Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siku ya Hukumu ya Yehova I Karibu!

Siku ya Hukumu ya Yehova I Karibu!

Siku ya Hukumu ya Yehova I Karibu!

“Hiyo siku ya BWANA iliyo kuu i karibu; I karibu, nayo inafanya haraka sana.”—SEFANIA 1:14.

1. Mungu alitoa onyo gani kupitia Sefania?

YEHOVA MUNGU atawachukulia waovu hatua karibuni. Sikiliza! Hili ndilo onyo lake: “Nitamkomesha mwanadamu . . . nami nitamkatilia mbali mwanadamu, asionekane juu ya uso wa nchi.” (Sefania 1:3) Maneno hayo ya Yehova, Bwana Mwenye Enzi Kuu yalisemwa kupitia nabii wake Sefania, ambaye huenda alikuwa kilembwe wa Mfalme Hezekia mwaminifu. Tangazo hilo, lililotolewa siku za Mfalme Yosia mzuri, halikuashiria mema kwa waovu walioishi Yuda.

2. Kwa nini matendo ya Yosia hayakuizuia siku ya hukumu ya Yehova?

2 Bila shaka, unabii wa Sefania ulifanya Yosia afahamu hata zaidi kwamba kulikuwa na uhitaji wa kuondoa ibada isiyo safi nchini Yuda. Hata hivyo, matendo ya mfalme huyo ya kuondoa nchini dini zisizo za kweli hayakuondoa uovu wote miongoni mwa watu wala kufunika dhambi za babu yake, Mfalme Manase, ambaye “aliujaza Yerusalemu damu zisizo na hatia.” (2 Wafalme 24:3, 4; 2 Mambo ya Nyakati 34:3) Kwa hiyo, bila shaka siku ya hukumu ya Yehova ingekuja.

3. Twawezaje kuwa na hakika kwamba inawezekana kuokoka “siku ya hasira ya BWANA”?

3 Hata hivyo, watu fulani wangeokoka siku hiyo yenye kutia hofu. Kwa hiyo, nabii wa Mungu alihimiza hivi: “Kabla haijazaa hiyo amri, kabla haijapita siku ile kama makapi, kabla haijawajilia hasira kali ya BWANA, kabla haijawajilia siku ya hasira ya BWANA. Mtafuteni BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.” (Sefania 2:2, 3) Tunapozingatia tumaini la kuokoka siku ya hukumu ya Yehova, acheni tuchunguze kitabu cha Biblia cha Sefania. Kiliandikwa huko Yuda kabla ya mwaka wa 648 K.W.K. nacho ni sehemu ya “neno la unabii” la Mungu, ambalo sote twapaswa kusikiliza kwa moyo wote.—2 Petro 1:19.

Mkono wa Yehova Wanyoshwa

4, 5. Andiko la Sefania 1:1-3 lilitimizwaje juu ya waovu wa Yuda?

4 “Neno la BWANA” kwa Sefania laanza kwa onyo lililotajwa hapo awali. Mungu atangaza: “Nitavikomesha kabisa vitu vyote, visionekane juu ya uso wa nchi, asema BWANA. Nitamkomesha mwanadamu na mnyama; nitakomesha ndege wa angani, na samaki wa baharini, na hayo makwazo pamoja na wabaya; nami nitamkatilia mbali mwanadamu, asionekane juu ya uso wa nchi, asema BWANA.”—Sefania 1:1-3.

5 Naam, Yehova angekomesha uovu wenye kupita kiasi nchini Yuda. Mungu angemtumia nani ‘kukomesha kabisa vitu vyote visionekane juu ya uso wa nchi’? Kwa kuwa yaonekana Sefania alitabiri mwanzoni mwa utawala wa Mfalme Yosia, ulioanza mwaka wa 659 K.W.K., maneno hayo ya unabii yalitimizwa wakati Yuda na jiji lake kuu, Yerusalemu, lilipofanywa ukiwa na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K. Wakati huo, waovu waliokuwa Yuda ‘walikomeshwa kabisa.’

6-8. Ni nini kilichotabiriwa kwenye Sefania 1:4-6, na unabii huo ulitimizwaje katika Yuda ya kale?

