Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mjengwe na Upendo

Mjengwe na Upendo

Mjengwe na Upendo

“Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” —MATHAYO 22:37.

1. (a) Ni baadhi ya sifa zipi zinazositawishwa na Mkristo? (b) Ni sifa ipi ya Kikristo iliyo ya maana zaidi, na kwa nini?

MKRISTO husitawisha sifa nyingi ili awe mhudumu mwenye matokeo. Kitabu cha Mithali hukazia thamani ya ujuzi, uelewevu, na hekima. (Mithali 2:1-10) Mtume Paulo alikazia uhitaji wa kuwa na imani thabiti na tumaini lenye nguvu. (Waroma 1:16, 17; Wakolosai 1:5; Waebrania 10:39) Uvumilivu na kujidhibiti ni sifa muhimu pia. (Matendo 24:25; Waebrania 10:36) Hata hivyo, kuna sifa moja ambayo ikikosekana hupunguza thamani ya sifa nyingine zote na hata yaweza kuzifanya zisiwe na thamani yoyote. Sifa hiyo ni upendo.—1 Wakorintho 13:1-3, 13.

2. Yesu alionyeshaje umuhimu wa upendo, na jambo hilo latokeza maswali gani?

2 Yesu alionyesha umuhimu wa upendo aliposema hivi: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Kwa kuwa upendo ndiyo alama ya kutambulisha Mkristo wa kweli, twahitaji kuuliza maswali kama vile, Upendo ni nini? Kwa nini upendo ni muhimu sana, hivi kwamba Yesu alisema kwamba huo hasa ndio hutambulisha wanafunzi wake? Twaweza kusitawishaje upendo? Twapaswa kuwapenda nani? Acheni tuzungumzie maswali hayo.

Upendo Ni Nini?

3. Upendo waweza kufafanuliwaje, na kwa nini wahusisha akili na moyo?

3 Ufafanuzi mmoja kuhusu upendo ni, ‘uhusiano mchangamfu na wa kibinafsi au shauku yenye kina, kupendezwa sana na mtu mwingine.’ Ni sifa ambayo huchochea watu wafanye mambo yanayowanufaisha wengine, nyakati nyingine wakifanya hivyo kwa kujidhabihu sana. Kulingana na ufafanuzi wa Biblia, upendo wahusisha akili na moyo. Akili, au uwezo wa kufikiri, hutimiza fungu fulani kwa sababu mtu anayependa hufanya hivyo akitambua kwamba yeye pamoja na wanadamu wengine anaowapenda, wana udhaifu na vilevile sifa zenye kuvutia. Uwezo wa kufikiri wahusika hata zaidi kwa kuwa kuna wale ambao Mkristo huwapenda—nyakati nyingine, hata ingawa nyuto zao hazimpendezi—kwa kuwa kutokana na kuisoma Biblia anajua kwamba Mungu anataka afanye hivyo. (Mathayo 5:44; 1 Wakorintho 16:14) Hata hivyo, kwa asili upendo hutoka moyoni. Upendo halisi kama uonyeshwavyo katika Biblia hautegemei tu uwezo wa kufikiri. Wahusisha unyofu mwingi na kujitoa kabisa kihisia-moyo.—1 Petro 1:22.

4. Upendo ni kifungo chenye nguvu katika njia gani?

4 Ni nadra sana kwa watu ambao ni wenye ubinafsi kudumisha uhusiano wenye upendo wa kweli kwa sababu mtu anayependa huwa tayari kutanguliza masilahi ya mwingine. (Wafilipi 2:2-4) Maneno ya Yesu “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea” ni ya kweli hasa wakati kutoa kunapokuwa tendo la upendo. (Matendo 20:35) Upendo ni kifungo chenye nguvu. (Wakolosai 3:14) Mara nyingi upendo hutia ndani urafiki, lakini vifungo vya upendo ni vyenye nguvu zaidi ya vifungo vya urafiki. Uhusiano wa kimahaba kati ya mume na mke wake nyakati nyingine husemwa kuwa upendo; hata hivyo, upendo ambao Biblia hututia moyo tusitawishe hudumu kuliko uvutio wa kimwili. Mume na mke wanapopendana kwelikweli, huendelea kuwa pamoja hata isipowezekana tena kuwa na uhusiano wa kimwili kwa sababu ya udhaifu unaosababishwa na uzee au kwa sababu mmoja wao hajiwezi.

