Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupata Usalama Katika Ulimwengu Wenye Hatari Nyingi

Kupata Usalama Katika Ulimwengu Wenye Hatari Nyingi

Kupata Usalama Katika Ulimwengu Wenye Hatari Nyingi

KUTEMBEA katika eneo lililotegwa mabomu ardhini kunaweza kusababisha kifo. Je, si ingesaidia sana kama ungekuwa na ramani inayoonyesha sehemu mbalimbali ambapo mabomu hayo yametegwa? Kwa kuongozea, tuseme umezoezwa kutambua mabomu mbalimbali yaliyotegwa ardhini. Ni wazi kwamba ujuzi huo ungekupunguzia sana hatari ya kulemazwa au kuuawa.

Biblia inaweza kulinganishwa na ramani hiyo na mazoezi hayo ya kutambua mabomu. Biblia ina hekima isiyo na kifani kwa habari ya kuepuka hatari kubwa na kutatua matatizo yanayotokea maishani.

Ona ahadi hii yenye kutia moyo kwenye Mithali 2:10, 11: “Hekima itaingia moyoni mwako, na maarifa [“ujuzi,” NW] yatakupendeza nafsi yako; busara itakulinda; ufahamu utakuhifadhi.” Hekima na ujuzi ambazo zimetajwa hapa hazitokani na mwanadamu bali zatokana na Mungu. ‘Bali kila asikilizaye hekima ya Mungu atakaa salama, naye atatulia bila kuogopa mabaya.’ (Mithali 1:33) Hebu tuone jinsi Biblia iwezavyo kuboresha usalama wetu na kutusaidia kuepuka matatizo mengi.

Kuepuka Aksidenti Zenye Kusababisha Kifo

Tarakimu ambazo hivi majuzi zilichapishwa na Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) zaonyesha kwamba watu wapatao 1,171,000 hufa kutokana na aksidenti za magari kila mwaka. Watu wengine karibu milioni 40 hujeruhiwa na zaidi ya milioni 8 kulemazwa kwa muda mrefu.

Ingawa haiwezekani kuwa salama kabisa tunapoendesha magari, usalama wetu kibinafsi unaongezeka sana tunapotii sheria za barabarani. Inapozungumza kuhusu wenye mamlaka serikalini, ambao hutoa na kutekeleza sheria za barabarani, Biblia husema: “Acheni kila nafsi iwe katika ujitiisho kwa mamlaka zilizo kubwa.” (Waroma 13:1) Waendeshaji magari wanaofuata ushauri huo hupunguza hatari ya kupatwa na aksidenti na matokeo yake ambayo mara nyingi huwa mabaya mno.

Jambo jingine linalotuchochea tuendeshe magari kwa usalama ni kuheshimu uhai. Biblia yasema hivi kuhusu Yehova Mungu: “Maana kwako wewe iko chemchemi ya uzima.” (Zaburi 36:9) Kwa hiyo uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu. Hivyo basi, hatuna haki ya kuondoa zawadi hiyo kutoka kwa yeyote au kutoheshimu uhai, kutia ndani, bila shaka, uhai wetu wenyewe.—Mwanzo 9:5, 6.

Kwa kawaida, kuheshimu uhai hutia ndani kuhakikisha kwamba magari yetu na makao yetu ni salama kadiri iwezekanavyo. Katika Israeli la kale, usalama ulipewa umuhimu wa kwanza kabisa katika sehemu zote za maisha. Kwa mfano, nyumba ilipojengwa, Sheria ya Mungu ilitaka kwamba paa yake—mahali ambapo familia ilifanyia shughuli nyingi—iwe na ukuta kando-kando. “Fanya ukuta kando-kando ya dari lako, usije ukaleta damu juu ya nyumba yako, mtu akianguka huko.” (Kumbukumbu la Torati 22:8) Ikiwa mtu fulani alianguka kwa sababu sheria hiyo ya usalama haikufuatwa, mwenye nyumba alikuwa na hatia mbele za Mungu. Hapana shaka kwamba kutumia kanuni yenye upendo ambayo imejumuishwa katika sheria hiyo kungepunguza aksidenti mahali pa kazi au hata mahali pa tafrija.

