Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Upendo Wako Umepanuka Kadiri Gani?

Upendo Wako Umepanuka Kadiri Gani?

Upendo Wako Umepanuka Kadiri Gani?

“Lazima umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.”—MATHAYO 22:39.

1. Ikiwa tunampenda Yehova, kwa nini ni lazima tupende jirani yetu pia?

WAKATI Yesu alipoulizwa ni amri ipi iliyo kubwa zaidi, alijibu hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” Kisha akanukuu amri ya pili inayofanana na hiyo ya kwanza: “Lazima umpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mathayo 22:37, 39) Ndiyo, kupenda jirani ni alama ya Mkristo. Kwa kweli, ikiwa tunampenda Yehova, lazima tupende jirani yetu. Kwa nini? Kwa sababu tunaonyesha twampenda Mungu kwa kutii Neno lake, nalo Neno lake hutuamuru tupende jirani yetu. Kwa hiyo, ikiwa hatupendi ndugu na dada zetu, hatuwezi kumpenda Mungu kikweli.—Waroma 13:8; 1 Yohana 2:5; 4:20, 21.

2. Twapaswa kuonyesha jirani yetu upendo wa aina gani?

2 Yesu aliposema kwamba tupende jirani yetu, hakuwa akizungumzia urafiki tu. Alikuwa akirejezea upendo ulio tofauti na ule ambao kwa kawaida huwa katika familia au kati ya mwanamume na mwanamke. Alikuwa akizungumzia aina ya upendo alio nao Yehova kwa watumishi wake waliojiweka wakfu na ule ambao watumishi wake wako nao kwake. (Yohana 17:26; 1 Yohana 4:11, 19) Mwandishi Myahudi—ambaye, kama Yesu alivyotambua, alikuwa anasema kwa kutumia akili—alikubaliana na Yesu kwamba upendo kwa Mungu wapaswa kuwa “kwa moyo wote wa mtu na kwa uelewevu wote wa mtu na kwa nguvu zote za mtu.” (Marko 12:28-34) Alikuwa sahihi. Upendo ambao Mkristo husitawisha kwa Mungu na kwa jirani wahusisha hisia-moyo zetu na uwezo wetu wa kufikiri. Unahisiwa moyoni na kuelekezwa na akili.

3. (a) Yesu alimfundishaje “mtu fulani aliyekuwa na ujuzi mwingi katika Sheria” kwamba anapaswa kuwa na maoni yaliyopanuka kuhusu ni nani aliye jirani yake? (b) Mfano wa Yesu watumikaje kwa Wakristo leo?

3 Kama inavyoripotiwa na Luka, Yesu aliposema kwamba twapaswa kupenda jirani yetu, “mtu fulani mwenye ujuzi mwingi katika Sheria” aliuliza: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Yesu alimjibu kwa kutumia mfano. Mtu fulani alipigwa, akapokonywa vitu, akaachwa nusura kufa kando ya barabara. Kwanza kuhani, kisha Mlawi walipitia barabara hiyo. Wote wawili hawakujishughulisha naye. Hatimaye Msamaria akatokea, akamwona mtu huyo aliyejeruhiwa, na kumtendea kwa fadhili nyingi. Kati ya watu hao watatu ni yupi aliyekuwa jirani ya mtu aliyejeruhiwa? Jibu lilikuwa wazi. (Luka 10:25-37) Huenda mtu huyo aliyekuwa na ujuzi mwingi katika Sheria alishangaa kusikia Yesu akisema kwamba Msamaria aweza kuwa jirani bora kuliko kuhani na Mlawi. Ni wazi kwamba Yesu alikuwa anamsaidia mtu huyo ampende jirani yake kwa njia pana zaidi. Wakristo pia huonyesha upendo kwa njia hiyo. Fikiria watu wote ambao Wakristo huwaonyesha upendo.