Upendo—Sifa Muhimu

5. Kwa nini upendo ni sifa muhimu kwa Mkristo?

5 Kwa nini upendo ni sifa muhimu kwa Mkristo? Kwanza, ni kwa sababu Yesu aliamuru wafuasi wake wapendane. Alisema hivi: “Nyinyi ni marafiki wangu ikiwa mwafanya lile ninalowaamuru nyinyi. Mambo haya nawaamuru nyinyi, kwamba mpendane.” (Yohana 15:14, 17) Pili, tukiwa waabudu wa Yehova twapaswa kumwiga kwa kuwa yeye ndiye mfano halisi wa sifa ya upendo. (Waefeso 5:1; 1 Yohana 4:16) Biblia husema kwamba kutwaa ujuzi kuhusu Yehova na Yesu kwamaanisha uhai udumuo milele. Twawezaje kusema twamjua Mungu ikiwa hatujitahidi kuwa kama yeye? Mtume Yohana alisababu hivi: “Yeye ambaye hapendi hajaja kujua Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.

6. Upendo unawezaje kusawazisha hali mbalimbali maishani mwetu?

6 Upendo ni muhimu kwa sababu hii ya tatu: Hutusaidia kusawazisha hali mbalimbali maishani mwetu na kufanya tuwe na nia nzuri tufanyapo mambo fulani. Kwa mfano, ni muhimu kuendelea kutwaa ujuzi wa Neno la Mungu. Ujuzi huo ni kama chakula kwa Mkristo. Humsaidia Mkristo akue hadi kufikia ukomavu na kutenda kupatana na mapenzi ya Mungu. (Zaburi 119:105; Mathayo 4:4; 2 Timotheo 3:15, 16) Hata hivyo, Paulo alionya hivi: “Ujuzi hututumuka, lakini upendo hujenga.” (1 Wakorintho 8:1) Hakuna ubaya wowote wa kuwa na ujuzi sahihi. Sisi ndio wenye tatizo—tuna maelekeo ya dhambi. (Mwanzo 8:21) Ikiwa hakuna upendo wa kusawazisha hali, ujuzi waweza kumfanya mtu atutumuke, na kujiona kuwa bora kuliko wengine. Jambo hilo haliwezi kutokea ikiwa anachochewa haswa na upendo. “Upendo . . . haujigambi, haujitutumui.” (1 Wakorintho 13:4) Mkristo anayechochewa na upendo hajigambi, hata anapokuwa na ujuzi mwingi. Upendo humfanya aendelee kuwa mnyenyekevu na humzuia asijitafutie sifa.—Zaburi 138:6; Yakobo 4:6.

7, 8. Upendo hutusaidiaje tukazie fikira mambo yaliyo ya maana zaidi?

7 Paulo aliwaandikia Wafilipi hivi: “Hili ndilo mimi huendelea kusali, kwamba upendo wenu upate kuzidi bado hata zaidi na zaidi pamoja na ujuzi sahihi na ufahamu kamili; kwamba mpate kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:9, 10) Upendo wa Kikristo utatusaidia kutii kitia-moyo hicho ili kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi. Kwa mfano, fikiria maneno ya Paulo kwa Timotheo: “Ikiwa mtu yeyote anajitahidi kufikilia cheo cha mwangalizi, yeye ni mwenye kutamani kazi bora.” (1 Timotheo 3:1) Katika mwaka wa utumishi wa 2000, idadi ya makutaniko ulimwenguni iliongezeka kwa kiwango cha 1,502, na hivyo kufikia jumla mpya ya 91,487. Kwa hiyo, wazee zaidi wanahitajika, na wale wanaojitahidi kufikia mapendeleo hayo wapaswa kupongezwa.

8 Hata hivyo, wale wanaojitahidi kufikia mapendeleo ya usimamizi wanadumisha usawaziko unaofaa wakikumbuka kusudi la pendeleo hilo. Kuwa na madaraka tu au kuwa mashuhuri siyo jambo la maana. Wazee wanaompendeza Yehova huchochewa na upendo kwake na kwa ndugu zao. Hawatafuti umashuhuri au kuvutia wengine. Baada ya kuwashauri wazee wa kutaniko wadumishe mtazamo unaofaa, mtume Petro alikazia uhitaji wa kuwa na “hali ya akili ya kujishusha chini.” Aliwashauri wote katika kutaniko hivi: “Jinyenyekezeni chini ya mkono wa Mungu wenye uweza.” (1 Petro 5:1-6) Yafaa yeyote anayejitahidi kufikia mapendeleo afikirie kielelezo cha wazee wengi sana ulimwenguni pote ambao wanafanya kazi kwa bidii, ni wanyenyekevu, na hivyo wanakuwa baraka kwa makutaniko yao.—Waebrania 13:7.