Kupambana na Uraibu Wenye Kuua

Kulingana na WHO, leo kuna wavutaji sigareti zaidi ya bilioni moja ulimwenguni, na watu wapatao milioni nne hufa kila mwaka kwa sababu ya kutumia tumbaku. Tarakimu hiyo inatarajiwa kuongezeka hadi watu milioni 10 hivi katika miaka 20 hadi 30 ijayo. Mamilioni ya wavutaji sigareti wengine, na vilevile watumizi wa dawa za “kujiburudisha,” wataharibu afya yao na ubora wa maisha yao kwa sababu ya uraibu wao.

Ingawa Neno la Mungu halitaji kihususa matumizi ya tumbaku na dawa za kulevya, kanuni zake zaweza kutulinda na mazoea hayo. Kwa mfano, andiko la 2 Wakorintho 7:1 lashauri: “Acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na wa roho.” Hakuna shaka kwamba kemikali nyingi hatari zilizomo katika tumbaku na dawa za kulevya huuchafua mwili, au kuutia unajisi. Isitoshe, Mungu hutaka miili yetu iwe ‘mitakatifu,’ yaani iwe safi. (Waroma 12:1) Je, hukubali kwamba kutumia kanuni hizi kutapunguza hatari kubwa kwa uhai wa mtu?

Kushinda Mazoea Hatari

Watu wengi hula na kunywa kupita kiasi. Matokeo ya kula kupita kiasi yaweza kutia ndani ugonjwa wa sukari, kansa, na maradhi ya moyo. Matumizi mabaya ya kileo hutokeza matatizo ya ziada kama ulevi wa kupindukia, ugonjwa wa ini, kuvunjika kwa familia, na aksidenti za magari. Kwa upande ule mwingine, kujinyima chakula ili kupunguza unene kwaweza pia kudhuru na kusababisha matatizo yanayohatarisha uhai kama vile kutokuwa na hamu ya chakula.

Ingawa Biblia si kitabu cha tiba, inatoa ushauri ulio wazi juu ya uhitaji wa kuwa na kiasi katika kula na kunywa. “Sikia, mwanangu, uwe na hekima, na kuuongoza moyo wako katika njia njema. Usiwe miongoni mwa wanywao mvinyo; miongoni mwao walao nyama kwa pupa. Kwa maana mlevi na mlafi huingia umaskini.” (Mithali 23:19-21) Hata hivyo, Biblia husema kwamba kula na kunywa kwapasa kufurahisha. “Ni karama ya Mungu kila mtu apate kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote.”—Mhubiri 3:13.

Biblia pia hutuhimiza tuwe na mtazamo wenye usawaziko kuhusiana na mazoezi ya kimwili, ikisisitiza kwamba “mazoezi ya kimwili ni yenye manufaa kidogo.” Lakini inaongeza kusema: “Ujitoaji-kimungu ni wenye manufaa kwa mambo yote, kwa kuwa una ahadi ya uhai wa sasa na ule utakaokuja.” (1 Timotheo 4:8) Huenda ukauliza, ‘ujitoaji-kimungu unanufaishaje hata sasa?’ Kwa njia nyingi. Mbali na kuboresha hali ya mtu ya kiroho, ujitoaji-kimungu hukuza sifa zenye manufaa kama upendo, shangwe, amani, na kujidhibiti, na zote huchangia kuwa na maoni yafaayo na afya nzuri.—Wagalatia 5:22, 23.

