Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unahisi Umeeleweka Vibaya?

Je, Unahisi Umeeleweka Vibaya?

Je, Unahisi Umeeleweka Vibaya?

ANTONIO alikuwa na wasiwasi. Kwa ghafula na bila kumweleza chochote, Leonardo, rafiki yake wa karibu, alianza kuwa na ubaridi kumwelekea. * Mara kwa mara alikosa kuitikia salamu za Antonio. Wakawa hawana ukaribu tena. Antonio alianza kuwa na wasiwasi kwamba lazima awe alifanya au kusema jambo fulani ambalo rafiki yake alikosa kulielewa. Lakini jambo gani?

Kutoelewana ni jambo la kawaida. Kutoelewana kwingi hutokea katika mambo madogo-madogo yawezayo kusuluhishwa kwa urahisi. Kutoelewana kwingine kunaweza kukatisha tamaa, hasa ikiwa mtu anaendelea kuwa na maoni yasiyofaa licha ya jitihada nyingi za kuyaondoa. Kwa nini kutoelewana hutokea? Kunaathirije wanaohusika? Unaweza kufanya nini ikiwa wengine wanakosa kuelewa jambo fulani ufanyalo? Je, kwa kweli unadhuriwa na yale ambayo wengine wanafikiri kukuhusu?

Ukweli Usioweza Kuepukika

Kwa kuwa watu wengine hawawezi kujua mawazo na nia zetu, ipo siku ambapo maneno au matendo yetu yataeleweka vibaya. Kuna uwezekano mkubwa wa kutokea kwa hali ya kutoelewana. Mara kwa mara, sisi hushindwa tu kueleza mawazo yetu kwa njia nzuri na yenye kueleweka. Huenda kelele na vikengeusha fikira vikafanya iwe vigumu kwa wengine kutusikiliza kwa makini.

Njia na tabia fulani pia zaweza kueleweka vibaya. Kwa mfano, huenda mtu mwenye haya akaonekana kimakosa kuwa mwenye ubaridi, asiyejishughulisha na wengine, au mwenye kiburi. Katika hali fulani, huenda mambo yaliyompata mtu wakati uliopita yakafanya atende kwa kuongozwa na hisia-moyo badala ya kuongozwa na kusababu kuzuri. Tofauti za kitamaduni na za kilugha zaweza kufanya iwe vigumu kuelewana. Isitoshe, panapokuwa na ripoti zisizo za kweli na porojo, si ajabu kwamba wakati mwingine mambo yaliyosemwa au kufanywa yataeleweka tofauti na ilivyokusudiwa. Bila shaka, yote hayo hayawafariji wale wanaoona kwamba nia zao zimeeleweka vibaya.

Kwa mfano, Anna alitaja kwa moyo mweupe jinsi rafiki yake, ambaye hakuwepo wakati huo, anavyopendwa na watu wengi. Rafiki yake alielezwa maneno hayo kwa njia isiyofaa, kisha Anna akashangaa na kuudhika wakati rafiki huyo alipomshutumu mbele ya watu kadhaa kwamba alikuwa anamwonea wivu kwa sababu alionyeshwa upendezi na rafiki fulani mwanamume. Maneno ya Anna yalikuwa yameeleweka vibaya kabisa, naye hakufaulu kumhakikishia rafiki yake kwamba hakuwa na nia mbaya. Hali hiyo iliumiza sana, na ilichukua muda mrefu sana kuweza kusuluhisha kabisa kutoelewana huko.

Wengine wanakadiria kufaa kwako kulingana na jinsi wanavyoelewa nia yako. Hivyo, ni kawaida kuudhika watu wanapoelewa kimakosa nia yako. Unaweza kukasirika, ukihisi kwamba hakuna yeyote anayepaswa kukuelewa vibaya. Unaona kwamba wanakadiria kufaa kwako kwa njia ya ubaguzi, kwa kuchambua, au hata kwa kutokukuelewa kabisa, na wanaweza kukuumiza sana—hasa ikiwa wale wanaokadiria kufaa kwako kwa njia isiyofaa ni watu unaothamini maoni yao.

Ingawa unaweza kuudhiwa na jinsi watu wanavyokuona, lakini inafaa kuheshimu maoni ya wengine. Si jambo la Kikristo kupuuza maoni ya wengine, nasi hatungetaka kamwe maneno au matendo yetu yadhuru wengine. (Mathayo 7:12; 1 Wakorintho 8:12) Kwa hiyo, huenda mara kwa mara ukahitaji kujitahidi kurekebisha maoni yasiyofaa ya mtu fulani kukuhusu. Hata hivyo, kuhangaikia mno kupata kibali cha wengine kwaweza kuwa na matokeo yasiyokusudiwa, kukifanya ukose kujistahi au kuhisi umekataliwa na wengine. Lakini jinsi wewe ulivyo kikweli hakutegemei maoni ya wengine.