Upendo Katika Familia

4. Ni wapi ambapo Mkristo hudhihirisha upendo kwanza?

4 Wakristo huwapenda washiriki wao wa familia—wake huwapenda waume, waume huwapenda wake, wazazi huwapenda watoto. (Mhubiri 9:9; Waefeso 5:33; Tito 2:4) Ni kweli kwamba kwa kawaida familia nyingi hupendana. Hata hivyo, ripoti za ndoa zilizovunjika, kutendwa vibaya kwa wenzi, kutojali au kutenda watoto vibaya, zaonyesha kwamba leo familia zinakabili mkazo nao upendo wa asili katika familia hautoshi kuiunganisha. (2 Timotheo 3:1-3) Ili kufanikisha kwelikweli maisha yao ya familia, Wakristo wanahitaji kudhihirisha aina ya upendo ambao Yehova na Yesu wanao.—Waefeso 5:21-27.

5. Wazazi humtegemea nani awasaidie kulea watoto wao, na wengi wamepata matokeo gani?

5 Wazazi Wakristo huwaona watoto wao kama kitu chenye thamani sana kutoka kwa Yehova, nao humtegemea Yehova awasaidie kuwalea. (Zaburi 127:3-5; Mithali 22:6) Katika njia hiyo wanasitawisha upendo wa Kikristo, ambao huwasaidia kulinda watoto wao na uvutano mbaya unaoweza kuathiri vijana. Tokeo ni kwamba wazazi wengi Wakristo wamepata shangwe kama ya mama mmoja nchini Uholanzi. Baada ya kutazama mwana wake akibatizwa—akiwa mmoja wa watu 575 waliobatizwa nchini Uholanzi mwaka jana—aliandika yafuatayo: “Sasa mradi wa kulea ambao nimeufanya kwa miaka 20 iliyopita umekuwa na matokeo. Wakati wote na nguvu—na vilevile maumivu, jitihada, na majonzi—sasa vimesahaulika.” Anafurahi kama nini kwamba mwana wake, alichagua mwenyewe, kumtumikia Yehova. Kilele cha wahubiri 31,089 walioripoti nchini Uholanzi mwaka jana chatia ndani wengi waliojifunza kumpenda Yehova kutoka kwa wazazi wao.

6. Upendo wa Kikristo waweza kusaidiaje kuimarisha kifungo cha ndoa?

6 Paulo aliuita upendo “kifungo kikamilifu cha muungano,” nao waweza kuokoa ndoa hata wakati wa magumu. (Wakolosai 3:14, 18, 19; 1 Petro 3:1-7) Wakati mwanamume mmoja katika kisiwa kidogo cha Rurutu kilicho umbali wa kilometa 700 kutoka Tahiti alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, mke wake alimpinga sana. Hatimaye, mke alichukua watoto, akamwacha mume na kwenda kuishi Tahiti. Hata hivyo, mwanamume huyo bado alionyesha upendo wake kwa kumtumia pesa kwa ukawaida na kupiga simu ili kujua ikiwa mke au watoto walihitaji kitu chochote. Kwa hiyo alifanya yote aliyoweza ili kutimiza wajibu wake mbalimbali wa Kikristo. (1 Timotheo 5:8) Alisali daima ili familia yake iungane tena, na hatimaye mke wake akarudi. Aliporudi, alimtendea kwa “upendo, uvumilivu, tabia-pole.” (1 Timotheo 6:11) Mwanamume huyo alibatizwa mwaka wa 1998, na baadaye alifurahi sana mke wake alipokubali kujifunza Biblia. Funzo hilo lilikuwa mojawapo ya mafunzo 1,351 yaliyoongozwa mwaka jana katika eneo lililo chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi ya Tahiti.

7. Kulingana na mwanamume mmoja nchini Ujerumani, ni nini kilichoimarisha ndoa yake?

7 Nchini Ujerumani mwanamume mmoja alimpinga mke wake aliyeonyesha upendezi katika kweli ya Biblia na alisadiki kwamba Mashahidi wa Yehova walitaka kumdanganya mke wake. Hata hivyo, baadaye, alimwandikia barua mtu aliyezungumza na mke wake mara ya kwanza: “Asante kwa kumjulisha mke wangu kwa Mashahidi wa Yehova. Hapo mwanzoni, nilikuwa na wasiwasi kwa sababu nilikuwa nimesikia mambo mengi mabaya kuwahusu. Lakini sasa, baada ya kuhudhuria mikutano pamoja na mke wangu, nimetambua jinsi nilivyokuwa nimekosea. Ninajua kwamba hii ndiyo kweli, na imeimarisha ndoa yetu zaidi.” Mashahidi wa Yehova 162,932 nchini Ujerumani—na wale 1,773 katika visiwa vilivyo chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi ya Tahiti—watia ndani familia nyingi ambazo zimeunganishwa na upendo wa kimungu.

