Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

India—“Wenye Umoja Wajapokuwa Tofauti”

India—“Wenye Umoja Wajapokuwa Tofauti”

Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme

India—“Wenye Umoja Wajapokuwa Tofauti”

“WENYE umoja wajapokuwa tofauti” ni usemi unaopendwa na kutumiwa kufafanua umoja nchini India. Si rahisi kuleta umoja katika nchi hiyo yenye utamaduni, lugha, vyakula, koo, mavazi, na dini tofautitofauti. Hata hivyo, umoja huo unapatikana miongoni mwa wajitoleaji wanaofanya kazi katika ofisi ya usimamizi ya Mashahidi wa Yehova nchini India. Wao ni wenyeji wa majimbo na maeneo ya muungano mbalimbali, nao huongea lugha tofautitofauti.

• Kwa mfano, Rajrani ni mwanamke kijana wa sehemu ya kaskazini-magharibi mwa India iitwayo Punjab. Rajrani alipokuwa shuleni, mmoja wa wanafunzi wenzake alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Msichana huyo alijaribu kumvutia Rajrani apendezwe na Biblia. Mwanafunzi huyo alimwomba Rajrani amtafsirie gazeti la Mnara wa Mlinzi, katika Kiingereza, kwa kuwa gazeti hilo halikupatikana katika Kipunjabi wakati huo. Kile ambacho Rajrani alisoma katika gazeti la Mnara wa Mlinzi kilimvutia sana hivi kwamba alifanya maendeleo kufikia kuweka wakfu maisha yake kwa Yehova Mungu ijapokuwa wazazi wake walimpinga. Leo anatumikia kwenye Betheli huko India, akifanya kazi ileile ambayo ilimsaidia kuelewa ukweli. Yeye hutafsiri vichapo vya Kikristo katika Kipunjabi!

• Fikiria pia Bijoe, ambaye ni wa jimbo la India la kusini-magharibi, Kerala. Bijoe alifukuzwa shuleni kwa sababu ya msimamo wake wa kutoshiriki katika sherehe za kizalendo. * Bijoe alirudi shuleni baada ya kesi ya mahakamani iliyochukua muda mrefu kumalizika, ambayo ilileta ushindi mkubwa kwa ibada safi. Alifuatia pia elimu ya chuo. Hata hivyo, aliacha chuo hicho baada ya muhula wa kwanza, kwa maana ukosefu wa maadili chuoni ulisumbua dhamiri yake. Leo, baada ya kutumikia Betheli kwa miaka kumi anaona kwamba amenufaika zaidi kutokana na kuwa mshiriki wa familia ya Betheli yenye umoja ijapokuwa washiriki ni tofauti kwa njia nyingi, kuliko jinsi ambavyo angalifaidika kama angaliendelea kufuatia elimu ya juu.

• Norma na Lily wana umri wa zaidi ya miaka 70, nao wamekuwa wajane kwa miaka mingi. Wote wawili wamekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 40. Lily amefanya kazi kwenye ofisi ya tawi kwa miaka 20 hivi kama mtafsiri wa lugha ya Kitamil. Norma alienda Betheli miaka 13 iliyopita baada ya kufiwa na mume wake. Mbali na kuwa mifano mizuri kwa habari ya kufanya kazi kwa bidii na kwa makini, pia wanachangia umoja katika familia ya Betheli. Wanapenda sana kukaribisha wageni, nao wanafurahia kushirikiana na Wanabetheli wachanga,na kuwaelezea juu ya miaka yao mingi ya maisha ya Kikristo. Nao Wanabetheli wachanga huwakaribisha kwenye vyumba vyao na kuwasaidia wanapohitaji msaada. Wao ni mifano mizuri kama nini!

Wajitoleaji hao wenye furaha wanafanya kazi pamoja kutumikia wengine wakiwa washiriki wa familia ya Betheli ya India yenye umoja maana wameshinda tofauti ambazo husababisha zogo na ugomvi mahali-mahali.—Zaburi 133:1.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Soma gazeti la Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 1987, ukurasa wa 21.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]

Mandharinyuma: Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.