Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kukabiliana na Kivunja-Moyo!

Unaweza Kukabiliana na Kivunja-Moyo!

Unaweza Kukabiliana na Kivunja-Moyo!

MTU fulani mwenye hekima aliandika hivi wakati mmoja: “Ukizimia siku ya taabu, nguvu zako ni chache.” (Mithali 24:10) Ikiwa umewahi kuvunjwa moyo, yaelekea utakubaliana na maneno hayo.

Hakuna mtu asiyeweza kuvunjika moyo. Unaweza kuvunjika moyo kidogo kwa siku moja au mbili kisha urudie hali yako ya kawaida. Lakini hisia zinapoumizwa au uchungu wa moyo unapohusika, tatizo hilo laweza kudumu kwa muda mrefu zaidi. Wakristo fulani ambao wamekuwa waaminifu kwa miaka mingi wamevunjika moyo sana hivi kwamba hata wameacha kuhudhuria mikutano ya kutaniko na kushiriki huduma ya shambani.

Ukihisi umevunjika moyo, usikate tamaa! Watumishi waaminifu wa nyakati za kale walikabiliana na vivunja-moyo kwa mafanikio, wewe pia unaweza kufanya hivyo kwa msaada wa Mungu.

Unapoumizwa Hisia na Wengine

Huwezi kutarajia kuepuka kila neno au tendo linalofanywa bila kufikiri. Hata hivyo, unaweza kuzuia kutokamilika kwa wengine kusivuruge utumishi wako kwa Yehova. Ikiwa mtu fulani ameumiza hisia zako, huenda ukaona inafaa kufikiria jinsi Hana, mamake Samweli, alivyoshughulika na hali fulani yenye kuvunja moyo.

Hana alitaka sana kupata watoto, lakini alikuwa tasa. Penina, aliyekuwa mke wa pili wa mumewe, tayari alikuwa amemzalia wana na mabinti. Badala ya kumhurumia Hana, Penina alimwona kuwa mshindani, akawa na mtazamo uliomfanya Hana ‘alie na kukosa kula chakula.’—1 Samweli 1:2, 4-7.

Siku moja Hana alienda hekaluni kusali. Eli, kuhani wa cheo cha juu wa Israeli, alimwona akifumba na kufumbua midomo. Pasipo kutambua kwamba Hana alikuwa anasali, Eli alikata kauli kwamba lazima awe amelewa. “Utakuwa mlevi hata lini?” akauliza. “Achilia mbali divai yako.” (1 Samweli 1:12-14) Je, unaweza kuwazia jinsi Hana alivyohisi? Alikuwa amekuja kwenye tabenakulo ili kutiwa moyo. Bila shaka hakutarajia kushtakiwa kimakosa na mmojawapo wa wanaume wenye uwezo zaidi katika Israeli!

Hali hiyo ingeweza kumfanya Hana avunjike moyo sana. Angeweza kuondoka kwenye tabenakulo mara moja, na kuapa kutorudi kamwe maadamu Eli anatumikia huko akiwa kuhani wa cheo cha juu. Hata hivyo, ni wazi kwamba Hana alithamini uhusiano wake pamoja na Yehova. Alijua kwamba hangempendeza Yehova kwa kuchukua hatua kama hiyo. Tabenakulo ilikuwa kituo cha ibada safi. Yehova alikuwa ameweka jina lake huko. Hata ingawa Eli alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu, Yehova alikuwa amemchagua kuwa mwakilishi wake.

Twapata kielelezo chema sana leo kutokana na jibu la utii la Hana kuelekea shtaka la Eli. Hakujiruhusu ashtakiwe kimakosa, lakini alijibu kwa heshima kubwa. Alijibu “Hasha! bwana wangu, mimi ni mwanamke mwenye roho ya huzuni, mimi sikunywa divai wala kileo, ila nimeimimina roho yangu mbele za BWANA. Usimdhanie mjakazi wako kuwa ni mwanamke asiyefaa kitu; kwa kuwa katika wingi wa kuugua kwangu na kusikitika kwangu ndivyo nilivyonena hata sasa.”—1 Samweli 1:15, 16.

Je, Hana alieleweka? Bila shaka. Hata hivyo, alizungumza na Eli kwa busara, bila kujaribu kumchambua kwa sababu ya kumshtaki kimakosa. Eli, naye, alimjibu kwa fadhili kwa kusema: “Enenda kwa amani; na Mungu wa Israeli akujalie haja yako uliyomwomba.” Baada ya jambo hilo kutatuliwa, Hana “akaenda zake, naye akala chakula, wala uso wake haukukunjamana tena.”—1 Samweli 1:17, 18.

Twajifunza nini kutokana na simulizi hilo? Hana alitenda kwa haraka kusahihisha hali ya kutoelewana, lakini alifanya hivyo kwa staha nyingi. Tokeo ni kwamba alidumisha uhusiano mzuri pamoja na Yehova na Eli. Ni mara nyingi kama nini mawasiliano mazuri na kutumia busara kidogo huzuia matatizo madogo yasiwe makubwa!

