Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wale Wanaotembea Katika Nuru Hushangilia

Wale Wanaotembea Katika Nuru Hushangilia

Wale Wanaotembea Katika Nuru Hushangilia

“Njoni twende katika nuru ya BWANA.”—ISAYA 2:5.

1, 2. (a) Nuru ni muhimu kadiri gani? (b) Kwa nini onyo la kwamba giza lingeifunika dunia ni zito sana?

YEHOVA ndiye Chanzo cha nuru. Biblia humtaja kuwa “awapaye watu jua, ili kuwa nuru wakati wa mchana, na amri za mwezi na nyota, ili kuwa nuru wakati wa usiku.” (Yeremia 31:35; Zaburi 8:3) Yeye ndiye aliyeumba jua letu, ambalo kwa kweli ni tanuri kubwa sana ya nyuklia inayotoa nishati nyingi sana, baadhi yake ikiwa nuru na joto. Kiasi kidogo cha nishati hiyo ambayo hutufikia ikiwa nuru ya jua hutegemeza uhai duniani. Hatungeweza kuishi pasipo nuru hiyo ya jua. Dunia ingekuwa sayari isiyo na uhai.

2 Tunapozingatia hilo, tunaweza kuelewa uzito wa hali inayofafanuliwa na nabii Isaya. Alisema hivi: “Tazama, giza litaifunika dunia, na giza kuu litazifunika kabila za watu.” (Isaya 60:2) Ni wazi kwamba giza hilo si giza halisi. Isaya hakumaanisha kwamba siku fulani jua, mwezi, na nyota zitaacha kuangaza. (Zaburi 89:36, 37; 136:7-9) Badala yake, alikuwa akizungumzia giza la kiroho. Lakini giza la kiroho laweza kusababisha kifo. Hatuwezi kuishi bila nuru ya kiroho kwa muda mrefu kama vile tusivyoweza kuishi bila nuru halisi.—Luka 1:79.

3. Kwa kuzingatia maneno ya Isaya, Wakristo wapaswa kufanya nini?

3 Kwa kuzingatia hilo, ni jambo muhimu kutambua kwamba ijapokuwa maneno ya Isaya yalitimizwa katika Yuda la kale, yanatimizwa kwa kiwango kikubwa zaidi leo. Naam, katika wakati wetu ulimwengu umefunikwa na giza la kiroho. Katika hali hiyo hatari, nuru ya kiroho ni muhimu kuliko mambo yote. Ndiyo sababu inafaa Wakristo watii himizo hili la Yesu: “Acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu.” (Mathayo 5:16) Wakristo waaminifu wanaweza kuwaangazia nuru wapole walio katika giza, na hivyo kuwapa fursa ya kupata uhai.—Yohana 8:12.

Nyakati Zenye Giza Katika Israeli

4. Maneno ya kiunabii ya Isaya yalitimizwa lini mara ya kwanza, lakini tayari kulikuwa na hali gani katika siku zake?

4 Maneno ya Isaya kuhusu jinsi ambavyo giza lingeifunika dunia yalitimizwa mara ya kwanza Yuda lilipofanywa ukiwa na watu wake walipokuwa katika utekwa Babiloni. Hata hivyo, hata kabla ya wakati huo, katika siku za Isaya mwenyewe, tayari sehemu kubwa ya taifa hilo ilikuwa imefunikwa na giza la kiroho, jambo lililomchochea awasihi hivi watu wa nchi yake: “Enyi wa nyumba ya Israeli, njoni twende katika nuru ya BWANA”!—Isaya 2:5; 5:20.

5, 6. Ni mambo gani yaliyochangia giza katika siku za Isaya?

5 Isaya alitoa unabii katika Yuda “siku za Uzia, Yothamu, Ahazi na Hezekia, wafalme wa Yuda.” (Isaya 1:1) Zilikuwa nyakati zenye ghasia na misukosuko ya kisiasa, unafiki wa kidini, kupotoshwa kwa haki, na kuonewa kwa maskini. Hata wakati wa wafalme waaminifu, kama vile Yothamu, kulikuwepo madhabahu za miungu isiyo ya kweli kwenye vilele vya milima. Wakati wa watawala wasio waaminifu, hali zilikuwa mbaya hata zaidi. Kwa mfano, Mfalme Ahazi mwovu, hata alimtoa mwana wake kuwa dhabihu katika dhabihu za tambiko kwa mungu aitwaye Moleki. Hilo lilikuwa giza la ajabu!—2 Wafalme 15:32-34; 16:2-4.

