Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kupata Furaha ya Kweli

Jinsi ya Kupata Furaha ya Kweli

Jinsi ya Kupata Furaha ya Kweli

KIONGOZI mmoja wa dini ya Buddha aitwaye Dalai Lama alisema hivi: “Ninaamini kwamba kusudi hasa la maisha yetu ni kutafuta furaha.” Kisha akaeleza kwamba anaamini kuwa furaha yaweza kupatikana kwa kuzoeza, au kutia nidhamu akili na moyo. Alisema, “akili ni kifaa cha msingi tunachohitaji ili kupata furaha kamili.” Si lazima kuamini Mungu, yeye asisitiza. *

Kinyume cha hilo, mfikirie Yesu, aliyekuwa na imani yenye nguvu katika Mungu na ambaye mafundisho yake yameathiri mamilioni ya watu katika karne zilizopita. Yesu alitaka wanadamu wawe na furaha. Alianza Mahubiri yake maarufu ya Mlimani kwa kutaja furaha mara tisa—semi tisa zinazoanza: “Wenye furaha ni . . .” (Mathayo 5:1-12) Katika mahubiri hayohayo, aliwafundisha wasikilizaji wake kuchunguza, kutakasa na kudhibiti akili na mioyo yao na kufikiria mambo ya amani, safi, na yenye upendo badala ya mambo ya jeuri, yasiyo ya adili, na ya ubinafsi. (Mathayo 5:21, 22, 27, 28; 6:19-21) Kama mwanafunzi wake mmoja alivyohimiza baadaye, twapaswa ‘kuendelea kufikiria’ mambo yaliyo ya ‘kweli, ya hangaikio zito, ya uadilifu, safi kiadili, ya kupendeka, ya kusemwa vema, ya wema wa adili, na ya kustahili sifa.’—Wafilipi 4:8.

Yesu alijua kwamba furaha ya kweli hutia ndani kuwa na uhusiano na wengine. Kiasili sisi wanadamu hupenda kushirikiana na wengine, hivyo hatuwezi kuwa wenye furaha kwelikweli tukijitenga na wengine au tukizozana daima na wale walio karibu nasi. Tunaweza kuwa wenye furaha tu ikiwa tunahisi tunapendwa na ikiwa tunapenda wengine. Yesu alifundisha kwamba ni muhimu kuwa na uhusiano na Mungu ili kuwa na upendo huo. Kuhusu hilo hasa, mafundisho ya Yesu yanatofautiana na yale ya Dalai Lama, kwa kuwa Yesu alifundisha kwamba wanadamu hawawezi kuwa wenye furaha wasipokuwa na uhusiano na Mungu. Kwa nini iwe hivyo?—Mathayo 4:4; 22:37-39.

Fikiria Mahitaji Yako ya Kiroho

Mojawapo ya zile furaha alizotaja husema: “Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Kwa nini Yesu alisema hivyo? Kwa sababu, tofauti na wanyama, sisi tuna mahitaji ya kiroho. Kwa kuwa tuliumbwa katika mfano wa Mungu, tunaweza kwa kadiri fulani kusitawisha sifa za kimungu, kama vile upendo, haki, rehema, na hekima. (Mwanzo 1:27; Mika 6:8; 1 Yohana 4:8) Mahitaji yetu ya kiroho yanatia ndani uhitaji wa kuishi maisha yenye kusudi.

Tunaweza kutoshelezaje mahitaji hayo ya kiroho? Si kupitia kutafakari sana kupita kiasi au kujichunguza kibinafsi tu. Badala yake, Yesu alisema: “Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4) Ona kwamba Yesu alisema kuwa Mungu ndiye chanzo cha “kila tamko” ambalo ni muhimu kwa maisha yetu. Mungu tu ndiye awezaye kutusaidia kujibu maswali fulani. Ufahamu huo hasa ni wa wakati ufaao leo, kwa sababu ya kuenea kwa nadharia nyingi kuhusu kusudi la maisha na njia ya kupata furaha. Maduka ya vitabu hutenga sehemu nzima kwa ajili ya vitabu vinavyowatolea wasomaji matumaini ya kuwa na afya, mali, na furaha. Vituo vya Internet ambavyo kihususa huonyesha jinsi ya kupata furaha vimeanzishwa.

