Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fundi wa Miwani Apanda Mbegu

Fundi wa Miwani Apanda Mbegu

Fundi wa Miwani Apanda Mbegu

Fundi mmoja wa miwani huko Lviv, Ukrainia alifanya jitihada gani kuhusiana na kuanzishwa kwa kutaniko la Kirusi huko Haifa, Israel, lililo umbali wa kilometa zipatazo 2,000 na umbali wa nchi kadhaa kutoka Ukrainia? Hiki ni kisa kinachodhihirisha ukweli wa maneno haya ya Muhubiri 11:6: “Asubuhi panda mbegu zako, wala jioni usiuzuie mkono wako. Kwa maana wewe hujui ni zipi zitakazofanikiwa.”

KISA chetu chaanza mwaka wa 1990 wakati Ella, mwanamke kijana mwenye asili ya Kiyahudi, alipokuwa akiishi Lviv. Ella na familia yao walikuwa wanajitayarisha kuhamia Israel. Muda mfupi kabla ya kuondoka, Ella alienda kumwona fundi wa miwani ambaye ni Shahidi wa Yehova. Wakati huo kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku huko Ukrainia. Hata hivyo, fundi huyo wa miwani alizungumza na Ella kuhusu imani yake yenye kutegemea Biblia. Alimshangaza kwa kusema kwamba Mungu ana jina la kibinafsi. Jambo hilo lilifanya Ella atake kujua zaidi, na mazungumzo mazuri ya Biblia yakafuatia.

Ella alifurahia mazungumzo hayo sana hivi kwamba aliomba wawe na mazungumzo mengine juma lililofuata na bado akaomba wazungumze tena juma lililofuata hilo. Upendezi wake ulikuwa unakua, lakini kulikuwa na tatizo. Wakati wa familia hiyo wa kuhamia Israel ulikuwa unakaribia kwa kasi. Na bado Ella alikuwa na mambo mengi sana ya kujifunza! Ili aweze kutumia vema zaidi wakati uliobaki, aliomba wajifunze Biblia kila siku hadi atakapoondoka. Ingawa Ella hakuanza tena kujifunza mara tu alipofika Israel, mbegu ya kweli ilikuwa imeanza kusitawi moyoni mwake. Kufikia mwisho wa mwaka, alikuwa anajifunza Biblia tena, na kwa bidii.

Vita vilizuka katika Ghuba la Uajemi na Israel ikashambuliwa kwa makombora na Iraq. Vita hivyo vilizungumziwa mara nyingi. Siku moja kwenye duka moja kubwa, Ella alisikia familia moja ya wahamiaji wapya ikiongea Kirusi. Ingawa yeye mwenyewe alikuwa bado anajifunza Biblia, Ella aliikaribia familia hiyo na kuzungumza nao juu ya ahadi ya Biblia ya ulimwengu wenye amani. Matokeo yakawa kwamba nyanya Galina; mama, Natasha; mwana, Sasha (Ariel); na binti, Ilana, wote walijiunga na funzo la Biblia la Ella.

Sasha alikuwa mshiriki wa kwanza wa familia hiyo kufikia ubatizo—licha ya majaribu mengi. Ingawa alikuwa mwanafunzi wa daraja la juu, alifukuzwa shuleni kwa sababu dhamiri yake ya Kikristo haingemruhusu kushiriki katika mazoezi ya kijeshi, mazoezi yaliyokuwa sehemu ya mtaala wa shule. (Isaya 2:2-4) Kesi ya Sasha ilipelekwa kwa Mahakama Kuu ya Israel jijini Jerusalem, ambayo yastahili pongezi kwa kuagiza Sasha arudishwe shuleni ili aweze kumaliza muhula wa shule. Kesi hiyo ilitangazwa nchini kote. Hivyo, Waisraeli wengi wakapata kujua imani ya Mashahidi wa Yehova. *

Baada ya kuhitimu shule ya sekondari, Sasha alijiunga na huduma ya wakati wote ya Mashahidi wa Yehova. Leo anatumikia akiwa painia wa pekee na mzee wa kutaniko. Dadake, Ilana, amejiunga naye katika huduma ya wakati wote. Mama yao na nyanya yao ni Mashahidi waliobatizwa. Mbegu ambayo yule fundi wa miwani alipanda ilikuwa ingali inazaa matunda!

