Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nimetegemezwa na Yehova Maisha yangu Yote

Nimetegemezwa na Yehova Maisha yangu Yote

Simulizi la Maisha

Nimetegemezwa na Yehova Maisha yangu Yote

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA FORREST LEE

Polisi walikuwa wametoka kutunyang’anya gramafoni na vichapo vyetu vya Biblia. Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili wapinzani wamshawishi gavana mkuu mpya wa Kanada atangaze utendaji wa Mashahidi wa Yehova kuwa si halali. Hilo lilitokea mnamo Julai 4, 1940.

BILA kuhofu, tulichukua vichapo zaidi kutoka pale vilipokuwa vimewekwa na tukaendelea kuhubiri. Sikuzote nitakumbuka maneno ya Baba wakati huo: “Hatuachi kwa urahisi. Yehova ametuamuru tuhubiri.” Wakati huo, nilikuwa kijana mwenye nguvu mwenye umri wa miaka kumi. Lakini hata leo, azimio la baba na bidii yake katika huduma ingali kikumbusha daima cha jinsi ambavyo Mungu wetu Yehova, hutegemeza waaminifu-washikamanifu wake.

Polisi walipotusimamisha tena, hawakuchukua tu vichapo vyetu bali pia walimfunga Baba jela, wakimwacha Mama peke yake na watoto wanne. Hilo lilitokea mnamo Septemba 1940 huko Saskatchewan. Punde baada ya hapo nilifukuzwa shuleni kwa sababu ya kufuata dhamiri yangu iliyozoezwa na Biblia na kutoisalimu bendera au kuimba wimbo wa taifa. Kuendelea na masomo yangu kwa njia ya posta kulinipa ratiba inayofaa, na nikashiriki kikamili kazi ya kuhubiri.

Katika mwaka wa 1948 mwito ulitolewa kwa mapainia, wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, wahamie sehemu ya pwani ya mashariki ya Kanada. Nikaenda kupainia huko Halifax, Nova Scotia, na Cape Wolfe, Kisiwa cha Prince Edward. Mwaka uliofuata, nilikubali mwaliko wa kufanya kazi kwa majuma mawili katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Toronto. Hayo majuma mawili yakawa miaka sita ya utumishi wenye kuthawabisha. Hatimaye, nilikutana na Myrna, ambaye alikuwa na upendo kwa Yehova kama mimi, na tukaoana mnamo Desemba 1955. Tuliishi Milton, Ontario, na punde si punde kutaniko jipya likaanzishwa hapo. Sehemu ya nyumba yetu iliyo chini ya ardhi ikawa Jumba la Ufalme.

Tamaa ya Kupanua Huduma Yetu

Miaka iliyofuata, tukazaa watoto sita kwa kufuatana sana. Binti yetu Miriam ndiye aliyekuwa wa kwanza. Kisha Charmaine, Mark, Annette, Grant, na hatimaye Glen. Mara nyingi nilirudi nyumbani kutoka kazini na kupata watoto wameketi chini mahali pa kuotea moto, huku Myrna akiwasomea Biblia, akiwasimulia masimulizi ya Biblia na kukaza kikiki katika mioyo yao upendo wa kweli kwa Yehova. Kwa sababu ya tegemezo lake lenye upendo, watoto wetu wote walipata ujuzi wa kutosha kuhusu Biblia walipokuwa na umri mchanga sana.

Bidii ya Baba yangu katika huduma ilidumu katika akili yangu na moyo wangu. (Mithali 22:6) Kwa hiyo, katika mwaka wa 1968, familia za Mashahidi wa Yehova zilipoalikwa kuhamia Amerika ya Kati na ya Kusini ili kusaidia katika kazi ya kuhubiri, familia yetu ilitamani kukubali mwito huo. Wakati huo watoto wetu walikuwa na umri wa kati ya miaka 5 hadi 13, na hakuna mmoja wetu aliyejua hata neno moja la Kihispania. Kwa kufuata mwelekezo uliotolewa, nilisafiri kwenda nchi mbalimbali nikichunguza hali za maisha za huko. Niliporudi, tulisali pamoja na kuchunguza uchaguzi wetu mbalimbali na tukaamua kuhamia Nikaragua.

