Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kushinda Udhaifu wa Kibinadamu

Kushinda Udhaifu wa Kibinadamu

Kushinda Udhaifu wa Kibinadamu

“Kuweka akili juu ya mwili humaanisha kifo.”—WAROMA 8:6.

1. Watu wengine huuonaje mwili wa binadamu, na ni swali gani linalostahili kuzingatiwa?

“NITAKUSHUKURU kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha.” (Zaburi 139:14) Akaimba mtunga-zaburi Daudi alipokuwa anatafakari juu ya mwili wa binadamu ambao ni mmojawapo wa uumbaji wa Yehova. Badala ya kutoa sifa hiyo ya kweli, walimu fulani wa kidini huuona mwili kuwa mahali dhambi inapojificha, chombo cha dhambi. Umeitwa ‘vazi la ujinga, chanzo cha uovu, maiti iliyo hai, maiti inayotembea.’ Ni kweli vile mtume Paulo alivyosema: “Katika mwili wangu, halikai jambo lolote jema.” (Waroma 7:18) Lakini je, hilo lamaanisha kwamba tumenaswa katika mwili wetu wenye dhambi bila matumaini?

2. (a) “Kuweka akili juu ya mwili” humaanisha nini? (b) Ni mapambano gani kati ya “mwili” na “roho” yanayotukia ndani ya wanadamu wanaotamani kumpendeza Mungu?

2 Mara kwa mara Maandiko hutumia neno “mwili” kurejezea mtu katika hali yake ya kutokamilika akiwa mzao wa Adamu mwasi. (Waefeso 2:3; Zaburi 51:5; Waroma 5:12) Kile tulichorithi kutoka kwa Adamu kimetokeza “udhaifu wa mwili.” (Waroma 6:19) Naye Paulo alionya: “Kuweka akili juu ya mwili humaanisha kifo.” (Waroma 8:6) “Kuweka akili juu ya mwili” humaanisha kuongozwa na kuchochewa na tamaa za mwili wenye dhambi. (1 Yohana 2:16) Kwa hiyo ikiwa tunajitahidi kumpendeza Mungu, kuna mapambano daima kati ya hali yetu ya kiroho na hali yetu yenye dhambi ambayo hutushinikiza bila kukoma tufanye “kazi za mwili.” (Wagalatia 5:17-23; 1 Petro 2:11) Baada ya kueleza mapambano hayo yenye kuumiza yaliyokuwa ndani yake, Paulo alitamka hivi: “Mwenye taabu mimi! Ni nani ataniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?” (Waroma 7:24) Je, Paulo alikuwa mhasiriwa wa kishawishi asiye na kinga? Biblia hujibu kwa mkazo, la!

Uhalisi wa Kishawishi na Dhambi

3. Watu wengi huionaje dhambi na kishawishi, lakini Biblia hutoa onyo gani kuhusu mtazamo kama huo?

3 Dhambi ni dhana isiyokubalika kwa watu wengi leo. Wengine hutumia “dhambi” kiutani kama neno la kizamani la kufafanua dosari ndogondogo za kibinadamu. Hawatambui kwamba “lazima sisi sote tufanywe dhahiri mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, ili kila mmoja apate thawabu yake kwa mambo yaliyofanywa kuupitia mwili, kulingana na mambo ambayo amezoea, kama ni jambo jema au jambo ovu.” (2 Wakorintho 5:10) Huenda wengine wakaonyesha kwamba hawachukui kishawishi kwa uzito. Wengine huishi katika jamii ya watu ambao wanazingatia sana kujitosheleza mara moja, haidhuru ni kwa chakula, ngono, kujifurahisha, au kwa kutimiza jambo fulani. Wanataka kila kitu na wanakitaka sasa hivi! (Luka 15:12) Hawazingatii shangwe ya wakati ujao ya “uhai ulio halisi” bali huzingatia raha ya papo hapo tu. (1 Timotheo 6:19) Hata hivyo, Biblia hutufundisha kufikiria kwa makini na kuzingatia mambo ya wakati ujao, tukiepuka lolote ambalo laweza kutudhuru kiroho au vinginevyo. Mithali moja yenye kupuliziwa yasema: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.”—Mithali 27:12.

