Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Habari Njema ya Ufalme Yahusu Nini?

Habari Njema ya Ufalme Yahusu Nini?

Habari Njema ya Ufalme Yahusu Nini?

Mwaka uliopita katika nchi 235 duniani pote, watu 6,035,564, vijana kwa wazee, walitumia muda wa saa 1,171,270,425 kusema na wengine juu ya habari njema. Mbali na kuieneza kwa mdomo, walitangaza na kuieneza kwa vichapo zaidi ya milioni 700. Pia waliitangaza kwa kugawanya maelfu ya kaseti na vidio. Habari hiyo njema yahusu nini?

YAHUSU Ufalme wa Mungu. Kwa kweli, “habari njema hii ya ufalme” imehubiriwa siku hizi kwa kiwango ambacho haijawahi kuhubiriwa katika historia ya wanadamu.—Mathayo 24:14.

Wote wanaofanya kazi hiyo ya kuhubiri na kufundisha ni wajitoleaji. Huenda ulimwengu ukawa na maoni kwamba hawafai kufanya kazi hiyo. Basi, ujasiri na mafanikio yao yanatokana na nini? Ujasiri wao na mafanikio yao hutokana na nguvu ya habari njema, kwa kuwa habari hiyo yahusu baraka ambazo wanadamu watapokea. Baraka hizo zinatamaniwa na watu wote—furaha, maisha yasiyo na magumu ya kifedha, serikali nzuri, amani na usalama, na jambo lingine ambalo walio wengi hata hawawezi kualimini—uhai udumuo milele! Kwa kweli, hiyo ni habari njema kwa watu wanaotaka kujua maana na kusudi la maisha. Naam, ukikubali na kuitikia kwa njia inayofaa kutangazwa kwa habari njema ya Ufalme utaweza kupokea baraka hizo zote na nyingine nyingi.

Ufalme Ni Nini?

Basi Ufalme huo unaotangazwa kuwa habari njema ni nini? Ni ule Ufalme ambao mamilioni ya watu wamefundishwa kuomba uje kwa maneno haya yanayojulikana sana: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe. Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mathayo 6:9, 10.

Ni Ufalme ambao ulitajwa na Danieli, nabii Mwebrania, zaidi ya miaka 2,500 iliyopita alipoandika hivi: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.

Kwa hiyo, habari njema yahusu Ufalme, au serikali, ya Mungu itakayomaliza uovu wote kisha utawale dunia yote kwa amani. Ufalme huo utatimiza kusudi la awali la Muumba kuhusiana na wanadamu na dunia.—Mwanzo 1:28.

“Ufalme wa Mbingu Umekaribia”

Yapata miaka 2,000 iliyopita, habari njema ya Ufalme ilihubiriwa mara ya kwanza na mwanamume mwenye bidii, ambaye alikuwa na sura na tabia zilizovutia fikira za watu. Mwanamume huyo alikuwa Yohana Mbatizaji, mwana wa kuhani Myahudi Zekaria na mke wake Elizabeti. Yohana alivaa nguo za manyoya ya ngamia na mshipi wa ngozi viunoni mwake, kama nabii Eliya, ambaye alikuwa mfano wa kiunabii wa Yohana. Hata hivyo, wengi walivutiwa hasa na ujumbe wake. “Tubuni,” alitangaza, “kwa maana ufalme wa mbingu umekaribia.”—Mathayo 3:1-6.

Wasikilizaji wa Yohana walikuwa Wayahudi waliodai kuwa waabudu wa Mungu wa kweli, Yehova. Taifa hilo lilikuwa limepokea agano la Sheria kupitia Musa miaka 1,500 hivi mapema. Hekalu lenye fahari bado lilikuwapo Yerusalemu, ambamo dhabihu zilitolewa kwa kupatana na Sheria. Wayahudi walikuwa na uhakika kwamba ibada yao ilikubalika mbele za Mungu.