6 Likitabiri matendo ya Mungu dhidi ya waabudu wasio wa kweli, andiko la Sefania 1:4-6 lasema hivi: “Nitaunyosha mkono wangu juu ya Yuda, na juu ya watu wote wakaao Yerusalemu; nami nitayakatilia mbali mabaki ya Baali, yasionekane mahali hapa, na hilo jina la Wakemari pamoja na makuhani; na wale walisujudiao jeshi la mbinguni juu ya dari za nyumba; na hao waabuduo, waapao kwa BWANA na kuapa pia kwa Malkamu; na hao waliorudi nyuma, na kuacha kumfuata BWANA; na hao wasiomtafuta BWANA, wala kumwulizia.”

7 Mkono wa Yehova ulikuwa umenyoshwa dhidi ya watu wa Yuda na Yerusalemu. Alikuwa ameazimia kukatilia mbali katika kifo waabudu wa Baali aliyekuwa mungu wa Kanaani wa uzazi. Miungu kadhaa ya huko iliitwa Mabaali kwa kuwa walioiabudu walidhani kuwa miungu hiyo ina uvutano fulani katika mahali maalumu. Kwa mfano, kulikuwa na Baali aliyeabudiwa na Wamoabi na Wamidiani kwenye Mlima Peori. (Hesabu 25:1, 3, 6) Kotekote nchini Yuda, Yehova angewakatilia mbali makuhani wa Baali pamoja na makuhani Walawi wasio waaminifu ambao walikuwa wanakiuka sheria ya Mungu kwa kushirikiana na makuhani hao wa Baali.—Kutoka 20:2, 3.

8 Pia, Mungu angewakatilia mbali wale ‘walisujudiao jeshi la mbinguni,’ ambao yamkini walikuwa wanajimu na waliabudu jua. (2 Wafalme 23:11; Yeremia 19:13; 32:29) Hasira ya kisasi cha Mungu ingewapata pia wale waliojaribu kuchanganya ibada ya kweli na dini isiyo ya kweli kwa ‘kuapa kwa Yehova na kuapa pia kwa Malkamu.’ Huenda Malkamu ni jina jingine la Moleki, mungu mkuu wa Waamoni. Ibada ya Moleki ilitia ndani kutoa watoto dhabihu.—1 Wafalme 11:5; Yeremia 32:35.

Mwisho wa Jumuiya ya Wakristo Unakaribia!

9. (a) Jumuiya ya Wakristo ina hatia gani? (b) Tofauti na watu wa Yuda wasio waaminifu, twapaswa kuazimia kufanya nini?

9 Huenda yote hayo yakatukumbusha Jumuiya ya Wakristo, ambayo imekolea ibada isiyo ya kweli na unajimu. Nako kule kudhabihu mamilioni ya watu kwenye madhabahu ya vita vinavyoungwa mkono na makasisi ni jambo lenye kuchukiza kwelikweli! Na tusiwe kamwe kama watu wasio waaminifu wa Yuda, ‘walioacha kumfuata Yehova,’ wakawa wasiojali chochote na kuacha kabisa kumtafuta au kutafuta mwelekezo wake. Badala yake, na tudumishe uaminifu-maadili wetu kwa Mungu.

10. Unaweza kuelezaje maana ya unabii wa Sefania 1:7?

10 Maneno yanayofuata ya nabii huyo yawafaa wakosaji wa Yuda na waovu wa leo. Andiko la Sefania 1:7 lasema hivi: “Nyamaza kimya mbele za Bwana MUNGU; kwa maana siku ya BWANA i karibu; kwa kuwa BWANA ameweka tayari dhabihu, amewatakasa wageni wake.” Yaonekana kwamba “wageni wake” walikuwa Wakaldayo ambao walikuwa maadui wa Yuda. “Dhabihu” ilikuwa Yuda yenyewe, pamoja na jiji lake kuu. Hivyo Sefania alitangaza kusudi la Mungu la kuharibu Yerusalemu, na unabii huo uliashiria pia kuharibiwa kwa Jumuiya ya Wakristo. Kwa kweli, kwa kuwa siku ya hukumu ya Mungu i karibu sana leo ulimwengu wote wapaswa ‘kunyamaza kimya mbele za Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova’ na kusikia asemayo kupitia “kundi dogo” la wafuasi watiwa-mafuta wa Yesu na wenzao, ‘kondoo wake wengine.’ (Luka 12:32; Yohana 10:16) Wale wote ambao hawatasikiliza na hivyo kujipanga dhidi ya utawala wa Ufalme wa Mungu wataangamizwa.—Zaburi 2:1, 2.