Kutumikia Huko Nikaragua

Kufikia Oktoba 1970 tulikuwa kwenye makao yetu mapya, na katika juma la tatu nikagawiwa sehemu ndogo kwenye programu ya mkutano wa kutaniko. Niling’ang’ana na sehemu yangu katika Kihispania cha juujuu tu na nikamalizia kwa kualika kutaniko zima nyumbani mwetu kwa ajili ya cerveza siku ya Jumamosi saa 3:30 asubuhi. Nilimaanisha servicio, neno linalomaanisha utumishi wa shambani, kumbe nilikuwa nikialika kila mtu kuja kunywa pombe. Kujifunza lugha kulikuwa na ugumu kwelikweli.

Mwanzoni, niliandika utoaji wa mahubiri mkononi mwangu na kuurudia nilipokuwa nikienda mlangoni. Nilisema hivi: “Pamoja na kitabu utapata funzo la Biblia la nyumbani bila malipo.” Mtu mmoja aliyekubali toleo alisema baadaye kwamba ilimbidi aje kwenye mikutano ili aelewe nilichokuwa nikijaribu kumwambia. Mtu huyu alikuja kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kuna uthibitisho kama nini kwamba Mungu ndiye anayekuza mbegu katika mioyo minyenyekevu, kama alivyokiri mtume Paulo!—1 Wakorintho 3:7.

Baada ya miaka miwili hivi katika jiji kuu la Managua, tuliombwa tuhamie sehemu ya kusini ya Nikaragua. Tulipokuwa huko tulishiriki na kutaniko la Rivas na vikundi vya watu wenye kupendezwa vya maeneo yaliyojitenga kwenye ujirani. Pedro Peña, Shahidi mzeemzee mwaminifu, aliandamana nami tulipotembelea vikundi hivyo. Kikundi kimoja kilikuwa kwenye kisiwa cha volkeno katika Ziwa Nikaragua, ambapo kulikuwa na familia moja tu ya Mashahidi wa Yehova.

Ijapokuwa familia hii haikuwa na vitu vingi vya kimwili, ilijitahidi sana kuonyesha kwamba walithamini ziara yetu. Tulipofika jioni hiyo, chakula kilikuwa kimetayarishwa kwa ajili yetu. Tulikaa huko kwa juma moja, na watu wengi wapendwa waliopenda Biblia walishiriki chakula chao nasi. Tulifurahi sana kuona watu 101 waliohudhuria hotuba ya watu wote ya Biblia Jumapili.

Nahisi kwamba nguvu ya Yehova yenye kutegemeza ilikuwa wazi katika pindi moja, wakati tulipotaka kutembelea kikundi cha watu wenye kupendezwa milimani karibu na mpaka wa Kosta Rika. Siku ya kuondoka, Pedro alikuja kunichukua, lakini nilikuwa nimelala kitandani kwa sababu ya malaria. “Siwezi kwenda Pedro,” nikamwambia. Akiwekelea mkono wake kwenye kipaji cha uso wangu, alinijibu: “Una homa kali, lakini ni lazima twende! Akina ndugu wanangoja.” Kisha akatoa sala ya kutoka moyoni ambayo sikuwa nimepata kusikia kabla ya hapo.

Baadaye, nilisema: “Nenda ukanywe fresco (maji ya matunda). Nitajitayarisha na kuja baada ya dakika kumi.” Familia mbili za Mashahidi wa Yehova katika eneo tulilotembelea walitutunza sana. Siku iliyofuata tulienda mahubiri pamoja nao, ijapokuwa bado nilikuwa dhaifu kwa sababu ya homa. Lilikuwa jambo lenye kutia nguvu kama nini kuona wahudhuriaji mia moja katika mkutano wetu wa Jumapili!

Twahama Tena

Katika mwaka wa 1975 tulizaa mtoto wetu wa saba, Vaughn. Mwaka uliofuata, tulilazimika kurudi Kanada kwa sababu ya kifedha. Kuondoka Nikaragua hakukuwa jambo rahisi kwa sababu kwa kweli tulikuwa tumehisi nguvu ya Yehova ya kutegemeza tulipoishi huko. Kufikia wakati tulipoondoka, zaidi ya watu 500 katika eneo la kutaniko letu walikuwa wakihudhuria mikutano.

Mwanzoni, mimi na binti yetu Miriam tulipowekwa kuwa mapainia wa pekee huko Nikaragua, Miriam aliniuliza hivi: “Baba, mkirudi Kanada siku moja, mtaniacha niishi hapa?” Sikuwa nimekusudia kuondoka hata kidogo, kwa hiyo nikasema: “Naam, bila shaka!” Kwa hiyo tulipoondoka, Miriam alibaki ili aendelee na huduma ya wakati wote. Baadaye, aliolewa na Andrew Reed. Katika mwaka wa 1984 walihudhuria darasa la 77 la Gileadi, shule ya mishonari ya Mashahidi wa Yehova, iliyokuwa Brooklyn, New York. Miriam sasa anatumikia pamoja na mume wake huko Jamhuri ya Dominika, akitimiza tamaa aliyokaziwa kikiki na mishonari bora huko Nikaragua.

