Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumaliza Madhara ya Vita

Kumaliza Madhara ya Vita

Kumaliza Madhara ya Vita

ABRAHAM alikuwa katika jeshi la wapiganaji wa kuvizia kwa muda wa miaka 20. * Lakini ameacha kupigana na hataenda vitani tena. Hata baadhi ya maadui wake wa zamani sasa ni marafiki wake wa karibu zaidi. Ni nini kilichomfanya abadilike? Ni Biblia. Ilimpa Abraham tumaini na ufahamu wenye kina, ikamsaidia kuona shughuli za wanadamu jinsi Mungu azionavyo. Biblia iliondolea mbali tamaa yake ya kupigana, na huzuni, majonzi, chuki, na uchungu alizokuwa nazo zikaanza kwisha. Aligundua kwamba Biblia ina tiba yenye nguvu kwa moyo.

Biblia humsaidiaje mtu kumaliza maumivu ya kihisia-moyo? Biblia haingeweza kubadili yale yaliyompata Abraham. Hata hivyo, kusoma na kutafakari Neno la Mungu kulipatanisha mawazo yake na yale ya Muumba. Sasa ana tumaini la wakati ujao, na ana mambo mapya ya kutanguliza. Mambo yaliyo muhimu kwa Mungu yamekuwa muhimu kwake pia. Maumivu aliyokuwa nayo moyoni yalianza kwisha alipoanza kufanya hivyo. Hivyo ndivyo Abraham alivyosaidiwa kubadilika.

Aingia Katika Vita ya Wenyewe kwa Wenyewe

Abraham alizaliwa katika miaka ya 1930 barani Afrika. Baada ya vita ya ulimwengu ya pili, nchi ya Abraham ilitawaliwa na nchi jirani yenye nguvu, lakini wengi wa wananchi wenzake walitaka uhuru. Katika mwaka wa 1961, Abraham alijiunga na wanaharakati wa kupigania uhuru ambao walipigana vita ya kuvizia dhidi ya ile nchi jirani yenye nguvu.

“Walikuwa maadui wetu. Walipanga kutuua, hivyo sisi tukachukua hatua ya kuwaua pia,” aeleza Abraham.

Mara nyingi maisha ya Abraham yalikuwa hatarini, kwa hiyo mwaka wa 1982, baada ya miaka 20 ya mapigano ya kutumia silaha, akakimbilia Ulaya. Wakati huo alikuwa na umri wa miaka 40 na kitu na alikuwa na wakati wa kufikiria maisha yake. Ilikuwaje kwa matumaini yake? Alitarajia nini wakati ujao? Abraham alikutana na Mashahidi wa Yehova fulani na kuanza kuhudhuria mikutano yao. Alikumbuka kwamba akiwa Afrika miaka kadhaa awali, alikuwa amesoma trakti fulani aliyokuwa amepewa na Shahidi. Trakti hiyo ilieleza paradiso inayokuja duniani na serikali ya mbinguni ambayo ingetawala wanadamu. Je, hilo kwa hakika laweza kuwa kweli?

Abraham asema: “Nilijifunza kutoka katika Biblia kwamba miaka hiyo yote ambayo nilitumia vitani ilikuwa imepotea bure. Serikali pekee itakayotendea kila mtu kwa haki ni Ufalme wa Mungu.”

Muda mfupi baada ya Abraham kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, mwanamume aitwaye Robert alikimbia kutoka Afrika kwenda jiji la Ulaya ambako Abraham alikuwa anaishi. Robert na Abraham walikuwa wamepigana katika vita ileile lakini wakiwa pande tofauti. Mara nyingi Robert alikuwa akijiuliza kusudi halisi la maisha. Alikuwa mtu wa kidini, na kwa kuwa alikuwa amesoma sehemu fulani za Biblia, alijua jina la Mungu ni Yehova. Wakati Mashahidi wa kutaniko la Abraham walipojitolea kumsaidia Robert aielewe Biblia vyema zaidi, alikubali mara moja.

Robert aeleza: “Tangu mwanzo kabisa, nilivutiwa na njia ambayo Mashahidi hutumia jina la Yehova na la Yesu, wakikiri kwamba hao ni watu wawili walio tofauti. Jambo hilo lilipatana na yale ambayo tayari nilikuwa nimejifunza kutoka katika Biblia. Mashahidi pia huvalia kinadhifu na huonyesha wengine fadhili, hata wawe ni wa taifa gani. Mambo hayo yalinivutia sana.”