Hata hivyo, mara nyingi mawazo ya mwanadamu kuhusu hali hizo yamepotoka. Hayo huelekea kumfanya awe na tamaa za ubinafsi au majisifu. Mawazo hayo hutegemea ujuzi na uzoefu kidogo, na mara nyingi hutegemea dhana zisizo za kweli. Kwa mfano, waandishi wa vitabu vya kujisaidia kibinafsi wana mwelekeo unaozidi kuimarika wa kutegemeza maoni yao juu ya nadharia ya “saikolojia ya kimageuzi,” inayosema kwamba hisia za kibinadamu zinatokana na chanzo chetu ambacho hudhaniwa ni wanyama. Ukweli ni kwamba, jitihada yoyote ya kutafuta furaha inayotegemea nadharia fulani ambayo hupuuza jukumu la Muumba wetu haiwezi kuwa halali nayo hatimaye itasababisha kukata tamaa. Nabii mmoja wa kale alisema: “Wenye hekima wametahayari . . . tazama, wamelikataa neno la BWANA, wana akili gani ndani yao?”—Yeremia 8:9.

Yehova Mungu anajua maumbile yetu na kile kitakachotufanya tuwe wenye furaha kwelikweli. Anajua ni kwa nini alimweka mwanadamu duniani na anajua mambo ya wakati ujao, naye hutujulisha habari hizo katika Biblia. Anayofunua katika kitabu hicho kilichopuliziwa hufanya wale wenye mwelekeo ufaao waitikie ifaavyo na kuwachochea wawe wenye furaha. (Luka 10:21; Yohana 8:32) Ilitukia hivyo kwa wanafunzi wawili wa Yesu. Walikuwa na majonzi baada ya kifo chake. Lakini baada ya kujifunza moja kwa moja kutoka kwa Yesu, ambaye alikuwa amefufuliwa, kuhusu jukumu lake katika kusudi la Mungu kwa ajili ya wokovu wa wanadamu, walisema: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akisema nasi barabarani, alipokuwa akitufungulia kabisa yale Maandiko?”—Luka 24:32.

Furaha hiyo huongezeka sana tunaporuhusu kweli ya Biblia ituongoze maishani. Kwa habari hiyo, furaha yaweza kulinganishwa na upinde wa mvua. Huo hutokea hali zinapokuwa nzuri, lakini hung’aa zaidi—hata kutokeza pinde mbili—hali zinapokuwa nzuri kabisa. Acheni sasa tuchunguze mifano kadhaa kuhusu jinsi kutumia mafundisho ya Biblia kuwezavyo kuzidisha furaha yetu.

Ishi Maisha Sahili

Kwanza, tazama ushauri wa Yesu kuhusu mali. Baada ya kushauri dhidi ya kutanguliza utafutaji wa mali maishani, alisema maneno yenye kutokeza. Alisema: “Basi, ikiwa jicho lako ni sahili, mwili wako wote utakuwa mwangavu.” (Mathayo 6:19-22) Kimsingi, alisema kwamba tukifuatia kwa bidii mali, uwezo, au miradi mingine yoyote ambayo watu hujiwekea, tutakosa mambo muhimu zaidi. Kwa sababu, kama Yesu alivyosema pindi nyingine, “hata wakati mtu ana wingi uhai wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Tukitanguliza mambo ambayo kwa kweli ni muhimu, kama vile uhusiano wetu na Mungu, mambo yanayohusu familia, na mambo mengine kama hayo, basi “jicho” letu litakuwa “sahili,” lenye kuona vizuri.

