Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtafuteni Yehova Kabla ya Siku Yake ya Hasira

Mtafuteni Yehova Kabla ya Siku Yake ya Hasira

Mtafuteni Yehova Kabla ya Siku Yake ya Hasira

“Mtafuteni BWANA . . . itafuteni haki [“uadilifu,” “NW”], utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.”—SEFANIA 2:3.

1. Hali ya kiroho ya Yuda ilikuwaje wakati Sefania alipoanza kutoa unabii?

SEFANIA alianza kutoa unabii wakati muhimu katika historia ya Yuda. Hali ya kiroho ya taifa hilo ilikuwa imefikia kiwango cha chini sana. Watu walikuwa wakitegemea uongozi wa makuhani wapagani na wanajimu, badala ya kumtumaini Yehova. Ibada ya Baali, pamoja na sherehe zake za ibada ya uzazi, ilikuwa imeenea sana nchini humo. Viongozi wa serikali—wakuu, wenye nguvu, na makadhi—walikuwa wakiwaonea watu ambao walipaswa kulinda. (Sefania 1:9; 3:3) Ndiyo sababu Yehova aliamua ‘kuunyosha mkono wake’ dhidi ya Yuda na Yerusalemu ili kuziharibu!—Sefania 1:4.

2. Kulikuwa na tumaini gani kwa watumishi waaminifu wa Mungu nchini Yuda?

2 Hata hivyo, ingawa hali ilikuwa mbaya, kulikuwa na tumaini japo kidogo. Yosia, mwana wa Amoni, sasa alikuwa akitawala. Ingawa alikuwa kivulana tu, Yosia alimpenda Yehova kikweli. Iwapo mfalme huyo mpya angerudisha ibada safi nchini Yuda, hilo lingekuwa jambo lenye kutia moyo kama nini kwa wale wachache waliokuwa wakimtumikia Mungu kwa uaminifu! Huenda hata wengine wangechochewa kujiunga nao na kuhifadhiwa pia katika siku ya hasira ya Yehova.

Matakwa ya Kuhifadhiwa

3, 4. Ni matakwa gani matatu ambayo lazima yatimizwe ili mtu ahifadhiwe katika “siku ya hasira ya BWANA”?

3 Je, kwa kweli watu fulani wangeweza kuhifadhiwa katika siku ya hasira ya Yehova? Ndiyo, maadamu walitimiza matakwa matatu yaliyo kwenye Sefania 2:2, 3. Tusomapo mistari hiyo, acheni tuzingatie matakwa hayo. Sefania aliandika: “Kabla haijazaa hiyo amri, kabla haijapita siku ile kama makapi, kabla haijawajilia hasira kali ya BWANA, kabla haijawajilia siku ya hasira ya BWANA. Mtafuteni BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki [“uadilifu,” NW], utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.”

4 Basi, ili kuhifadhiwa, mtu alipaswa (1) kumtafuta Yehova, (2) kuutafuta uadilifu, na (3) kuutafuta unyenyekevu. Twapendezwa sana na matakwa hayo leo. Kwa nini? Kwa sababu kama vile Yuda na Yerusalemu zilivyohukumiwa katika karne ya saba K.W.K., ndivyo mataifa ya Jumuiya ya Wakristo na, kwa kweli, waovu wote wanavyoelekea kukabiliana na Yehova Mungu kwenye “dhiki kubwa” inayokuja. (Mathayo 24:21) Wowote ambao wangependa kufichwa wakati huo lazima wachukue hatua madhubuti sasa. Jinsi gani? Kwa kumtafuta Yehova, kuutafuta uadilifu, na kuutafuta unyenyekevu, kabla haijawa kuchelewa mno!