Maneno ya Baba yalikuwa yangali moyoni mwangu, “hatuachi kwa urahisi.” Kwa hiyo kufikia mwaka wa 1981 tulipokuwa tumeweka fedha za kutosha kurudi Amerika ya Kati, tulihama tena, safari hii kwenda Kosta Rika. Tulipokuwa tukitumikia huko, tulialikwa kusaidia katika ujenzi wa majengo mapya ya ofisi ya tawi. Hata hivyo, katika mwaka wa 1985, mwana wetu Grant alihitaji utunzi wa kitiba, kwa hiyo tukarudi Kanada. Glen alibaki Kosta Rika akifanya kazi katika ujenzi wa ofisi ya tawi, huku Annette na Charmaine wakitumikia wakiwa mapainia wa pekee. Tulipoondoka Kosta Rika hatukuwazia kwamba hatungerudi huko tena.

Kushughulika na Janga

Septemba 17, 1993 ilianza ikiwa siku nyangavu. Mimi na mwana wetu mkubwa, Mark, tulikuwa tunaezeka paa. Tulifanya kazi pamoja huku tukiongea kuhusu mambo ya kiroho, kama ilivyokuwa kawaida yetu. Lakini nikapoteza usawaziko na kuanguka chini kutoka paani. Nilipopata fahamu, nilichoweza kuona tu kilikuwa taa zenye kung’aa na watu waliovalia mavazi meupe. Nilikuwa katika kitengo cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum hospitalini.

Kwa sababu ya yale ambayo Biblia husema, jambo ambalo nilitaka kusema lilikuwa “Usinitie damu, usinitie damu!” (Matendo 15:28, 29) Nilifarijika kama nini kusikia Charmaine akisema: “Ni sawa, Baba. Sote tupo hapa.” Baadaye nilipata kujua kwamba madaktari waliona hati yangu ya kitiba, kwa hiyo matumizi ya damu hayakuwa suala kubwa. Nilikuwa nimevunjika shingo na kupooza kabisa, hata singeweza kupumua bila msaada.

Nikiwa siwezi kuondoka, nilihitaji kutegemezwa na Yehova kuliko wakati wowote. Upasuaji wa koo, uliofanywa kuingiza mrija wa kupumulia, ulizuia sehemu ya kuingilia hewa kwenye vinyuzi vya sauti. Sikuweza kuzungumza. Ilibidi watu wasome midomo yangu ili waelewe kile nilichokuwa nikisema.

Gharama ziliongezeka upesi. Kwa kuwa mke wangu na watoto wangu wengi walikuwa katika huduma ya wakati wote, nilijiuliza kama wangelazimika kuacha utumishi huu ili kushughulikia gharama hizo. Hata hivyo, Mark aliweza kupata kazi ambayo kwa miezi mitatu tu ililipia sehemu kubwa ya gharama hiyo. Hivyo, wote waliweza kubaki katika huduma ya wakati wote isipokuwa mimi na mke wangu.

Mamia ya kadi na barua kutoka nchi sita zilijaa ukutani mwa chumba changu cha hospitali. Kwa kweli Yehova alikuwa ananitegemeza. Kutaniko pia lilisaidia familia yangu kwa kuandaa chakula wakati wa miezi mitano na nusu nilipokuwa katika kitengo cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum. Kila siku alasiri, mzee Mkristo alikuwa akikaa nami, akinisomea Biblia na vichapo vya Biblia, na pia kunisimulia mambo yaliyoonwa yenye kupendeza. Washiriki wawili wa familia walitayarisha mikutaniko ya kutaniko pamoja nami, kwa hiyo sikukosa chakula cha maana cha kiroho.

Nilipokuwa ningali hospitalini, mpango ulifanywa nihudhurie programu ya siku ya kusanyiko la pekee. Wafanyakazi wa hospitali walipanga ili mwuguzi aliyesajiliwa na mtaalamu wa kunisaidia kupumua aandamane nami siku yote. Lilikuwa jambo lenye kupendeza kama nini kuwa pamoja na ndugu na dada zangu Wakristo tena! Sitasahau kamwe mamia ya watu waliokuwa wamepiga foleni wakingoja zamu yao ya kunisalimia.

