Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Paradiso ya Kiroho Ni Nini?

Paradiso ya Kiroho Ni Nini?

Paradiso ya Kiroho Ni Nini?

GUSTAVO alilelewa katika jiji dogo huko Brazili. * Tangu utotoni alikuwa amefunzwa kwamba watu wema huenda mbinguni baada ya kifo. Hakujua chochote kuhusu kusudi la Mungu kuwa kuna wakati ambapo wanadamu waaminifu wangefurahia maisha makamilifu katika paradiso ya kidunia. (Ufunuo 21:3, 4) Na pia kuna jambo jingine ambalo hakujua. Hakuwa ametambua kwamba hata sasa, angeweza kuwa katika paradiso ya kiroho.

Je, umepata kusikia juu ya paradiso hiyo ya kiroho? Je, wajua paradiso hiyo ni nini na ni nini kinachohusika ili kuwa ndani yake? Mtu yeyote anayetaka kuwa mwenye furaha kwelikweli anahitaji kuijua paradiso hiyo.

Kuipata Paradiso ya Kiroho

Kusema kwamba hata leo mtu anaweza kuishi katika paradiso kwaweza kusikika kuwa jambo lisilo la kweli. Ulimwengu huu si paradiso hata kidogo. Kuna watu wengi mno wanaopatwa na kile ambacho mfalme Mwebrania wa kale alisimulia hivi: “Tazama, machozi yao waliodhulumiwa, ambao walikuwa hawana mfariji; na upande wa wale waliowadhulumu kulikuwa na uwezo, walakini wale walikuwa hawana mfariji.” (Mhubiri 4:1) Mamia ya mamilioni huteseka chini ya mifumo yenye ufisadi ya kisiasa, kidini, na ya kiuchumi, nao hawana msaada, wala “mfariji.” Wengine wengi hujitahidi kulipia gharama zao, kulea watoto wao, na kufanya mambo mengine mengi ili kuendelea kuishi. Hao pia yamkini watafurahia kupata mfariji, yaani, mtu fulani wa kupunguza mzigo wao angalau. Kwao wote, maisha si ya kiparadiso kamwe.

Basi, iko wapi hiyo paradiso ya kiroho? Neno la Kiswahili “paradiso” linahusiana na maneno ya Kigiriki, Kiajemi, na Kiebrania ambayo yote huwa yana maana ya bustani, mahali pa starehe pa mapumziko. Biblia yaahidi kwamba siku moja dunia itakuwa paradiso halisi, makao ya kibustani kwa jamii ya wanadamu isiyo na dhambi. (Zaburi 37:10, 11) Tukikumbuka hilo, twaona kwamba paradiso ya kiroho ni mazingira yanayopendeza macho na yenye kuburudisha, yanayofanya mtu afurahie amani pamoja na mwanadamu mwenzake na pamoja na Mungu. Leo, kama Gustavo alivyoona, kuna paradiso ya aina hiyo, nayo huhusisha watu wengi sana.

Alipokuwa na umri wa miaka 12, Gustavo aliamua kwamba alitaka kuwa kasisi wa Katoliki ya Kiroma. Kwa kibali cha wazazi wake, aliingia katika seminari ya kidini. Alipokuwa huko alijiingiza katika muziki, michezo ya kuigiza, na siasa, ambazo zilikuwa zikiendelezwa na kanisa ili kuwavutia vijana. Alijua kwamba kasisi alipaswa kujitoa kwa ajili ya watu na kwamba hangeoa. Lakini, baadhi ya makasisi na wanaseminari ambao Gustavo alijua walijiingiza katika mazoea ya ukosefu wa adili. Katika hali hizo, Gustavo akaanza kulewa kupindukia. Ni wazi, hakuwa amepata paradiso ya kiroho.

Siku moja, Gustavo alisoma trakti ya Biblia iliyoongea kuhusu paradiso ya kidunia. Ilimfanya afikiri kuhusu kusudi la maisha. Yeye anasema: “Nilianza kusoma Biblia kwa ukawaida, lakini sikuielewa. Hata sikuona kwamba Mungu ana jina.” Aliacha seminari na akawaendea Mashahidi wa Yehova, akitafuta msaada wakuelewa Biblia. Baada ya hapo, alifanya maendeleo haraka na upesi akaweka maisha yake wakfu kwa Mungu. Gustavo alikuwa anajifunza juu ya paradiso ya kiroho.