Maadui Wawa Marafiki

Robert na Abraham, ambao zamani walikuwa maadui, sasa ni marafiki wa karibu. Wanatumikia wakiwa waeneza-evanjeli wa wakati wote katika kutaniko lilelile la Mashahidi wa Yehova. “Wakati wa vita, mara nyingi nilijiuliza jinsi ilivyowezekana kwa watu kutoka nchi jirani—wengi ambao walikuwa wa dini ileile—kuchukiana,” aeleza Abraham. “Mimi na Robert tulikuwa wafuasi wa kanisa lilelile, na bado tulipigana vitani. Sasa sote wawili ni Mashahidi wa Yehova, na imani yetu imetuunganisha.”

“Hiyo ndiyo tofauti,” aongeza Robert. “Sasa sisi ni wafuasi wa dini ambayo hutufanya kuwa sehemu ya udugu wa kweli. Hatuwezi kwenda vitani tena.” Biblia imekuwa na uvutano wenye nguvu katika mioyo ya maadui hawa wa zamani. Chuki na uchungu zimetoweka polepole na mahali pake pakachukuliwa na kutumainiana na urafiki.

Wakati uleule Abraham na Robert walipokuwa vitani, wanaume wengine wawili vijana walipigana kwenye pande tofauti katika vita kati ya nchi mbili zilizo majirani. Muda si muda Biblia ilikuwa tiba yenye nguvu sana ya kuponya mioyo yao pia. Jinsi gani?

Ua—Kisha Ufe Kifo cha Mfia-Imani

Gabriel, ambaye alilelewa katika familia ya kidini, alifundishwa kwamba nchi yake ya kuzaliwa ilikuwa katika mapambano ya vita takatifu. Hivyo, akiwa na umri wa miaka 19, alijitolea kutumikia jeshini na kuomba apelekwe kwenye eneo la vita. Kwa miezi 13 alipigana vita kali sana, wakati mwingine akiwa umbali wa kilometa moja na nusu kutoka kwa adui. “Ninakumbuka pindi moja hasa,” asema. “Kamanda wetu alituambia kwamba adui angeshambulia usiku huo. Tulikuwa na wasiwasi mwingi sana hivi kwamba tulirusha makombora usiku kucha.” Aliwaona watu wa nchi jirani kuwa maadui wake, waliostahili kufa. “Nilitaka tu kuua watu wengi iwezekanavyo. Kisha, kama marafiki wangu wengi, nilitaka nife kifo cha mfia-imani.”

Hata hivyo, baada ya muda Gabriel alivunjika moyo. Alikimbilia milimani, akavuka mpaka kwa tahadhari na kuingia katika nchi isiyounga mkono upande wowote, kisha akasafiri kwenda Ulaya. Aliendelea kumwuliza Mungu sababu iliyofanya maisha yawe magumu sana, na kama matatizo ni adhabu kutoka kwake. Alikutana na Mashahidi wa Yehova, ambao walimwonyesha kutoka katika Biblia ni kwa nini maisha yamejaa matatizo leo.—Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5.

Kadiri Gabriel alivyozidi kujifunza Biblia, ndivyo alivyozidi kung’amua kwamba ina kweli. “Nilijifunza kwamba tunaweza kuishi milele katika dunia paradiso. Inashangaza kwamba hilo ni jambo nililotamani tangu nilipokuwa mtoto.” Gabriel alifarijiwa na Biblia ambayo ilituliza moyo wake ambao hadi wakati huo ulikuwa wenye kusumbuka. Maumivu makali ya kihisia-moyo aliyokuwa nayo yakaanza kwisha. Kwa hiyo, wakati alipokutana na Daniel, adui wake wa zamani, Gabriel hakumchukia kamwe. Lakini nini kilichomfanya Daniel aende Ulaya?

“Ikiwa kwa Kweli Uko, Tafadhali Nisaidie!”

Daniel alilelewa akiwa Mkatoliki na aliitwa kutumikia jeshini akiwa na umri wa miaka 18. Alipelekwa kupigana katika vita ileile ambayo Gabriel alipigana lakini akiwa upande tofauti. Karibu na eneo la mapigano, Daniel alikuwa amepanda kifaru wakati kiliposhambuliwa kwa kombora. Marafiki wake waliuawa, naye akajeruhiwa vibaya na kuchukuliwa kuwa mfungwa. Alikaa katika hospitali na katika kambi miezi mingi kabla ya kuhamishiwa nchi isiyounga mkono upande wowote. Akiwa peke yake na fukara, alifikiria kujiua. Daniel alimwomba Mungu hivi: “Ikiwa kwa kweli uko, tafadhali nisaidie!” Siku iliyofuata, Mashahidi wa Yehova walimtembelea na kujibu maswali mengi aliyokuwa nayo. Mwishowe alisafiri kwenda Ulaya akiwa mkimbizi. Kwa mara nyingine tena, Daniel alishirikiana na Mashahidi na kujifunza Biblia. Yale aliyojifunza yalituliza wasiwasi na uchungu aliokuwa nao.

