Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wokovu kwa Wanaochagua Nuru

Wokovu kwa Wanaochagua Nuru

Wokovu kwa Wanaochagua Nuru

“BWANA ni nuru yangu na wokovu wangu, nimwogope nani?”—ZABURI 27:1.

1. Yehova huandaa mambo gani yenye kuhuisha?

YEHOVA ndiye Chanzo cha nuru ya jua ambayo hutegemeza uhai duniani. (Mwanzo 1:2, 14) Yeye pia ndiye Muumba wa nuru ya kiroho, ambayo huondoa giza linaloweza kuua la ulimwengu wa Shetani. (Isaya 60:2; 2 Wakorintho 4:6; Waefeso 5:8-11; 6:12) Wale wanaochagua nuru wanaweza kujiunga na mtunga-zaburi kusema: “BWANA ni nuru yangu na wokovu wangu, nimwogope nani?” (Zaburi 27:1a) Hata hivyo, kama ilivyokuwa katika siku za Yesu wale wanaopendelea giza wanaweza tu kutarajia hukumu isiyopendeza.—Yohana 1:9-11; 3:19-21, 36.

2. Ni nini kilichowapata watu waliokataa nuru ya Yehova na wale waliosikiliza neno lake katika nyakati za kale?

2 Katika siku za Isaya, watu wengi wa Yehova waliokuwa wamefanya agano naye walikataa nuru. Kwa sababu hiyo, Isaya aliona uharibifu wa ufalme wa kaskazini wa taifa la Israeli. Na katika mwaka wa 607 K.W.K., Yerusalemu na hekalu lake liliharibiwa na wakazi wa Yuda wakapelekwa katika utekwa. Hata hivyo, wale waliosikiliza neno la Yehova waliimarishwa kukinza uasi-imani wa siku hizo. Kuhusu mwaka wa 607 K.W.K., Yehova aliahidi kwamba wale ambao wangemsikiliza wangeokoka. (Yeremia 21:8, 9) Leo, sisi ambao tunapenda nuru twaweza kujifunza mengi kutokana na mambo yaliyotukia wakati huo.—Waefeso 5:5.

Furaha ya Wale Walio Katika Nuru

3. Leo twaweza kuwa na uhakika gani, twapenda ‘taifa gani lenye haki’ na ni ‘mji gani ulio na nguvu’ ambao “taifa” hilo linao?

3 “Sisi tunao mji ulio na nguvu; [Mungu] ataamuru wokovu kuwa kuta na maboma. Wekeni wazi malango yake, taifa lenye haki, lishikalo kweli liingie.” (Isaya 26:1, 2) Hayo ni maneno yenye shangwe ya watu waliomtumaini Yehova. Wayahudi waaminifu katika siku za Isaya walimtegemea Yehova kuwa Chanzo pekee cha usalama wa kweli, wala si miungu isiyo ya kweli ya watu wa nchi yao. Leo, tuna uhakika kama huo. Isitoshe, tunalipenda “taifa lenye haki” la Yehova—“Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16; Mathayo 21:43) Yehova hulipenda pia taifa hili kwa sababu ya mwenendo wake wa uaminifu. Kwa sababu ya baraka zake, Israeli wa Mungu ana “mji ulio na nguvu,” tengenezo lililo kama mji ambalo hutegemeza na kulinda taifa hilo.

4. Yafaa tusitawishe mtazamo gani wa akili?

4 Wale walio ndani ya “mji” huu wanatambua kwamba ‘Yehova atamlinda yeye ambaye moyo wake umemtegemea katika amani kamilifu, kwa kuwa anamtumaini.’ Yehova hutegemeza wale ambao humtumaini na kutii kanuni zake za uadilifu. Hivyo, wale waliokuwa waaminifu huko Yuda walitii himizo hili la Isaya: “Mtumainini BWANA siku zote maana BWANA [“Yah,” NW] YEHOVA ni mwamba wa milele.” (Isaya 26:3, 4; Zaburi 9:10; 37:3; Mithali 3:5) Wale walio na mtazamo huo wa akili humtegemea “BWANA YEHOVA” akiwa ndiye Mwamba pekee ulio salama. Wao hufurahia “amani kamilifu” pamoja naye.—Wafilipi 1:2; 4:6, 7.

Kuaibishwa kwa Maadui wa Mungu

5, 6. (a) Babiloni la kale liliaibishwaje? (b) “Babiloni Mkubwa” aliaibishwa katika njia gani?

