Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watekelezaji wa Neno la Munngu Hupata Furaha

Watekelezaji wa Neno la Munngu Hupata Furaha

Watekelezaji wa Neno la Munngu Hupata Furaha

“Twatambua kwamba mkusanyiko huu ni mojawapo ya maandalizi ya Yehova ya kututayarisha kwa ajili ya utendaji zaidi wa Ufalme,” akasema mmojawapo wa wasemaji mwanzoni mwa Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova wa “Watekelezaji wa Neno la Mungu.” Aliendelea kusema hivi: “Tumejitayarisha kuagizwa juu ya maisha yenye furaha ya familia, kutiwa moyo kudumu katika tengenezo la Yehova, kuhimizwa kudumisha bidii katika utumishi wa Ufalme, na kukumbushwa kwamba twapaswa kuendelea kuwa macho.”

TANGU mwishoni mwa Mei 2000, mamilioni ya watekelezaji wa neno la Mungu na marafiki wao walifurika katika maelfu ya sehemu mbalimbali ulimwenguni pote ili kupokea elimu muhimu ya Biblia. Walijifunza nini katika siku hizo tatu za mkusanyiko?

Siku ya Kwanza—Kutosahau Matendo ya Yehova

Katika hotuba ya kufungua, mwenyekiti aliwakaribisha wasikilizaji wafurahie baraka zinazotokana na kumwabudu Yehova kwa umoja kwenye mikusanyiko. Wote waliohudhuria walihakikishiwa kwamba imani yao itaongezeka na uhusiano wao wa kibinafsi pamoja na Yehova utaimarishwa.

“Mungu mwenye furaha” ajua kile tunachohitaji ili tuwe na furaha. (1 Timotheo 1:11) Hivyo, hotuba yenye kichwa “Kutekeleza Mapenzi ya Mungu Huleta Furaha” ilikazia kwamba Neno la Yehova, Biblia, huonyesha njia bora zaidi ya maisha. (Yohana 13:17) Walipohojiwa, Mashahidi wa Yehova kadhaa ambao wametumikia kwa muda mrefu, walisema kwamba kufanya mapenzi ya Mungu chini ya hali mbalimbali hufanya maisha yetu yawe na kusudi zaidi. Hotuba iliyofuata, “Furahieni Wema wa Yehova,” ilikazia kwamba, wakiwa “waigaji wa Mungu,” Wakristo hutaka kutokeza “kila namna ya wema” maishani mwao. (Waefeso 5:1, 9) Njia moja yenye kutokeza ya kufanya hivyo ni kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi.—Zaburi 145:7.

Hotuba yenye kichwa “Endelea Ukiwa Imara Kama Ambaye Anaona Yeye Asiyeonekana” ilionyesha jinsi ambavyo imani yenye nguvu hutusaidia “kuona” Mungu asiyeonekana. Msemaji alieleza jinsi watu wa kiroho wanavyotambua sifa za Mungu, kutia ndani uwezo wake wa kujua hata yale tunayofikiri. (Mithali 5:21) Wale waliohojiwa walisimulia hatua ambazo wamechukua ili kusitawisha imani yenye nguvu zaidi na kutanguliza masilahi ya kiroho maishani mwao.

Kipindi cha asubuhi kilimalizika kwa hotuba ya msingi, “Msifuni Yehova—Mtekelezaji wa Mambo ya Ajabu.” Ilisaidia wasikilizaji wafahamu kwamba kadiri tujifunzavyo mengi kumhusu Yehova, ndivyo tupatavyo sababu zaidi za kumsifu akiwa Mtekelezaji wa mambo ya ajabu. Msemaji alisema: “Tunapotafakari kazi za ajabu za Mungu za uumbaji pamoja na mambo ya ajabu ambayo anatufanyia wakati huu, uthamini wa kutoka moyoni hutusukuma tumsifu. Tunapotafakari miujiza ambayo amefanya kwa niaba ya watu wake nyakati zilizopita, twataka kumsifu. Na kadiri tunavyotafakari ahadi na mambo ya ajabu ambayo bado Yehova atafanya, twatafuta njia za kuonyesha uthamini.”