5. Ni nini kinachomaanishwa na ‘kumtafuta Yehova’ leo?

5 Huenda ukasema hivi: ‘Mimi ni mtumishi wa Mungu, nimejiweka wakfu na kubatizwa, nami ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nimeyatimiza matakwa hayo, sivyo?’ Kusema kweli, mengi zaidi yahusika kuliko kujiweka wakfu kwa Yehova. Israeli lilikuwa taifa wakfu, lakini katika siku za Sefania watu wa Yuda hawakuwa wakiishi kulingana na wakfu huo. Kwa sababu hiyo, taifa hilo lilikatiliwa mbali hatimaye. ‘Kumtafuta Yehova’ leo humaanisha kusitawisha na kudumisha uhusiano mchangamfu wa kibinafsi pamoja naye na kushirikiana na tengenezo lake la kidunia. Kwamaanisha kupata kujua jinsi Mungu anavyoona mambo na kutilia maanani hisia zake. Sisi humtafuta Yehova tunapojifunza kwa makini Neno lake, kulitafakari na kutumia ushauri wa Neno hilo maishani. Tutafutapo pia mwelekezo wa Yehova kupitia sala ya bidii na kufuata mwongozo wa roho yake takatifu, uhusiano wetu naye huzidi kukua nasi huchochewa tumtumikie ‘kwa moyo wetu wote, na kwa roho yetu yote, na kwa nguvu zetu zote.’—Kumbukumbu la Torati 6:5; Wagalatia 5:22-25; Wafilipi 4:6, 7; Ufunuo 4:11.

6. ‘Tunautafutaje uadilifu,’ na kwa nini jambo hilo linawezekana hata katika ulimwengu huu?

6 Takwa la pili linalotajwa kwenye Sefania 2:3 ni ‘kuutafuta uadilifu.’ Wengi wetu tulifanya mabadiliko makubwa ili tustahili ubatizo wa Kikristo, lakini ni lazima tuendelee kutegemeza kanuni za uadilifu za Mungu katika maisha yetu yote. Watu fulani walioanza kwa bidii wamejiruhusu wachafuliwe na ulimwengu. Ni kweli kwamba, si rahisi kuutafuta uadilifu kwa kuwa twazungukwa na watu wanaoona ukosefu wa adili katika ngono, kusema uwongo, na dhambi nyinginezo kuwa mambo ya kawaida. Lakini tamaa yenye nguvu ya kumpendeza Yehova yaweza kuushinda mwelekeo wowote wa kutafuta kibali cha ulimwengu kwa kujaribu kujipatanisha nao. Watu wa Yuda walipoteza kibali cha Mungu kwa kuwa walijaribu kuiga mataifa jirani zao ambao hawakumwogopa Mungu. Basi badala ya kuuiga ulimwengu, na tuwe “waigaji wa Mungu,” tukisitawisha “utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.”—Waefeso 4:24; 5:1.

7. ‘Tunautafutaje unyenyekevu’?

7 Jambo la tatu linalotajwa kwenye Sefania 2:3 ni kwamba ikiwa twataka kufichwa katika siku ya hasira ya Yehova, ni lazima ‘tuutafute unyenyekevu.’ Kila siku, sisi huchangamana na wanaume, wanawake, na vijana ambao si wanyenyekevu hata kidogo. Wanaona kwamba kuwa na tabia ya upole ni dosari. Unyenyekevu huonwa kuwa udhaifu mkubwa sana. Wao ni wenye kudai mambo mno, wenye ubinafsi, wenye kushikilia kauli yao, na kuamini kwamba mambo wanayoyaona kuwa “haki” yao na mapendezi yao yapasa kukubaliwa na watu wote hata hali iweje. Lingekuwa jambo lenye kusikitisha kama nini iwapo tungelianza kuwa na maoni kama hayo! Huu ndio wakati wa ‘kuutafuta unyenyekevu.’ Jinsi gani? Kwa kujitiisha chini ya Mungu, kwa kukubali kwa unyenyekevu nidhamu yake na kutenda kupatana na mapenzi yake.

Kwa Nini “Huenda” Tukafichwa?

8. Ni nini kinachoonyeshwa na matumizi ya neno “huenda” kwenye Sefania 2:3?

8 Ona kwamba andiko la Sefania 2:3 lasema: “Huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.” Kwa nini Sefania alitumia neno “huenda” alipokuwa akiongea na “wanyenyekevu wa dunia?” Wanyenyekevu hao walikuwa wamechukua hatua zinazofaa, lakini hawakupaswa kujitumainia. Hawakuwa wamefikia mwisho wa maisha yao wakiwa waaminifu. Baadhi yao wangaliweza kufanya dhambi. Inaweza kuwa hivyo kwetu. Yesu alisema: “Yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:13) Naam, wokovu katika siku ya hasira ya Yehova wategemea kuendelea kwetu kufanya yaliyo sawa machoni pake. Je, umeazimia kwa dhati kuendelea kufanya yaliyo sawa?

