Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Afya Kitovuni Pako’

‘Afya Kitovuni Pako’

‘Afya Kitovuni Pako’

INAAMINIWA kwamba magonjwa mengi ya wanadamu yanasababishwa na mikazo ya kihisia moyo kama vile woga, huzuni, wivu, uchungu wa moyo, chuki na hatia. Kwa kuzingatia hayo, taarifa ya Biblia inafariji kama nini kwamba ‘kumcha Yehova’ ni “afya mwilini [kitovuni] pako, na mafuta mifupani mwako”!—Mithali 3:7, 8, kielezi-chini.

Mifupa ni kiunzi kinachotegemeza mwili. Hivyo, Biblia hutumia neno “mifupa” kwa njia ya mfano, kuwakilisha mtu mwenyewe—hasa kama anavyoathiriwa na hisia nzito za moyoni. Lakini kumcha Yehova kunakuwaje ‘afya kitovuni pako’?

Wasomi wa Biblia wana maoni yanayotofautiana kuhusu neno “kitovu” lililotajwa katika andiko hilo. Mfafanuzi mmoja asema kwamba kwa kuwa kitovu kiko “sehemu ya katikati ya mwili,” huenda kikawa chawakilisha viungo vyote muhimu vya mwili. Msomi mwingine adokeza kwamba huenda neno “kitovu” likawa lamaanisha kiunga-mwana, kama linavyotumiwa kwenye Ezekieli 16:4, NW. Ikiwa ndivyo ilivyo, huenda andiko la Mithali 3:8 likawa lakazia uhitaji wa kumtegemea Mungu kabisa—kama vile kijusi kisichojiweza kitegemeavyo mama yacho kabisa ili kupata chakula. Na bado wazo jingine ni kwamba huenda neno “kitovu” hapa likawa larejezea misuli na kano za mwili. Katika muktadha wa mstari huo, huenda ikawa kwamba sehemu hizi zinatofautishwa na “mifupa”—sehemu ngumu zaidi za mwili.

Hata maana yake hususa iwe nini, jambo moja ni hakika: Ni hekima kumwonyesha Yehova hofu yenye staha. Kufuata viwango vya Mungu kwaweza kutusaidia tuwe na afya nzuri sasa. Isitoshe, kunaweza kufanya tupate kibali cha Yehova, jambo ambalo litaongoza kwenye uhai wa milele tukiwa na afya bora kabisa—kimwili na kihisia-moyo—katika ulimwengu wake mpya ujao.—Isaya 33:24; Ufunuo 21:4; 22:2.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 32]

Dr. G. Moscoso/SPL/Photo Researchers