Kipindi cha alasiri kilianza kwa hotuba “Usife Moyo Katika Kufanya Lililo Bora,” ambayo iliwakumbusha wasikilizaji wote kwamba mikazo ya ulimwengu huu yathibitisha kwamba mwisho uko karibu. (2 Timotheo 3:1) Hata hivyo, kwa kutokata tamaa, twaweza kuthibitisha kwamba sisi ni “namna iliyo na imani kuelekea kuhifadhi hai nafsi.”—Waebrania 10:39.

Ni shauri gani la Biblia lililotolewa kuhusu maisha ya familia? Mfululizo wa kwanza wa mkusanyiko—“Tii Neno la Mungu”—ulianza kwa sehemu yenye kichwa “Katika Kuchagua Mwenzi wa Ndoa.” Mojawapo ya maamuzi mazito zaidi ambayo watu hufanya ni kuchagua mwenzi wa ndoa. Hivyo, Wakristo wanataka kungoja hadi wakomae ndipo wafunge ndoa, na wanapaswa kuoa au kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Sehemu iliyofuata ya mfululizo huo ilizungumzia jinsi Yehova anavyotamani familia zote za Kikristo zifanikiwe zikiwa familia zenye nguvu, na ilitaja njia mbalimbali zenye kutumika ambazo kupitia hizo jambo hilo laweza kutimizwa. Sehemu ya mwisho iliwakumbusha wazazi kwamba wampende Mungu kwanza ndipo wawafundishe watoto wao kumpenda.

Mambo yaliyotajwa katika hotuba yenye kichwa “Jihadharini na Uvumi na Porojo” yaliwasaidia wote kuona kwamba ingawa mambo ya kushangaza hutokea, twapaswa kutenda kwa hekima, si kijinga, tunaposikia ripoti zenye kusisimua. Wakristo hunufaika wanapozungumza mambo wanayojua kuwa ni ya kweli—habari njema za Ufalme. Wengi waliona hotuba iliyofuata, “Kuvumilia ‘Mwiba Katika Mwili’” kuwa yenye kufariji sana na yenye kutia moyo. Iliwasaidia kuona kwamba licha ya majaribu yenye kuendelea ambayo huenda tukakabili, Yehova aweza kutuimarisha kupitia roho yake takatifu, Neno lake, na udugu wetu wa Kikristo. Kuhusiana na hilo, tulitiwa moyo sana na mambo yaliyompata mtume Paulo kibinafsi.—2 Wakorintho 12:7-10; Wafilipi 4:11, 13.

Siku ya kwanza iliisha kwa hotuba yenye kichwa “Kwenda Sambamba na Tengenezo la Yehova.” Nyanja tatu hasa ambazo tengenezo la Mungu limesonga mbele, zilizungumziwa: (1) kuendelea kuelewa nuru ya kiroho kutoka kwa Yehova, (2) huduma ambayo Yehova ametukabidhi, na (3) marekebisho ya wakati ufaao katika utaratibu mbalimbali wa kitengenezo. Kisha msemaji alisema hivi kwa uhakika: “Twasisimuliwa na mataraja yaliyo mbele.” Akauliza: “Je, kwaweza kuwa na shaka yoyote ya kwamba tuna kila sababu ya kudumisha uhakika tuliokuwa nao kwanza ukiwa imara hadi mwisho?” (Waebrania 3:14) Jibu lilikuwa wazi. Ndipo broshua mpya yenye kichwa Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu! ilipotolewa. Itatumika kuwa kifaa cha kufundishia chenye matokeo sana katika kusaidia watu wenye elimu ya chini au wasiojua kusoma wajifunze juu ya Yehova.