Siku ya Kilio I Karibu!

11. Ni nini maana ya andiko la Sefania 1:8-11?

11 Kuhusu siku ya Yehova andiko la Sefania 1:8-11 laongeza kusema hivi: “Na itakuwa, katika siku ile ya dhabihu ya BWANA, nitawaadhibu wakuu, na wana wa mfalme, na watu wote waliovaa mavazi ya kigeni. Na katika siku ile nitawaadhibu hao wote warukao juu ya kizingiti, waijazao nyumba ya bwana wao udhalimu na udanganyifu. Na katika siku ile, asema BWANA kutakuwako sauti ya kilio kutoka lango la samaki, na mlio mkuu katika mtaa wa pili, na mshindo mkuu kutoka milimani. Haya! lieni, ninyi mkaao katika Makteshi, maana wafanya biashara wote wameangamia; hao wote waliokuwa na mizigo ya fedha wamekatiliwa mbali.”

12. Inakuwaje kwamba watu fulani wanapatikana wakiwa ‘wamevaa mavazi ya kigeni’?

12 Yehoahazi, Yehoyakimu, na Yekonia wangetawala baada ya Mfalme Yosia. Kisha Yerusalemu lingeharibiwa wakati wa utawala wa Zedekia. Ingawa walikuwa wanakabiliwa na maafa hayo, yaonekana watu fulani walitafuta kibali cha mataifa jirani kwa ‘kuvaa mavazi ya kigeni.’ Vivyo hivyo wengi leo hudhihirisha kwa njia mbalimbali kwamba wao si sehemu ya tengenezo la Yehova. Kwa kuwa wanathibitika kuwa sehemu ya tengenezo la Shetani, wataadhibiwa.

13. Kwa kupatana na unabii wa Sefania, ni nini ambacho kingetukia wakati Wababiloni wangeshambulia Yerusalemu?

13 “Siku ile” ambayo Yuda ilitozwa hesabu yalingana na siku ya Yehova ya kutekeleza hukumu yake dhidi ya maadui wake, kukomesha uovu, na kuthibitisha ukuu wake. Wababiloni washambuliapo Yerusalemu, kilio kingetoka katika Lango la Samaki. Huenda liliitwa hivyo kwa kuwa lilikuwa karibu na soko la samaki. (Nehemia 13:16) Magenge ya Babiloni yangeingia sehemu iitwayo mtaa wa pili, na huenda ikawa “mshindo mkuu kutoka milimani” warejezea kishindo cha Wakaldayo wanaokaribia. Wakazi wa Makteshi, yamkini sehemu ya juu ya Bonde la Tiropoa, ‘wangelia.’ Kwa nini wangelia? Kwa sababu biashara, kutia ndani biashara ya “waliokuwa na mizigo ya fedha,” ingekoma.

14. Mungu angewachunguza kwa undani kadiri gani wale wanaodai kuwa waabudu wake?

14 Yehova angewachunguza kwa undani kadiri gani wale wanaodai kuwa wanamwabudu? Unabii huo waendelea kusema hivi: “Kisha itakuwa wakati ule, nitauchunguza Yerusalemu kwa taa; nami nitawaadhibu watu walioganda juu ya sira zao; wasemao katika mioyo yao, BWANA hatatenda mema, wala hatatenda mabaya. Na huko utajiri wao utakuwa mateka, na nyumba zao zitakuwa ukiwa; naam, watajenga nyumba, lakini hawatakaa ndani yake; nao watapanda mizabibu, lakini hawatakunywa divai yake.”—Sefania 1:12, 13.

15. (a) Ni nini ambacho kingewapata makuhani waasi-imani wa Yerusalemu? (b) Ni nini kitakachowapata waabudu wa dini isiyo ya kweli leo?