6 Hali ya kimataifa ilikuwa yenye kuhuzunisha pia. Moabu, Edomu, na Ufilisti yalizingira mipaka ya Yuda kwa njia yenye kutisha. Ingawa ufalme wa kaskazini wa Israeli ulikuwa na uhusiano wa kijamaa na Yuda, sasa ulionyesha uadui waziwazi. Mbali kaskazini, Siria ilitishia amani ya Yuda. Hatari kubwa hata zaidi ilikuwa ile serikali ya Ashuru yenye ukatili, ambayo ilijitahidi daima kupanua mamlaka yake. Katika kipindi ambacho Isaya alitoa unabii, Ashuru ilishinda Israeli na ikakaribia kuiharibu Yuda. Wakati fulani, Ashuru ilikuwa imeshinda kila mji nchini Yuda isipokuwa Yerusalemu.—Isaya 1:7, 8; 36:1.

7. Israeli na Yuda zilichagua njia gani, naye Yehova alitendaje?

7 Watu wa Mungu waliokuwa wamefanya agano pamoja naye walipatwa na misiba hiyo kwa sababu Israeli na Yuda zilikosa uaminifu-mshikamanifu kwake. Kama wale wanaotajwa katika kitabu cha Mithali, walikuwa ‘wakiacha njia za unyofu, ili kuziendea njia za giza.’ (Mithali 2:13) Hata ingawa Yehova alikasirishwa na watu wake, hakuwaacha kabisa. Badala yake, alimwinua Isaya na manabii wengine ili waangaze nuru ya kiroho kwa yeyote katika taifa hilo aliyetaka bado kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Nuru iliyotolewa kupitia manabii hao ilikuwa yenye thamani kwelikweli. Ilikuwa yenye kuhuisha.

Nyakati za Giza Leo

8, 9. Ni mambo gani yanayochangia giza la ulimwengu leo?

8 Hali katika siku za Isaya yafanana sana na mambo tunayoona leo. Katika kipindi chetu, watawala wa kibinadamu wamemkataa Yehova na Mfalme wake aliyetawazwa, Yesu Kristo. (Zaburi 2:2, 3) Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wamedanganya makundi yao. Viongozi hao hudai kumtumikia Mungu, lakini kwa kweli wengi wao huunga mkono miungu ya ulimwengu huu—utukuzo wa taifa, utumizi wa nguvu za kijeshi, utajiri, na watu mashuhuri—mbali na kufundisha mafundisho ya kipagani.

9 Dini za Jumuiya ya Wakristo zimejihusisha katika vita na maangamizi ya jamii na matisho mengine mahali mahali. Isitoshe, badala ya kutetea maadili yanayotegemea Biblia, makanisa mengi ama yanapuuza ama kuunga mkono kwa bidii mazoea yasiyo ya adili kama uasherati na ugoni-jinsia-moja. Kwa sababu ya kukataa viwango vya Biblia, makundi ya Jumuiya ya Wakristo ni sawa na watu waliotajwa na mtunga-zaburi wa kale: “Hawajui wala hawafahamu, hutembea gizani.” (Zaburi 82:5) Kwa kweli, Jumuiya ya Wakristo kama vile Yuda la kale, iko katika giza nene.—Ufunuo 8:12.

10. Nuru huangazaje katika giza leo, na wapole hunufaikaje?

10 Katikati ya giza hilo, Yehova anasababisha nuru iangaze kwa ajili ya wapole. Ili kutimiza hilo, anatumia watumishi wake waliotiwa mafuta walioko duniani, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” nao ‘hung’aa wakiwa wamulikaji katika ulimwengu.’ (Mathayo 24:45; Wafilipi 2:15) Jamii hiyo ya mtumwa, ikiungwa mkono na mamilioni ya waandamani wao “kondoo wengine” huangaza nuru ya kiroho inayotegemea Neno la Mungu, Biblia. (Yohana 10:16) Katika ulimwengu huu uliojaa giza, nuru hiyo huwapa wapole tumaini, huwasaidia kuwa na uhusiano na Mungu, na kuepuka mitego ya kiroho. Ni yenye thamani, na huhuisha.