5 Namna gani wale wanaomtumaini Yehova wakipatwa na dhiki? Hawahitaji kuogopa. Yehova huruhusu mambo hayo kwa muda, lakini hatimaye huleta kitulizo, naye anawahukumu wale wanaosababisha dhiki hiyo. (2 Wathesalonike 1:4-7; 2 Timotheo 1:8-10) Fikiria hali ya ‘mji fulani ulioinuka.’ Isaya asema: “[Yehova] amewashusha wakaao juu, mji ule ulioinuka, aushusha, aushusha hata nchi, auleta hata mavumbini. Mguu utaukanyaga chini, naam, miguu yao walio maskini, na hatua zao walio wahitaji.” (Isaya 26:5, 6) Labda mji ulioinuka ambao unatajwa hapa ni Babiloni. Bila shaka mji huo ulitaabisha watu wa Mungu. Lakini ni nini kilichoupata Babiloni? Katika mwaka wa 539 K.W.K. ulishindwa na Wamedi na Waajemi. Kulikuwa kutwezwa kulikoje!

6 Katika siku zetu maneno ya kiunabii ya Isaya yafafanua vizuri kile ambacho kimetukia kwa “Babiloni Mkubwa” tangu mwaka wa 1919. Mji huo ulioinuka ulianguka kwa aibu mwaka huo wakati ulipolazimishwa kuwaachilia watu wa Yehova kutoka utekwa wa kiroho. (Ufunuo 14:8) Jambo lililofuatia liliaibisha hata zaidi. Kikundi hicho kidogo cha Wakristo nacho kikaanza kumkanyagia chini mtekaji wao wa awali. Mwaka wa 1922 walianza kutangaza mwisho unaokuja wa Jumuiya ya Wakristo, wakitangaza hadharani ile mipigo ya tarumbeta ya malaika wanne wa Ufunuo 8:7-12 na zile ole tatu zilizotabiriwa katika Ufunuo 9:1–11:15.

“Njia Yake Mwenye Haki Ni Unyofu”

7. Wale wanaogeukia nuru ya Yehova hupata mwongozo gani, nao humtumaini nani na kuthamini nini?

7 Yehova huwaokoa wale wanaogeukia nuru yake, naye huelekeza njia yao, kama Isaya aendeleavyo kuonyesha: “Njia yake mwenye haki ni unyofu; wewe uliye mnyofu wainyosha njia ya mwenye haki. Naam, katika njia ya hukumu zako sisi tumekungoja, Ee BWANA; shauku ya nafsi zetu inaelekea jina lako na ukumbusho wako.” (Isaya 26:7, 8) Yehova ni Mungu mwenye haki, na wale wanaomwabudu lazima watii viwango vyake vya uadilifu. Wanapofanya hivyo, Yehova huwaongoza, na kunyoosha njia yao. Kwa kutii mwelekezo wake, wapole hao huonyesha kwamba wanamtumaini Yehova na kuthamini jina lake—“ukumbusho” wake—kwa moyo wote.—Kutoka 3:15.

8. Isaya alionyesha kielelezo gani cha kuigwa kuhusu mtazamo?

8 Isaya alilipenda jina la Yehova. Hilo laonyeshwa waziwazi na maneno yake yafuatayo: “Kwa nafsi yangu nimekutamani wakati wa usiku; naam, kwa nafsi yangu ndani yangu nitakutafuta mapema; maana hukumu zako zikiwapo duniani, watu wakaao duniani hujifunza haki [“uadilifu,” NW].” (Isaya 26:9) Isaya alimtamani Yehova ‘kwa nafsi yake’ yote. Wazia nabii huyo akitumia wakati wa usiku wenye utulivu kusali kwa Yehova, akimweleza mawazo yake ya ndani zaidi na kutafuta kwa bidii mwongozo wake. Ni kielelezo kizuri kama nini! Isitoshe, Isaya alijifunza uadilifu kutokana na hukumu za Yehova. Kwa njia hiyo, atukumbusha uhitaji wa kuwa macho daima, kuendelea kuwa chonjo ili kufahamu mapenzi ya Yehova.

Wengine Huchagua Giza

9, 10. Yehova alifanya matendo gani ya fadhili kwa taifa lake lisilo na uaminifu, lakini walitendaje?

9 Yehova alionyesha fadhili-upendo kubwa sana kwa Yuda, lakini kwa kusikitisha si wote waliozikubali. Mara nyingi, wengi walichagua uasi-imani badala ya nuru ya kweli ya Yehova. Isaya alisema: “Mtu mbaya ajapofadhiliwa, hata hivyo, hatajifunza haki; katika nchi ya unyofu atatenda udhalimu. Wala hatauona utukufu wa BWANA.”—Isaya 26:10.

