Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Neno la Yehova Likaendelea Kukua”

“Neno la Yehova Likaendelea Kukua”

“Neno la Yehova Likaendelea Kukua”

“Huipeleka amri yake juu ya nchi, neno lake lapiga mbio sana.”—ZABURI 147:15.

1, 2. Yesu aliwapa wanafunzi wake mgawo gani, nao ulihusisha nini?

MOJAWAPO ya unabii wenye kushangaza zaidi katika Biblia wapatikana kwenye Matendo 1:8. Muda mfupi kabla hajapaa mbinguni, Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake waaminifu: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu iwasilipo juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” Hiyo ingekuwa kazi kubwa mno kama nini!

2 Lazima wanafunzi hao wachache waliopokea mgawo wa kutangaza neno la Mungu duniani pote wawe waliuona kuwa mgumu. Fikiria mambo yaliyohusika. Iliwabidi kuwasaidia watu waelewe habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Kutoa ushahidi juu ya Yesu kulihitaji pia wajulishe wengine mafundisho yake yenye nguvu na kuwaeleza daraka lake katika kusudi la Yehova. Isitoshe, kazi hiyo ilitia ndani kufanya watu wawe wanafunzi na kuwabatiza. Na kazi hiyo ingefanywa ulimwenguni pote!—Mathayo 28:19, 20.

3. Yesu aliwahakikishia nini wafuasi wake, nao walifanyaje kazi waliyopewa?

3 Hata hivyo, Yesu aliwahakikishia wafuasi wake kwamba roho takatifu ingekuwa pamoja nao wanapofanya kazi aliyowapa. Hivyo, licha ya mgawo huo kuwa mkubwa na pia jitihada kali za wapinzani za kujaribu kuwanyamazisha, wanafunzi wa mapema wa Yesu walifaulu kufanya kazi waliyoagizwa. Hilo ni jambo hakika lililoandikwa ambalo haliwezi kukanushwa.

4. Upendo wa Mungu ulidhihirikaje katika agizo la kuhubiri na kufundisha wengine?

4 Kampeni inayofanywa ulimwenguni pote ya kuhubiri na kufundisha ilikuwa wonyesho wa upendo wa Mungu kwa wale wasiomjua. Iliwapa fursa ya kumkaribia Yehova na kupata msamaha wa dhambi. (Matendo 26:18) Agizo la kuhubiri na kufundisha lilidhihirisha pia upendo wa Mungu kwa wale wanaotoa ujumbe huo, kwa kuwa liliwawezesha kuonyesha ujitoaji wao kwa Yehova na kuwaonyesha upendo wanadamu wenzao. (Mathayo 22:37-39) Mtume Paulo alithamini sana huduma ya Kikristo hivi kwamba aliiita “hazina.”—2 Wakorintho 4:7.

5. (a) Ni wapi tupatapo historia yenye kutegemeka zaidi kuhusu Wakristo wa mapema, nayo hueleza ukuzi gani? (b) Kwa nini kitabu cha Matendo ni muhimu kwa watumishi wa Mungu leo?

5 Historia yenye kutegemeka zaidi kuhusu kazi ya kuhubiri iliyofanywa na Wakristo wa mapema yapatikana katika kitabu kilichopuliziwa cha Matendo, ambacho kiliandikwa na mwanafunzi Luka. Kinaonyesha ukuzi wa kushangaza na wa haraka. Ukuzi huo wa ujuzi wa Neno la Mungu watukumbusha andiko la Zaburi 147:15, linalosema: “[Yehova] huipeleka amri yake juu ya nchi, neno lake lapiga mbio sana.” Simulizi juu ya Wakristo wa mapema, waliotiwa nguvu na roho takatifu, ni lenye kuvutia na lenye umuhimu mkubwa kwetu leo. Mashahidi wa Yehova hufanya kazi hiyohiyo ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, lakini kwa kiwango kikubwa zaidi. Pia twakabili matatizo sawa na yale waliyokabili Wakristo katika karne ya kwanza. Tunapochunguza jinsi Yehova alivyowabariki na kuwatia nguvu Wakristo wa mapema, imani yetu kwamba anatutegemeza inaimarishwa.

Ongezeko la Idadi ya Wanafunzi

6. Ni fungu gani la maneno linalohusiana na ukuzi ambalo hupatikana mara tatu katika kitabu cha Matendo, nalo hurejezea nini?