4. Paulo alitoa ushauri gani kwenye 1 Wakorintho 10:12, 13?

4 Paulo alipowaandikia Wakristo walioishi Korintho—jiji lililojulikana kwa upotovu wake wa maadili—alitoa onyo la busara dhidi ya kishawishi na nguvu ya dhambi. Alisema: “Acheni yeye ambaye afikiri kuwa amesimama ajihadhari kwamba asianguke. Hakuna kishawishi ambacho kimewapata nyinyi ila kilicho kawaida kwa watu. Lakini Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha nyinyi mshawishwe kupita vile mwezavyo kuhimili, bali pamoja na hicho kishawishi ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kuvumilia hilo.” (1 Wakorintho 10:12, 13) Sisi sote—vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake—hukabili vishawishi vingi shuleni, kazini, au kwingineko. Kwa hiyo, acheni tuchunguze maneno ya Paulo na kuona yanamaanisha nini kwetu.

Usijitumaini Kupita Kiasi

5. Kwa nini ni hatari kujitumaini kupita kiasi?

5 Paulo asema: “Acheni yeye ambaye afikiri kuwa amesimama ajihadhari kwamba asianguke.” Ni hatari kutumaini kupita kiasi nguvu zetu za kiadili. Hilo laonyesha hatuelewi hali na nguvu ya dhambi. Kwa kuwa watu kama Musa, Daudi, Solomoni na mtume Petro walifanya dhambi, je, tuhisi kwamba sisi tu salama? (Hesabu 20:2-13; 2 Samweli 11:1-27; 1 Wafalme 11:1-6; Mathayo 26:69-75) “Mwenye hekima huogopa, akajitenga na uovu; bali mpumbavu ana ufidhuli, na kujitumai,” lasema andiko la Mithali 14:16. Isitoshe, Yesu alisema: “Roho ni yenye hamu, lakini mwili ni dhaifu.” (Mathayo 26:41) Kwa kuwa hakuna mwanadamu asiye mkamilifu ambaye hawezi kudhuriwa na tamaa zilizopotoka, twahitaji kuchukua onyo la Paulo kwa uzito na kukinza kishawishi, la sivyo tutakuwa katika hatari ya kuanguka.—Yeremia 17:9.

6. Yatupasa kujitayarisha lini na jinsi gani kwa ajili ya kishawishi?

6 Ni jambo la hekima kujitayarisha kwa matatizo ambayo huenda yakatokea bila kutarajiwa. Mfalme Asa alitambua kwamba kipindi cha amani ndio wakati uliofaa kwake kuimarisha ulinzi wake. (2 Mambo ya Nyakati 14:2, 6, 7) Alijua kwamba ingekuwa kuchelewa mno kujitayarisha wakati wa shambulio. Vivyo hivyo, maamuzi kuhusu yale tupaswayo kufanya vishawishi vinapotokea hufanywa vizuri zaidi wakati akili imetulia na mazingira ni yenye amani. (Zaburi 63:6) Danieli na marafiki wake wenye kumhofu Mungu walifanya uamuzi wao wa kuwa waaminifu kwa sheria ya Yehova kabla hawajashinikizwa kula vyakula vitamu vya mfalme. Hivyo, walishikilia imani yao, wakakataa kula chakula kisicho safi. (Danieli 1:8) Kabla hali zenye kushawishi hazijatokea, acheni tuimarishe azimio letu la kudumu tukiwa safi kiadili. Ndipo tutakapoweza kukinza dhambi.

7. Kwa nini inafariji kujua kwamba wengine wamefaulu kukinza kishawishi?

7 Tunapata faraja iliyoje kutokana na maneno ya Paulo: “Hakuna kishawishi ambacho kimewapata nyinyi ila kilicho kawaida kwa watu”! (1 Wakorintho 10:13) Mtume Petro aliandika: “Chukueni msimamo wenu dhidi ya [Ibilisi], mkiwa thabiti katika imani, mkijua kwamba mambo yaleyale kwa njia ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zenu katika ulimwengu.” (1 Petro 5:9) Naam, wengine wamekabili vishawishi kama hivyo na kwa msaada wa Mungu wamefaulu kuvikinza, nasi pia twaweza kufanya hivyo. Hata hivyo, tukiwa Wakristo wa kweli tunaoishi katika ulimwengu uliopotoka, sote tunaweza kutarajia kushawishiwa siku moja. Basi, tunawezaje kuwa na hakika kwamba tutashinda udhaifu wa kibinadamu na kishawishi cha kufanya dhambi?

