Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Umeifanya Kweli Iwe Mali Yako Mwenyewe?

Je, Umeifanya Kweli Iwe Mali Yako Mwenyewe?

Je, Umeifanya Kweli Iwe Mali Yako Mwenyewe?

“Mgeuzwe umbo kwa kufanya upya akili yenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—WAROMA 12:2.

1, 2. Kwa nini si rahisi kuwa Mkristo wa kweli leo?

SI RAHISI kuwa Mkristo wa kweli katika siku hizi za mwisho—“nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Kwa kweli ili kufuata kielelezo cha Kristo ni lazima mtu aushinde ulimwengu. (1 Yohana 5:4) Kumbuka yale aliyosema Yesu kuhusu njia ya Kikristo: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.” Pia alisema hivi: “Ikiwa yeyote ataka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuchukua mti wake wa mateso siku baada ya siku na kunifuata kwa kuendelea.”—Mathayo 7:13, 14; Luka 9:23.

2 Baada ya kuipata njia yenye kufinyana inayoongoza kwenye uhai, jambo jingine lililo gumu ambalo Mkristo anahitaji kufanya ni kudumu katika njia hiyo. Kwa nini hilo ni jambo gumu? Ni kwa sababu tunapojiweka wakfu na kubatizwa tunakuwa shabaha ya matendo ya ujanja ya Shetani, au mbinu zake zenye hila. (Waefeso 6:11; kielezi-chini katika New World Translation of the Holy Scriptures With References) Yeye anatambua udhaifu wetu na hujaribu kuutumia ili kudhoofisha hali yetu ya kiroho. Hata alijaribu kudhoofisha hali ya kiroho ya Yesu, kwa hiyo tusitarajie kwamba atatuacha.—Mathayo 4:1-11.

Mbinu za Ujanja za Shetani

3. Shetani alitiaje shaka katika akili ya Hawa?

3 Mbinu moja anayotumia Shetani ni kutia shaka katika akili zetu. Yeye hutafuta udhaifu katika silaha zetu za kiroho. Hapo mwanzo kabisa, alitumia mbinu hiyo kwa Hawa, kwa kumwuliza: “Ati! hivi ndivyo alivyosema Mungu, msile matunda ya miti yote ya bustani?” (Mwanzo 3:1) Yaani, Shetani alikuwa anasema, ‘Je, yawezekana kweli kwamba Mungu amewawekea kizuizi kama hiki? Je, angewanyima kitu kizuri kama hiki? Kwani, Mungu anajua kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo mtafumbuliwa macho nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya!’ Kwa hiyo Shetani alitia shaka katika akili ya Hawa kana kwamba alipanda mbegu na kusubiri iote.—Mwanzo 3:5.

4. Ni shaka zipi zinazoweza kuathiri watu fulani leo?

4 Shetani hutumiaje mbinu hiyo leo? Tukipuuza usomaji wetu wa Biblia, funzo letu la kibinafsi, sala zetu, na huduma yetu ya Kikristo na mikutano, twaweza kuathiriwa na shaka zinazotokezwa na wengine. Kwa mfano: “Twajuaje kwamba hii ni kweli iliyofundishwa na Yesu?” “Je, kwa kweli hizi ndizo siku za mwisho? Vyovyote vile, tayari tuko katika karne ya 21.” “Je, Har-Magedoni imekaribia sana, au iko mbali sana?” Shaka hizo zikitokea, tunaweza kufanya nini ili kuziondoa?

5, 6. Twapaswa kufanya nini tunapopatwa na shaka?

5 Yakobo alitoa shauri la busara alipoandika hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, acheni afulize kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo. Lakini acheni afulize kuomba katika imani, bila kutia shaka hata kidogo, kwa maana yeye atiaye shaka ni kama wimbi la bahari liendeshwalo na upepo na kupeperushwa huku na huku. Kwa kweli, acheni mtu huyo asidhani kwamba atapokea kitu chochote kutoka kwa Yehova; yeye ni mtu wa kusitasita kuamua, asiye imara katika njia zake zote.”—Yakobo 1:5-8.

6 Basi, twapaswa kufanya nini? Twapaswa ‘kufuliza kumwomba Mungu’ kwa sala ili kupata imani na ufahamu na kuimarisha jitihada zetu za kujifunza kibinafsi kuhusu maswali au shaka zozote. Tunaweza pia kuwaomba msaada wale walio na imani yenye nguvu, bila kuwa na shaka kamwe kwamba Yehova atatupa utegemezo tunaohitaji. Pia Yakobo alisema hivi: “Basi, jitiisheni wenyewe kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” Naam, shaka zetu zitaisha tunapoendelea kumkaribia Mungu kupitia funzo na sala.—Yakobo 4:7, 8.