6 Njia moja ya kuchunguza utimizo wa Matendo 1:8 ni kufikiria usemi “neno la Yehova likaendelea kukua.” Fungu hili la maneno limetumiwa mara tatu tu katika Biblia, kwa kubadilishwa-badilishwa kidogo, kwenye kitabu cha Matendo peke yake. (Matendo 6:7; 12:24; 19:20) “Neno la Yehova,” au “neno la Mungu,” katika maandiko hayo larejezea habari njema—ujumbe wa kusisimua wa kweli ya Mungu, ujumbe wenye nguvu sana ambao ulibadili maisha ya wale walioukubali.—Waebrania 4:12.

7. Ukuzi wa neno la Mungu wahusianishwa na nini kwenye Matendo 6:7, na ni nini kilichotukia siku ya Pentekoste 33 W.K.?

7 Ukuzi wa neno la Mungu warejezewa kwa mara ya kwanza kwenye Matendo 6:7. Twasoma hivi katika andiko hilo: “Kwa sababu hiyo neno la Mungu likaendelea kukua, na idadi ya wanafunzi ikafuliza kuzidi sana katika Yerusalemu; na umati mkubwa wa makuhani ukaanza kuwa mtiifu kwa imani.” Hapa, ukuzi wahusianishwa na ongezeko la idadi ya wanafunzi. Mapema, katika siku ya Pentekoste 33 W.K., roho takatifu ya Mungu ilimwagwa juu ya wanafunzi wapatao 120 waliokusanyika katika chumba cha juu. Kisha mtume Petro akatoa hotuba yenye kusisimua, na watu wapatao 3,000, kati ya wale waliosikiliza, wakawa waamini siku hiyohiyo. Lazima kulitokea hekaheka nyingi kama nini maelfu ya watu walipoelekea kwenye kidimbwi au vidimbwi vilivyokuwa Yerusalemu na karibu na jiji hilo ili wabatizwe katika jina la Yesu, mtu aliyekuwa ametundikwa mtini kama mhalifu siku 50 zilizotangulia!—Matendo 2:41.

8. Idadi ya wanafunzi iliongezekaje katika miaka ya baada ya Pentekoste 33 W.K.?

8 Bila shaka, huo ulikuwa mwanzo tu. Jitihada kabambe za viongozi wa dini ya Kiyahudi za kukomesha kazi ya kuhubiri hazikufanikiwa. Viongozi hao walivunjika moyo sana kwa kuwa, “Yehova a[li]endelea kuongeza kwao [wanafunzi] kila siku wale wenye kuokolewa.” (Matendo 2:47) Punde si punde, “idadi ya wanaume ikawa karibu elfu tano.” Baada ya hapo, “waamini katika Bwana wakafuliza kuwa wakiongezwa, umati wa wanaume na pia wa wanawake.” (Matendo 4:4; 5:14) Katika pindi nyingine baadaye, twasoma hivi: “Kwa kweli, kutaniko kotekote katika Yudea na Galilaya na Samaria likaingia katika kipindi cha amani, likijengwa; nalo lilipokuwa likitembea katika hofu ya Yehova na katika faraja ya roho takatifu likafuliza kuzidi.” (Matendo 9:31) Miaka kadhaa baadaye, labda mwaka wa 58 W.K. hivi, andiko lilirejezea “maelfu mengi ya waamini.” (Matendo 21:20) Kufikia wakati huo, kulikuweko pia waamini wengi wa watu wasio Wayahudi.

9. Ungewafafanuaje Wakristo wa mapema?

9 Ongezeko la idadi ya wanafunzi lilitokana hasa na watu wapya waliogeuzwa imani. Dini hiyo ilikuwa mpya—lakini ilitenda kwa bidii. Badala ya kuwa washiriki wa kanisa wasiotenda, wanafunzi walikuwa wamejitoa kikamili kwa Yehova na Neno lake, nyakati nyingine wakiwa wamejifunza kweli kutoka kwa wale walionyanyaswa vikali. (Matendo 16:23, 26-33) Wale walioukubali Ukristo walifanya hivyo baada ya kufikiria kwa makini uamuzi wao ambao ulitegemea ujuzi. (Waroma 12:1) Walifundishwa katika njia za Mungu; kweli ilikuwa katika akili na mioyo yao. (Waebrania 8:10, 11) Walikuwa tayari kufa kwa ajili ya imani yao.—Matendo 7:51-60.