‘Nalihimidi Jina Lako’

11. Yehova alitoa habari gani katika siku za Isaya?

11 Yehova aliandaa mwongozo gani katika siku zenye giza ambazo Isaya aliishi na hata katika siku zilizokuwa na giza zaidi wakati Wababiloni walipoteka taifa la Yehova? Mbali na kutoa mwongozo wa kiadili, alionyesha waziwazi hapo kimbele jinsi ambavyo angetimiza makusudi yake kuhusiana na watu wake. Kwa mfano, fikiria unabii mzuri sana unaopatikana katika Isaya sura ya 25 hadi 27. Sura hizo zaonyesha jinsi Yehova alivyoshughulikia mambo wakati huo na jinsi afanyavyo hivyo leo.

12. Isaya asema maneno gani ya kutoka moyoni?

12 Kwanza, Isaya atangaza hivi: “Ee BWANA [“Yehova,” NW], wewe u Mungu wangu; nitakutukuza na kulihimidi jina lako.” Hayo yalikuwa maneno yenye sifa ya kutoka moyoni kama nini! Mbona nabii huyo alitoa sala ya aina hiyo? Sababu moja kuu yafunuliwa kwenye sehemu iliyobaki ya mstari huo, ambapo twasoma hivi: “Kwa kuwa [wewe Yehova] umetenda mambo ya ajabu, mashauri ya kale, kwa uaminifu na kweli.”—Isaya 25:1.

13. (a) Ni ujuzi gani uliomtia Isaya nguvu amthamini Yehova? (b) Tunawezaje kujifunza kutokana na kielelezo cha Isaya?

13 Kufikia siku za Isaya, Yehova alikuwa amefanya matendo mengi ya ajabu kwa ajili ya Israeli, nayo yakaandikwa. Ni wazi kwamba Isaya aliyafahamu maandiko hayo. Kwa mfano, alijua kwamba Yehova alikuwa amewakomboa watu wake kutoka utumwa wa Misri na kuwaokoa kutoka kwa hasira ya majeshi ya Farao kwenye Bahari Nyekundu. Alijua kwamba Yehova alikuwa amewaongoza watu wake katika nyika na kuwaleta katika Nchi ya Ahadi. (Zaburi 136:1, 10-26) Masimulizi hayo ya kihistoria yalionyesha kwamba Yehova Mungu ni mwaminifu na ni mwenye kutumainika. “Mashauri” yake—mambo yote anayokusudia—hutimia. Ujuzi sahihi uliotolewa na Mungu ulimtia Isaya nguvu aendelee kutembea katika nuru. Hivyo basi, akawa kielelezo kizuri kwetu. Tukijifunza kwa makini Neno la Mungu lililoandikwa na kulitumia maishani, sisi pia tutadumu katika nuru.—Zaburi 119:105; 2 Wakorintho 4:6.

Jiji Laharibiwa

14. Ni nini kilichotabiriwa kuhusu mji fulani, na yaelekea mji huo ni upi?

14 Kielelezo kimoja cha mashauri ya Mungu kipo kwenye Isaya 25:2, ambapo twasoma: “Umefanya mji kuwa ni chungu; mji wenye boma kuwa ni magofu; jumba la wageni kuwa si mji; hautajengwa tena milele.” Ni mji upi huo? Huenda Isaya alikuwa akitabiri juu ya Babiloni. Kwa kweli, wakati ulifika ambapo Babiloni ulikuwa rundo la mawe.

15. Ni “jiji [gani] kubwa” lililopo leo, nalo litapatwa na nini?

15 Je, mji anaoutaja Isaya wafanana na mji wowote leo? Ndiyo. Kitabu cha Ufunuo chasema juu ya “jiji kubwa lililo na ufalme juu ya wafalme wa dunia.” (Ufunuo 17:18) Jiji hilo kuu ni “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. (Ufunuo 17:5) Sehemu kuu ya Babiloni Mkubwa leo ni Jumuiya ya Wakristo, ambayo makasisi wake huongoza katika kupinga kazi ya kuhubiri Ufalme ya watu wa Yehova. (Mathayo 24:14) Hata hivyo, kama vile Babiloni wa kale, Babiloni Mkubwa litaharibiwa hivi karibuni, halitainuka tena kamwe.

16, 17. Maadui wa Yehova wamemtukuzaje katika nyakati za kale na za leo?