7, 8. Ni zipi baadhi ya kanuni za msingi za kutambulisha aina ya ibada aliyofundisha Yesu, na ni nani wanaotimiza kanuni hizo?

7 Kwa mfano, fikiria swali hili: Tunajuaje kwamba tunafuata aina ya ibada aliyofundisha Yesu? Ili kujibu swali hilo, ni kanuni gani zinazopasa kufikiriwa? Biblia husema kwamba Wakristo wa kweli wapaswa kuwa na upendo wa kweli miongoni mwao wenyewe. (Yohana 13:34, 35) Lazima walitakase jina la Mungu, Yehova. (Isaya 12:4, 5; Mathayo 6:9) Na lazima wajulishe watu jina hilo.—Kutoka 3:15; Yohana 17:26.

8 Jambo jingine linalotambulisha ibada ya kweli ni kustahi Neno la Mungu, Biblia. Ndicho kitabu cha pekee kinachofunua utu wa Mungu na makusudi yake. (Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:16, 17) Kwa kuongezea, Wakristo wa kweli hutangaza Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la mwanadamu kwa uhai udumuo milele katika paradiso duniani. (Marko 13:10; Ufunuo 21:1-4) Wanajitenga na siasa zenye upotovu za ulimwengu huu na njia yake ya maisha yenye kuchafua. (Yohana 15:19; Yakobo 1:27; 4:4) Ni nani leo ambao wametimiza kanuni hizo? Mambo ya hakika yathibitisha kwamba kuna jibu moja tu—Mashahidi wa Yehova.

Namna Gani Shaka Ikiendelea kwa Muda Mrefu?

9, 10. Twaweza kufanya nini ili kushinda shaka inayoendelea kwa muda mrefu?

9 Vipi tukilemewa na shaka? Tufanye nini basi? Mfalme Solomoni mwenye hekima atoa jibu: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu.”Mithali 2:1-5.

10 Je, hilo si wazo la kushangaza? Tukikubali kuzingatia kwa makini hekima ya Mungu, ‘tutapata kumjua Mungu.’ Naam, twaweza kupata ujuzi wa Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu ikiwa tuko tayari kupokea na kuthamini maneno yake. Hilo lamaanisha kumfikia Yehova katika sala na kupitia funzo la kibinafsi. Hazina zilizositirika za Neno lake zaweza kuondoa shaka zozote kupitia nuru ya kweli.

11. Mtumishi wa Elisha aliathiriwaje na shaka?

11 Mfano mzuri wa jinsi sala ilivyomsaidia mtumishi mmoja wa Mungu aliyekuwa na hofu na shaka wapatikana katika andiko la 2 Wafalme 6:11-18. Mtumishi wa Elisha hakuwa na ufahamu wa kiroho. Hangeweza kufahamu kwamba kulikuwa na majeshi ya kimbingu yaliyokuwa yakimtegemeza nabii wa Mungu, aliyekuwa amezingirwa na majeshi ya Shamu. Akiwa na hofu, mtumishi huyo alipaza sauti hivi: “Ole wetu! bwana wangu tufanyeje?” Elisha alijibuje? “Usiogope; maana walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao.” Lakini mtumishi huyo angesadikishwaje? Hangeweza kuona majeshi ya kimbingu.

12. (a) Shaka za mtumishi ziliondolewaje? (b) Twaweza kuondoaje shaka zozote tulizo nazo?

12 “Elisha akaomba, akasema, Ee BWANA, nakusihi, mfumbue macho yake, apate kuona. BWANA akamfumbua macho yule mtumishi; naye akaona, na tazama, kile kilima kilikuwa kimejaa farasi na magari ya moto yaliyomzunguka Elisha pande zote.” Kwa hiyo, Yehova alimwezesha mtumishi huyo kuona majeshi ya kimbingu yaliyokuwa yanamlinda Elisha. Hata hivyo, hatupaswi kutarajia msaada kama huo kutoka kwa Mungu leo. Kumbuka, yule mtumishi wa nabii hakuwa na Biblia kamili ya kujifunza ili kuimarisha imani yake. Sisi tuna Biblia. Tukiitumia vizuri, imani yetu yaweza kuimarishwa jinsi hiyo. Kwa mfano, twaweza kutafakari masimulizi kadhaa yanayomfafanua Yehova akiwa katika makao yake ya kimbingu. Masimulizi hayo hutusaidia tusiwe na shaka yoyote kwamba Yehova ana tengenezo la kimbingu linalotegemeza watumishi wake katika kazi ya kuelimisha watu ulimwenguni pote leo.—Isaya 6:1-4; Ezekieli 1:4-28; Danieli 7:9, 10; Ufunuo 4:1-11; 14:6, 7.

Jihadhari na Mbinu za Shetani!