10. Wakristo wa mapema walikubali daraka gani, na twaona ulinganisho gani leo?

10 Wale waliokubali mafundisho ya Kikristo walitambua daraka lao la kuwaelezea wengine ile kweli. Jambo hilo lilichangia moja kwa moja ongezeko la idadi ya wanafunzi. Msomi mmoja wa Biblia alisema hivi: “Kueneza imani hakukuonwa kuwa haki ya wale wenye bidii peke yao au ya waeneza-evanjeli waliowekwa rasmi. Kueneza-evanjeli kulikuwa haki na daraka la kila mshiriki wa Kanisa. . . . Jitihada za Wakristo wote kwa ujumla zilichochea sana kuenea kwa Ukristo tangu pale mwanzo.” Aliongezea kuandika hivi: “Kueneza-evanjeli kulikuwa muhimu kabisa kwa Wakristo wa mapema.” Ndivyo ilivyo na Wakristo wa kweli leo.

Maeneo Yaongezeka

11. Ni ukuzi gani unaoelezwa kwenye Matendo 12:24, nao ulitukiaje?

11 Ukuzi wa neno la Mungu warejezewa mara ya pili kwenye Matendo 12:24: “Neno la Yehova likaendelea kukua na kusambaa.” Hapa fungu hilo la maneno lahusianishwa na ongezeko la maeneo yaliyohubiriwa. Licha ya upinzani wa serikali, kazi iliendelea kusitawi. Roho takatifu ilimwagwa kwanza Yerusalemu, na tokea hapo neno likasambaa haraka. Mnyanyaso huko Yerusalemu ulitawanya wanafunzi kwenda maeneo mbalimbali kotekote katika Yudea na Samaria. Matokeo yakawaje? “Wale waliokuwa wametawanywa walipita katika nchi wakitangaza habari njema ya lile neno.” (Matendo 8:1, 4) Filipo alielekezwa akamtolee ushahidi mwanamume mmoja ambaye, baada ya kubatizwa, alipeleka ujumbe hadi Ethiopia. (Matendo 8:26-28, 38, 39) Upesi kweli ilisitawi katika Lida, Uwanda wa Sharoni, na Yopa. (Matendo 9:35, 42) Baadaye, mtume Paulo alisafiri maelfu ya kilometa baharini na katika nchi kavu, akianzisha makutaniko kotekote katika nchi nyingi za Mediterania. Mtume Petro alienda Babiloni. (1 Petro 5:13) Miaka 30 baada ya roho takatifu kumwagwa siku ya Pentekoste, Paulo aliandika kwamba habari njema ilikuwa ‘imehubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu,’ labda akirejezea ulimwengu uliojulikana wakati huo.—Wakolosai 1:23.

12. Wapinzani wa Ukristo walikiri nini kuhusu ukuzi wa neno la Mungu katika maeneo mbalimbali?

12 Hata wapinzani wa Ukristo walikiri kwamba neno la Mungu lilikuwa limesitawi kotekote katika Milki ya Roma. Kwa mfano, andiko la Matendo 17:6 lasema kwamba katika Thesalonike, kaskazini mwa Ugiriki, wapinzani walipaaza sauti kwa kusema: “Watu hawa ambao wamepindua dunia inayokaliwa wako hapa pia.” Isitoshe, mwanzoni mwa karne ya pili, Pliny Mchanga akiwa Bithinia, alimwandikia barua Maliki Mroma Trajan kuhusu Ukristo. Alilalamika hivi: “[Haupo] mijini tu, lakini umesambaza upotovu wake katika vijiji na nchi jirani.”

13. Upendo wa Mungu kwa wanadamu ulidhihirikaje kuhusiana na ukuzi katika maeneo mbalimbali?

13 Ukuzi katika maeneo mbalimbali ulikuwa udhihirisho wa upendo mwingi wa Yehova kwa wanadamu wanaoweza kukombolewa. Petro alipoona roho takatifu ikijidhihirisha kwa Kornelio mtu asiye Myahudi, alisema hivi: “Kwa hakika nahisi kwamba Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Naam, habari njema zilikuwa ujumbe kwa watu wote na zingali hivyo hata sasa, na ukuzi wa neno la Mungu katika maeneo mbalimbali uliwapa watu kila mahali fursa ya kuitikia upendo wa Mungu. Katika karne hii ya 21, neno la Mungu limesambaa karibu sehemu zote za dunia.