Gabriel na Daniel sasa ni marafiki sana, walioungana katika udugu wa kiroho wakiwa Mashahidi wa Yehova waliobatizwa. “Kumpenda Yehova na ujuzi wa Biblia zimenisaidia kuona mambo jinsi ayaonavyo. Daniel si adui yangu tena. Miaka kadhaa iliyopita singesita kumwua. Biblia imenifunza jambo lililo kinyume kabisa cha hilo—kuwa tayari kufa kwa ajili yake,” asema Gabriel.

“Niliona watu wa dini na mataifa mbalimbali wakiuana,” asema Daniel. “Na kwenye pande tofauti za vita kulikuwa na watu wa dini ileile waliokuwa wakiuana. Nilipoona hayo, nilihisi kwamba Mungu ndiye aliyestahili kulaumiwa. Sasa najua kwamba Shetani ndiye husababisha vita vyote. Mimi na Gabriel sasa ni waamini wenzi. Hatutapigana tena kamwe!”

“Neno la Mungu Liko Hai na Hukazia Nguvu”

Kwa nini Abraham, Robert, Gabriel, na Daniel walibadilika kwa njia ya kutazamisha hivyo? Waliwezaje kuondoa chuki nyingi sana na majonzi kutoka mioyoni mwao?

Kila mmoja wa watu hao alisoma, akatafakari, na kujifunza kweli kutoka katika Biblia, ambayo ni “hai na hukazia nguvu.” (Waebrania 4:12) Mtungaji wa Biblia ndiye Muumba wa wanadamu, ambaye anajua jinsi ya kuvuta ifaavyo moyo wa mtu ambaye yu tayari kusikiliza na kujifunza. “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” Msomaji anaporuhusu Biblia imwongoze, anaanza kufuata kanuni na viwango vipya. Anaanza kujifunza jinsi ambavyo Yehova huona mambo. Kufanya hivyo humletea manufaa nyingi, kutia ndani kumaliza madhara ya vita.—2 Timotheo 3:16.

Neno la Mungu linaeleza kwamba hakuna watu wa taifa fulani, jamii, au kabila ambao ni bora kuliko wengine. “Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” Msomaji anayekubaliana na maneno hayo husaidiwa polepole kushinda chuki ya kijamii au ya kitaifa.—Matendo 10:34, 35.

Unabii mbalimbali wa Biblia huonyesha kwamba karibuni Mungu ataondoa mfumo wa sasa wa utawala wa kibinadamu na kuleta Ufalme wake wa Kimesiya. Kupitia serikali hiyo, Mungu “avikomesha vita hata mwisho wa dunia.” Mashirika ambayo huendeleza vita na kuchochea watu kupigana yataondolewa. Wahasiriwa wa vita watafufuliwa na kupewa fursa ya kuishi katika dunia paradiso. Hakuna mtu atakayelazimika kukimbia kwa kutishwa na mchokozi au mkandamizaji.—Zaburi 46:9; Danieli 2:44; Matendo 24:15.

Kuhusu wanadamu watakaoishi wakati huo Biblia yasema: “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake . . . Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu.” Hakuna hasara wala madhara ambayo hayatamalizwa. Kuweka imani katika tumaini kama hilo huondoa majonzi na huzuni polepole kutoka katika moyo wa mtu.—Isaya 65:21-23.

Biblia ni tiba ya moyo yenye nguvu kwelikweli. Mafundisho yake tayari yanamaliza madhara ya vita. Waliokuwa maadui zamani wanaunganishwa katika udugu wa kimataifa. Kumalizwa kwa madhara hayo kutaendelea katika mfumo mpya wa Mungu hadi wakati ambapo hakutakuwa tena na chuki na uchungu, huzuni na majonzi katika mioyo ya wanadamu. Muumba anaahidi kwamba “mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.”—Isaya 65:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

“Nilijifunza kutoka katika Biblia kwamba miaka hiyo yote ambayo nilitumia vitani ilikuwa imepotea bure”

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Biblia inaweza kuwa na uvutano wenye nguvu katika mioyo ya maadui wa zamani

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Chuki na uchungu hutoweka polepole na mahali pake huchukuliwa na kutumainiana na urafiki

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Msomaji anaporuhusu Biblia imwongoze, anaanza kufuata kanuni na viwango vipya

[Picha katika ukurasa wa 7]

Waliokuwa maadui zamani sasa wanaunganishwa katika udugu wa kimataifa

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]

Kambi ya Wakimbizi: UN PHOTO 186811/J. Isaac