Kuwapenda Ndugu Zetu Wakristo

8, 9. (a) Ni nani atufundishaye kuwapenda ndugu zetu, nao upendo hutuchochea kufanya nini? (b) Toa mfano wa jinsi upendo unavyoweza kusaidia ndugu wategemezane.

8 Paulo alisema hivi kwa Wakristo wa Thesalonike: “Nyinyi wenyewe hufundishwa na Mungu kupendana.” (1 Wathesalonike 4:9) Ndiyo, wale ‘wanaofundishwa na Yehova’ hupendana. (Isaya 54:13) Upendo wao hudhihirishwa kwa matendo, kama Paulo alivyoonyesha aliposema hivi: “Kupitia upendo mtumikiane kama watumwa.” (Wagalatia 5:13; 1 Yohana 3:18) Kwa mfano, wanafanya hivyo, wakati wanapotembelea ndugu na dada walio wagonjwa, wanapowatia moyo walioshuka moyo, na kutegemeza walio dhaifu. (1 Wathesalonike 5:14) Upendo wetu halisi wa Kikristo huchangia ukuzi wa paradiso yetu ya kiroho.

9 Katika Kutaniko la Ancón—mojawapo ya makutaniko 544 nchini Ekuado—akina ndugu walionyesha upendo wao kwa matendo. Tatizo la kifedha lilifanya wakose kazi au mapato, kwa hiyo wahubiri wakaamua kuchanga pesa kwa kuuza chakula kwa wavuvi wa eneo hilo wakati wavuvi hao waliporudi nyumbani usiku baada ya uvuvi. Wote walishirikiana kutia ndani watoto. Walihitaji kuanza kazi saa 7:00 za usiku ili chakula kiwe tayari ifikapo saa 10:00 za usiku, wakati wavuvi waliporudi. Akina ndugu waligawanya pesa walizochanga miongoni mwao wenyewe kulingana na mahitaji yao. Kusaidiana huko kulidhihirisha upendo halisi wa Kikristo.

10, 11. Twaweza kuonyeshaje upendo kwa ndugu tusiowajua kibinafsi?

10 Hata hivyo, upendo wetu hauhusishi tu Wakristo tunaowajua kibinafsi. Mtume Petro alisema hivi: “Iweni na upendo kwa ushirika mzima wa ndugu.” (1 Petro 2:17) Tunawapenda ndugu na dada zetu wote kwa sababu tunashirikiana nao katika kumwabudu Yehova Mungu. Twaweza kupata fursa ya kudhihirisha upendo huo wakati wa matatizo. Kwa mfano, katika mwaka wa utumishi wa 2000, mafuriko mabaya yaliathiri Msumbiji, na vita vya wenyewe kwa wenyewe vinavyoendelea nchini Angola vikaacha wengi wakiwa maskini. Idadi kubwa ya akina ndugu 31,725 nchini Msumbiji na 41,222 nchini Angola wameathiriwa na matukio hayo. Kwa hiyo, Mashahidi katika nchi jirani ya Afrika Kusini wametuma misaada mingi kwa ndugu zao katika nchi hizo ili kupunguza taabu yao. Utayari wao wa kutoa “ziada” yao kwa ndugu zao wenye uhitaji ulidhihirisha upendo wao.—2 Wakorintho 8:8, 13-15, 24.