16 Isaya atabiri nini kingine kuhusu “mji wenye boma”? Isaya amwambia Yehova hivi: “Watu walio hodari watakutukuza, mji wa mataifa watishao utakuogopa.” (Isaya 25:3) Mji huo wenye uadui, “mji wa mataifa watishao,” wawezaje kumtukuza Yehova? Kumbuka kilichompata Mfalme Nebukadreza wa Babiloni mwenye nguvu nyingi sana. Baada ya kupatwa na jambo lenye kuamsha fikira lililoonyesha udhaifu wake mwenyewe, alilazimika kukiri ukuu wa Yehova na nguvu za uweza Wake wote. (Danieli 4:34, 35) Yehova anapodhihirisha nguvu zake, hata maadui wake hulazimika kukiri matendo yake yenye nguvu hata ingawa ni kwa kusitasita.

17 Je, Babiloni Mkubwa aliwahi kulazimika kukiri matendo ya Yehova yenye nguvu? Ndiyo. Katika vita ya ulimwengu ya kwanza, watumishi wa Yehova waliotiwa mafuta walihubiri chini ya dhiki. Mwaka wa 1918 waliingia katika utekwa wa kiroho wakati wasimamizi wa Watch Tower Society walipotiwa gerezani. Kazi iliyopangwa ya kuhubiri karibu ikome. Kisha, mwaka wa 1919, Yehova aliwarudisha na kuwatia nguvu upya kwa roho yake, ambapo walitoka ili kutimiza utume wa kuhubiri habari njema katika dunia yote inayokaliwa. (Marko 13:10) Yote hayo yalitabiriwa katika kitabu cha Ufunuo, na pia athari ambazo zingewapata maadui wao. Hawa “wakawa wenye kuogopa na kumpa utukufu Mungu wa mbinguni.” (Ufunuo 11:3, 7, 11-13) Si kwamba wote waligeuzwa imani, lakini walilazimika kutambua matendo ya Yehova yenye nguvu katika pindi hiyo, kama vile Isaya alivyokuwa ametabiri.

“Ngome ya Maskini”

18, 19. (a) Kwa nini wapinzani wameshindwa kuvunja uaminifu-maadili wa watu wa Yehova? (b) “Wimbo wa hao watishao” utashushwa jinsi gani?

18 Akielekeza fikira zake sasa kwa matendo ya fadhili ya Yehova kwa wale wanaotembea katika nuru, Isaya amwambia Yehova hivi: “Umekuwa ngome ya maskini, ngome ya mhitaji katika dhiki yake, mahali pa kukimbilia wakati wa tufani, kivuli wakati wa hari; wakati uvumapo upepo wa watu watishao, kama dhoruba ipigayo ukuta. Kama vile hari katika mahali pakavu utaushusha mshindo wa wageni; kama ilivyo hari kwa kivuli cha wingu, wimbo wa hao watishao utashushwa.”—Isaya 25:4, 5.

19 Tangu mwaka wa 1919, wakatili wamejaribu juu chini kuvunja uaminifu-maadili wa waabudu wa kweli, lakini hawajafaulu. Kwa nini? Kwa sababu Yehova ni ngome na kimbilio la watu wake. Yeye huandaa kivuli kutoka kwa joto lenye kuchoma la mnyanyaso na husimama kama ukuta imara dhidi ya dhoruba za upinzani. Sisi tunaotembea katika nuru ya Mungu hutazamia kwa uhakika wakati ambapo “wimbo wa hao watishao utashushwa.” Naam, twatazamia kwa hamu siku ambayo maadui wa Yehova watakuwa wametoweka.

20, 21. Ni karamu gani anayoandaa Yehova, na karamu hiyo itatia ndani nini katika ulimwengu mpya?

20 Yehova hufanya mengi kuliko tu kuwalinda watumishi wake. Yeye huwaandalia akiwa Baba yao mpendwa. Baada ya kuwakomboa watu wake kutoka Babiloni Mkubwa mwaka wa 1919, aliwaandalia karamu ya ushindi, chakula kingi cha kiroho. Hayo yalitabiriwa kwenye Isaya 25:6, ambapo twasoma hivi: “Katika mlima huu BWANA wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, iliyochujwa sana.” Tumebarikiwa kama nini kushiriki katika karamu hiyo! (Mathayo 4:4) Kwa kweli “meza ya Yehova” imejaa vitu vizuri vya kula. (1 Wakorintho 10:21) Kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” tunapewa chochote ambacho tungehitaji kiroho.