Kwa upande mwingine, huenda ukatambua kwamba kuna sababu nzuri za kuchambuliwa. Hilo laweza kuumiza pia, lakini ukikubali kasoro zako kwa wepesi na kwa unyofu, uchambuzi huo unaweza kuwa na matokeo yafaayo, na kukuchochea ufanye marekebisho yanayohitajiwa.

Matokeo Yasiyofaa

Huenda kuelewa jambo vibaya kukawa au kusiwe na matokeo mabaya. Kwa mfano, ukimsikia mtu akizungumza kwa sauti kubwa kwenye mkahawa, huenda ukakata kauli kwamba yeye ni mcheshi au ni mwenye majisifu. Huenda ukawa umekosea. Mtu anayezungumza naye anaweza kuwa na tatizo la kusikia. Au labda unaona kana kwamba muuza-duka ni mtu asiye na urafiki, lakini huenda akawa hajisikii vizuri. Japo hali hiyo ya kutoelewa jambo vizuri hutokeza maoni mabaya, yaelekea haitakuwa na matokeo mabaya au yenye kudumu. Hata hivyo, wakati mwingine kutoelewana kwaweza kuchochea maafa. Fikiria matukio mawili katika historia ya Israeli la kale.

Wakati Nahashi mfalme wa Amoni alipokufa, Daudi alituma wajumbe wakamfariji mwanawe, Hanuni, aliyechukua utawala baada ya babake. Hata hivyo, ziara ya wajumbe hao ilieleweka vibaya kuwa upelelezi wenye uhasama wa nchi ya Waamoni, jambo lililomfanya Hanuni awafedheheshe wajumbe hao, kisha akaanzisha vita na Israeli. Matokeo yalikuwa kwamba watu 47,000 walikufa—kwa sababu tu nia iliyokuwa nzuri ilieleweka vibaya.—1 Mambo ya Nyakati 19:1-19.

Mapema katika historia ya Israeli, kutoelewana kwingine kulisuluhishwa kwa njia tofauti. Makabila ya Reubeni na Gadi na nusu ya kabila la Manase walijenga madhabahu yenye kuonekana waziwazi kando ya Mto Yordani. Waisraeli wale wengine waliona jambo hilo kuwa tendo la kukosa imani, uasi dhidi ya Yehova. Kwa hiyo wakajikusanya ili wapigane nao. Kabla ya kuchukua hatua yoyote kubwa, Waisraeli hao walituma wajumbe kulalamikia tendo ambalo waliliona kuwa ukosefu wa uaminifu. Walifanya vizuri kuchukua hatua hiyo, kwa kuwa wajenzi wa madhabahu hiyo waliwaeleza kwamba hawakuwa na nia ya kuacha ibada safi. Kinyume cha hilo, madhabahu hiyo ingekuwa ukumbusho wa uaminifu wao kwa Yehova. Kutoelewana huko kungeweza kusababisha mauaji ya watu wengi, lakini kutumia hekima kulizuia matokeo ambayo yangekuwa mabaya.—Yoshua 22:10-34.

Eleza Mambo Wazi kwa Roho ya Upendo

Tunajifunza jambo fulani kwa kulinganisha masimulizi hayo. Bila shaka ni jambo la hekima kueleza jambo vizuri. Ni nani ajuaye ni watu wangapi waliookoka katika tukio tulilozungumzia mwisho, kwa sababu tu watu pande zote mbili walizungumza? Katika visa vingi, huenda kutojua nia ya mtu hasa kusihatarishe maisha, lakini urafiki unaweza kuhatarishwa. Kwa hiyo, ukihisi kwamba mtu fulani amekutendea isivyofaa, je, una hakika kwamba unaelewa hali ilivyo hasa, au unaielewa vibaya? Yule mwingine alikuwa na nia gani? Mwulize. Je, unahisi ulieleweka vibaya? Zungumzia jambo hilo. Usiache kiburi kikuzuie.

Yesu alitoa kichocheo kizuri cha kusuluhisha kutoelewana: “Basi, ikiwa wewe unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na huko wakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, toa zawadi yako.” (Mathayo 5:23, 24) Hivyo, inafaa kuzungumza na mtu huyo faraghani, bila kuhusisha wengine. Mambo yatakuwa mabaya hata zaidi ikiwa aliyekukosea atasikia malalamiko yako kwanza kutoka kwa mtu mwingine. (Mithali 17:9) Lengo lako lapasa kuwa kutafuta amani kwa roho ya upendo. Kwa utulivu, eleza tatizo hilo waziwazi na kwa maneno sahili yasiyoshutumu. Eleza jinsi hali hiyo inavyokufanya uhisi. Kisha kwa unyofu usikilize maoni ya yule mwingine. Usiwe mwepesi wa kufikiria wengine vibaya. Uwe tayari kutumaini kwamba yule mwingine hakuwa na nia mbaya. Kumbuka, upendo “huamini mambo yote.”—1 Wakorintho 13:7.