11 Upendo huonekana pia, wakati akina ndugu wanapochangia ujenzi wa Majumba ya Ufalme na Majumba ya Kusanyiko katika nchi zenye umaskini. Mfano mmoja ni Visiwa vya Solomon. Licha ya misukosuko mingi, Visiwa vya Solomon vilikuwa na ongezeko la wahubiri la asilimia 6 mwaka jana, na kilele cha 1,697. Walipanga kujenga Jumba la Kusanyiko. Ingawa wakazi wengi wa kisiwa hicho walikuwa wanaikimbia nchi hiyo, wafanyakazi wa kujitolea walikuja kutoka Australia ili kusaidia katika kazi ya ujenzi. Hatimaye, wafanyakazi hao wa kujitolea wakalazimika kuondoka, lakini wakafanya hivyo baada ya kuzoeza ndugu wenyeji ili kukamilisha jengo hilo. Kiunzi cha feleji cha jumba hilo ambacho kilijengwa kimbele, kililetwa kwa meli kutoka Australia, na kukamilishwa kwa jengo hilo zuri la ibada—wakati ambapo majengo mengi yameachwa bila kukamilishwa—kutakuwa ushahidi mzuri kwa jina la Yehova na kwa upendo wa akina ndugu.

Kama Mungu, Twaupenda Ulimwengu

12. Tunamwigaje Yehova kwa mtazamo wetu kuelekea wale ambao si wa imani moja nasi?

12 Je, upendo wetu wahusisha tu familia yetu na udugu wetu? La, kwa kuwa sisi ni “waigaji wa Mungu.” Yesu alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” (Waefeso 5:1; Yohana 3:16) Kama Yehova, twawatendea wote kwa upendo—kutia ndani wale ambao si wa imani moja nasi. (Luka 6:35, 36; Wagalatia 6:10) Kwa habari hii hasa, twahubiri habari njema za Ufalme na kuwaambia wengine kuhusu tendo kubwa la Mungu la upendo alilotenda kwa niaba yao. Hilo laweza kuleta wokovu kwa yeyote anayesikiliza.—Marko 13:10; 1 Timotheo 4:16.

13, 14. Ni baadhi ya mambo yapi yaliyoonwa na akina ndugu walioonyesha upendo kwa watu ambao si Mashahidi, hata kwa kujitaabisha sana kibinafsi?

13 Fikiria wahudumu mapainia wa pekee wanne nchini Nepal. Walipewa mgawo katika jiji fulani lililo kusini-magharibi mwa nchi, na kwa miaka mitano iliyopita, wameonyesha upendo wao kwa kuhubiri kwa saburi katika jiji hilo na vijiji vilivyo mbali. Ili kuhubiri eneo lao, mara nyingi wanasafiri kwa baiskeli kwa muda wa saa nyingi kukiwa na halijoto ya nyuzi 40 Selsiasi. Upendo wao na “kuvumilia katika kazi iliyo njema” kulileta matokeo mazuri wakati funzo la kitabu lilipoanzishwa katika mojawapo ya vijiji hivyo. (Waroma 2:7) Mnamo Machi 2000, watu 32 walikuja kusikia hotuba ya watu wote iliyotolewa na mwangalizi wa mzunguko aliyekuwa anazuru. Nepal ilikuwa na kilele cha wahubiri 430 mwaka jana—ongezeko la asilimia 9. Ni wazi kwamba Yehova anabariki bidii na upendo wa ndugu katika nchi hiyo.

14 Nchini Kolombia mapainia wa pekee wa muda walienda kuhubiria Wahindi wa Wayuu. Ili kuwahubiria, walihitaji kujifunza lugha mpya, lakini hangaiko lao lenye upendo lilithawabishwa wakati watu 27 walipohudhuria hotuba ya watu wote, licha ya mvua nyingi. Jitihada yenye upendo kama hiyo iliyoonyeshwa na mapainia hao ilichangia ongezeko la asilimia 5 nchini Kolombia na kilele cha wahubiri 107,613. Nchini Denmark dada mmoja mzeemzee alitaka kushiriki habari njema na wengine, lakini alikuwa mlemavu. Pasipo kuzuiwa na hali hiyo, aliwasiliana na watu wenye kupendezwa kwa kuandika barua. Kwa sasa, anawasiliana kwa barua na watu 42 na kuongoza mafunzo ya Biblia 11. Yeye ni miongoni mwa kilele cha wahubiri 14,885 walioripoti nchini Denmark mwaka jana.

Penda Maadui Wako

15, 16. (a) Yesu alisema upendo wetu wapaswa kupanuka kadiri gani? (b) Ndugu wenye madaraka walishughulikaje kwa njia ya upendo na mtu fulani aliyetoa mashtaka yasiyo ya kweli dhidi ya Mashahidi wa Yehova?