Hata hivyo, walipomsikiliza Yohana baadhi ya watu walianza kutambua kwamba dini yao haikuwa dini ya kweli. Utamaduni na falsafa za Ugiriki zilikuwa zimeingizwa katika mafundisho ya kidini ya Wayahudi. Sheria iliyotolewa na Mungu kupitia Musa ilikuwa imechafuliwa, hata ilikuwa imebatilishwa kwa mafundisho na mapokeo ya wanadamu. (Mathayo 15:6) Watu wengi walikuwa wameacha kuabudu Mungu kwa njia inayofaa, kwa sababu walikuwa wamepotoshwa na viongozi wao wa kidini wakali na wasio na huruma. (Yakobo 1:27) Walihitaji kutubu dhambi zao dhidi ya Mungu na agano la Sheria.

Wakati huohuo, Wayahudi wengi walikuwa wakingoja Mesiya aliyeahidiwa, au Kristo, na baadhi yao wakauliza kuhusu Yohana: “Je, labda yeye ndiye Kristo?” Hata hivyo, Yohana alisema kwamba yeye si Mesiya kisha akawaelekeza kwa mwingine na kusema hivi kumhusu: “Gidamu ya makubazi yake mimi sistahili kufungua.” (Luka 3:15, 16) Alipomjulisha Yesu kwa wanafunzi wake Yohana alitangaza hivi: “Ona, Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu!”—Yohana 1:29.

Kwa hakika hiyo ilikuwa habari njema, kwa sababu Yohana alikuwa akiwaonyesha watu wote njia ya kupata uzima na furaha—Yesu, yule ambaye “huondolea mbali dhambi ya ulimwengu.” Wanadamu wote wamezaliwa chini ya udhalimu wa dhambi na kifo, kwa kuwa wote ni wazao wa Adamu na Hawa. Andiko la Waroma 5:19 laeleza hivi: “Kama vile kupitia kutotii kwa mtu mmoja [Adamu] wengi walifanywa watenda-dhambi, hivyohivyo pia kupitia utii wa mtu mmoja [Yesu] wengi watafanywa waadilifu.” Yesu, kama mwana-kondoo wa dhabihu, alikuja ili ‘aondolee mbali dhambi’ na kubadili kabisa hali zenye kuhuzunisha za wanadamu. Biblia yaeleza kwamba “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uhai udumuo milele kwa njia ya Kristo Yesu Bwana wetu.”—Waroma 6:23.

Kama mwanadamu mkamilifu—mtu mkuu aliyepata kuishi—Yesu alianza kuhubiri habari njema. Simulizi la Biblia katika Marko 1:14, 15 latuambia hivi: “Basi baada ya Yohana kukamatwa Yesu akaenda katika Galilaya, akihubiri habari njema ya Mungu na kusema: ‘Wakati uliowekwa rasmi umetimizwa, na ufalme wa Mungu umekaribia. Iweni wenye kutubu, nyinyi watu, na iweni na imani katika habari njema.’”

Wale waliokubali ujumbe wa Yesu na kudhihirisha imani katika habari njema walibarikiwa sana. Andiko la Yohana 1:12 lasema: “Wengi kadiri ileile waliompokea [Yesu], aliwapa mamlaka ya kuwa watoto wa Mungu, kwa sababu walikuwa wakidhihirisha imani katika jina lake.” Walistahili kupokea zawadi ya uhai udumuo milele, kwa sababu walikuwa watoto, au wana, wa Mungu.—1 Yohana 2:25.

Hata hivyo, pendeleo la kupokea baraka za Ufalme halikuwa la watu wa karne ya kwanza pekee. Kama ilivyotajwa mapema, habari njema ya Ufalme wa Mungu hutangazwa na kufundishwa katika dunia yote inayokaliwa leo. Kwa hiyo, baraka za Ufalme bado zinapatikana. Ni lazima ufanye nini ili upokee baraka hizo? Makala inayofuata itaeleza.