Wakati huohuo, Ella alizidi kufanya maendeleo ya kiroho na muda si muda akawa anahubiri nyumba hadi nyumba. Kwenye mlango aliogonga kwanza, Ella alimpata Faina, ambaye alikuwa amefika juzijuzi tu kutoka Ukrainia. Faina alikuwa ameshuka moyo. Baadaye, Ella alitambua kwamba muda mfupi kabla ya kugonga mlango wa Faina, mwanamke huyo mwenye majonzi alikuwa amesali kwa Mungu hivi: “Sijui wewe ni nani, lakini ikiwa wanisikia, nisaidie.” Yeye na Ella walikuwa na mazungumzo yenye kusisimua. Faina aliuliza maswali mengi na kuchunguza kwa makini majibu aliyopewa. Baada ya muda, alisadiki kuwa Mashahidi wa Yehova hufundisha kweli kutoka katika Biblia. Alirekebisha programu yake ya mafunzo ya chuo kikuu ili aweze kutumia muda mwingi zaidi kutanikoni na katika kazi ya kuhubiri. Faina alibatizwa mnamo Mei 1994. Yeye pia alianza utumishi wa painia, akijitegemeza kwa kazi ya muda inayohusu kompyuta.

Mnamo Novemba 1994, Ella alijisikia mnyonge sana kwa ghafula alipokuwa anahubiri. Alienda hospitalini ambapo uchunguzi ulionyesha ana vidonda vya tumbo. Kufikia jioni hemoglobini ya Ella ilikuwa imeshuka hadi 7.2. Mzee fulani katika kutaniko la Ella, ambaye ni mwenyekiti wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali (HLC), aliwapasha madaktari habari juu ya mbinu nyingi za kitiba ambazo hazihitaji damu. * Ella alipona kabisa baada ya upasuaji uliofanywa kwa mafanikio bila kutumia damu.—Matendo 15:28, 29.

Jambo hilo lilimvutia sana Karl, daktari wa Ella wa magonjwa ya wanawake ambaye ni Myahudi aliyezaliwa Ujerumani. Kisha akakumbuka kwamba wazazi wake, ambao waliokoka Maangamizi Makubwa, waliwajua Mashahidi wa Yehova kwenye kambi za mateso. Karl aliuliza maswali mengi. Ingawa alikuwa na kazi nyingi sana katika kliniki yake, Karl alitafuta wakati wa kujifunza Biblia kwa ukawaida. Kufikia mwaka uliofuata, alikuwa anahudhuria mikutano ya Kikristo ya kila juma.

Mbegu iliyopandwa na fundi wa miwani imetokeza nini? Tayari tumeona yaliyotokea kwa Sasha na familia yao. Kuhusu Ella, yeye ni mhudumu painia wa pekee. Bintiye Eina, ambaye alimaliza shule hivi majuzi, ameanza kazi-maisha ya upainia. Faina pia hutumikia akiwa painia wa pekee. Sasa Karl, yule daktari wa Ella wa magonjwa ya wanawake, ni Shahidi aliyebatizwa na mtumishi wa huduma, anayeshiriki nguvu za kuponya za kweli ya Biblia pamoja na wagonjwa wake na wengineo.

Kikundi kidogo cha wahamiaji wenye kuzungumza Kirusi ambacho kilianza kikiwa sehemu ya Kutaniko la Haifa la Kiebrania sasa kimekuwa kutaniko la Kirusi lenye bidii ambalo lina wahubiri wa Ufalme zaidi ya 120. Kwa sehemu, ongezeko hilo limetokana na uhakika wa kwamba fundi mmoja wa miwani huko Lviv alitumia fursa fulani kupanda mbegu!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ili kupata habari zaidi, ona toleo la Amkeni! la Novemba 8, 1994, ukurasa wa 12-15.

^ fu. 9 Ndugu walio katika HLC huwakilisha Mashahidi wa Yehova ulimwenguni kote, wakisaidia katika mawasiliano baina ya wagonjwa na wafanyakazi wa hospitali. Wao pia hutoa habari kuhusu matibabu ya badala yanayotegemea utafiti wa karibuni zaidi wa kitiba.

[Ramani katika ukurasa wa 29]

 

UKRAINIA

ISRAEL

[Hisani]

Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Ella na binti yake, Eina

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kikundi chenye furaha cha Mashahidi wenye kuzungumza Kirusi huko Haifa. Kushoto hadi kulia: Sasha, Ilana, Natasha, Galina, Faina, Ella, Eina,na Karl