Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu wa Yehova Waliorudishwa Wamsifu Duniani Pote

Watu wa Yehova Waliorudishwa Wamsifu Duniani Pote

Watu wa Yehova Waliorudishwa Wamsifu Duniani Pote

‘Nitawapa mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la Yehova.’—SEFANIA 3:9.

1. Kwa nini ujumbe mbalimbali wa maangamizi ulitimizwa dhidi ya Yuda na mataifa mengine?

YEHOVA alimpulizia Sefania atoe ujumbe mbalimbali wa hukumu na wenye nguvu kama nini! Ujumbe huo wa maangamizi ulitimizwa dhidi ya Yuda na jiji lake kuu, Yerusalemu, kwa sababu viongozi na watu kwa ujumla hawakuwa wakifanya mapenzi ya Yehova. Mataifa jirani pia, kama vile Ufilisti, Moabu, na Amoni, yangepatwa na hasira ya kisasi ya Mungu. Kwa nini? Kwa sababu yamewapinga watu wa Yehova kwa ukatili kwa karne nyingi. Serikali ya ulimwengu ya Ashuru ingeharibiwa kwa sababu hiyohiyo, isiweze kusimama tena.

2. Yaonekana andiko la Sefania 3:8 lawahusu nani?

2 Hata hivyo, kulikuwa na watu fulani wenye mwelekeo mzuri katika Yuda ya kale. Walitazamia kwa hamu kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu dhidi ya waovu na yaonekana kwamba maneno haya yanawahusu: “Ningojeni, asema BWANA, hata siku ile nitakapoondoka kuteka mateka; maana nimeazimia kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu; kwa maana dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu.”—Sefania 3:8.

“Lugha Iliyo Safi” kwa Ajili ya Nani?

3. Sefania alipuliziwa kutoa ujumbe gani wa tumaini?

3 Naam, Sefania alitangaza ujumbe mbalimbali wa maangamizi wa Yehova. Lakini nabii huyo alipuliziwa pia kuandika ujumbe mzuri ajabu wa tumaini—ujumbe ambao ungewafariji sana watu ambao wangedumu wakiwa waaminifu kwa Yehova. Kwenye Sefania 3:9, Yehova Mungu alitangaza hivi: “Ndipo nitakapowarudishia [“nitakapowapa,” NW] mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la BWANA, wamtumikie kwa nia moja.”

4, 5. (a) Ni nini ambacho kingewapata watu wasio waadilifu? (b) Ni nani ambao wangenufaika na jambo hilo, na kwa nini?

4 Kungekuwa na watu ambao hawangepewa lugha safi. Unabii huo unawataja, ukisema hivi: “Nitawaondoa watu wako wanaotakabari na kujivuna, wasiwe kati yako.” (Sefania 3:11) Kwa hiyo wenye kujivuna, waliodharau sheria za Mungu na ambao walitenda mambo yasiyo ya uadilifu, wangeondolewa. Na ni nani wangenufaishwa na jambo hilo? Andiko la Sefania 3:12, 13 lasema: “Lakini [mimi Yehova] nitasaza ndani yako watu walioonewa na maskini, nao watalitumainia jina la BWANA. Mabaki ya Israeli hawatatenda uovu, wala kusema uongo; wala ulimi wa hadaa hautaonekana kinywani mwao; kwa maana watakula na kulala, wala hapana mtu atakayewaogofya.”

5 Mabaki waaminifu wa Israeli la kale ndio wangenufaika. Kwa nini? Kwa sababu walitenda kupatana na maneno haya: “Mtafuteni BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.”—Sefania 2:3.