10 Katika siku za Isaya Yehova alipolinda Yuda dhidi ya maadui wake, wengi walikataa kutambua jambo hilo. Alipowabariki kwa amani yake, taifa hilo halikuonyesha shukrani. Kwa hiyo, Yehova akawaacha watumikie “mabwana wengine,” hatimaye akaruhusu Wayahudi wapelekwe katika utekwa huko Babiloni mwaka wa 607 K.W.K. (Isaya 26:11-13) Hata hivyo, hatimaye mabaki ya taifa hilo walirudi katika nchi yao wakiwa wametiwa nidhamu.

11, 12. (a) Watekaji wa Yuda walikuwa na tumaini gani? (b) Mwaka wa 1919 watekaji wa awali wa watumishi watiwa-mafuta wa Yehova walikuwa na tumaini gani?

11 Namna gani watekaji wa Yuda? Isaya ajibu kwa kutoa unabii huu: “Wao wamekufa, hawataishi; wamekwisha [“kufa,” NW], hawatafufuka; kwa sababu hiyo umewajilia, na kuwaangamiza, na kuupoteza ukumbusho wao.” (Isaya 26:14) Ndiyo, baada ya anguko lake mwaka wa 539 K.W.K., Babiloni haukuwa na tumaini lolote. Baada ya muda, mji huo haungekuwapo tena. Ungekuwa ‘umekwisha kufa’ nayo milki yake kubwa ingekuwa imetoweka kabisa. Ni onyo lililoje kwa wale wanaotumaini watu wenye nguvu wa ulimwengu huu!

12 Mambo mbalimbali yanayohusu unabii huo yalitimizwa Mungu alipowaruhusu watumishi wake watiwa-mafuta wapelekwe katika utekwa wa kiroho mwaka wa 1918 kisha akawakomboa mwaka wa 1919. Kuanzia wakati huo na kuendelea, mtekaji wao wa awali hasa Jumuiya ya Wakristo, hakuwa na tumaini lolote. Lakini watu wa Yehova wangepata baraka nyingi kwelikweli.

“Umeliongeza Hilo Taifa”

13, 14. Watumishi watiwa-mafuta wa Yehova wamefurahia baraka gani nyingi tangu 1919?

13 Mungu alibariki mtazamo huo wa toba wa watumishi wake watiwa-mafuta katika mwaka wa 1919 na kuwapa ongezeko. Kwanza, walizingatia kukusanywa kwa washiriki wa mwisho wa Israeli wa Mungu, kisha “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” ukaanza kukusanywa. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Baraka hizo zilitabiriwa katika unabii huu wa Isaya: “Umeliongeza hilo taifa, BWANA umeliongeza taifa; wewe umetukuzwa, umeipanua mipaka yote ya nchi hii. BWANA katika taabu zao walikwenda kwako; waliomba maombi mengi wakati adhabu yako ilipokuwa juu yao.”—Isaya 26:15, 16.

14 Leo, mipaka ya Israeli wa Mungu imepanuka na kuenea duniani pote, na umati mkubwa ambao umeongezwa sasa umefikia watu milioni sita wanaoshiriki kwa shangwe kazi ya kuhubiri habari njema. (Mathayo 24:14) Ni baraka iliyoje kutoka kwa Yehova! Hilo huleta utukufu ulioje kwa jina lake! Jina hilo husikiwa leo katika nchi 235—utimizo wa ajabu wa ahadi yake.

15. Ni ufufuo gani wa ufananisho uliotukia mwaka wa 1919?

15 Yuda ilihitaji msaada wa Yehova ili kuponyoka kutoka utekwa wa Babiloni. Hawangeweza kufanya hivyo bila msaada. (Isaya 26:17, 18) Vivyo hivyo, kukombolewa kwa Israeli wa Mungu mwaka wa 1919 kulikuwa ithibati ya utegemezo wa Yehova. Haingeweza kutukia hivyo pasipo msaada wake. Hali yao ilibadilika kwa njia ya kushtusha sana hivi kwamba Isaya aliilinganisha na ufufuo: “Wafu wako wataishi, maiti zangu zitafufuka; amkeni, kaimbeni, nyinyi mnaokaa mavumbini, kwa maana umande wako ni kama umande wa mimea, nayo ardhi itawatoa waliokufa.” (Isaya 26:19; Ufunuo 11:7-11) Naam, wale waliokufa ni kana kwamba watazaliwa tena kwa ajili ya utendaji mpya!