Tunaweza Kukinza Kishawishi!

8. Ni njia ipi rahisi ya kuepuka kishawishi?

8 Njia rahisi ya kuacha “kuwa watumwa wa dhambi” ni kuepuka kishawishi inapowezekana. (Waroma 6:6) Andiko la Mithali 4:14, 15 latusihi: “Usiingie katika njia ya waovu, wala usitembee katika njia ya wabaya. Jiepushe nayo, usipite karibu nayo, igeukie mbali, ukaende zako.” Mara nyingi tunajua kimbele kama hali fulani zingeelekea kutuongoza kwenye dhambi. Kwa hiyo, jambo lifaalo kufanya tukiwa Wakristo ni ‘kwenda zetu,’ tukiepuka yeyote na chochote na mahali popote ambapo panaweza kuamsha tamaa mbaya na kuchochea hisia kali za mapenzi zisizo safi.

9. Kukimbia hali zenye kushawishi kunakaziwaje katika Maandiko?

9 Kukimbia hali yenye kushawishi ni hatua nyingine rahisi ya kushinda kishawishi. Paulo alishauri: “Ukimbieni uasherati.” (1 Wakorintho 6:18) Naye aliandika: “Ikimbieni ibada ya sanamu.” (1 Wakorintho 10:14) Mtume huyo pia alimwonya Timotheo akimbie tamaa inayopita kiasi ya vitu vya kimwili, na vilevile “tamaa zenye kutukia ujanani.”—2 Timotheo 2:22; 1 Timotheo 6:9-11.

10. Ni vielelezo gani viwili vyenye kutofautiana vinavyoonyesha manufaa ya kukimbia kishawishi?

10 Hebu fikiria kisa cha Mfalme Daudi wa Israeli. Alipokuwa akitazama kutoka paa la jumba lake la kifalme, aliona mwanamke mrembo akioga na moyo wake ukajaa tamaa mbaya. Angeondoka kwenye paa hilo na kukimbia kishawishi hicho. Badala yake, aliuliza kuhusu mwanamke huyo—Bathsheba—na matokeo yakawa mabaya sana. (2 Samweli 11:1–12:23) Kwa upande mwingine, Yosefu alitendaje wakati mke mwenye kukosa maadili wa bwana-mkubwa wake alipomsihi alale naye? Simulizi hilo latuambia: “Aliendelea kumshawishi Yosefu siku baada ya siku, lakini Yosefu hakumsikiliza wala kukubali kulala naye kamwe.” Hata bila amri za Sheria ya Kimusa, ambayo haikuwa imetolewa, Yosefu alimjibu kwa kusema: “Nitawezaje basi kufanya uovu mbaya kama huo, na kumkosea Mungu”? Siku moja akamshika, akisema: “Lala na mimi!” Je, Yosefu aliendelea kukaa hapo na kujaribu kusababu naye? La. ‘Alikimbilia nje.’ Yosefu hakuruhusu kishawishi cha kufanya ngono kimshinde. Alikimbia!—Mwanzo 39:7-16, Biblia Habari Njema.

11. Huenda tukafanya nini ikiwa tunakabili kishawishi kinachotokea mara kwa mara?

11 Wakati mwingine kukimbia huonekana kama tendo la woga, lakini mara nyingi kujiondoa kutoka katika hali fulani ndilo jambo la hekima kufanya. Labda tunakabili kishawishi mahali pa kazi ambacho kinatokea mara kwa mara. Ingawa huenda isiwezekane kubadili kazi, kunaweza kuwa na njia nyinginezo za kujiondoa kutoka katika hali zenye kushawishi. Tunahitaji kukimbia chochote tunachojua kuwa hakifai, na kuazimia kufanya tu yale yafaayo. (Amosi 5:15) Kwingineko, kukimbia kishawishi kungemaanisha kuepuka vituo vya ponografia vya Internet na sehemu za vitumbuizo zenye kutilika shaka. Huenda kukimbia kishawishi pia kukamaanisha kuondolea mbali gazeti fulani au kutafuta marafiki wapya—wanaompenda Mungu na wanaoweza kutusaidia. (Mithali 13:20) Litakuwa jambo la hekima kukataa katakata jambo lolote ambalo latushawishi tufanye dhambi.—Waroma 12:9.