Siku ya Pili—Endelea Kutangaza Kazi za Ajabu za Mungu

Baada ya kuchunguza andiko la siku, siku ya pili ya mkusanyiko iliendelea kwa mfululizo wenye kichwa “Wahudumu wa Neno la Mungu.” Sehemu ya kwanza ilikazia fikira mafanikio tunayopata sasa tunapofanya kazi yetu ya kuhubiri ulimwenguni pote. Hata hivyo, unakuwa ni mwito wa ushindani kuendelea na kazi hiyo kwa sababu wengi wanapinga ujumbe wa Ufalme. Wahubiri kadhaa ambao wametumikia kwa muda mrefu walieleza jinsi wanavyodumisha shangwe yao katika huduma kwa kuimarisha akili na mioyo yao kukabiliana na ubaridi au upinzani. Sehemu ya pili ilikumbusha wahudhuriaji wa mkusanyiko kwamba Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufikia watu kila mahali, kirasmi na kivivi hivi. Nayo sehemu ya mwisho ilieleza njia nyingi mbalimbali ambazo Wakristo wote wanaweza kupanua huduma yao ya kibinafsi. Msemaji alikazia kwamba ili kufanya hivyo, twahitaji kutanguliza kabisa Ufalme wa Mungu, hata ikiwa kufanya hivyo kwamaanisha taabu na kujinyima mapendezi ya kibinafsi.—Mathayo 6:19-21.

Kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu usiomhofu Mungu ambamo mna tamaa nyingi sana ya vitu vya kimwili, hotuba yenye kichwa “Sitawisha Ujitoaji-Kimungu na Ujitoshelevu” ilitolewa kwa wakati unaofaa kabisa. Akitumia 1 Timotheo 6:6-10, 18, 19, msemaji alionyesha jinsi ujitoaji-kimungu husaidia Wakristo waepuke kupenda fedha, ambako kwaweza kuwapotosha na kusababisha maumivu mengi. Alikazia kwamba hata hali yetu ya kiuchumi iweje, furaha yategemea uhusiano wetu na Yehova na kuwa na hali njema ya kiroho. Wengi walichochewa na mambo yaliyotajwa katika hotuba yenye kichwa “Kutomwaibisha Mungu Katika Njia Yoyote.” Alikazia uhakika wa kwamba Yehova hasahau kamwe Mashahidi wake waaminifu. Kielelezo kisicho na kifani cha Yesu Kristo—ambaye “ni yuleyule jana na leo, na milele”—kitawasaidia wengi waendelee kukimbia shindano la mbio la uhai kwa uvumilivu.—Waebrania 13:8.

Kipindi cha asubuhi kilimalizika kwa hotuba ya ubatizo—ambayo sikuzote huwa tukio muhimu kwenye mikusanyiko mikubwa ya Mashahidi wa Yehova. Ilikuwa shangwe iliyoje kuona wapya waliojiweka wakfu na wanaofuata hatua za Yesu wakikubali kubatizwa katika maji! (Mathayo 3:13-17) Wote ambao wanachukua hatua hiyo tayari wametimiza mengi wakiwa watekelezaji wa neno la Mungu. Isitoshe, wanapobatizwa wanakuwa wahudumu walioagizwa rasmi wa habari njema, wanaopata shangwe nyingi kwa kujua kwamba wanashiriki kulitakasa jina la Yehova.—Mithali 27:11.

Shauri la waziwazi lilitolewa katika hotuba yenye kichwa “Ukomavu Wahitajika ili ‘Kutofautisha Lililo Sahihi na Lililo Kosa Pia.’” Inasikitisha sana kwamba viwango vya ulimwengu vya mema na mabaya havifai. Kwa hiyo twahitaji kutegemea viwango vya Yehova. (Waroma 12:2) Wote walitiwa moyo wafanye kazi kwa bidii ili kupata uelewevu sahihi wa njia za Mungu na kukua hadi kufikia ukomavu. Kisha, kwa kujizoeza, nguvu zetu za ufahamu zitazoezwa “kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia.”—Waebrania 5:11-14.