Kudumisha Hali ya Kiroho

Mwaka mmoja hivi baada ya aksidenti hiyo, niliweza kurudi nyumbani kwa familia yangu, ijapokuwa bado nilihitaji uuguzi wa muda wa saa 24 kila siku. Gari lenye vifaa vya pekee huniwezesha kufika mikutanoni, ambayo mara nyingi sikosi kuhudhuria. Ingawa hivyo, lazima nikiri kwamba, nahitaji kujikaza kufanya hivyo. Tangu nirudi nyumbani, nimeweza kuhudhuria mikusanyiko yote ya wilaya.

Hatimaye, katika Februari 1997, nilirudiwa na uwezo wa kuongea kwa kiwango kidogo. Baadhi ya wauguzi wangu husikiliza kwa uthamini ninapowaambia tumaini langu linalotegemea Biblia. Mwuguzi mmoja amenisomea kitabu kizima cha Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu na pia vichapo vingine vya Watch Tower. Mimi huandikia watu barua kwa kutumia kijiti kupiga chapa kwenye kompyuta. Ijapokuwa kuandika kwa njia hii kunachosha, kujihusisha katika huduma ni jambo lenye kuthawabisha.

Nina maumivu mengi ya neva. Lakini yaonekana kwamba ninapowahubiria wengine kweli za Biblia au kuzisikia zikisomwa, nahisi kitulizo. Mara kwa mara, mimi huhubiri barabarani pamoja na mke wangu mwenye kunitegemeza, ambaye hunifasilia ninapohitaji msaada. Kwenye pindi kadhaa nimeweza kutumikia nikiwa painia-msaidizi. Kutumikia nikiwa mzee Mkristo hunipa shangwe, hasa ndugu wanaponijia kwenye mikutano au kunitembelea nyumbani, nami naweza kuwasaidia na kuwatia moyo.

Lazima nikubali kwamba ni rahisi kushuka moyo. Kwa hiyo, ninaposhuka moyo, mara moja husali ili niweze kupata shangwe. Usiku na mchana naomba Yehova aendelee kunitegemeza. Barua au kutembelewa na mtu hunichangamsha. Kusoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! pia hujaza akili yangu mawazo yenye kujenga. Wauguzi tofauti-tofauti hunisomea magazeti haya nyakati nyingine. Tangu aksidenti yangu, nimesikiliza usomaji wa Biblia yote kupitia kaseti mara saba. Hizo ni baadhi ya njia ambazo Yehova amenitegemeza.—Zaburi 41:3.

Badiliko la hali zangu limenifanya niwe na wakati mwingi wa kutafakari jinsi ambavyo Mfunzi wetu Mtukufu, Yehova, hutuelimisha maishani. Yeye hutupa ujuzi sahihi wa mapenzi na makusudi yake, huduma yenye maana, ushauri kuhusu siri ya kupata furaha ya familia, na ufahamu wa kujua jinsi ya kukabiliana na janga. Yehova amenibariki na mke mwaminifu na mzuri ajabu. Watoto wangu pia wamenitegemeza sana, na ni shangwe yangu kwamba wote wameshiriki katika huduma ya wakati wote. Katika Machi 11, 2000, mwana wetu Mark na mke wake, Allyson, walihitimu katika darasa la 108 la Shule ya Gileadi na walipewa mgawo wa kwenda Nikaragua. Mimi na mke wangu tuliweza kuhudhuria siku yao ya kuhitimu. Kwa kweli naweza kusema kwamba janga limebadili maisha yangu lakini si moyo wangu.—Zaburi 127:3, 4.

Namshukuru Yehova kwa hekima aliyonipa ya kuweza kuipa familia yangu urithi wa kiroho niliopokea. Naimarishwa na kutiwa moyo kuona watoto wangu wakimtumikia Muumba wao na mtazamo kama wa baba yangu, aliyesema, “Hatuachi kwa urahisi. Yehova ametuamuru tuhubiri.” Kwa kweli, Yehova amenitegemeza mimi na familia yangu siku zote.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nikiwa na Baba, ndugu zangu, na dada yangu, kando ya nyumba yetu ya gari, iliyotumiwa wakati wa upainia. Niko upande wa kulia

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na mke wangu, Myrna

[Picha katika ukurasa wa 26]

Picha ya karibuni ya familia yetu

[Picha katika ukurasa wa 27]

Ningali ninatoa ushahidi kwa njia ya barua