13. Shetani hutumia njia zipi kutudhoofisha tusidumu katika kweli?

13 Shetani hutumia baadhi ya njia zipi kudhoofisha hali yetu ya kiroho na kufanya tusidumu katika kweli? Mojawapo ni ukosefu wa adili unaojidhihirisha katika njia tofauti-tofauti. Katika ulimwengu wa leo wenye ashiki nyingi ya kimapenzi, kuwa na uhusiano wa kimapenzi nje ya ndoa (yaani kutokuwa mwaminifu kwa mwenzi wa ndoa) au kufanya ngono usiku mmoja tu (ngono za ovyoovyo) kumekuwa jambo la kawaida kwa kizazi kinachopenda anasa ambacho kimeazimia kujifurahisha bila kujali chochote. Sinema, televisheni, na vidio huendeleza mtindo huo wa maisha. Vyombo vya habari hasa Internet, vimejaa ponografia. Wale wanaotazama ponografia kwa sababu ya udadisi wanakabili kishawishi.—1 Wathesalonike 4:3-5; Yakobo 1:13-15.

14. Kwa nini Wakristo fulani wameshindwa na mbinu za Shetani?

14 Wakristo fulani wameshindwa kudhibiti udadisi wao na kuchafua akili zao na mioyo yao kwa kutazama picha za ponografia zisizoonyesha ngono waziwazi sana au hata zile zinazoonyesha ngono waziwazi kabisa. Wamejiruhusu kuanguka katika mtego wa Shetani wenye kuvutia. Kufanya hivyo, mara nyingi kumesababisha madhara ya kiroho yasiyoweza kurekebika. Watu hao wameshindwa kudumu wakiwa “watoto wachanga sana kuhusu ubaya.” Hawajawa “watu wazima katika nguvu za kuelewa.” (1 Wakorintho 14:20) Kila mwaka, maelfu hupatwa na matokeo mabaya kwa kutotii kanuni na viwango vya Neno la Mungu. Wamepuuza kuvaa na kudumisha “suti [yao] kamili ya silaha kutoka kwa Mungu.”—Waefeso 6:10-13; Wakolosai 3:5-10; 1 Timotheo 1:18, 19.

Tuthamini Tulicho Nacho

15. Kwa nini huenda wengine wakaona ugumu wa kuthamini urithi wao wa kiroho?

15 “Mtajua kweli, na kweli itawaweka nyinyi huru,” akasema Yesu. (Yohana 8:32) Mashahidi wengi wamelazimika kuacha mtindo wao wa maisha wa zamani na ushirika wa kidini. Kwa hiyo, huenda wakathamini kwa urahisi zaidi uhuru unaoletwa na ile kweli. Kwa upande mwingine, vijana fulani ambao wamelelewa na wazazi walio katika kweli huenda wakaona ugumu wa kuthamini urithi wao wa kiroho. Hawajawahi kuwa sehemu ya dini isiyo ya kweli au sehemu ya ulimwengu huu unaokazia ufuatiaji wa anasa, uraibu wa dawa za kulevya, na ukosefu wa adili. Kwa sababu hiyo, huenda wakakosa kuona tofauti kubwa iliyopo kati ya paradiso yetu ya kiroho na ulimwengu mpotovu wa Shetani. Huenda hata wengine wakashawishiwa kuonja sumu ya ulimwengu ili wajue kile walichokosa!—1 Yohana 2:15-17; Ufunuo 18:1-5.

16. (a) Huenda tukajiuliza maswali gani? (b) Tunafundishwa na kutiwa moyo kufanya nini?

16 Je, kwa kweli twahitaji kuunguza vidole vyetu ili tufahamu maumivu na kuteseka? Je, hatuwezi kujifunza kutokana na mambo mabaya yanayowapata wengine? Je, twahitaji kugeukia “matope” ya ulimwengu huu ili kujua kama tumekosa kitu fulani? (2 Petro 2:20-22) Petro aliwakumbusha hivi Wakristo wa karne ya kwanza ambao hapo awali walikuwa sehemu ya ulimwengu wa Shetani: “Wakati ambao umepita watosha kwenu kuwa mmefanyiza mapenzi ya mataifa wakati mlipoendelea katika vitendo vya mwenendo mlegevu, uchu, mazidio ya kunywa divai, sherehe zenye kelele za ulevi, mashindano ya kunywa, na ibada haramu za sanamu.” Bila shaka, hatuhitaji kujiingiza katika “dimbwi [la ulimwengu] la ufasiki” ili kuona maisha yanaweza kupotoka kadiri gani. (1 Petro 4:3, 4) Kinyume na hilo, tunafundishwa viwango vya juu vya maadili vya Yehova kwenye Majumba yetu ya Ufalme, ambayo ni vituo vya elimu ya Biblia. Na tunatiwa moyo tutumie nguvu zetu za kufikiri ili kujithibitishia wenyewe kwamba tuna kweli na hivyo kufanya kweli iwe mali yetu wenyewe.—Yoshua 1:8; Waroma 12:1, 2; 2 Timotheo 3:14-17.