Lazima tutambue kwamba kusuluhisha matatizo kati yetu na wengine hutaka sote tuwe wanyenyekevu na wenye kubadilikana. Mwamini mwenzako akikataa kukubali jitihada zako za kuondoa tofauti zenu, waweza kuacha jambo hilo mikononi mwa Yehova ukitumaini kwamba atalishughulikia kwa wakati wake na kwa njia yake.

Je, Umepoteza Pendeleo la Utumishi?

Wengine wamevunjika moyo kwa sababu ya kulazimika kuacha pendeleo walilothamini katika utumishi wa Mungu. Walifurahi kutumikia ndugu zao, na walipopoteza pendeleo hilo, walihisi kwamba hawakufaa tena kwa Yehova au katika tengenezo lake. Ikiwa unahisi hivyo, unaweza kupata ufahamu kwa kuchunguza kielelezo cha mwandikaji wa Biblia Marko, aliyeitwa pia Yohana Marko.—Matendo 12:12.

Marko aliandamana na Paulo na Barnaba katika safari yao ya kwanza ya mishonari, lakini wakiwa katikati ya safari, aliwaacha na kurudi Yerusalemu. (Matendo 13:13) Baadaye, Barnaba alitaka wamchukue Marko kwa safari nyingine. Hata hivyo, Biblia husema: “Paulo hakufikiri kuwa yafaa kumchukua huyu pamoja nao, kwa kuwa yeye alikuwa amewaacha Pamfilia na hakuwa ameenda nao kwenye kazi.” Barnaba hakukubali. “Ndipo,” simulizi laendelea, “kukatokea mfoko mkali wa hasira, hivi kwamba [Paulo na Barnaba] wakatengana; na Barnaba akamchukua Marko pamoja naye na kusafiri kwa mashua kwenda Saiprasi. Paulo alimchagua Sila akaondoka kwenda zake.”—Matendo 15:36-40.

Lazima Marko awe alivunjika moyo sana kufahamu kwamba mtume Paulo aliyeheshimiwa hakutaka kufanya kazi pamoja naye na kwamba bishano lililohusu kustahili kwake lilisababisha Paulo na Barnaba watengane. Lakini mambo hayakuishia hapo.

Bado Paulo na Sila walihitaji mwenzi wa kusafiri naye. Walipofika Listra, walipata mtu wa kuchukua mahali pa Marko, kijana aliyeitwa Timotheo. Kufikia wakati huo, huenda Timotheo alikuwa amebatizwa kwa muda wa miaka miwili au mitatu tu wakati alipochaguliwa. Kwa upande mwingine, Marko alikuwa ameshirikiana na kutaniko la Kikristo tangu lilipoanzishwa—muda mrefu, hata kuliko Paulo mwenyewe. Hata hivyo, Timotheo ndiye aliyepokea pendeleo hilo.—Matendo 16:1-3.

Marko aliitikiaje alipofahamu kwamba mahali pake pamechukuliwa na mwanamume mchanga zaidi, asiye na ujuzi? Biblia haisemi chochote kuhusu hilo. Hata hivyo, inaonyesha kwamba Marko aliendelea kuwa mtendaji katika utumishi wa Yehova. Alitumia kwa manufaa mapendeleo aliyopewa. Ijapokuwa hakuweza kutumikia pamoja na Paulo na Sila, aliweza kusafiri na Barnaba hadi Saiprasi, eneo alikotoka Barnaba. Marko pia alitumikia pamoja na Petro huko Babiloni. Hatimaye, alikuwa na fursa ya kufanya kazi pamoja na Paulo—na Timotheo—huko Roma. (Wakolosai 1:1; 4:10; 1 Petro 5:13) Baadaye Marko hata alipuliziwa kuandika mojawapo ya Gospeli nne!

Tunapata somo lenye thamani kutokana na yote hayo. Marko hakuhangaika sana kwa kupoteza pendeleo kiasi cha kushindwa kuthamini mapendeleo ambayo bado angeweza kufikia. Marko alikuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Yehova, naye Yehova alimbariki.

Kwa hiyo, ikiwa umepoteza pendeleo fulani, usivunjike moyo. Ukidumisha mtazamo unaofaa na kuwa na mengi ya kufanya, huenda ukapewa mapendeleo mengine. Kuna mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.—1 Wakorintho 15:58.

Mtumishi Mwaminifu Avunjika Moyo

Si rahisi kufanya pigano kali la imani. Huenda nyakati nyingine ukavunjika moyo. Kisha huenda hata ukahisi kuwa na hatia kwa sababu ya kuvunjika moyo na kukata kauli kwamba mtumishi mwaminifu wa Mungu hapaswi kuhisi hivyo kamwe. Mfikirie Eliya, mmojawapo wa manabii wa Israeli wenye kutokeza.