Kisha ulifuata mfululizo wenye kichwa “Jitahidi Kusitawisha Hali ya Kiroho.” Wakristo wa kweli hutambua umuhimu wa kusitawisha na kudumisha hali ya kiroho. Hilo latia ndani kufanya kazi kwa bidii—kusoma, kujifunza, na kutafakari. (Mathayo 7:13, 14; Luka 13:24) Watu wa kiroho pia huendeleza “kila namna ya sala na dua.” (Waefeso 6:18) Twatambua kwamba sala zetu hufunua kina cha imani na ujitoaji wetu, kiwango chetu cha hali ya kiroho, na vilevile yale tunayoona kuwa “mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10) Umuhimu wa kusitawisha uhusiano mchangamfu na wenye upendo pamoja na Yehova kama ule unaofurahiwa na mtoto mtiifu aliye na baba mwenye fadhili, ulikaziwa pia. Sisi hatufuati dini kama desturi tu—ijapokuwa ni ya kweli—lakini twataka kusitawisha imani yenye nguvu, ‘kama tunaona Mungu.’—Waebrania 11:6, 27.

Habari inayohusu maendeleo ya kiroho ilizungumziwa zaidi katika hotuba yenye kichwa “Dhihirisha Maendeleo Yako.” Sehemu tatu za kufanya maendeleo hayo zilichunguzwa: (1) kuongeza ujuzi, uelewevu, na hekima, (2) kuonyesha matunda ya roho ya Mungu, na (3) kutekeleza wajibu wetu mbalimbali tukiwa washiriki wa familia.

Baada ya hotuba ya mwisho ya kumalizia siku, “Kutembea Katika Nuru Inayoongezeka ya Neno la Mungu,” wahudhuriaji wa mkusanyiko walifurahi kupokea kitabu kipya, Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote I. Hili ni buku la kwanza kati ya mabuku mawili yanayozungumzia unabii wa kitabu cha Biblia cha Isaya sura baada ya sura. “Kitabu cha Isaya kina ujumbe kwetu leo,” akasema msemaji. Aliendelea kusema: “Naam, unabii wake mwingi ulitimia siku za Isaya. . . . Hata hivyo, unabii mwingi wa Isaya unatimia leo, na mwingine utatimia katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi.”

Siku ya Tatu—Iweni Watekelezaji wa Neno la Yehova

Siku ya mwisho ya mkusanyiko ilianza kwa kuzungumzia andiko la siku. Kisha ukafuata mfululizo wenye kichwa “Unabii Muhimu wa Sefania kwa Wale Wanaofanya Mapenzi ya Mungu.” Hotuba tatu za mfululizo huo zilionyesha kwamba, kama vile Yehova alivyofanya katika siku za Yuda lililoasi, ataleta dhiki kwa wale ambao sasa wanakataa kutii onyo lake. Kwa sababu wanatenda dhambi dhidi ya Mungu, watatembea-tembea kama vipofu wasiojiweza, na kushindwa kupata wokovu. Hata hivyo, Wakristo wa kweli huendelea kumtafuta Yehova kwa uaminifu, nao watafichwa katika siku ya hasira ya Mungu. Isitoshe, wanafurahia baraka nyingi hata sasa. Wamebarikiwa kusema “lugha iliyo safi” ya kweli ya Biblia. (Sefania 3:9) Msemaji alisema: “Kusema lugha safi hutia ndani kuamini kweli, kuwafundisha wengine na pia kufanya mwenendo wetu upatane na sheria na kanuni za Mungu.”

