Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Wakristo wa kweli waoneje mazoea ya kawaida ya watu wanaowapa wengine nakala za programu za kibiashara za kompyuta?

Huenda wengine wakajaribu kimakosa kutoa udhuru kuhusu tabia hiyo wakirejezea maneno ya Yesu: “Mlipokea bure, toeni bure.” Bila shaka, Yesu hakuwa akitaja kutoa bure nakala za vichapo au programu za kompyuta zilizo na haki za kunukuu, ambazo hutumiwa kupatana na sheria. Alimaanisha utoaji ukiwa sehemu ya huduma. Yesu aliwaambia mitume wake waliokuwa wanaenda kwenye miji na vijiji mbalimbali kwamba walipaswa kuhubiri Ufalme, kuponya wagonjwa na kufukuza roho waovu. Badala ya kutoza watu kazi hizo, mitume walipaswa “kutoa bure.”—Mathayo 10:7, 8.

Kukiwa na idadi kubwa sana ya kompyuta za kibinafsi na za kibiashara, watu wengi wamehitaji programu za kompyuta. Mara nyingi, lazima zinunuliwe. Watu fulani huandika programu ambazo huzitoa bila malipo na ambazo wao husema kwamba zaweza kunakiliwa na kupewa wengine pia. Lakini programu nyingi za kompyuta zauzwa kwa makusudi ya biashara. Iwe ni za kutumiwa nyumbani au ni za matumizi ya kibiashara, wenye kutumia programu hizo wanatazamiwa kuzinunua, na kuzilipia. Mtu akichukua au kunakili furushi la programu za kompyuta bila kuzilipia, hilo halingekuwa jambo la halali, kama vile kufanya fotokopi vitabu, hata kama fotokopi hizo zinapeanwa bure.

Programu nyingi za kompyuta (kutia ndani michezo ya kompyuta) zina leseni, huku mwenyewe/mtumiaji akitakikana afuate masharti na vizuizi hususa. Nyingi za leseni hizo hueleza kwamba ni mtu mmoja tu ambaye anaweza kuweka na kutumia programu hiyo—mara nyingi akiiweka kwenye kompyuta moja tu, iwe ya nyumbani au ya mahali pa biashara au shuleni. Leseni fulani hueleza kwamba mtumiaji anaweza kuwa na nakala ya ziada, lakini hawezi kufanyia watu wengine nakala. Ikiwa mwenye programu hiyo anataka kupeana programu nzima (kutia ndani leseni na uhifadhi wa nyaraka), anaweza kufanya hivyo. Hata hivyo, akifanya hivyo anakuwa hana haki ya kuitumia. Leseni hutofautiana, kwa hiyo mtu anayenunua au anayepewa programu apaswa kuuliza leseni hiyo ina masharti gani.

Mataifa mengi yana mapatano ya ushirika ambayo hulinda “mali ya kitaaluma,” kama vile programu za kompyuta, nayo hujaribu kutekeleza sheria za haki ya kunukuu. Kwa mfano, gazeti The New York Times la Januari 14, 2000, liliripoti kwamba “maofisa wa polisi, mmoja Mjerumani na yule mwingine Mdenishi, walishika washiriki wa kikundi walichokiita genge kubwa la wezi wa programu za kompyuta” ambao walikuwa wakifanya nakala na kugawanya programu na michezo ya kompyuta na hata kuuza nyinginezo kupitia Internet.

Msimamo wa kutaniko la Kikristo ni upi kuhusu jambo hilo? Yesu alisema: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mlipeni Mungu vitu vya Mungu.” (Marko 12:17) Jambo hilo lataka Wakristo watii sheria za nchi ambazo hazipingani na sheria ya Mungu. Kuhusu serikali, mtume Paulo aliandika hivi: “Acheni kila nafsi iwe katika ujitiisho kwa mamlaka zilizo kubwa . . . Yeye aipingaye mamlaka amechukua msimamo dhidi ya mpango wa Mungu; wale ambao wamechukua msimamo dhidi ya huo watapokea hukumu juu yao wenyewe.”—Waroma 13:1, 2.

Wazee katika kutaniko la Kikristo hawana daraka la kuchunguza kompyuta za wengine kana kwamba wameidhinishwa kufasiri na kutekeleza sheria za haki za kunukuu. Lakini wanaamini na kufundisha kwamba Wakristo wanapaswa waepuke kuchukua kitu kisicho chao na wanapaswa kujitahidi kutii sheria. Hilo hulinda Wakristo wasije wakaadhibiwa kuwa wavunja-sheria, na huwawezesha kuwa na dhamiri safi mbele za Mungu. Paulo aliandika hivi: “Kwa hiyo kuna sababu yenye kushurutisha nyinyi watu kuwa katika ujitiisho, si kwa sababu ya hasira hiyo ya kisasi tu, bali pia kwa sababu ya dhamiri yenu.” (Waroma 13:5) Vivyo hivyo, Paulo alieleza tamaa ya Wakristo wa kweli kwa maneno haya: “Twaitibari tuna dhamiri yenye kufuata haki, kwa kuwa twataka kujiendesha wenyewe kwa kufuata haki katika mambo yote.”—Waebrania 13:18.

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

Kampuni na shule kadhaa hununua leseni za watumiaji wengi ambazo huwa na mapatano ya kuruhusu watumiaji kadhaa watumie programu hizo. Mwaka wa 1995, makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yalizungumzia makala iliyotia ndani ushauri huu:

“Kampuni zilizo nyingi zinazotayarisha na kuuza programu za kompyuta huhifadhi haki zazo za uchapaji, nazo huandaa leseni zikionyesha jinsi programu hizo zaweza kutumiwa kisheria. Kwa kawaida leseni husema kwamba mwenyeji hawezi kuwapa wengine nakala za programu hiyo; kwa kweli, sheria ya haki ya uchapaji ya kimataifa hufanya iwe haramu kufanya hivyo. . . . Kampuni fulani kubwa zinauza kompyuta zenye programu zilizowekwa ndani kimbele na kupewa leseni. Hata hivyo, maduka fulani ya kompyuta hayatoi leseni kwa sababu programu ambazo yanaweka ndani kimbele ni nakala haramu, hiyo ikimaanisha kwamba mwenye kununua anakiuka sheria kwa kutumia programu hizo. Kuhusiana na hili, Wakristo wapaswa kuepuka kuingiza katika, au kunakili kutoka katika mifumo ya simu iliyounganishwa na kompyuta, habari ya kielektroni ambayo haki zayo za uchapaji zimehifadhiwa (kama vile vichapo vya Sosaiti) na ambayo inanakiliwa bila ruhusa ya kisheria kutoka kwa wenyeji.”