Ona kwamba Yesu hakuwa anaunga mkono maisha ya kujinyima raha kupita kiasi. Hata Yesu mwenyewe hakujinyima raha kupita kiasi. (Mathayo 11:19; Yohana 2:1-11) Badala yake, alifundisha kwamba wale ambao huona maisha kuwa fursa tu ya kurundika mali kwa kweli hawayafurahii.

Akieleza juu ya watu fulani ambao walipata kuwa matajiri sana mapema maishani, tabibu mmoja wa kisaikolojia huko San Francisco, Marekani, alisema kwamba watu hao huona pesa kuwa “chanzo cha mikazo na mivurugo.” Aliongezea kusema kwamba watu hao “hununua nyumba mbili au tatu, gari, na kutumia pesa kununua vitu. Na wasipopata furaha kwa kufanya hivyo, wao hupatwa na mshuko-moyo, hisia za kutoridhika, wasijue wafanye nini na maisha yao.” Kinyume cha hilo, yaelekea sana kwamba wale wanaofuata ushauri wa Yesu wa kuishi maisha sahili kuhusiana na vitu vya kimwili na kuwa na wakati kwa ajili ya mambo ya kiroho hupata furaha ya kweli.

Tom, ambaye ni mjenzi anayeishi Hawaii, alijitolea kusaidia kujenga majengo ya ibada kwenye visiwa vya Pasifiki ambako watu ni maskini. Tom alitambua jambo fulani kuhusiana na watu hao wa hali ya chini. Alisema hivi: “Ndugu na dada zangu Wakristo kwenye visiwa hivi walikuwa wenye furaha kikweli. Walinisaidia kuelewa vizuri zaidi kwamba pesa na mali siyo siri ya kupata furaha.” Alitazama pia wajitoleaji waliofanya kazi pamoja naye kwenye visiwa hivyo na kuona jinsi walivyokuwa wameridhika. “Wangeweza kuchuma pesa nyingi,” Tom akasema. “Lakini walichagua kutanguliza mambo ya kiroho na kuishi maisha sahili.” Kwa kuchochewa na mifano hiyo, Tom alisahilisha maisha yake ili aweze kutumia wakati mwingi zaidi pamoja na familia yake na katika mambo ya kiroho—na hajajuta kamwe kwa kufanya hivyo.

Furaha na Kujistahi

Ili kuwa mwenye furaha ni muhimu kujiheshimu, au kujistahi. Kwa sababu ya hali ya kutokamilika ya mwanadamu na udhaifu unaosababishwa na hali hiyo, wengine wana maoni yasiyofaa kujihusu, na wengi wamekuwa nayo tangu utotoni. Huenda ikawa vigumu kushinda hisia ambazo zimetia mizizi ndani yetu, lakini inawezekana. Suluhisho ni kutumia Neno la Mungu.

Biblia hueleza jinsi Muumba ahisivyo kutuhusu. Je, maoni yake si muhimu zaidi kuliko ya mwanadamu yeyote yule—hata yetu wenyewe? Mungu ni mfano halisi wa sifa ya upendo naye hututazama bila ubaguzi au nia mbaya. Yeye hutuona jinsi tulivyo, na vilevile jinsi tunavyoweza kuwa. (1 Samweli 16:7; 1 Yohana 4:8) Kwa kweli, yeye huona wale wanaotaka kumpendeza kuwa wenye thamani, naam, wenye kutamanika, hata wawe na kasoro gani.—Danieli 9:23; Hagai 2:7.

Bila shaka, Mungu huona udhaifu wetu na dhambi zozote tufanyazo. Yeye hutarajia tujitahidi sana kufanya yaliyo sawa, naye hututegemeza tunapofanya hivyo. (Luka 13:24) Hata hivyo, Biblia husema: “Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, ndivyo BWANA anavyowahurumia wamchao.” Pia Biblia husema: “BWANA, kama wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna msamaha ili wewe uogopwe.”—Zaburi 103:13; 130:3, 4.