6. Ni nini kilichotukia wakati wa utimizo wa kwanza wa unabii wa Sefania?

6 Katika utimizo wa kwanza wa unabii wa Sefania, Mungu aliadhibu Yuda isiyo na imani kwa kuruhusu Serikali ya Ulimwengu ya Babiloni kuishinda na kuteka watu wake mwaka wa 607 K.W.K. Baadhi ya watu, kutia ndani nabii Yeremia, walihifadhiwa na wengine waliendelea kuwa waaminifu kwa Yehova wakiwa mateka. Mnamo mwaka wa 539 K.W.K., milki ya Babiloni ilipinduliwa na Wamedi na Waajemi wakiwa chini ya Mfalme Koreshi. Miaka miwili hivi baadaye, Koreshi alitoa amri iliyowawezesha mabaki Wayahudi warudi nyumbani kwao. Baadaye, hekalu la Yerusalemu likajengwa upya, nao makuhani wakapata uwezo tena wa kuwafundisha watu Sheria. (Malaki 2:7) Kwa hiyo Yehova aliwafanikisha mabaki waliorudishwa—maadamu walidumu wakiwa waaminifu.

7, 8. Maneno ya unabii wa Sefania 3:14-17 yaliwahusu nani, na kwa nini wajibu hivyo?

7 Sefania alitabiri hivi juu ya watu ambao wangefurahia kurudishwa huko: “Imba, Ee binti Sayuni; piga kelele, Ee Israeli; furahi na kushangilia kwa moyo wako wote, Ee binti Yerusalemu. BWANA ameziondoa hukumu zako, amemtupa nje adui yako; mfalme wa Israeli, naam, yeye BWANA, yu katikati yako; hutaogopa uovu tena. Katika siku ile Yerusalemu utaambiwa, usiogope, Ee Sayuni; mikono yako isilegee. BWANA, Mungu wako, yu katikati yako shujaa awezaye kuokoa; atakushangilia kwa furaha kuu, atakutuliza katika upendo wake, atakufurahia kwa kuimba.”—Sefania 3:14-17.

8 Maneno hayo ya unabii yaliwahusu mabaki waliokusanywa kutoka utekwa wa Babiloni na kurudishwa nchi ya babu zao. Jambo hilo ladhihirishwa kwenye andiko la Sefania 3:18-20, ambapo twasoma: “[Mimi Yehova] nitawakusanya wanaousikitikia mkutano wa ibada, hao waliokuwa wa kwako; ambao mzigo uliokuwa juu yake ulikuwa fedheha kwao. Tazama, wakati huo nitawapatiliza watu wote wanaokutesa; nami nitamponya yeye achechemeaye, nami nitamkusanya yeye aliyefukuzwa; nami nitawafanya kuwa sifa na jina, hao ambao fedheha yao ilikuwa katika dunia yote. Wakati huo nitawaingizeni, na wakati huo nitawakusanya; kwa maana nitawafanya ninyi kuwa sifa na jina, miongoni mwa watu wote wa dunia, nitakapowarudisha wafungwa wenu mbele ya macho yenu, asema BWANA.”

9. Yehova alijileteaje sifa kuhusiana na Yuda?

9 Hebu wazia jinsi mataifa jirani waliokuwa adui za watu wa Mungu walivyoshtuka! Wakazi wa Yuda walikuwa wametekwa na Babiloni yenye nguvu, pasipo tumaini lolote la kuachiliwa huru. Isitoshe, nchi yao ilikuwa ukiwa. Lakini, Mungu alitumia nguvu zake kuwarudisha nyumbani kwao baada ya miaka 70, nayo mataifa adui yalikuwa yakikaribia kuangamizwa. Yehova alijiletea sifa iliyoje kwa kuwarudisha mabaki hao waaminifu! Aliwafanya “kuwa sifa na jina, miongoni mwa watu wote wa dunia.” Kurudishwa huko kulileta sifa iliyoje kwa Yehova na kwa wale wanaoitwa kwa jina lake!

Ibada ya Yehova Yakwezwa

10, 11. Unabii wa Sefania wa kurudishwa ungetimizwa lini kwa njia kubwa, nasi twajuaje hilo?