Jinsi Sala Iwezavyo Kusaidia

12. Tunamwomba Mungu nini tunaposali: “Usituingize katika kishawishi”?

12 Paulo atoa uhakikisho huu wenye kutia moyo: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha nyinyi mshawishwe kupita vile mwezavyo kuhimili, bali pamoja na hicho kishawishi ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kuvumilia hilo.” (1 Wakorintho 10:13) Njia moja ambayo Yehova hutusaidia ni kwa kujibu sala zetu za kupata msaada wake wa kupambana na kishawishi. Yesu Kristo alitufundisha kusali hivi: “Usituingize katika kishawishi, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.” (Mathayo 6:13) Kwa kujibu sala hiyo ya kutoka moyoni, Yehova hatatuacha tushawishiwe; atatukomboa kutoka kwa Shetani na vitendo vyake vya hila. (Waefeso 6:11, NW, kielezi-chini) Yatupasa kumwomba Mungu atusaidie kutambua vishawishi na kuwa na nguvu za kuvikinza. Tukimsihi asiruhusu tushindwe tunaposhawishiwa, atatusaidia tusidanganywe na “yule mwovu,” Shetani.

13. Tunapaswa kufanya nini tunapokabili kishawishi chenye kuendelea?

13 Tunahitaji hasa kusali kwa bidii tunapokabili kishawishi chenye kuendelea. Vishawishi vingine vinaweza kutokeza mapambano makali sana ya akili, tukipambana na mawazo na mitazamo ambayo hutukumbusha kwa njia yenye kutokeza jinsi tulivyo dhaifu. (Zaburi 51:5) Kwa mfano, twaweza kufanya nini ikiwa tunasumbuliwa na kumbukumbu za zoea fulani potovu la zamani? Namna gani ikiwa tunashawishiwa kulirudia? Badala ya kujaribu tu kuzuia hisia hizo, mjulishe Yehova jambo hilo kupitia sala—tena na tena ikihitajika. (Zaburi 55:22) Kwa nguvu za Neno lake na roho yake takatifu, anaweza kutusaidia kuondoa maelekeo yasiyo safi akilini mwetu.—Zaburi 19:8, 9.

14. Kwa nini sala ni muhimu ili kukabiliana na kishawishi?

14 Alipoona mitume wake wakisinzia katika bustani ya Gethsemane, Yesu aliwasihi: “Fulizeni kulinda na kusali kwa kuendelea, ili msipate kuingia ndani ya jaribu. Bila shaka, roho ni yenye hamu, lakini mwili ni dhaifu.” (Mathayo 26:41) Njia moja ya kushinda kishawishi ni kuwa macho kutambua njia mbalimbali ambazo kishawishi kinaweza kutokea na kujua njia zake zenye hila. Ni muhimu pia kusali bila kukawia kuhusu kishawishi hicho ili tuweze kuwa tayari kiroho kupambana nacho. Kwa kuwa kishawishi hutushambulia sehemu ambazo sisi ni dhaifu zaidi, hatuwezi kukikinza peke yetu. Sala ni muhimu kwa sababu nguvu ambazo Mungu hutoa zaweza kutegemeza kinga yetu dhidi ya Shetani. (Wafilipi 4:6, 7) Huenda pia tukahitaji usaidizi wa kiroho na sala za “wanaume wazee wa kutaniko.”—Yakobo 5:13-18.

Kinza Kishawishi kwa Bidii

15. Ni nini kinachohusika katika kukinza kishawishi?

15 Mbali na kuepuka kishawishi inapowezekana, ni lazima tukikinze kwa bidii hadi kipite au hali ibadilike. Yesu aliposhawishiwa na Shetani, alimkinza hadi Ibilisi akaenda zake. (Mathayo 4:1-11) Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia.” (Yakobo 4:7) Ukinzani unaanza kwa kuimarisha akili yetu kwa Neno la Mungu na kuazimia kwa dhati kwamba tutashikamana na viwango vyake. Tunafanya vema kukariri na kutafakari maandiko muhimu yanayozungumzia udhaifu wetu hususa. Lingekuwa jambo la hekima kutafuta Mkristo mkomavu—labda mzee—ambaye tunaweza kumwambia mahangaiko yetu na ambaye tunaweza kumwomba msaada tunaposhawishiwa kufanya jambo baya.—Mithali 22:17.