21 Karamu hiyo ambayo Mungu ameandaa ina mengi zaidi. Karamu ya kiroho tunayofurahia sasa hutukumbusha wingi wa chakula cha kimwili kitakachokuwepo katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi. Kisha, “karamu ya vitu vinono” itatia ndani chakula kingi cha kimwili. Hakuna yeyote atakayelazimika kuona njaa ya kimwili au ya kiroho. Itakuwa faraja iliyoje kwa waamini wenzetu wapendwa ambao sasa huteseka kwa sababu ya “upungufu wa chakula” uliotabiriwa, ambao ni sehemu ya “ishara” ya kuwapo kwa Yesu! (Mathayo 24:3, 7) Maneno ya mtunga-zaburi yanawafariji kwelikweli. Alisema: “Nchi na izae nafaka kwa wingi, vilima vijae mavuno.”—Zaburi 72:16, Biblia Habari Njema.

22, 23. (a) Ni “utaji” au “sitara” gani itakayoondolewa, na jinsi gani? (b) ‘Aibu ya watu wa Yehova’ itaondolewaje?

22 Sasa isikilize ahadi nzuri hata zaidi. Akilinganisha dhambi na kifo na “utaji,” au “sitara,” Isaya asema hivi: “Katika mlima huu [Yehova] atauharibu uso wa sitara iliyowekwa juu ya watu wote, na utaji ule uliotandwa juu ya mataifa yote.” (Isaya 15:7) Hebu wazia! Dhambi na kifo, ambazo zimewalemea wanadamu kama blanketi inayomzuia mtu kupumua, hazitakuwapo tena. Twatazamia kwa hamu kama nini siku ambayo wanadamu watiifu na waaminifu watanufaishwa kikamili na dhabihu ya fidia ya Yesu!—Ufunuo 21:3, 4.

23 Akirejezea wakati huo mzuri ajabu, nabii aliyepuliziwa atuhakikishia hivi: “[Mungu] amemeza mauti hata milele; na BWANA Mungu atafuta machozi katika nyuso zote; na aibu ya watu wake ataiondoa katika ulimwengu wote; maana BWANA amenena hayo.” (Isaya 25:8) Hakuna atakayekufa kutokana na sababu za kiasili wala kulia kwa sababu ya kifo cha mpendwa. Ni mabadiliko yenye baraka kama nini! Isitoshe, suto na propaganda ya uwongo, mambo ambayo Mungu na watumishi wake wamevumilia kwa muda mrefu hayatasikika popote duniani. Kwa nini? Kwa sababu Yehova ataondoa mwenye kuyasababisha—baba ya uwongo, Shetani Ibilisi, pamoja na mbegu yote ya Shetani.—Yohana 8:44.

24. Wale wanaotembea katika nuru huitikiaje matendo ya Yehova yenye nguvu anayowafanyia?

24 Baada ya kutafakari udhihirisho huo wa nguvu za Yehova, wale wanaotembea katika nuru wanachochewa kutangaza hivi: “Tazama, huyu ndiye Mungu wetu, ndiye tuliyemngoja atusaidie; huyu ndiye BWANA tuliyemngoja, na tushangilie na kufurahia wokovu wake.” (Isaya 25:9) Karibuni, wanadamu waadilifu watafurahi kwelikweli. Giza litaondoshwa kabisa, nao waaminifu watafurahia nuru ya Yehova kwa umilele. Je, kuna tumaini lingine tukufu kuliko hilo? Kwa kweli hakuna!

Je, Unaweza Kueleleza?

• Kwa nini ni muhimu kutembea katika nuru leo?

• Kwa nini Isaya alihimidi jina la Yehova?

• Kwa nini maadui hawatavunja kamwe uaminifu-maadili wa watu wa Mungu?

• Wale wanaotembea katika nuru watapokea baraka gani kwa wingi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Wakazi wa Yuda walidhabihu watoto kwa Moleki

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kujua matendo makuu ya Yehova kulimchochea Isaya alihimidi jina la Yehova

[Picha katika ukurasa wa 16]

Waadilifu watafurahia nuru ya Yehova milele