Malkia wa Israeli Yezebeli, mtetezi shupavu wa ibada ya Baali alipojua kwamba manabii wa Baali walikuwa wameuawa na Eliya, aliapa kumwua. Eliya alikuwa amekabili maadui wakubwa zaidi kuliko Yezebeli, lakini alivunjika moyo kwa ghafula hivi kwamba alitamani afe. (1 Wafalme 19:1-4) Jambo hilo lingetukiaje? Alikuwa amesahau jambo fulani.

Eliya alikuwa amesahau kumtegemea Yehova kuwa Chanzo cha nguvu zake. Ni nani aliyekuwa amempa Eliya nguvu za kufufua mfu na kukabiliana na manabii wa Baali? Ni Yehova. Bila shaka, Yehova angeweza kumpa nguvu za kukabiliana na hasira ya kisasi ya Malkia Yezebeli.—1 Wafalme 17:17-24; 18:21-40; 2 Wakorintho 4:7.

Mtu yeyote anaweza kusitasita kwa muda mfupi katika kumtumaini Yehova. Kama Eliya, huenda nyakati nyingine ukawa na maoni ya kibinadamu kuhusu tatizo fulani badala ya kutumia “hekima ya kutoka juu” kulishughulikia. (Yakobo 3:17) Hata hivyo, Yehova hakumwacha Eliya kwa sababu ya kosa hilo la muda.

Eliya alitorokea Beer-sheba kisha akaenda nyikani, mahali ambapo alifikiri hakuna mtu angeweza kumpata. Lakini Yehova alimpata. Alituma malaika amfariji. Malaika huyo alihakikisha kwamba Eliya amepata mkate wa kula uliotoka tu kuokwa na maji ya kunywa yenye kuburudisha. Eliya alipopumzika, malaika alimwagiza asafiri umbali wa kilometa 300 hivi hadi Mlima Horebu, ambapo angeimarishwa zaidi na Yehova.—1 Wafalme 19:5-8.

Akiwa katika Mlima Horebu, Eliya alishuhudia jambo lenye kuimarisha imani linaloonyesha nguvu za Yehova. Kisha, kwa sauti tulivu ya chini, Yehova alimhakikishia kwamba hakuwa peke yake. Yehova alikuwa pamoja naye, hali kadhalika ndugu zake 7,000, ijapokuwa Eliya hakuwajua. Hatimaye, Yehova alimpa kazi. Hakuwa ameacha kumtumia Eliya kuwa nabii wake!—1 Wafalme 19:11-18.

Msaada Wapatikana

Ikiwa pindi kwa pindi unahisi kuvunjika moyo kidogo, huenda ukaona kwamba utahisi vyema ukipumzika zaidi au kula chakula chenye kutia nguvu. Wakati fulani Nathan H. Knorr, aliyetumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova hadi alipokufa mwaka wa 1977, alisema kwamba matatizo makubwa huonekana kuwa madogo zaidi baada ya kupata usingizi wa kutosha usiku. Hata hivyo, tatizo hilo likidumu zaidi, huenda suluhisho hilo lisitoshe—utahitaji msaada ili kupambana na kivunja-moyo.

Yehova alituma malaika amwimarishe Eliya. Leo, Mungu hutoa kitia-moyo kupitia wazee na Wakristo wengine wakomavu. Kwa kweli wazee wanaweza “[kuwa] kama mahali pa kujificha na upepo.” (Isaya 32:1, 2) Lakini ili upate kitia-moyo kutoka kwao, huenda ukalazimika kuchukua hatua ya kwanza. Hata ingawa Eliya alikuwa amevunjika moyo, alisafiri hadi Mlima Horebu ili kupokea maagizo kutoka kwa Yehova. Tunapokea maagizo yenye kuimarisha kupitia kutaniko la Kikristo.

Tunapokubali msaada na kukabiliana na majaribu kwa ujasiri, kama vile kuumizwa hisia au kupoteza mapendeleo, twaunga mkono upande wa Yehova kuhusu suala lililo muhimu. Suala gani? Shetani alisisitiza kwamba wanadamu humtumikia Yehova ili kujinufaisha tu. Shetani hakatai kwamba tutamtumikia Mungu wakati mambo yote ni shwari maishani, lakini anasisitiza kwamba tutaacha kumtumikia Mungu tunapopatwa na matatizo. (Ayubu, sura ya 1 na ya 2) Kwa kuendelea bila kuyumbayumba katika utumishi wa Yehova licha ya kivunja-moyo, tunaweza kusaidia kutoa jibu kwa shtaka la Ibilisi lenye uchongezi.—Mithali 27:11.

Hana, Marko, na Eliya walikuwa na matatizo yaliyokatisha shangwe yao kwa muda mfupi. Hata hivyo, walikabiliana na matatizo yao na kuishi maisha yenye mafanikio. Kwa msaada wa Yehova, wewe pia unaweza kukabiliana na kivunja-moyo!