Watu kwa Ajili ya Jina la Mungu

Gustavo alijifunza kwamba jina la Mungu, Yehova, si habari ya juujuu tu kwa mwanafunzi wa Biblia. (Kutoka 6:3) Ni sehemu muhimu ya ibada ya kweli. Yesu alifundisha wafuasi wake kusali hivi: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Akiongea kuhusu watu Wasio Wayahudi ambao walikuja kuwa Wakristo, mwanafunzi Yakobo alisema hivi: “Mungu . . . [alielekeza] uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwayo watu kwa ajili ya jina lake.” (Matendo 15:14) Katika karne ya kwanza, “watu kwa ajili ya jina lake” walikuwa kutaniko la Kikristo. Je, leo kuna watu kwa ajili ya jina la Mungu? Ndiyo, na Gustavo alikuja kutambua kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu hao.

Mashahidi wa Yehova wanatenda katika nchi na maeneo yapatayo 235. Idadi yao ni wahudumu zaidi ya milioni sita, na watu wengine wenye kupendezwa milioni nane wamehudhuria mikutano yao. Wanajulikana sana kwa huduma yao ya peupe, nao hutimiza maneno haya ya Yesu: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Hata hivyo, kwa nini Gustavo alihisi kwamba amepata paradiso ya kiroho aliposhirikiana na Mashahidi wa Yehova? Anasema hivi: “Nililinganisha yale niliyoona ulimwenguni na hasa katika seminari na yale niliyopata miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Tofauti kubwa zaidi ni upendo miongoni mwa Mashahidi.”

Wengine wamesema vivyo hivyo kuhusu Mashahidi wa Yehova. Miriam, kijana mwanamke Mbrazili, alisema hivi: “Sikujua jinsi ya kuwa mwenye furaha, hata katika familia yangu. Mara ya kwanza kuona upendo ukionyeshwa ilikuwa miongoni mwa Mashahidi wa Yehova.” Mwanamume anayeitwa Christian alisema hivi: “Mara kwa mara nilijihusisha kijuujuu na mambo ya uwasiliani-roho, lakini dini haikuwa muhimu kwangu. Nilizingatia sana cheo changu na kazi yangu nikiwa mhandisi. Lakini, mke wangu alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, niliona badiliko kwake. Pia nilivutiwa na shangwe na bidii ya wanawake Wakristo waliomtembelea.” Kwa nini watu husema mambo kama hayo kuhusu Mashahidi wa Yehova?

Paradiso ya Kiroho Ni Nini?

Jambo moja linalofanya Mashahidi wa Yehova wawe tofauti ni uthamini wao wa ujuzi wa Biblia. Wanaamini kwamba Biblia ni ya kweli na kwamba ni Neno la Mungu. Kwa sababu hiyo, hawatosheki kujua tu mambo ya msingi ya dini yao. Wana ratiba yenye kuendelea ya funzo la kibinafsi na usomaji wa Biblia. Kadiri mtu aendeleavyo kushirikiana na Mashahidi wa Yehova, ndivyo ajifunzavyo zaidi kuhusu Mungu na mapenzi Yake yanayoonyeshwa katika Biblia.

Ujuzi huo huwaweka Mashahidi wa Yehova huru kutokana na mambo yanayonyang’anya watu wengi furaha, kama vile ushirikina na mawazo yenye kudhuru. Yesu alisema: “Kweli itawaweka nyinyi huru,” na Mashahidi wa Yehova wamethibitisha jambo hilo. (Yohana 8:32) Fernando, ambaye wakati mmoja alizoea kuwasiliana na roho waovu, asema hivi: “Kujifunza juu ya uhai udumuo milele kulikuwa msaada mkubwa sana. Nilikuwa na hofu ya kwamba ama mimi au wazazi wangu tungekufa.” Kweli ilimweka Fernando huru kutokana na hofu yake ya ulimwengu wa roho na yale yaitwayo eti maisha baada ya kifo.