10 Kurudishwa kwingine kulitukia katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida, wakati ambapo Yesu Kristo alikusanya mabaki ya Israeli waingie katika ibada ya kweli. Kurudishwa huko kuliashiria mambo ambayo bado yangekuja, kwa kuwa utimizo mkubwa zaidi wa kurudishwa ungetukia wakati ujao. Unabii wa Mika ulitabiri hivi: “Lakini itakuwa katika siku za mwisho, ya kwamba mlima wa nyumba ya BWANA [“Yehova,” NW] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na watu wa mataifa watauendea makundi makundi.”—Mika 4:1.

11 Hilo lingetukia lini? Kama unabii ulivyosema, jambo hilo lingetukia katika “siku za mwisho”—naam wakati wa ‘siku hizi za mwisho.’ (2 Timotheo 3:1) Hilo lingetukia kabla ya mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo wakati ambapo mataifa bado yangekuwa yakiabudu miungu isiyo ya kweli. Andiko la Mika 4:5 lasema hivi: “Mataifa yote watakwenda, kila moja kwa jina la mungu wake.” Na vipi waabudu wa kweli? Unabii wa Mika wajibu: “Na sisi tutakwenda kwa jina la BWANA [“Yehova,” NW], Mungu wetu, milele na milele.”

12. Ibada ya kweli imekwezwaje katika siku hizi za mwisho?

12 Kwa hiyo, katika siku hizi za mwisho, “mlima wa nyumba ya Yehova u[me]wekwa imara juu ya vilima.” Ibada ya kweli ya Yehova iliyoinuka sana imerudishwa, ikafanywa imara, na kukwezwa juu ya aina nyingine zote za dini. Kama unabii wa Mika ulivyotabiri tena, “watu wa mataifa watauendea makundi makundi.” Na wale wanaofuata dini ya kweli ‘watakwenda kwa jina la Yehova, Mungu [wao], milele na milele.’

13, 14. “Siku za mwisho” za ulimwengu huu zilianza lini, na tangu wakati huo ni nini ambacho kimekuwa kikiendelea kuhusiana na ibada ya kweli?

13 Matukio yanayotimiza unabii wa Biblia yathibitisha kwamba “siku za mwisho” za ulimwengu huu zilianza mwaka wa 1914. (Marko 13:4-10) Historia yaonyesha kwamba Yehova alianza kukusanya tena mabaki waaminifu wa watiwa-mafuta waliokuwa na tumaini la kimbingu, waingie katika ibada ya kweli. Halafu, “umati mkubwa . . . kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha”—watu walio na tumaini la kuishi milele duniani umekuwa ukikusanywa.—Ufunuo 7:9.

14 Tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza hadi leo, ibada ya Yehova inayotolewa na wale wanaoitwa kwa jina lake, imesonga mbele sana chini ya mwelekezo wake. Tangu baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza hadi sasa, idadi ya waabudu wa Yehova imeongezeka tokea maelfu machache ya watu na kufikia karibu watu milioni sita, wanaokusanywa katika makutaniko yapatayo 91,000 katika nchi 235. Kila mwaka, watangazaji hawa wa Ufalme hutumia muda wa zaidi ya saa bilioni moja wakimsifu Mungu hadharani. Ni wazi kwamba Mashahidi hao wa Yehova ndio wanaotimiza maneno ya Yesu ya unabii: “Na habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

15. Andiko la Sefania 2:3 linatimizwaje leo?

15 Andiko la Sefania 3:17 lasema: “BWANA, Mungu wako, yu katikati yako shujaa awezaye kuokoa.” Ufanisi wa kiroho ambao watu wa Yehova wanafurahia katika siku hizi za mwisho unatokana moja kwa moja na kuwa naye ‘katikati yao’ akiwa Mungu wao mwenye nguvu zote. Kama ilivyokuwa wakati watu wa Yuda ya kale waliporudishwa nyumbani kwao mwaka wa 537 K.W.K., ndivyo ilivyo leo. Hivyo tunaweza kuona jinsi andiko la Sefania 3:17 linavyotimizwa kwa njia kubwa wakati wetu linaposema: ‘Mtafuteni BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia.’ Mwaka wa 537 K.W.K., neno “nyote” lilirejezea mabaki ya Wayahudi waliorudi kutoka utekwa wa Babiloni. Leo neno hilo larejezea wanyenyekevu wa mataifa yote duniani pote, wale ambao huitikia vizuri kuhubiriwa kwa Ufalme ulimwenguni pote na ambao huuendea ‘mlima wa nyumba ya Yehova makundi makundi.’