Wahudhuriaji wa mkusanyiko walingoja kwa hamu drama yenye kichwa “Vielelezo vya Kuonya Leo.” Drama hiyo ambapo waigizaji walivalia mavazi maalum ilionyesha jinsi maelfu ya Waisraeli walivyokufa mpakani mwa Bara Lililoahidiwa kwa sababu walimsahau Yehova na kutongozwa na wanawake wapagani wafanye uasherati na kuabudu sanamu. Mmoja wa wahusika wakuu—Yamini—hapo mwanzoni alipata shida kuchagua kati ya uvutio wa wanawake Wamoabu na kujitoa kwake kwa Yehova. Kusababu kimakosa na kufikiri kwa udanganyifu kwa Zimri na imani na kujitoa kwa Finehasi, ni mambo yaliyokaziwa sana. Hatari ya kujihusisha na watu wasiompenda Yehova ilionyeshwa waziwazi.

Drama ilitutayarisha kwa ajili ya hotuba iliyofuata “Msiwe Wasikiaji Wasahaulifu.” Andiko la 1 Wakorintho 10:1-10 lilipochanganuliwa lilionyesha kwamba Yehova hujaribu utii wetu ili kujua kama twastahili kupokea urithi katika ulimwengu mpya. Wengine huruhusu tamaa za kimwili zisonge miradi ya kiroho hata sasa, tunapokaribia kuingia katika mfumo mpya. Wote walitiwa moyo wasipoteze fursa ya ‘kuingia ndani ya pumziko la Yehova.’—Waebrania 4:1.

Hotuba ya watu wote ilikuwa na kichwa “Umuhimu wa Kuzingatia Kazi za Ajabu za Mungu.” “Kazi za ajabu” za Yehova huonyesha hekima na mamlaka yake juu ya uumbaji wake wote unaotuzunguka. (Ayubu 37:14) Maswali kadhaa yenye kuamsha fikira kutoka kwa Yehova yalitosha kumfanya Yobu avutiwe na uwezo wa Muumba mweza yote. Wakati ujao pia Yehova atafanya “kazi za ajabu” kwa niaba ya watumishi wake waaminifu. Msemaji alimalizia hivi: “Tuna sababu nyingi za kuzingatia kazi za ajabu za Yehova —mambo aliyofanya wakati uliopita, anayofanya leo katika uumbaji wake, na anayoahidi kufanya karibuni.”

Baada ya muhtasari wa makala ya funzo la Mnara wa Mlinzi la juma hilo, hotuba ya mwisho ya mkusanyiko ilitolewa. Hotuba hiyo yenye kuchochea yenye kichwa “Thamini Sana Pendeleo Lako la Kuwa Mtekelezaji wa Neno la Mungu,” ilikazia kwamba ni heshima kuwa watekelezaji wa neno la Mungu. (Yakobo 1:22) Wasikilizaji walikumbushwa kwamba pendeleo letu tukiwa watekelezaji wa neno la Mungu ni la pekee, na kadiri tunavyolitumia kwa muda mrefu, ndivyo tunavyolithamini zaidi. Wote waliohudhuria walitiwa moyo wafikirie jinsi walivyonufaika na kichocheo cha mkusanyiko huo wa wilaya kwa kutamani kutekeleza neno la Mungu kadiri wawezavyo. Hiyo ndiyo njia pekee ya kupata furaha kubwa zaidi!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]

Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!

Ijumaa alasiri broshua mpya yenye kichwa Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu! ilitolewa. Kuna uhitaji mkubwa wa kutoa elimu sahili ya Biblia katika sehemu nyingi ulimwenguni, na broshua hiyo itatumiwa kutimiza uhitaji huo. Itakuwa baraka kubwa kwa watu wenye elimu ya chini au wasioweza kusoma vizuri.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26]

Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote

Waliohudhuria mkusanyiko walisisimuka kupokea Buku la I kati ya mabuku mawili ya kitabu Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote. Kichapo hiki kinakazia manufaa yenye kutumika ya unabii wa Isaya katika siku zetu.