9. Mfalme Yosia kijana alichukua hatua gani za unyofu?

9 Yaonekana kwa kuitikia maneno ya Sefania, Mfalme Yosia alichochewa ‘kumtafuta BWANA.’ Maandiko yanasema: “Katika mwaka wa nane wa kutawala kwake, naye [Yosia] akali mchanga [akiwa na umri wa miaka 16 hivi], alianza kumtafuta Mungu wa Daudi babaye.” (2 Mambo ya Nyakati 34:3) Yosia pia aliendelea ‘kutafuta uadilifu,’ kwa kuwa twasoma hivi: “Katika mwaka wa kumi na mbili [Yosia alipokuwa na umri wa miaka 20 hivi] akaanza kusafisha Yuda na Yerusalemu kwa kuondoa mahali pa juu, na kwa kuondoa maashera, na sanamu za kuchora, nazo za kusubu. Wakazibomoa madhabahu za mabaali machoni pake.” (2 Mambo ya Nyakati 34:3, 4) Yosia ‘alitafuta unyenyekevu’ pia, kwa kuchukua hatua ya unyenyekevu ya kuitakasa nchi kwa kuondoa ibada ya sanamu na mazoea mengine ya dini isiyo ya kweli kusudi ampendeze Yehova. Ni lazima wanyenyekevu wengine wawe walishangilia kama nini walipoona jinsi alivyotenda!

10. Ni nini kilichotukia Yuda mwaka wa 607 K.W.K., lakini ni nani waliohifadhiwa?

10 Wayahudi wengi walimrudia Yehova wakati wa utawala wa Yosia. Hata hivyo, baada ya mfalme huyo kufa, wengi walirudia njia zao za kale—mazoea yasiyokubalika kwa Mungu hata kidogo. Kama vile Yehova alivyokuwa ameagiza, Wababiloni walishinda Yuda na kuharibu jiji lake kuu, Yerusalemu, mwaka wa 607 K.W.K. Hata hivyo, kuna waliosalia. Nabii Yeremia, Ebed-meleki Mwethiopia, wazao wa nyumba ya Yonadabu, na wengine waliokuwa waaminifu kwa Mungu walifichwa katika siku hiyo ya hasira ya Yehova.—Yeremia 35:18, 19; 39:11, 12, 15-18.

Maadui wa Mungu—Tahadharini!

11. Kwa nini si rahisi kudumu ukiwa mwaminifu kwa Mungu leo, lakini maadui wa watu wa Yehova wapaswa kuzingatia nini?

11 Tungojeapo siku ya hasira ya Yehova dhidi ya mfumo huu mwovu, ‘tunakutana na majaribu ya namna mbalimbali.’ (Yakobo 1:2) Katika nchi kadhaa ambazo hudai kuthamini uhuru wa ibada, makasisi wenye hila wametumia uwezo wao katika mamlaka za kilimwengu ili kutokeza mnyanyaso mkali dhidi ya watu wa Mungu. Watu wasio na maadili wamewachongea Mashahidi wa Yehova, kwa kuwaita “madhehebu hatari.” Mungu anajua matendo yao naye hana budi kuwaadhibu. Maadui wa Mungu wapaswa kufikiria kilichowapata maadui wa watu wake nyakati za kale kama vile Wafilisti. Unabii wasema hivi: “Gaza utaachwa, na Ashkeloni utakuwa ukiwa; wataufukuzia mbali Ashdodi wakati wa adhuhuri, na Ekroni utang’olewa.” Majiji ya Wafilisti ya Gaza, Ashkeloni, Ashdodi, na Ekroni yangeharibiwa.—Sefania 2:4-7.

12. Ni nini kilichopata Ufilisti, Moabu, na Amoni?

12 Unabii huo waendelea kusema: “Mimi nimeyasikia matukano ya Moabu, na dhihaka za wana wa Amoni, ambazo kwa hizo wamewatukana watu wangu, na kujitukuza juu ya mpaka wao.” (Sefania 2:8) Ni kweli kwamba Misri na Ethiopia waliteseka mikononi mwa wavamizi Wababiloni. Lakini Mungu angehukumuje Moabu na Amoni, mataifa ambayo ni uzao wa Loti, mpwa wa Abrahamu? Yehova alitabiri hivi: “Hakika Moabu atakuwa kama Sodoma, na wana wa Amoni kama Gomora.” Tofauti na wazazi wao wa kale—wale binti wawili wa Loti, waliosalimika kuharibiwa kwa Sodoma na Gomora—Moabu na Amoni yenye majivuno hawangefichwa wasipatwe na hukumu za Mungu. (Sefania 2:9-12; Mwanzo 19:16, 23-26, 36-38) Taifa la Ufilisti pamoja na majiji yake, liko wapi leo? Namna gani Moabu na Amoni ambayo wakati mmoja yalikuwa na majivuno? Hata ukiyatafuta namna gani, hutayapata.