Kulindwa Nyakati za Hatari

16, 17. (a) Katika mwaka wa 539 K.W.K., Wayahudi walihitaji kufanya nini ili kuokoka anguko la Babiloni? (b) Huenda “vyumba vya ndani” vyafananisha nini leo, navyo hutunufaishaje?

16 Watumishi wa Yehova wanahitaji ulinzi wake sikuzote. Hata hivyo, hivi karibuni atanyoosha mkono wake mara ya mwisho dhidi ya ulimwengu wa Shetani, nao waabudu wake watahitaji msaada wake kuliko wakati mwingine wowote. (1 Yohana 5:19) Kuhusu wakati huo wa hatari, Yehova atuonya hivi: “Njoni, watu wangu, ingia wewe ndani ya vyumba vyako [“vyumba vya ndani,” NW], ukafunge mlango nyuma yako ujifiche kitambo kidogo, mpaka ghadhabu hii itakapopita. Kwa maana, tazama, BWANA anakuja kutoka mahali pake, ili kuwaadhibu wakaao duniani, kwa sababu ya uovu wao; ardhi nayo itafunua damu yake, wala haitawafunika tena watu wake waliouawa.” (Isaya 26:20, 21; Sefania 1:14) Onyo hili lilionyesha Wayahudi jinsi ya kuokoka anguko la Babiloni mwaka wa 539 K.W.K. Wale waliotii onyo hilo wangekaa katika nyumba zao, wakiwa salama bila kusumbuliwa na majeshi yenye kushinda yaliyokuwa barabarani.

17 Leo, “vyumba vya ndani” vinavyotajwa katika unabii huo huenda vyafananisha makumi ya maelfu ya makutaniko ya watu wa Yehova ulimwenguni pote. Makutaniko hayo ni ulinzi hata sasa, ni mahali ambapo Wakristo hupata usalama miongoni mwa ndugu zao, chini ya uangalizi wenye upendo wa wazee. (Isaya 32:1, 2; Waebrania 10:24, 25) Ni kweli hasa tunapozingatia jinsi ambavyo mwisho wa mfumo huu wa mambo umekaribia wakati ambapo wokovu utategemea utii.—Sefania 2:3.

18. Yehova ‘atamwuaje yule joka aliye baharini’ hivi karibuni?

18 Kuhusu wakati huo, Isaya atabiri hivi: “Katika siku hiyo BWANA, kwa upanga wake ulio mkali, ulio mkubwa, ulio na nguvu, atamwadhibu lewiathani, nyoka yule mwepesi, na lewiathani, nyoka yule mwenye kuzonga-zonga; naye atamwua yule joka aliye baharini.” (Isaya 27:1) “Lewiathani” wa siku hizi ni nani? Yaonekana, ni “nyoka wa awali,” Shetani mwenyewe, pamoja na mfumo wake mwovu wa mambo, anaotumia kupiga vita dhidi ya Israeli wa Mungu. (Ufunuo 12:9, 10, 17; 13:14, 16, 17) Mwaka wa 1919, Lewiathani alishindwa kuzuia watu wa Mungu. Baada ya muda, atatoweka kabisa. (Ufunuo 19:19-21; 20:1-3, 10) Hivyo, Yehova “atamwua yule joka aliye baharini.” Kwa sasa, chochote ambacho Lewiathani anafanya dhidi ya watu wa Yehova hakitakuwa na mafanikio ya kudumu. (Isaya 54:17) Inafariji kama nini kuhakikishiwa hivyo!

“Shamba la Mizabibu la Mvinyo”

19. Hali ya mabaki ikoje leo?

19 Kwa kuzingatia nuru hii yote kutoka kwa Yehova, je, hatuna kila sababu ya kushangilia? Kwa kweli, ndiyo! Isaya afafanua vizuri shangwe ya watu wa Yehova aandikapo hivi: “Katika siku hiyo; shamba la mizabibu la mvinyo, liimbieni. Mimi, BWANA nalilinda, nitalitia maji kila dakika, asije mtu akaliharibu; usiku na mchana nitalilinda.” (Isaya 27:2, 3) Yehova amelitunza “shamba [lake] la mizabibu” mabaki ya Israeli wa Mungu, na waandamani wao wanaofanya kazi kwa bidii. (Yohana 15:1-8) Matokeo yamekuwa kwamba kumekuwa na matunda yaletayo utukufu kwa jina lake na kufanya watumishi wake duniani washangilie sana.