15 Yesu alimwambia mtu aliyekuwa na ujuzi mwingi katika Sheria kwamba Msamaria angeweza kuonwa kuwa jirani. Katika Mahubiri yake ya Mlimani Yesu aliongezea kusema: “Nyinyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Lazima umpende jirani yako na kuchukia adui yako.’ Hata hivyo, mimi nawaambia nyinyi: Endeleeni kupenda maadui wenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowanyanyasa nyinyi; ili mpate kujithibitisha wenyewe kuwa wana wa Baba yenu aliye katika mbingu.” (Mathayo 5:43-45) Hata tunapopingwa na mtu fulani, tunajaribu ‘kufuliza kushinda lililo ovu kwa lililo jema.’ (Waroma 12:19-21) Ikiwezekana, tunamweleza kweli ambayo ndiyo kitu cha thamani zaidi kwetu.

16 Katika Ukrainia makala moja katika gazeti Kremenchuk Herald ilisema kwamba Mashahidi wa Yehova ni madhehebu hatari. Shtaka hilo lilikuwa zito kwa sababu barani Ulaya watu fulani huwaita Mashahidi wa Yehova madhehebu ili kushawishi watu kwamba utendaji wa Mashahidi wapaswa kuzuiwa au kupigwa marufuku. Kwa hiyo, mhariri alifikiwa na kuombwa achapishe makala mpya ya kusahihisha makala hiyo. Alikubali, lakini katika makala hiyo mpya akachapisha taarifa kwamba makala ya kwanza ilitegemea habari za kweli. Kwa hiyo ndugu wenye madaraka walimfikia tena wakiwa na habari zaidi. Hatimaye, mhariri huyo alitambua kwamba makala ya kwanza haikuwa sahihi na kuchapisha makala ya kukanusha habari hizo. Kushughulika naye kwa njia iliyo wazi na ya fadhili kulikuwa njia bora ya kushughulikia jambo hilo, na kulileta matokeo mazuri.

Twaweza Kusitawishaje Upendo?

17. Ni nini kionyeshacho kwamba huenda isiwe rahisi sikuzote kutendea wengine kwa upendo?

17 Mtoto anapozaliwa, wazazi wake humpenda mara moja. Kushughulika na watu wazima kwa upendo hakuwi jambo la asili sikuzote. Yaelekea hiyo ndiyo sababu Biblia hutuambia mara nyingi tupendane—ni jambo tunalohitaji kufanyia kazi. (1 Petro 1:22; 4:8; 1 Yohana 3:11) Yesu alijua kwamba upendo wetu ungejaribiwa aliposema kwamba twapaswa kumsamehe ndugu yetu “mpaka mara sabini na saba.” (Mathayo 18:21, 22) Paulo pia alituhimiza “[tuendelee] kuchukuliana mtu na mwenzake.” (Wakolosai 3:12, 13) Si ajabu kwamba tunaambiwa: “Fuatieni upendo”! (1 Wakorintho 14:1) Twaweza kufanyaje hivyo?

18. Ni nini kitakachotusaidia kusitawisha upendo kwa wengine?

18 Kwanza, sikuzote twaweza kukumbuka upendo tulio nao kwa Yehova Mungu. Upendo huo ni kichocheo chenye nguvu cha kupenda jirani yetu. Kwa nini? Kwa sababu tunapofanya hivyo, tunampa Baba yetu wa kimbingu sifa na utukufu. (Yohana 15:8-10; Wafilipi 1:9-11) Pili, twaweza kujaribu kuwa na maoni kama ya Yehova. Kila mara tunapotenda dhambi, tunatenda dhambi dhidi ya Yehova; hata hivyo yeye hutusamehe tena na tena na kuendelea kutupenda. (Zaburi 86:5; 103:2, 3; 1 Yohana 1:9; 4:18) Tukisitawisha maoni kama ya Yehova, tutawapenda wengine na kuwasamehe makosa wanayotutenda. (Mathayo 6:12) Tatu, tunaweza kuwatendea wengine kama tunavyotaka watutendee. (Mathayo 7:12) Kwa kuwa sisi ni watu wasio wakamilifu, mara nyingi twahitaji msamaha. Kwa mfano, tunaposema mambo yanayowaumiza wengine, tunatumaini kwamba watakumbuka kwamba kila mtu hufanya dhambi mara kwa mara kupitia mambo asemayo. (Yakobo 3:2) Tukitaka wengine watutendee kwa upendo, twapaswa kuwatendea kwa upendo.