Kwa hiyo jifunze kujiona jinsi Mungu akuonavyo. Kujua kwamba yeye huwaona wale wampendao kuwa watu wenye kutamanika na kwamba ana uhakika nao—hata ingawa huenda wakajiona kuwa hawafai—kwaweza kuzidisha sana furaha ya mtu.—1 Yohana 3:19, 20.

Tumaini Ni Muhimu Ili Kupata Furaha

Dhana ya kisasa inayopendwa sana inayoitwa saikolojia ya kuwa na uhakika kamili yasema kwamba kutarajia mema, kunakositawishwa kwa kufikiria mambo yafaayo na kwa kuzingatia uwezo wa mtu binafsi, kunaweza kutokeza furaha. Ni watu wachache ambao wangekanusha kwamba kutarajia mema kuhusu maisha na wakati ujao huzidisha furaha yetu. Hata hivyo, kutarajia mema huko kwapasa kutegemee mambo ya hakika, si ndoto tu. Isitoshe, kutarajia mema au kufikiria mambo yafaayo hakuwezi kuondoa vita, kufa njaa, maradhi, uchafuzi, uzee, ugonjwa, au kifo—mambo ambayo huwakosesha wengi furaha. Hata hivyo, kutarajia mema kuna umuhimu wake.

Kwa kutokeza, Biblia haitumii maneno kutarajia mema; hutumia neno lenye nguvu zaidi—tumaini. Kamusi Vine’s Complete Expository Dictionary hufafanua neno “tumaini” kama linavyotumiwa na Biblia kuwa “matarajio yafaayo na hakika, . . . kutazamia mema kwa furaha.” Kama litumiwavyo katika Biblia, neno tumaini lina maana zaidi kuliko tu kuwa na matarajio mema kuhusu hali fulani. Neno hilo pia larejezea jambo ambalo mtu anaweka tumaini lake. (Waefeso 4:4; 1 Petro 1:3) Kwa mfano, tumaini la Kikristo ni kwamba mambo yasiyotamanika ambayo yametajwa katika fungu lililotangulia yataondolewa kabisa hivi karibuni. (Zaburi 37:9-11, 29) Lakini neno hilo lamaanisha mengi zaidi.

Wakristo hutazamia wakati ambapo wanadamu waaminifu watafikia uhai mkamilifu kwenye dunia paradiso. (Luka 23:42, 43) Andiko la Ufunuo 21:3, 4 lasema hivi likifafanua zaidi tumaini hilo: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa vikundi vya watu wake. . . . Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”

Yeyote anayetarajia kuwa na tumaini kama hilo ana sababu nzuri za kuwa mwenye furaha, hata ingawa hali zake za sasa haziridhishi kabisa. (Yakobo 1:12) Kwa hiyo mbona usichunguze Biblia na kujua ni kwa nini unaweza kuiamini. Imarisha tumaini lako kwa kusoma Biblia kila siku. Kufanya hivyo kutaboresha hali yako ya kiroho, kutakusaidia uepuke mambo ambayo huwakosesha watu furaha, na kuzidisha uradhi wako. Naam, siri kuu ya kupata furaha ya kweli ni kufanya mapenzi ya Mungu. (Mhubiri 12:13) Maisha yanayotegemea kutii kanuni za Biblia ni yenye furaha, kwa kuwa Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”—Luka 11:28.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Kuamini Mungu si jambo la lazima kwa Mbuddha.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Furaha haiwezi kupatikana kwa kurundika mali, kujitenga na wengine, au kwa kutumaini ujuzi kidogo wa mwanadamu

[Picha katika ukurasa wa 6]

Maisha yenye furaha ni yale yanayotegemea kutii Neno la Mungu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Tumaini la Kikristo hufanya mtu awe na furaha