Jina Letu Si Kitambulisho Tu

17. Tunawezaje kuwa Mashahidi wa Yehova wenye matokeo?

17 Tukiifanya kweli iwe mali yetu wenyewe, tutajitahidi kuwajulisha wengine katika kila fursa inayofaa. Hii haimaanishi kwamba tutajaribu kulazimisha wale wasiopendezwa. (Mathayo 7:6) Badala yake, hatutaona haya kujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova. Mtu fulani akionyesha upendezi kidogo kwa kuuliza swali la unyofu au kwa kukubali kichapo kinachotegemea Biblia, tutakuwa tayari kumjulisha tumaini letu. Bila shaka, jambo hilo ladokeza kwamba sikuzote tuwe na vichapo vya namna fulani popote tulipo—nyumbani, kazini, shuleni, madukani, au katika sehemu za tafrija.—1 Petro 3:15.

18. Kujitambulisha wenyewe waziwazi kuwa Wakristo kwawezaje kuwa jambo linalonufaisha maishani mwetu?

18 Tunapojitambulisha waziwazi kuwa Wakristo, tunaimarisha kinga yetu dhidi ya mashambulizi yenye hila ya Shetani. Ikiwa kuna karamu ya siku ya kuzaliwa au ya Krismasi au kamari inayochezwa ofisini, mara nyingi wafanyakazi wenzetu watasema, “Msijishughulishe naye. Yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.” Kufanya hivyo kwaweza pia kuzuia watu wasifanye mizaha michafu mbele zetu. Hivyo, kujulisha msimamo wetu wa Kikristo ni jambo linaloweza kutunufaisha sana maishani, kama alivyosema mtume Petro: “Kwa kweli, ni nani huyo mtu ambaye atawadhuru nyinyi ikiwa mwawa wenye bidii kwa lililo jema? Lakini hata mkiteseka kwa ajili ya uadilifu, nyinyi ni wenye furaha.”—1 Petro 3:13, 14.

19. Tunajuaje kwamba tuko katika siku za mwisho kabisa?

19 Faida nyingine ya kufanya kweli iwe mali yetu wenyewe ni kwamba tutasadikishwa kuwa kwa kweli hizi ni siku za mwisho wa mfumo huu wa mambo. Tutajua kwamba unabii mwingi wa Biblia unafikia upeo wake wakati wetu. * Onyo la Paulo kwamba “katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa” lathibitishwa vya kutosha na matukio yenye kuogofya ya karne iliyopita. (2 Timotheo 3:1-5; Marko 13:3-37) Makala moja ya gazeti la hivi karibuni kuhusu karne ya 20 ilikuwa na kichwa “Itakumbukwa Kuwa Kipindi cha Ukatili.” Makala hiyo ilisema: “Mwaka wa 1999 ulikuwa mwaka wenye mauaji mengi zaidi katika nusu ya pili ya karne yenye mauaji mengi zaidi.”

20. Sasa ni wakati wa kufanya nini?

20 Sasa sio wakati wa kusitasita. Ni wazi kwamba Yehova anabariki kazi kubwa zaidi ya kuelimisha watu juu ya Biblia ambayo imepata kufanywa ulimwenguni pote kuwa ushahidi kwa mataifa. (Mathayo 24:14) Ifanye kweli iwe mali yako mwenyewe, na kuijulisha wengine. Wakati wako ujao wa milele wategemea yale unayofanya sasa. Kufanya kazi kwa ulegevu hakutaleta baraka za Yehova. (Luka 9:62) Badala yake, ni wakati wa “[kuwa] imara, usiyeondoleka, sikuzote ukiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, ukijua kwamba kazi yako ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.”—1 Wakorintho 15:58.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Ona Mnara wa Mlinzi, Januari 15, 2000, ukurasa wa 12-14. Fungu la 13-18 latoa sababu sita za uthibitisho wenye kusadikisha unaoonyesha kwamba tumekuwa tukiishi katika siku za mwisho tangu mwaka wa 1914.

Je, Unakumbuka?

• Tunawezaje kuondoa shaka?

• Twaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa mtumishi wa Elisha?

• Sikuzote twapaswa kujilinda dhidi ya vishawishi gani vya kiadili?

• Kwa nini twapaswa kujitambulisha waziwazi kuwa Mashahidi wa Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kujifunza Biblia na kusali kwa ukawaida kwaweza kutusaidia kuondoa shaka

[Picha katika ukurasa wa 11]

Shaka za mtumishi wa Elisha ziliondolewa alipoona maono

[Picha katika ukurasa wa 12]

Tunafundishwa viwango vya juu vya maadili vya Yehova kwenye Majumba ya Ufalme kama hili lililo huko Benin