Matokeo Yenye Uchungu ya Ukosefu wa Adili

Leo watu wengi sana wamejiachilia kabisa kiadili. Mojawapo ya matokeo ya kufanya hivyo ni ugonjwa wa mlipuko wa UKIMWI. Kulingana na shirika la WHO, watu zaidi ya milioni 16 wamekufa tangu ugonjwa huo ulipuke, na wakati huu, watu wapatao milioni 34 wana virusi vya HIV vinavyosababisha UKIMWI. Wengi wanaougua UKIMWI walipata maradhi hayo kupitia kufanya ngono ovyo-ovyo, sindano chafu zinazotumiwa na waraibu wa dawa za kulevya, au kutiwa damu yenye virusi hivyo.

Matokeo mengine ya kuwa na maadili yaliyopotoka hutia ndani ugonjwa usababishao vidonda kwenye viungo vya uzazi, kisonono, mchochota wa ini aina ya B na C na kaswende. Ingawa majina hayo ya kitiba hayakutumiwa nyakati za Biblia, wakati huo viungo ambavyo kwa kawaida viliathiriwa na maradhi fulani yanayoambukizwa kingono vilijulikana. Kwa mfano, andiko la Mithali 7:23 laeleza matokeo yenye kuogofya ya kufanya uasherati kuwa ‘mshale uchomao maini.’ Ugonjwa wa kaswende na vile mchochota wa ini, huathiri ini. Ndiyo, ushauri wa Biblia kwamba Wakristo ‘wajiepushe na damu na uasherati’ ni wa wakati ufaao na wenye upendo kama nini!—Matendo 15:28, 29.

Mtego wa Kupenda Pesa

Katika jitihada ya kutajirika haraka, watu wengi hutumia pesa zao kutimiza miradi mikubwa iliyo hatari. Kwa kusikitisha, mara nyingi mtu hupoteza pesa au kufilisika kwa kufanya hivyo. Hata hivyo, Biblia humwambia mtumishi wa Mungu hivi: “Acheni afanye kazi ya bidii, akifanya kwa mikono yake kazi iliyo njema, ili apate kuwa na kitu fulani cha kugawa kwa mtu aliye katika uhitaji.” (Waefeso 4:28) Ni kweli kwamba si wakati wote yule afanyaye kazi kwa bidii hupata kuwa matajiri. Lakini, ana amani ya akili, anajiheshimu, na labda hata ana fedha ambazo anaweza kuchangia jambo lenye manufaa.

Biblia huonya: “Wale waazimiao kuwa matajiri huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo. Kwa maana kupenda fedha ni mzizi wa mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikilia kupenda huku wengine . . . wamejichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:9, 10) Ni wazi kwamba wengi “waazimiao kuwa matajiri” huwa matajiri. Lakini hupata hasara gani? Si kweli kwamba afya yao, familia, hali ya kiroho, na ubora wa usingizi wao huathirika?—Mhubiri 5:12.

Mtu mwenye hekima hutambua kwamba “uhai wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Pesa na vitu fulani ni vya lazima katika jamii nyingi. Kwa kweli, Biblia husema kwamba ‘fedha ni ulinzi,’ lakini yaongezea kusema kwamba “ubora wa maarifa ni ya kwamba hekima humhifadhi yeye aliye nayo.” (Mhubiri 7:12) Tofauti na pesa, maarifa na hekima ifaayo zinaweza kutusaidia katika hali zote, hasa katika mambo yanayoathiri maisha yetu.—Mithali 4:5-9.

Wakati Tutakapolindwa na Hekima Peke Yake

Karibuni hekima ya kweli ‘itawahifadhi hai wale walio nayo’ kwa njia isiyo na kifani—kwa kuwapa ulinzi katika “dhiki kubwa” inayokaribia kwa kasi, wakati Mungu awaharibupo waovu. (Mathayo 24:21) Kulingana na Biblia, wakati huo watu watakuwa wakitupa pesa zao barabarani kama “kitu cha unajisi.” Kwa sababu gani? Kwa sababu watakuwa wamejifunza kupitia hali ngumu kwamba dhahabu na fedha hazitawanunulia uhai wakati wa “siku ya ghadhabu ya BWANA.” (Ezekieli 7:19) Kwa upande mwingine, “umati mkubwa,” ambao kwa busara ‘walijiwekea hazina mbinguni’ kwa kutanguliza masilahi ya kiroho katika maisha yao, watanufaika kutokana na uwekezaji wao ulio hakika na kupata uhai wa milele katika dunia paradiso.—Ufunuo 7:9, 14; 21:3, 4; Mathayo 6:19, 20.