19. Twaweza kutafutaje msaada wa roho takatifu ili kusitawisha upendo?

19 Nne, twaweza kutafuta msaada wa roho takatifu kwa sababu upendo ni sehemu ya matunda ya roho. (Wagalatia 5:22, 23) Urafiki, kupenda watu wa familia, na upendo wa mahaba mara nyingi hutokea kiasili. Lakini twahitaji msaada wa roho ya Yehova ili kusitawisha upendo alio nao Yehova, upendo ambao ni kifungo kikamilifu cha muungano. Tunaweza kutafuta msaada wa roho takatifu kwa kusoma Biblia iliyopuliziwa. Kwa mfano, tunaposoma juu ya maisha ya Yesu, tutaona jinsi alivyoshughulika na watu, na tunaweza kujifunza kumwiga. (Yohana 13:34, 35; 15:12) Zaidi ya hayo, twaweza kumwomba Yehova roho takatifu, hasa katika hali ambazo hufanya iwe vigumu kutenda kwa upendo. (Luka 11:13) Hatimaye, twaweza kufuatia upendo kwa kuwa karibu na kutaniko la Kikristo. Kuwa pamoja na ndugu na dada wenye upendo hutusaidia kusitawisha upendo.—Mithali 13:20.

20, 21. Mashahidi wa Yehova walidhihirishaje upendo kwa njia yenye kutokeza katika mwaka wa utumishi wa 2000?

20 Mwaka jana, kulikuwa na kilele cha wahubiri wa habari njema 6,035,564 ulimwenguni pote. Mashahidi wa Yehova walitumia jumla ya saa 1,171,270,425 wakitafuta watu ili kuwaeleza habari njema. Upendo ndio uliowawezesha kuvumilia joto, mvua, na baridi walipokuwa wakifanya kazi hiyo. Upendo ndio uliowachochea kuzungumza na wanashule na wafanyakazi wenzi na kuzungumza na watu wasiowajua barabarani na kwingineko. Watu wengi waliotembelewa na Mashahidi walikuwa wenye ubaridi, na wachache walipinga. Hata hivyo, wengine walipendezwa, hivi kwamba Mashahidi walifanya ziara za kurudia 433,454,049 na kuongoza mafunzo ya Biblia 4,766,631. *

21 Utendaji huo wote ulikuwa udhihirisho ulioje wa upendo ambao Mashahidi wa Yehova wanao kwa Mungu wao na kwa jirani zao! Upendo huo hautapoa kamwe. Tuna hakika kwamba ushahidi mwingi hata zaidi utatolewa kwa wanadamu mwaka wa utumishi wa 2001. Baraka za Yehova na ziendelee kuwa pamoja na waabudu wake waaminifu-washikamanifu na wenye bidii huku ‘wakiacha mambo yao yote yatendeke kwa upendo’!—1 Wakorintho 16:14.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Kwa habari kamili kuhusu Ripoti ya Mwaka wa Utumishi wa 2000, ona chati katika ukurasa wa 18-21.

Je, Waweza Kueleza?

• Tunamwiga nani tunapopenda jirani yetu?

• Upendo wetu wapaswa kupanuka kadiri gani?

• Ni baadhi ya mambo yapi yaliyoonwa yanayodhihirisha upendo wa Kikristo?

• Twaweza kusitawishaje upendo wa Kikristo?

[Maswali ya Funzo]

[Chati Picha katika ukurasa wa 18-21]

RIPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA 2000 YA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE

(Ona toleo la 1/1/2001)

[Picha katika ukurasa wa 15]

Upendo wa Kikristo waweza kuunganisha familia

[Picha katika ukurasa wa 17]

Upendo hutuchochea kuwaeleza wengine tumaini letu