani, twahitaji pia kushirikiana na Wakristo wenzetu. Inatia moyo kukutana kwa ukawaida na wanaume, wanawake, na vijana wanaompenda Mungu na ambao wameazimia kumtumikia. Kielelezo chao chaweza kutuchochea kufanya utumishi wa Yehova kwa nafsi yote. Wanaweza kutiwa moyo vilevile wanapotuona kwenye Jumba la Ufalme.

Ni kweli kwamba tunaporudi nyumbani baada ya kufanya kazi ngumu au tunapovunjika moyo kwa sababu ya tatizo au udhaifu fulani, huenda isiwe rahisi kufikiria kuhudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme. Huenda tukahitaji kuwa imara nyakati hizo, ‘tukipiga-piga mwili wetu,’ kusema kitamathali, ili tutii amri ya kukutanika na Wakristo wenzetu.—1 Wakorintho 9:26, 27; Waebrania 10:23-25.

Tukilazimika kufanya hivyo, je, tuamue kwamba hatumpendi Yehova kikweli? Sivyo kamwe. Wakristo wakomavu wa kale ambao upendo wao kwa Mungu haungeweza kutiliwa shaka walilazimika kujitahidi sana ili kufanya mapenzi ya Mungu. (Luka 13:24) Mtume Paulo alikuwa mmoja wa Wakristo hao. Alieleza hisia zake waziwazi hivi: “Najua kwamba katika mimi, yaani, katika mwili wangu, halikai jambo lolote jema; kwa maana uwezo wa kutaka upo pamoja nami, bali uwezo wa kufanya lililo bora haupo. Kwa maana lile jema nitakalo silifanyi, bali lile baya nisilotaka ndilo nazoea kulifanya.” (Waroma 7:18, 19) Naye aliwaambia Wakorintho hivi: “Ikiwa, sasa, ninatangaza habari njema, hiyo si sababu ya mimi kujisifu, kwa maana nimewekewa sharti. . . . Ikiwa nafanya hilo kwa kupenda, nina thawabu; lakini ikiwa nafanya hilo dhidi ya kupenda kwangu, vyovyote vile nina usimamizi-nyumba niliokabidhiwa.”—1 Wakorintho 9:16, 17.

Kama wengi wetu, Paulo alikuwa na mielekeo ya dhambi iliyozuia tamaa yake ya kufanya lililokuwa sawa. Hata hivyo, alifanya pigano kali dhidi ya mielekeo hiyo, na mara nyingi akafaulu. Bila shaka, Paulo hakutimiza hayo kwa nguvu zake mwenyewe. Aliandika hivi: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.” (Wafilipi 4:13) Yehova aliyempa Paulo nguvu, atakupa nguvu pia kufanya lililo sawa ukimwomba msaada wake. (Wafilipi 4:6, 7) Kwa hiyo fanya “pigano kali kwa ajili ya imani,” na Yehova atakubariki.—Yuda 3.

Si lazima upigane vita hiyo ukiwa peke yako. Katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, wazee Wakristo wakomavu, wanaodumu katika “pigano kwa ajili ya imani” wako tayari kukusaidia. Ukimwendea mzee ili kupata msaada, atajaribu ‘kusema kwa kukuliwaza.’ (1 Wathesalonike 5:14) Mradi wake utakuwa kutumikia akiwa “mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba.”—Isaya 32:2.

“Mungu ni upendo,” naye anataka watumishi wake wamtumikie kwa kuchochewa na upendo. (1 Yohana 4:8) Ikiwa upendo wako kwa Mungu wahitaji kuchochewa tena, chukua hatua zinazofaa kufanya hivyo, kama inavyoonyeshwa juu. Utafurahi kwamba ulifanya hivyo.