Ibada ya Kweli Yasitawi

16. Yaelekea maadui wetu wanahisije kuhusiana na ufanisi wa watumishi wa Yehova siku hizi?

16 Baada ya mwaka wa 537 K.W.K., watu wengi katika mataifa jirani walishangazwa na kurudishwa kwa watumishi wa Mungu katika ibada ya kweli nyumbani kwao. Hata hivyo, kurudishwa huko kulikuwa kwa kiwango kidogo tu. Je, waweza kuwazia jambo ambalo watu fulani—hata adui za watu wa Mungu—wanasema sasa waonapo ukuzi, ufanisi, na maendeleo ya ajabu ya watumishi wa Yehova leo? Yaelekea sana kwamba baadhi ya maadui hao huhisi kama vile Mafarisayo walivyohisi walipoona jinsi watu walivyokusanyika alipokuwa Yesu. Walisema hivi kwa mshangao: “Oneni! Ulimwengu umemfuata.”—Yohana 12:19.

17. Mwandishi mmoja alisema nini kuhusu Mashahidi wa Yehova, nao wameona ukuzi gani?

17 Katika kitabu chake These Also Believe, Profesa Charles S. Braden alisema hivi: ‘Mashahidi wa Yehova wametoa ushahidi karibu duniani pote. Yaweza kusemwa kikweli kwamba hakuna dini nyingine ulimwenguni ambayo imeonyesha bidii na kudumu katika kujaribu kueneza habari njema ya Ufalme kuliko Mashahidi wa Yehova. Yaonekana dini hiyo itazidi kuwa na nguvu.’ Hakukosea hata kidogo! Alipoandika maneno hayo miaka 50 iliyopita, kulikuwako Mashahidi 300,000 hivi waliokuwa wakihubiri ulimwenguni. Angesema nini leo, wakati ambapo idadi ya wanaohubiri habari njema imeongezeka karibu mara 20—kufikia milioni sita hivi?

18. Lugha safi ni nini, naye Mungu amewapa nani lugha hiyo?

18 Kupitia nabii wake, Mungu aliahidi: ‘Nitawapa mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la Yehova, wamtumikie kwa nia moja.’ (Sefania 3:9) Katika siku hizi za mwisho, Mashahidi wa Yehova ndio wanaoliitia jina la Yehova, ndio wanaomtumikia kwa umoja katika kifungo kisichoweza kuvunjika cha upendo—naam, ndio wanaomtumikia “kwa nia moja.” Hao ndio watu ambao Yehova amewapa lugha safi. Lugha hiyo safi hutia ndani kumwelewa kikweli Mungu na makusudi yake. Yehova tu ndiye humpa mtu uelewevu huo kupitia roho yake takatifu. (1 Wakorintho 2:10) Yehova amewapa nani roho yake? ‘Wale tu wanaomtii yeye akiwa mtawala.’ (Matendo 5:32) Mashahidi wa Yehova peke yao ndio wana nia ya kumtii Mungu akiwa Mtawala wa vitu vyote. Ndiyo sababu wao hupokea roho takatifu ya Mungu na kuzungumza lugha safi, ile kweli juu ya Yehova na makusudi yake ya ajabu. Wao hutumia lugha hiyo safi ili kumsifu Yehova ulimwenguni pote kwa kiwango kikubwa kinachozidi kuongezeka.