Katika Biblia, ujuzi kuhusu Mungu wahusiana sana na paradiso. Nabii Isaya alisema: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

Bila shaka, ujuzi pekee hautoshi kuleta amani iliyotabiriwa na Isaya. Lazima mtu atende kulingana na yale anayojifunza. Fernando alitoa maelezo haya: “Mtu asitawishapo matunda ya roho, yeye huchangia paradiso ya kiroho.” Fernando alikuwa akirejezea maneno ya mtume Paulo, ambaye aliziita sifa nzuri ambazo Mkristo apaswa kusitawisha “matunda ya roho.” Aliyaorodhesha kuwa “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.”—Wagalatia 5:22, 23.

Waweza kuona ni kwa nini kushirikiana na jamii ya watu ambao hujitahidi kusitawisha sifa hizo kwa kweli kungekuwa kama kuwa katika paradiso? Paradiso ya kiroho iliyotabiriwa na nabii Sefania ingekuwako miongoni mwa watu hao. Yeye alisema hivi: “Hawatatenda uovu, wala kusema uongo; wala ulimi wa hadaa hautaonekana kinywani mwao; kwa maana watakula na kulala, wala hapana mtu atakayewaogofya.”—Sefania 3:13.

Umuhimu wa Upendo

Huenda umeona kwamba tunda la kwanza la roho linalotajwa na Paulo ni upendo. Hiyo ni sifa ambayo Biblia huongea sana juu yake. Yesu alisema hivi: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Ni kweli kwamba, Mashahidi wa Yehova si wakamilifu. Mara nyingine wana matatizo ya kutoafikiana miongoni mwao wenyewe kama walivyokuwa mitume wa Yesu. Lakini kwa kweli wanapendana sana, nao husali wasaidiwe na roho takatifu wanapositawisha sifa hiyo.

Tokeo ni kwamba, ibada yao haina kifani. Hakuna ukabila wala ubaguzi wa kitaifa wenye kuleta migawanyiko miongoni mwao. Mashahidi wa Yehova ambao wamejipata katikati ya mauaji ya kimakusudi ya makabila na maangamizi ya jamii nzimanzima miaka ya mwishomwisho ya karne ya 20 walilindana hata wakahatarisha maisha zao. Ijapokuwa ‘wanatoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha,’ wanafurahia umoja ambao ni vigumu kuuwazia hadi unapoushiriki mwenyewe.—Ufunuo 7:9.

Paradiso Miongoni mwa Wale Wafanyao Mapenzi ya Mungu

Paradiso ya kiroho hairuhusu pupa, ukosefu wa adili, na ubinafsi. Wakristo waambiwa hivi: “Komeni kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe umbo kwa kufanya upya akili yenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Tunapoishi maisha safi, yenye maadili na kufanya mapenzi ya Mungu katika njia nyingine, twasaidia kujenga paradiso ya kiroho na twajiletea wenyewe furaha. Carla aliona hilo kuwa la kweli. Anasema: “Baba yangu alinifundisha kufanya kazi kwa bidii ili nijitegemee kifedha. Lakini ingawa masomo yangu ya chuo kikuu yalinipa usalama, nilikosa umoja wa familia na usalama ambao huletwa tu na ujuzi kutoka katika Neno la Mungu.”

Bila shaka, kufurahia paradiso ya kiroho hakuondoi matatizo ya maisha. Wakristo huwa wagonjwa. Taifa wanaloishi huenda likawa na zogo la kiraia. Wengi huvumilia umaskini. Hata hivyo, kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova Mungu—ambao ni sehemu muhimu ya paradiso ya kiroho—humaanisha kwamba twamtegemea kupata msaada. Kwa kweli, yeye hutualika ‘tumtwike mizigo yetu,’ na wengi wanaweza kusema juu ya njia ya ajabu ambayo amewategemeza wakati wa hali ngumu zaidi. (Zaburi 55:22; 86:16, 17) Mungu anaahidi kuwa pamoja na waabudu wake hata katika “bonde la uvuli wa mauti.” (Zaburi 23:4) Uhakika wa kwamba Mungu yuko tayari kututegemeza hudumisha ‘amani yetu ya Mungu izidiyo fikira yote,’ ambayo ni ufunguo wa paradiso ya kiroho.—Wafilipi 4:7.