Nia Nzuri Hutusaidia Kuvumilia

9. Kwa nini Wakristo hukumbuka baraka ambazo Yehova amewaahidi?

9 Twaona umuhimu wa kuchochewa na upendo katika njia nyingine. Wale wanaofuatia ujitoaji-kimungu kwa kuchochewa na upendo, Biblia huwaahidi baraka tele sasa na baraka za ajabu zisizowazika wakati ujao. (1 Timotheo 4:8) Mkristo anayeamini kwa dhati baraka hizo na anayesadiki kwamba Yehova “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii” husaidiwa kudumu akiwa imara katika imani. (Waebrania 11:6) Wengi wetu twatamani kutimizwa kwa ahadi za Mungu na twarudia maoni ya mtume Yohana aliyesema hivi: “Ameni! Njoo, Bwana Yesu.” (Ufunuo 22:20) Naam, kutafakari baraka tulizoahidiwa ikiwa tunakuwa waaminifu hutuimarisha tuvumilie, kama vile Yesu alivyovumilia kwa kukumbuka “shangwe iliyowekwa mbele yake.”—Waebrania 12:1, 2.

10, 11. Kuchochewa na upendo hutusaidiaje kuvumilia?

10 Lakini vipi, ikiwa jambo pekee linalotuchochea zaidi kumtumikia Yehova ni tamaa ya kuishi katika ulimwengu mpya? Basi tunaweza kukosa subira kwa urahisi au kutoridhika mambo yanapokuwa magumu au yasipotukia kama tutakavyo au kwa wakati tunaotumaini. Twaweza kukabili hatari kubwa ya kupeperushwa mbali. (Waebrania 2:1; 3:12) Paulo alizungumza juu ya mwenzi wake wa zamani aliyeitwa Demasi, ambaye alimwacha. Kwa nini? Kwa sababu “aliupenda mfumo wa mambo uliopo.” (2 Timotheo 4:10) Mtu yeyote anayetumikia akiwa na sababu za kichoyo tu anakabili hatari ya kutenda vivyo hivyo. Huenda akavutiwa na fursa za sasa za kujiendeleza zipatikanazo katika ulimwengu na kutotaka kujidhabihu sasa kwa kutumainia baraka zitakazokuja.

11 Ingawa inafaa na ni jambo la kawaida kuwa na tamaa ya kupokea baraka za wakati ujao na kutumainia kuondolewa majaribu, upendo huzidisha uthamini wetu kwa jambo lipasalo kuwa la maana zaidi maishani mwetu. Mapenzi ya Yehova, wala si yetu ndilo jambo la maana. (Luka 22:41, 42) Naam, upendo hutujenga. Hutupa uradhi wa kumsubiri Mungu wetu, huku tukitosheka na baraka zozote anazotupa na kuwa na uhakika kwamba tutapokea kwa wakati wake kila kitu alichoahidi—na zaidi. (Zaburi 145:16; 2 Wakorintho 12:8, 9) Kwa sasa, upendo hutusaidia tuendelee kutumikia bila ubinafsi kwa sababu “upendo . . . hautafuti masilahi yao wenyewe.”—1 Wakorintho 13:4, 5.

Wakristo Wapaswa Kuwapenda Nani?

12. Kulingana na Yesu twapaswa kuwapenda nani?

12 Yesu alitoa kanuni ya msingi kuhusu watu tunaopaswa kuwapenda aliponukuu taarifa mbili kutoka Sheria ya Kimusa. Alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote” na, “Lazima umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.”—Mathayo 22:37-39.