20. Yehova hulindaje kutaniko la Wakristo?

20 Twaweza kufurahi kwamba hasira ambayo Yehova alikuwa nayo hapo awali dhidi ya watumishi wake watiwa-mafuta—iliyomfanya aruhusu wapelekwe katika utekwa wa kiroho mwaka wa 1918—imekoma. Yehova mwenyewe asema hivi: “Hasira sinayo ndani yangu; kama mibigili na miiba [“magugu,” NW] ingekuwa mbele zangu, ningepanga vita juu yake, ningeiteketeza yote pamoja. Au azishike nguvu zangu, afanye amani nami; naam, afanye amani nami.” (Isaya 27:4, 5) Ili kuhakikisha kwamba shamba lake la mizabibu litaendelea kutoa “mvinyo” kwa wingi, Yehova huvunja-vunja na kuharibu uvutano wowote ulio kama magugu unaoweza kuwapotosha. Kwa hiyo, mtu yeyote asihatarishe hali njema ya kutaniko la Kikristo! Acheni wote ‘wazishike nguvu za Yehova,’ wakitafuta kibali na ulinzi wake. Kwa kufanya hivyo, tutakuwa na amani na Mungu—jambo lililo muhimu sana hivi kwamba Isaya analitaja mara mbili.—Zaburi 85:1, 2, 8; Waroma 5:1.

21. Ni katika njia gani uso wa ulimwengu umejazwa “matunda”?

21 Baraka zaendelea: “Siku zijazo Yakobo atatia mizizi; Israeli atatoa maua na kuchipuka; nao watajaza uso wa ulimwengu matunda.” (Isaya 27:6) Mstari huo umetimizwa tangu 1919, ukionyesha uthibitisho wa ajabu wa nguvu za Yehova. Wakristo watiwa-mafuta wameijaza dunia “matunda,” chakula cha kiroho chenye lishe. Katikati ya ulimwengu mpotovu, wanategemeza kwa shangwe viwango vya Mungu. Naye Yehova anaendelea kuwabariki kwa ongezeko. Kwa sababu hiyo, mamilioni ya waandamani wao, kondoo wengine, “wanamtolea [Mungu] utumishi mtakatifu mchana na usiku.” (Ufunuo 7:15) Acheni tusipuuze kamwe pendeleo kubwa tulilo nalo la kula “matunda” na kuwapa wengine!

22. Wale wanaokubali nuru hupata baraka gani?

22 Katika nyakati hizi zenye hatari, wakati ambapo giza linaifunika dunia na giza kuu kufunika kabila za watu, je, hatushukuru kwamba Yehova anaangazia watu wake nuru ya kiroho? (Isaya 60:2; Waroma 2:19; 13:12) Kwa wote wanaoikubali, nuru hiyo yamaanisha amani ya akili na shangwe sasa na hata uhai udumuo milele wakati ujao. Basi, ni kwa sababu nzuri kwamba sisi ambao tunapenda nuru twainua mioyo yetu kumsifu Yehova na kujiunga na mtunga-zaburi kusema: “BWANA ni ngome ya uzima wangu, nimhofu nani? Umngoje BWANA, uwe hodari, upige moyo konde, naam, umngoje BWANA.”—Zaburi 27:1b, 14.

Je, Wakumbuka?

• Wale wanaowaonea watu wa Yehova, wana tumaini gani?

• Ni ongezeko gani linalotabiriwa katika Isaya?

• Twapaswa kubaki katika ‘vyumba gani vya ndani,’ na kwa nini?

• Kwa nini hali ya watu wa Yehova humletea sifa?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 22]

KICHAPO KIPYA

Habari nyingi ambayo imezungumziwa katika makala hizi mbili za funzo ilitolewa ikiwa hotuba katika programu ya mkusanyiko wa wilaya wa mwaka wa 2000/2001. Mwishoni mwa hotuba, kichapo kipya kilitolewa, chenye kichwa Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote I. Kitabu hiki chenye kurasa 416 kinajadili sura za kwanza 40 za kitabu cha Isaya mstari kwa mstari.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ni waadilifu peke yao wanaoruhusiwa katika “mji [wa Yehova] ulio na nguvu,” tengenezo lake

[Picha katika ukurasa wa 19]

Isaya alimtafuta Yehova “wakati wa usiku”

[Picha katika ukurasa wa 21]

Yehova hulinda “shamba [lake] la mizabibu” na hulifanya lizae matunda