Kuchangia Paradiso ya Kiroho

Watu wengi hufurahia kutembea kwenye bustani. Wanapenda kutembea katikati yake au kuketi kwenye benchi na kufurahia mazingira yake. Vivyo hivyo, wengi hufurahia kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Wao huona ushirika huo kuwa wenye kuburudisha, wenye amani, na wenye kuchangamsha. Hata hivyo, bustani yenye kupendeza yahitaji kutunzwa ili iendelee kuwa paradiso. Vivyo hivyo, paradiso ya kiroho inapatikana katika ulimwengu huu usio wa kiparadiso hata kidogo kwa sababu tu Mashahidi wa Yehova wanaisitawisha, na Mungu hubariki jitihada zao. Basi, mtu anaweza kuchangiaje kwa njia kubwa paradiso hiyo?

Kwanza, unahitaji kushirikiana na kutaniko la Mashahidi wa Yehova, ujifunze Biblia nao, na upate ujuzi wa Biblia ambao ni msingi wa paradiso hiyo ya kiroho. Carla alisema hivi: “Hakuna paradiso ya kiroho bila chakula cha kiroho.” Hilo latia ndani kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida na kutafakari yale unayosoma. Ujuzi utakaopata utakufanya umkaribie Mungu zaidi, na utapata kumpenda. Pia utajifunza kuongea naye katika sala na kumwomba mwongozo wake na roho yake ili ikutegemeze unapofanya mapenzi yake. Yesu alituambia tudumu katika sala. (Luka 11:9-13) Mtume Paulo alisema: “Salini bila kukoma.” (1 Wathesalonike 5:17) Pendeleo la kuongea na Mungu katika sala ukiwa na uhakika kabisa kwamba anakusikia ni sehemu muhimu ya paradiso ya kiroho.

Kadiri muda unavyopita, maisha yako yatabadilika yawe mazuri zaidi kwa sababu ya yale unayojifunza, na hatimaye utataka kuongea na wengine juu ya hayo. Kisha utaweza kutii amri hii ya Yesu: “Acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu, ili wapate kuona kazi zenu bora na kumpa utukufu Baba yenu aliye katika mbingu.” (Mathayo 5:16) Kufundisha wengine ujuzi kuhusu Yehova Mungu na Yesu Kristo na kuhimidi upendo mkuu walioonyesha wanadamu huleta furaha kubwa.

Wakati unakuja ambapo dunia yote itakuwa paradiso halisi—mahali pa kibustani pasipo na uchafuzi na patakuwa makao yafaayo wanadamu waaminifu. Kuwapo kwa paradiso ya kiroho katika “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo” ni ithibati ya uwezo wa Mungu na dalili ya yale anayoweza na atakayotimiza wakati ujao.—2 Timotheo 3:1.

Hata sasa, wale wanaofurahia paradiso ya kiroho wanaona utimizo wa unabii wa Isaya 49:10 wenye kusema: “Hawataona njaa, wala hawataona kiu; hari haitawapiga, wala jua; kwa maana yeye aliyewarehemu atawatangulia, naam, karibu na chemchemi za maji atawaongoza.” José atashuhudia ukweli huo. Alitamani kuwa mwanamuziki mashuhuri, lakini akapata uradhi zaidi katika kumtumikia Mungu katika kutaniko la Kikristo. Anasema hivi: “Sasa nafurahia maisha yenye maana. Nahisi nikiwa salama katika udugu wa Kikristo, na namjua Yehova kuwa Baba mwenye upendo ambaye twaweza kumwitibari.” Furaha ya José—na ya mamilioni wengine kama yeye—inasimuliwa vizuri katika Zaburi 64:10: “Mwenye haki atamfurahia BWANA na kumkimbilia.” Huo ni ufafanuzi mzuri kama nini wa paradiso ya kiroho!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Watu waliotajwa hapa ni watu halisi, lakini majina kadhaa yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Huku tukifurahia paradiso ya kiroho, tusaidie kuipanua!