Tunawezaje kupata wakati huo ujao wenye usalama? Yesu ajibu: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Watu wengi sana wamepata ujuzi huo katika Neno la Mungu, Biblia. Watu hao wana tumaini zuri sana la wakati ujao na pia wana kadiri fulani ya amani na usalama sasa. Ni kama vile mtunga-zaburi alivyosema: “Katika amani nitajilaza na kupata usingizi mara, maana Wewe BWANA, peke, yako, ndiwe unijaliaye kukaa salama.”—Zaburi 4:8.

Je, unaweza kufikiria chanzo kingine chochote cha habari kiwezacho kusaidia kupunguza hatari kwa afya na kwa maisha yako kadiri ambavyo Biblia hufanya? Hakuna kitabu kingine kilicho na mamlaka kama Biblia, na hakuna kitabu kingine kiwezacho kukusaidia kupata usalama wa kweli katika ulimwengu wa leo wenye hatari nyingi. Kwa nini usiichunguze zaidi?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Afya Bora na Usalama—Kwa Msaada wa Biblia

Ili kuepuka hali halisi za maisha, mwanamke mmoja kijana aitwaye Jane alitumia bangi, tumbaku, kokeini, amfetamini, LSD, na dawa nyingine za kulevya. Alikuwa pia akinywa kupita kiasi. * Jane asema kwamba hali ya mume wake ilikuwa vivyo hivyo. Hawakuwa na matumaini mazuri ya wakati ujao. Ndipo Jane akakutana na Mashahidi wa Yehova. Akaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kusoma gazeti Mnara wa Mlinzi na lile linaloambatana nalo, Amkeni!, magazeti ambayo alimpa mume wake asome pia. Wote wawili walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Kwa kusitawisha uthamini kwa viwango vya juu vya Yehova, waliacha kutumia dawa zote za kulevya. Matokeo yakawa nini? “Maisha yetu mapya yametuletea furaha nyingi sana,” Jane aliandika miaka kadhaa baadaye. “Ninamshukuru Yehova sana kwa nguvu zenye kutakasa za Neno lake na kwa maisha huru na yenye afya ambayo sasa tunaishi.”

Kisa cha Kurt, ambaye alifanya kazi iliyohusisha kutunza mifumo ya kompyuta, chatuandalia mfano mzuri wa manufaa ya kuwa mwajiriwa mnyofu. Wakati vifaa vipya vilipohitajika, mwajiri wa Kurt alimkabidhi daraka la kuvinunua kwa bei nafuu. Kurt alipata muuzaji mzuri, wakakubaliana bei. Hata hivyo, karani wa muuzaji huyo alifanya kosa katika kuandika risiti, kwa hiyo bei ikashuka kwa dola 40,000 za Marekani. Alipoona kosa hilo, Kurt aliwasiliana na kampuni hiyo, na meneja akasema kwamba katika kazi yake aliyokuwa ameifanya kwa miaka 25, hajawahi kuona unyofu wa aina hiyo. Kurt alieleza kwamba dhamiri yake ilifinyangwa na Biblia. Matokeo yakawa kwamba meneja huyo aliomba nakala 300 za toleo la Amkeni! lililokuwa likizungumzia unyofu katika biashara ili aweze kuwapa wafanyakazi wenzake. Kwa habari ya Kurt, unyofu wake ulifanya apandishwe cheo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 30 Majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 7]

“Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida.”ISAYA 48:17