15 Makuhani waasi-imani wa Yerusalemu walikuwa wakichanganya ibada ya Yehova na dini isiyo ya kweli. Ingawa waliona wako salama, Mungu angewatafuta kwa taa ambazo zingeangaza katika giza la kiroho ambamo wamejificha. Hakuna yeyote ambaye angeponyoka kutangazwa na kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu. Waasi-imani hao wasiojali walikuwa wametulia kama sira ndani ya pipa la divai. Hawakutaka kusumbuliwa na tangazo lolote la kuingiliwa na Mungu katika shughuli za wanadamu, lakini hawangeponyoka hukumu ya Mungu dhidi yao. Pia, waabudu wa dini isiyo ya kweli leo, kutia ndani wafuasi wa Jumuiya ya Wakristo hali kadhalika wale ambao wameasi ibada ya Yehova, hawataponyoka. Wakikana kwamba hizi si “siku za mwisho,” wanasema moyoni mwao, “BWANA hatatenda mema, wala hatatenda mabaya.” Lakini wamekosea kama nini!—2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:3, 4, 10.

16. Ni nini ambacho kingetukia wakati ambapo hukumu ya Mungu ingetekelezwa dhidi ya Yuda, na kujua hivyo kwapasa kutuathirije?

16 Waasi-imani wa Yuda walionywa kwamba Wababiloni wangepora mali zao, wangefanya nyumba zao ukiwa, na kutwaa matunda ya mashamba yao ya mizabibu. Mali za kimwili hazingekuwa na thamani yoyote wakati ambapo hukumu ya Mungu ingetekelezwa dhidi ya Yuda. Ndivyo itakavyokuwa siku ya hukumu ya Yehova itakapoujia mfumo huu wa mambo. Kwa hiyo, na tuwe na mtazamo wa kiroho na ‘kuweka hazina mbinguni’ kwa kuendelea kutanguliza utumishi wa Yehova maishani mwetu!—Mathayo 6:19-21, 33.

‘Siku ya Yehova Iliyo Kuu I Karibu’

17. Kulingana na Sefania 1:14-16, siku ya hukumu ya Yehova i karibu kadiri gani?

17 Siku ya hukumu ya Yehova i karibu kadiri gani? Kulingana na Sefania 1:14-16, Mungu ahakikisha hivi: “Hiyo siku ya BWANA iliyo kuu i karibu; i karibu, nayo inafanya haraka sana; naam, sauti ya siku ya BWANA; shujaa hulia kwa uchungu mwingi huko! Siku ile ni siku ya ghadhabu, siku ya fadhaa na dhiki, siku ya uharibifu na ukiwa, siku ya giza na utusitusi, siku ya mawingu na giza kuu, siku ya tarumbeta na ya kamsa, juu ya miji yenye maboma, juu ya buruji zilizo ndefu sana.”

18. Kwa nini hatupaswi kuamua kwamba siku ya hukumu ya Yehova i mbali sana?

18 Makuhani, wakuu, na watu wa Yuda wenye dhambi walionywa kwamba ‘siku ya BWANA iliyo kuu ilikuwa karibu.’ ‘Siku ya Yehova ingefanya haraka sana’ kwa ajili ya Yuda. Hali kadhalika leo, mtu yeyote asidhani ya kwamba kutekelezwa kwa hukumu ya Yehova dhidi ya waovu ku mbali sana. Badala yake, kama vile ambavyo Mungu alichukua hatua haraka huko Yuda, ndivyo ‘atakavyoharakisha’ siku yake ya kutekeleza hukumu. (Ufunuo 16:14, 16) Utakuwa wakati wenye uchungu kama nini kwa wote wanaopuuza maonyo ya Yehova yanayotolewa na Mashahidi wake na ambao hukataa ibada ya kweli!

19, 20. (a) Ni baadhi ya mambo gani yaliyohusika katika kudhihirishwa kwa hasira ya kisasi ya Mungu dhidi ya Yuda na Yerusalemu? (b) Kwa kuzingatia uharibifu utakaowapata watu waovu wa mfumo huu wa mambo, ni maswali gani yanayozuka?

19 Ilikuwa “siku ya fadhaa na dhiki” wakati Mungu alipodhihirisha ghadhabu yake dhidi ya Yuda na Yerusalemu. Wavamizi wa Babiloni walisababisha mateso mengi kwa wakazi wa Yuda, pamoja na maumivu makali ya akili, wakati walipokabili kifo na uharibifu. “Siku hiyo ya uharibifu na ukiwa” ilikuwa siku ya giza, mawingu, na utusitusi, huenda si katika njia ya ufananisho tu bali pia kihalisi kwa kuwa moshi na mauaji yalikuwa kila mahali. Ilikuwa “siku ya tarumbeta na ya kamsa,” lakini maonyo yalitolewa bure.