13. Twawezaje kujifunza kumpenda Yehova hata ingawa hatuwezi kumwona?

13 Kutokana na maneno ya Yesu, ni wazi kwamba kwanza kabisa twapaswa kumpenda Yehova. Lakini hatuzaliwi tukiwa tunampenda Yehova kikamili. Hilo ni jambo tunalopaswa kusitawisha. Tuliposikia mara ya kwanza kumhusu, tulivutwa kwake na mambo tuliyosikia. Hatua kwa hatua tukajifunza jinsi alivyotayarisha dunia kwa ajili ya wanadamu. (Mwanzo 2:5-23) Tulijifunza jinsi ambavyo ameshughulika na wanadamu, bila kutuacha wakati dhambi ya kwanza ilipoingia katika familia ya binadamu, lakini akachukua hatua za kutukomboa. (Mwanzo 3:1-5, 15) Alishughulika kwa fadhili na wale waliokuwa waaminifu, na hatimaye akatoa Mwana wake mzaliwa-pekee ili tusamehewe dhambi zetu. (Yohana 3:16, 36) Tulimthamini Yehova zaidi ujuzi huo ulipoongezeka. (Isaya 25:1) Mfalme Daudi alisema kwamba alimpenda Yehova kwa sababu ya utunzaji Wake wenye upendo. (Zaburi 116:1-9) Leo, Yehova hututunza, hutuongoza, hutuimarisha, na kututia moyo. Kadiri tuzidivyo kujifunza mengi kumhusu, ndivyo upendo wetu uzidivyo kuongezeka.—Zaburi 31:23; Sefania 3:17; Waroma 8:28.

Twawezaje Kuonyesha Upendo Wetu?

14. Twaweza kuonyeshaje kwamba tunampenda Mungu kikweli?

14 Bila shaka, watu wengi ulimwenguni husema kwamba wanampenda Mungu, lakini wanatenda kinyume cha dai lao. Twawezaje kujua kwamba tunampenda Yehova kwelikweli? Twaweza kuzungumza naye katika sala na kumweleza jinsi tunavyohisi. Na tunaweza kutenda kwa njia inayodhihirisha upendo wetu. Mtume Yohana alisema: “Yeyote yule ashikaye hasa neno [la Mungu], kwa kweli katika mtu huyu kumpenda Mungu kumefanywa kukamilifu. Kwa hili tuna ujuzi kwamba sisi tumo katika muungano na yeye.” (1 Yohana 2:5; 5:3) Kushirikiana pamoja na kuishi maisha safi kiadili ni baadhi ya mambo ambayo Neno la Mungu hutuambia tufanye. Tunaepuka unafiki, tunasema kweli, na kufikiria mambo yanayofaa. (2 Wakorintho 7:1; Waefeso 4:15; 1 Timotheo 1:5; Waebrania 10:23-25) Tunaonyesha upendo kwa kuwasaidia walio na uhitaji wa kimwili. (1 Yohana 3:17, 18) Na hatusiti kuwaeleza wengine kuhusu Yehova. Hilo latia ndani kushiriki kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote. (Mathayo 24:14; Waroma 10:10) Tunapotii Neno la Mungu katika mambo hayo twathibitisha kwamba tunampenda Yehova kikweli.

15, 16. Kumpenda Yehova kuliwaathirije wengi mwaka jana?

15 Kumpenda Yehova husaidia watu wafanye maamuzi mazuri. Mwaka jana, upendo huo ulichochea watu 288,907 wajiweke wakfu kwake na kuonyesha uamuzi huo kupitia ubatizo wa maji. (Mathayo 28:19, 20) Wakfu wao ulikuwa na kusudi. Uliashiria badiliko fulani maishani mwao. Kwa mfano, Gazmend alikuwa mmojawapo wa wachezaji mashuhuri wa mpira wa vikapu nchini Albania. Yeye na mke wake walijifunza Biblia kwa miaka kadhaa na licha ya vizuizi mbalimbali, hatimaye walistahili kuwa wahubiri wa Ufalme. Gazmend alibatizwa mwaka jana, akiwa miongoni mwa watu 366 waliobatizwa nchini Albania katika mwaka wa utumishi wa 2000. Gazeti moja lilichapisha makala kumhusu na kusema hivi: “Maisha yake yana kusudi, na kwa sababu hiyo, yeye na familia yake wanafurahia wakati ulio bora zaidi maishani mwao. Lililo muhimu kwake si kuona kadiri anavyoweza kujinufaisha bali ni jinsi anavyoweza kujitoa zaidi kusaidia wengine.”