13. Ni uvumbuzi gani wa kiakiolojia uliofanywa Ninawi?

13 Katika siku ya Sefania, Milki ya Ashuru ilikuwa imefikia kilele cha nguvu zake. Akifafanua sehemu moja ya jumba la mfalme ambalo alikuwa amechimbua katika Ninawi, jiji kuu la Ashuru, Mwakiolojia Austen Layard, aliandika hivi: “Paa . . . ziligawanywa na kuwa visehemu mraba, vilivyochorwa maua, au wanyama. Baadhi yake vilipambwa kwa pembe za ndovu, kila kisehemu kikiwa na mipaka na nakshi sanifu. Mihimili, hali kadhalika sehemu ya kandokando ya vyumba, ilifanywa ionekane kana kwamba ni dhahabu na fedha, au huenda hata ilifunikwa kwa dhahabu na fedha; nazo mbao adimu sana, hasa mbao za mwerezi, zilitumiwa.” Hata hivyo, kama ilivyotabiriwa katika unabii wa Sefania, Ashuru ingeharibiwa nalo jiji lake, Ninawi, lingekuwa “ukiwa.”—Sefania 2:13.

14. Unabii wa Sefania ulitimizwaje juu ya Ninawi?

14 Miaka 15 tu baada ya Sefania kutoa unabii huo, Ninawi lenye nguvu liliharibiwa, na jumba la mfalme lililokuwa tukufu likafanywa kuwa vifusi. Naam, jiji hilo lenye majivuno liliharibiwa kabisa. Kiwango cha uharibifu kilitabiriwa waziwazi katika maneno haya: “Mwari-nyuni na nungu watakaa juu ya vichwa vya nguzo zake [zilizoanguka]; sauti yao itasikiwa madirishani; vizingitini mwake mtakuwa ukiwa.” (Sefania 2:14, 15) Majengo ya fahari ya Ninawi yangefaa kukaliwa tu na nungu na mwari-nyuni. Makelele ya wafanya biashara hayangesikiwa tena barabarani, wala vilio vya wapiganaji, wala nyimbo za makuhani. Na kwenye barabara zilizokuwa na watu wengi wakati mmoja, kungesikiwa tu sauti ikiimba kwa woga dirishani, huenda ni sauti ya wimbo wa huzuni wa ndege au mvumo wa upepo. Adui wote wa Mungu na wakome vivyo hivyo!

15. Tunaweza kujifunza nini kutokana na yaliyopata Ufilisti, Moabu, Amoni, na Ashuru?

15 Tunaweza kujifunza nini kutokana na yaliyopata Ufilisti, Moabu, Amoni, na Ashuru? Kwamba: Tukiwa watumishi wa Yehova hatuna haja ya kuwaogopa maadui wetu. Mungu huona yale yanayofanywa na wale wanaopinga watu wake. Yehova aliwachukulia hatua maadui wake zamani, na hukumu zake zitatekelezwa dhidi ya dunia yote inayokaliwa leo. Lakini kutakuwako waokokaji—‘umati mkubwa kutoka katika mataifa yote.’ (Ufunuo 7:9) Unaweza kuwa miongoni mwao—iwapo tu utaendelea kumtafuta Yehova, kuutafuta uadilifu, na kuutafuta unyenyekevu.

Ole kwa Wakosaji Wenye Ufidhuli!

16. Unabii wa Sefania ulisema nini kuhusu wakuu na viongozi wa kidini wa Yuda, na kwa nini maneno hayo yanafafanua vizuri Jumuiya ya Wakristo?

16 Unabii wa Sefania waelekezwa kwa Yuda na Yerusalemu tena. Andiko la Sefania 3:1, 2 lasema: “Ole wake yeye aliyeasi na kutiwa unajisi, mji wa udhalimu! Hakuitii sauti; hakukubali kurudiwa; hakumwamini BWANA; hakumkaribia Mungu wake.” Yasikitisha kama nini kwamba jitihada za Yehova za kuwatia nidhamu watu wake hazikusikiwa kamwe! Ukatili wa wakuu, wenye nguvu, na makadhi, ulikuwa mbaya kwelikweli! Sefania alaumu ukosefu wa aibu wa viongozi wa kidini, akisema: “Manabii wake ni watu hafifu [“fidhuli,” NW], wadanganyifu; makuhani wake wamepatia unajisi patakatifu, wameifanyia sheria udhalimu.” (Sefania 3:3, 4) Maneno hayo yafafanua vizuri kama nini hali ya manabii na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo leo! Kwa ufidhuli, wameliondoa jina la Mungu kutoka katika tafsiri zao za Biblia na wamefundisha mafundisho yenye kupotosha juu ya Yule wanayedai kumwabudu.