20 Walinzi wa Yerusalemu walikuwa hoi wakati magogo ya Babiloni yalipovunja “buruji zilizo ndefu sana.” Ngome za mfumo huu mwovu wa mambo zitakuwa bure dhidi ya silaha za vita alizo nazo Mungu mbinguni, ambazo ziko tayari kutumiwa naye hivi karibuni anapoharibu watu waovu. Je, unatumaini kuhifadhiwa? Je, umechukua msimamo imara upande wa Yehova, ‘ambaye huwahifadhi wote wampendao, na kuwaangamiza wote wasio haki’?—Zaburi 145:20.

21, 22. Andiko la Sefania 1:17, 18 litatimizwaje wakati wetu?

21 Siku ya hukumu inayotabiriwa katika Sefania 1:17, 18, ni siku yenye kuogofya kama nini! “Nami nitawaletea wanadamu dhiki,” asema Yehova Mungu, “hata watakwenda kama vipofu, kwa sababu wamemtenda BWANA dhambi; na damu yao itamwagwa kama mavumbi, na nyama yao kama nami [“mavi,” Biblia Habari Njema]. Fedha yao wala dhahabu yao havitaweza kuwaokoa katika siku ile ya ghadhabu ya BWANA; bali nchi yote pia itateketezwa kwa moto wa wivu wake; maana atawakomesha watu wote wakaao katika nchi hii, naam, ukomo wa kutisha.”

22 Kama alivyofanya wakati wa Sefania, hivi karibuni Yehova atasononesha “watu wote wakaao katika nchi hii,” wale wanaokataa kutii onyo lake leo. Kwa sababu wanatenda dhambi dhidi ya Mungu, watakwenda wakipapasa-papasa kama vipofu, wasiweze kupata ukombozi. Katika siku ya hukumu ya Yehova, damu yao “itamwagwa kama mavumbi,” kama kitu kisichofaa. Mwisho wao utakuwa wenye kufedhehesha kwelikweli, kwa kuwa Mungu atatawanya miili pamoja na viungo vya ndani vya waovu hao juu ya dunia, “kama mavi.”

23. Ingawa wakosaji hawataponyoka “katika siku ya hasira ya BWANA,” unabii wa Sefania watutolea tumaini gani?

23 Hakuna awezaye kuwaokoa wale wanaopiga vita dhidi ya Mungu na watu wake. Fedha wala dhahabu hazikuwaokoa wakosaji wa Yuda, kama vile mali nyingi na hongo hazitalinda wala kuponyosha Jumuiya ya Wakristo na mfumo huu wa mambo katika ‘siku ya ghadhabu ya Yehova.’ Katika siku hiyo ya kukata maneno, ‘dunia yote itateketezwa’ kwa moto wa wivu wa Mungu akomeshapo waovu. Kwa kuwa tuna imani katika neno la Mungu la unabii, tuna hakika kwamba sasa tumo katika kipindi cha mwisho kabisa cha “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Siku ya hukumu ya Yehova i karibu, na hivi karibuni atalipiza kisasi dhidi ya maadui wake. Hata hivyo, unabii wa Sefania watoa tumaini la ukombozi. Hivyo basi, twatakiwa kufanya nini ili tufichwe katika siku ya hasira ya Yehova?

Ungejibuje?

• Unabii wa Sefania ulitimizwaje juu ya Yuda na Yerusalemu?

• Jumuiya ya Wakristo na waovu wote leo watapatwa na nini?

• Kwa nini hatupaswi kudhani kwamba siku ya hukumu ya Yehova iko mbali sana?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Sefania alitangaza kwa ujasiri kwamba siku ya hukumu ya Yehova ilikuwa karibu

[Hisani]

From the Self-Pronouncing Edition of the Holy Bible, containing the King James and the Revised versions

[Picha katika ukurasa wa 15]

Siku ya Yehova ilikuja dhidi ya Yuda na Yerusalemu kupitia Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Je, unatumaini kuhifadhiwa wakati Yehova aharibupo waovu?