16 Vivyo hivyo, dada aliyebatizwa hivi karibuni ambaye anafanya kazi katika kampuni ya mafuta nchini Guam aliahidiwa kazi yenye kuvutia. Baada ya kupandishwa cheo kwa miaka mingi, hatimaye alipewa fursa ya kuwa mwanamke wa kwanza makamu msimamizi katika historia ya kampuni hiyo. Hata hivyo, sasa alikuwa amejiweka wakfu kwa Yehova. Kwa hiyo baada ya kuzungumzia jambo hilo na mumewe, dada huyo mpya alikataa kazi hiyo na badala yake akapanga kutafuta kazi isiyo ya wakati wote ili afanye maendeleo na kuwa mhudumu wa wakati wote, yaani painia. Kumpenda Yehova kulimchochea atake kumtumikia akiwa painia badala ya kufuatia masilahi ya kifedha ya ulimwengu huu. Kwa kweli, upendo huo ulichochea watu 805,205 ulimwenguni pote kushiriki katika njia mbalimbali za huduma ya painia katika mwaka wa utumishi wa 2000. Mapainia hao walidhihirisha imani na upendo ulioje!

Wachochewa Kumpenda Yesu

17. Yesu anatuwekea kielelezo gani kizuri cha upendo?

17 Yesu ni kielelezo kizuri sana cha mtu aliyechochewa na upendo. Kabla ya kuwako kwake akiwa binadamu, alimpenda Baba yake na kuwapenda wanadamu. Akiwa mfano halisi wa sifa ya hekima, alisema hivi: “Ndipo nilipokuwa pamoja [na Yehova], kama stadi wa kazi; nikawa furaha yake kila siku; nikifurahi daima mbele zake; nikiifurahia dunia inayokaliwa na watu; na furaha yangu ilikuwa pamoja na wanadamu.” (Mithali 8:30, 31) Upendo wa Yesu ulimchochea kuacha makao yake ya kimbingu na kuzaliwa akiwa mtoto mchanga asiyejiweza. Alishughulika kwa saburi na fadhili na watu wasikivu na wa hali ya chini na kuteswa na maadui wa Yehova. Hatimaye akafa kwa ajili ya wanadamu wote kwenye mti wa mateso. (Yohana 3:35; 14:30, 31; 15:12, 13; Wafilipi 2:5-11) Ni kielelezo kizuri kama nini cha kichocheo kinachofaa!

18. (a) Tunasitawishaje upendo kwa Yesu? (b) Ni katika njia zipi tunadhihirisha kwamba twampenda Yesu?

18 Wale walio na mioyo mizuri wasomapo masimulizi ya maisha ya Yesu katika Gospeli na kutafakari baraka nyingi ambazo wamepata kwa sababu ya uaminifu wake, jambo hilo hufanya wampende zaidi kutoka moyoni. Sisi leo ni kama watu waliozungumziwa na Petro aliposema hivi: “Ingawa hamkumwona [Yesu] kamwe, mwampenda.” (1 Petro 1:8) Twaonyesha upendo tunapodhihirisha imani kwake na kuiga maisha yake ya kujidhabihu. (1 Wakorintho 11:1; 1 Wathesalonike 1:6; 1 Petro 2:21-25) Katika Aprili 19, 2000, watu 14,872,086 walikumbushwa sababu zetu za kumpenda Yesu walipohudhuria Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo chake. Ilikuwa idadi kubwa kama nini! Na inatia nguvu kama nini kujua kwamba watu wengi hivyo wanapendezwa na wokovu kupitia dhabihu ya Yesu! Kwa kweli, tunajengwa na upendo kwa Yehova na Yesu na upendo wao kwetu.

19. Ni maswali gani kuhusu upendo yatakayozungumziwa katika makala ifuatayo?

19 Yesu alisema kwamba twapaswa kumpenda Yehova kwa moyo wetu wote, nafsi, akili, na nguvu. Lakini alisema pia kwamba twapaswa kumpenda jirani yetu kama sisi wenyewe. (Marko 12:29-31) Upendo huo watia ndani nani? Na upendo kwa jirani hutusaidiaje kudumisha usawaziko mzuri na nia inayofaa? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala ifuatayo.

Je, Wakumbuka?

• Kwa nini upendo ni sifa muhimu?

• Twaweza kujifunzaje kumpenda Yehova?

• Mwenendo wetu hudhihirishaje kwamba tunampenda Yehova?

• Twaweza kudhihirishaje kwamba tunampenda Yesu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10, 11]

Upendo hutusaidia tungoje kitulizo kwa saburi

[Picha katika ukurasa wa 12]

Dhabihu kubwa ya Yesu hutuchochea tumpende