Bila shaka, hata wakati ambapo kutoelewana kumesuluhishwa, huenda bado mtu akaumia kihisia au kukawa na matokeo mabaya yenye kudumu. Tunaweza kufanya nini? Inapohitajika, inafaa kuomba msamaha kwa unyofu, na vilevile kuchukua hatua nyingine yoyote ifaayo ambayo yaweza kusuluhisha kutoelewana huko. Katika hali hizo zote, mtu aliyekosewa anapaswa kufuata ushauri huu uliopuliziwa: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kwa hiari, fanyeni hivyo nyinyi pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni wenyewe upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:13, 14; 1 Petro 4:8.

Maadamu sisi ni watu wasio wakamilifu, kutakuwa na kutoelewana na kuumia hisia. Mtu yeyote anaweza kukosea au kusema bila kujali wengine au kuwaonyesha fadhili. Biblia inasema: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyu ni mtu mkamilifu, awezaye kuuongoza kwa hatamu mwili wake wote pia.” (Yakobo 3:2) Kwa kuwa Yehova Mungu anajua jambo hilo, ametutolea maagizo haya: “Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako, maana hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu. Tena, usitie moyoni mwako maneno yote yaliyosemwa; usije ukamsikia mtumwa wako mwenyewe ali anakutukana. Kwa kuwa mara nyingi moyo wako pia unajua ya kwamba wewe mwenyewe umewatukana watu wengine.”—Mhubiri 7:9, 21, 22.

“BWANA Huipima Mioyo”

Namna gani ikionekana kana kwamba haiwezekani kurekebisha maoni mabaya ya mtu kukuhusu? Usikate tamaa. Endelea kusitawisha sifa za Kikristo kadiri uwezavyo. Mwombe Yehova akusaidie kufanya maendeleo sehemu unayohitaji kufanyia maendeleo. Jinsi ulivyo kikweli haiamuliwi hasa na watu wengine. Yehova pekee ndiye awezaye ‘kuipima mioyo’ kwa usahihi. (Mithali 21:2) Hata watu hawakumwona Yesu kuwa mtu wa maana nao walimdharau, lakini jambo hilo halikuathiri jinsi Yehova alivyomwona. (Isaya 53:3) Ingawa huenda wengine wakakuona isivyofaa, unaweza ‘kufunua moyo wako’ mbele za Yehova, ukiwa na hakika kwamba anakuelewa, “[kwa kuwa] BWANA haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” (Zaburi 62:8; 1 Samweli 16:7) Ukiendelea kufanya yaliyo mema, huenda hatimaye wale walio na maoni mabaya kukuhusu wakatambua makosa yao na kubadili maoni yao.—Wagalatia 6:9; 2 Timotheo 2:15.

Je, unamkumbuka Antonio, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii? Alipiga moyo konde kufuata ushauri wa Maandiko, ndipo akazungumza na rafiki yake Leonardo, akamwuliza ni nini alichofanya kikamwudhi. Matokeo yakawaje? Leonardo alishangaa sana. Alimwambia Antonio kwamba hakuwa amefanya jambo lolote lenye kumwudhi kisha akamhakikishia kwamba hakukusudia kuwa tofauti na alivyokuwa hapo awali. Kama alionekana mwenye ubaridi, labda alikuwa tu na mawazo mengi. Leonardo aliomba msamaha kwamba alikuwa ameumiza hisia za rafiki yake bila kujua na kumshukuru kwa kumjulisha jambo hilo. Aliongeza kusema kwamba wakati ujao, atakuwa mwangalifu zaidi ili wengine wasiwe na maoni kama hayo kumhusu. Kutoelewana kati yao kukaisha, na marafiki hao wawili wakawa na ukaribu hata zaidi.

Haifurahishi kuhisi umeeleweka vibaya. Hata hivyo, ukifanya yote uwezayo ili kueleza mambo wazi na kutumia kanuni za Kimaandiko za upendo na kusamehe, yaelekea sana kwamba hata wewe utapata matokeo mazuri kama hayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Majina fulani yamebadilishwa katika makala hii.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kueleza mambo wazi kwa roho ya upendo na kusamehe kwaweza kuwa na matokeo yenye furaha