16. Tunawezaje kudumu tukiwa wanyofu kiadili?

16 Maandiko yanatusihi tuvae utu mpya. (Waefeso 4:24) Hilo lamaanisha kuruhusu Yehova atufinyange na kutubadili. Alipomwandikia Timotheo mfanyakazi mwenzake, Paulo alisema: “Fuatia uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, tabia-pole. Pigana pigano bora la imani, pata mshiko imara juu ya uhai udumuo milele ambao uliitiwa.” (1 Timotheo 6:11, 12) Tunaweza “kufuatia uadilifu” kwa kusoma Neno la Mungu kwa bidii ili kupata ujuzi kamili wa utu wake, kisha kutenda kupatana na matakwa yake. Ratiba kamili ya utendaji wa Kikristo, kama vile kuhubiri habari njema na kuhudhuria mikutano, ni muhimu pia. Kumkaribia Mungu na kujinufaisha kikamili na maandalizi yake ya kiroho kutatusaidia kukua kiroho na kudumu tukiwa wanyofu kiadili.—Yakobo 4:8.

17. Tunajuaje kwamba Mungu hatatuachilia mbali wakati wa kishawishi?

17 Paulo anatuhakikishia kwamba kishawishi chochote kitupatacho hakitashinda uwezo tuliopewa na Mungu wa kushughulika nacho. Yehova ‘atafanya njia ya kutokea kusudi tuweze kukivumilia.’ (1 Wakorintho 10:13) Naam, Mungu haruhusu kishawishi kiwe chenye kulemea sana hivi kwamba tunakosa nguvu za kiroho za kutosha ili kudumisha uaminifu-maadili wetu ikiwa tunaendelea kumtegemea. Anataka tufaulu kukinza kwa bidii kishawishi cha kufanya yaliyo mabaya machoni pake. Isitoshe, tunaweza kuwa na imani katika ahadi hii yake: “Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote.”—Waebrania 13:5.

18. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika ya kushinda udhaifu wa kibinadamu?

18 Paulo alikuwa na hakika kuhusu matokeo ya pambano lake binafsi dhidi ya udhaifu wa kibinadamu. Hakujiona kuwa mtu wa kusikitikiwa au mtu asiyeweza kushinda tamaa zake za mwili. Kinyume cha hilo, yeye alisema: “Jinsi ninavyokimbia si bila uhakika; jinsi ninavyoelekeza ngumi zangu ni ili nisiwe nikipiga hewa; lakini napiga-piga mwili wangu ngumi na kuuongoza kama mtumwa, ili, baada ya mimi kuwa nimewahubiria wengine, mimi mwenyewe nisiwe mwenye kukataliwa kwa njia fulani.” (1 Wakorintho 9:26, 27) Sisi pia tunaweza kufanya vita kwa mafanikio dhidi ya mwili wetu usio mkamilifu. Kupitia Maandiko, vichapo vinavyotegemea Biblia, mikutano ya Kikristo, na Wakristo wenzetu waliokomaa, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo huandaa vikumbusha daima ambavyo hutusaidia kufuatia mwenendo mnyofu. Kwa msaada wake, tunaweza kushinda udhaifu wa kibinadamu!

Je, Unakumbuka?

• Yamaanisha nini “kuweka akili juu ya mwili”?

• Tunaweza kujitayarishaje kwa ajili ya kishawishi?

• Tunaweza kufanya nini ili kukabiliana na kishawishi?

• Sala hutimiza fungu gani katika kushughulika na kishawishi?

• Tunajuaje kwamba inawezekana kushinda udhaifu wa kibinadamu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Biblia haifundishi kwamba hatuwezi kushinda tamaa za kimwili

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kukimbia kishawishi ni njia moja rahisi ya kuepuka dhambi