17. Kwa nini tuendelee kutangaza habari njema hata watu wasikilize au wasisikilize?

17 Kwa kuwajali watu wake wa kale Yehova aliwaonya juu ya hatua ambayo angechukua. Aliwatuma watumishi wake manabii—Sefania na Yeremia, na wengine—wawasihi sana watu hao watubu. Naam, “BWANA . . . hatatenda uovu; kila asubuhi hudhihirisha hukumu yake, wala hakomi.” Waliitikiaje? “Bali mtu asiye haki hajui kuona haya,” akasema Sefania. (Sefania 3:5) Onyo kama hilo latolewa leo. Ikiwa wewe ni mhubiri wa habari njema, unashiriki kutoa onyo hilo. Endelea kutangaza habari njema bila kukoma! Watu wasikilize au wasisikilize, Mungu anaona kwamba huduma yako inafanikiwa maadamu unaendelea kuitekeleza kwa uaminifu; huhitaji kuaibika unapofanya kazi ya Mungu kwa bidii.

18. Andiko la Sefania 3:6 litatimizwaje?

18 Kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu kutahusisha mengi zaidi ya kufanywa ukiwa kwa Jumuiya ya Wakristo. Yehova ashutumu mataifa yote: “Nimekatilia mbali mataifa, buruji zao zina ukiwa; nimeziharibu njia kuu zao, hata hapana mmoja apitaye; miji yao imeangamizwa.” (Sefania 3:6) Maneno hayo ni yenye kutumainika hivi kwamba Yehova azungumza juu ya uharibifu huo kana kwamba tayari umetimia. Ni nini kilichoyapata majiji ya Ufilisti, Moabu, na Amoni? Namna gani Ninawi, jiji kuu la Ashuru? Kuharibiwa kwa majiji hayo kwapaswa kuwa onyo kwa mataifa ya leo. Mungu si wa kudhihakiwa.

Endelea Kumtafuta Yehova

19. Ni maswali gani yenye kuamsha fikira ambayo huenda tukauliza?

19 Wakati wa Sefania, hasira ya Mungu iliwapata wale ‘walioharibu matendo yao yote’ kwa uovu. (Sefania 3:7) Jambo hilohilo litatukia wakati wetu. Je, unaona uthibitisho kwamba siku ya Yehova i karibu? Je, unaendelea ‘kumtafuta Yehova’ kwa kusoma Neno lake kwa ukawaida—kila siku? Je, ‘unautafuta uadilifu’ kwa kuishi maisha safi kiadili kupatana na viwango vya Mungu? Na je, ‘unautafuta unyenyekevu’ kwa kujinyenyekeza na kuwa mtiifu kwa Mungu na mipango yake ya wokovu?

20. Tutachunguza maswali gani katika makala ya mwisho ya mfululizo huu wa unabii wa Sefania?

20 Tukiendelea kumtafuta Yehova, kuutafuta uadilifu, na kuutafuta unyenyekevu, tunaweza kutazamia kupata baraka nyingi sasa—naam, hata katika ‘siku hizi za mwisho’ zenye kujaribu imani. (2 Timotheo 3:1-5; Mithali 10:22) Lakini huenda tukauliza, ‘Tukiwa watumishi wa Yehova wa siku hizi tunabarikiwa kwa njia zipi, na ni baraka gani za wakati ujao ambazo unabii wa Sefania unaahidi wale watakaofichwa katika siku ya hasira ya Yehova inayokuja kwa kasi sana?’

Ungejibuje?

• Watu ‘humtafutaje Yehova’?

• Ni nini kinachomaanishwa na ‘kuutafuta uadilifu’?

• Tunawezaje ‘kuutafuta unyenyekevu’?

• Kwa nini tuendelee kumtafuta Yehova, kuutafuta uadilifu, na unyenyekevu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, unamtafuta Yehova kupitia funzo la Biblia na sala ya bidii?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Umati mkubwa wataokoka siku yake ya hasira kwa sababu wanaendelea kumtafuta Yehova