19. Kuzungumza lugha safi humaanisha nini?

19 Kuizungumza lugha safi kwamaanisha kuamini kweli na kuifundisha wengine na pia kupatanisha mwenendo wako na sheria na kanuni za Mungu. Wakristo watiwa-mafuta wamekuwa mstari wa mbele katika kumtafuta Yehova na kuinena lugha safi. Hebu wazia mambo ambayo yametimizwa! Ingawa idadi ya watiwa-mafuta haifiki 8,700, karibu watu wengine milioni sita, wenye tumaini la kidunia, wanaiga imani yao kwa kumtafuta Yehova na kusema lugha safi. Hao ndio umati mkubwa unaozidi kuongezeka kutoka katika mataifa yote ambao hudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu na kutoa utumishi mtakatifu katika ua wa kidunia wa hekalu la kiroho la Mungu, nao wataokoka “dhiki kubwa” ambayo hivi punde itaupata ulimwengu huu usio na uadilifu.—Ufunuo 7:9, 14, 15.

20. Watiwa-mafuta waaminifu na wale wa umati mkubwa wanatazamia mambo gani?

20 Umati mkubwa utaingizwa katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu. (2 Petro 3:13) Yesu Kristo na wale watiwa-mafuta 144,000, ambao wanafufuliwa kuishi mbinguni ili watumikie wakiwa wafalme na makuhani pamoja naye, ndio watawala wapya wa dunia. (Waroma 8:16, 17; Ufunuo 7:4; 20:6) Waokokaji wa dhiki kubwa watafanya kazi ya kuifanya dunia iwe paradiso na wataendelea kuzungumza lugha safi waliyopewa na Mungu. Kimsingi, maneno haya yanawahusu: “Watoto wako wote watafundishwa na BWANA; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi. Utathibitika katika haki.”—Isaya 54:13, 14.

Kazi Kubwa Zaidi ya Kufundisha Katika Historia

21, 22. (a) Kama ionyeshwavyo na andiko la Matendo 24:15, ni nani watakaohitaji kufundishwa lugha safi? (b) Ni kazi gani ya kufundisha isiyo na kifani ambayo itafanywa duniani chini ya utawala wa Ufalme?

21 Kikundi kikubwa sana cha watu ambao watapewa fursa ya kujifunza lugha safi katika ulimwengu mpya ni wale wanaotajwa kwenye andiko la Matendo 24:15, lisemalo: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Wakati uliopita, mabilioni ya watu wameishi na kufa kabla ya kupata ujuzi sahihi juu ya Yehova. Atawafufua kwa utaratibu fulani. Nao waliofufuliwa watahitaji kufundishwa ile lugha safi.

22 Litakuwa pendeleo lililoje kushiriki katika kazi hiyo kubwa ya kufundisha! Hiyo ndiyo itakayokuwa kazi kubwa zaidi ya kufundisha katika historia ya wanadamu. Yote itatimizwa chini ya utawala mwema wa Kristo Yesu akiwa na mamlaka ya Ufalme. Hatimaye wanadamu wataona utimizo wa andiko la Isaya 11:9, lisemalo hivi: “Dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”

23. Kwa nini unaweza kusema kwamba sisi tuna pendeleo kubwa sana tukiwa watu wa Yehova?

23 Tuna pendeleo lililoje siku hizi za mwisho la kufanya matayarisho kwa ajili ya wakati huo mzuri ajabu ambapo kwa kweli ujuzi juu ya Yehova utaijaza dunia! Na tuna pendeleo lililoje sasa hivi la kuwa watu wa Mungu ambao wanaona utimizo wa maneno ya unabii yaliyo kwenye Sefania 3:20! Hapo twaona uhakikisho wa Yehova: “Nitawafanya ninyi kuwa sifa na jina, miongoni mwa watu wote wa dunia.”

Ungejibuje?

• Unabii wa Sefania wa kurudishwa umepata utimizo gani mbalimbali?

• Ibada ya kweli imeendeleaje kusitawi katika siku hizi za mwisho?

• Ni kazi gani kubwa ya kufundisha itakayofanywa katika ulimwengu mpya?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 25]

Watu wa Yehova walirudi nyumbani kwao ili kurudisha ibada safi. Je, unajua maana ya jambo hili leo?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kwa kuzungumza “lugha safi,” Mashahidi wa Yehova huwatolea watu ujumbe wa Biblia wenye kufariji