Ukuzi Ulioshinda

14. Ni ukuzi wa aina gani unaofafanuliwa kwenye Matendo 19:20, na neno la Mungu lilishinda mambo gani?

14 Ukuzi wa neno la Mungu warejezewa mara ya tatu kwenye Matendo 19:20: “Katika njia yenye uweza neno la Yehova likafuliza kukua na kuweza,” (au kushinda). Neno la awali la Kigiriki lililotafsiriwa “kuweza” ladokeza wazo la “kutumia nguvu.” Mistari inayotangulia yasema kwamba wengi katika Efeso wakawa waamini, na watu kadhaa waliozoea ufundi wa mizungu wakachoma vitabu vyao mbele ya watu wote. Hivyo, neno la Mungu lilishinda imani zote za dini zisizo za kweli. Habari njema pia zilishinda vizuizi vingine, kama vile mnyanyaso. Hakuna kitu ambacho kingeweza kuzuia habari njema. Jambo hilo lafanana kwa njia yenye kutokeza na Ukristo wa kweli leo.

15. (a) Mwanahistoria mmoja wa Biblia aliandika nini kuhusu Wakristo wa mapema? (b) Wanafunzi walimpa nani sifa kwa mafanikio waliyopata?

15 Mitume na Wakristo wengine wa mapema walitangaza neno la Mungu kwa bidii. Mwanahistoria mmoja wa Biblia alisema hivi kuwahusu: “Watu wanapokuwa na nia ya kuzungumza juu ya Bwana wao, wanapata njia nyingi za kufanya hivyo. Kwa kweli, twavutiwa zaidi na kichocheo cha wanaume na wanawake hao kuliko njia walizotumia.” Hata hivyo, Wakristo hao wa mapema walitambua kwamba ili wafanikiwe katika huduma walihitaji mengi zaidi ya jitihada yao. Waliagizwa na Mungu kutekeleza kazi yao, na walipata utegemezo wake ili kuitimiza. Ukuzi wa kiroho hutoka kwa Mungu. Mtume Paulo alikiri jambo hilo katika barua yake kwa kutaniko la Korintho. Aliandika hivi: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji, lakini Mungu akafuliza kuikuza. Kwa maana sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu.”—1 Wakorintho 3:6, 9.

Roho Takatifu Ikitenda

16. Ni nini kinachoonyesha kwamba roho takatifu iliwatia nguvu wanafunzi kusema kwa ujasiri?

16 Kumbuka kwamba Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba roho takatifu ingetimiza fungu fulani katika ukuzi wa neno la Mungu na ingewatia nguvu wanafunzi wake katika kazi yao ya kuhubiri. (Matendo 1:8) Jambo hilo lilitukiaje? Muda mfupi baada ya roho takatifu kumwagwa juu ya mitume kwenye Pentekoste, Petro na Yohana waliitwa mbele ya Sanhedrini ya Wayahudi, mahakama kuu zaidi ya nchi, ambayo mahakimu wake walikuwa na hatia ya kumwua Yesu Kristo. Je, mitume wangetetemeka kwa hofu wakiwa mbele ya kusanyiko hilo mashuhuri na lenye uhasama? Sivyo kamwe! Roho takatifu ilimtia nguvu Petro na Yohana kusema kwa ujasiri hivi kwamba wapinzani wao walishangaa sana, “wakaanza kutambua juu yao kwamba walikuwa na kawaida ya kuwa pamoja na Yesu.” (Matendo 4:8, 13) Roho takatifu ilimwezesha Stefano pia atoe ushahidi kwa ujasiri mbele ya Sanhedrini. (Matendo 6:12; 7:55, 56) Mapema kidogo, roho takatifu ilikuwa imewachochea wanafunzi wahubiri kwa ujasiri. Luka aripoti hivi: “Walipokuwa wameomba dua, hapo mahali walipokuwa wamekusanyika pamoja pakatikiswa; nao wote wakajazwa roho takatifu na wakawa wakisema neno la Mungu kwa ujasiri.”—Matendo 4:31.

17. Roho takatifu ilisaidia wanafunzi katika huduma yao katika njia gani nyingine?

17 Kupitia roho yake takatifu yenye nguvu, Yehova pamoja na Yesu aliyefufuliwa, walielekeza kazi ya kuhubiri. (Yohana 14:28; 15:26) Roho takatifu ilipomwagwa juu ya Kornelio, jamaa zake, na marafiki wake wa karibu, mtume Petro alitambua kwamba watu wasio Wayahudi ambao hawakuwa wametahiriwa wangeweza kustahili kubatizwa katika jina la Yesu Kristo. (Matendo 10:24, 44-48) Baadaye, roho takatifu ilitimiza fungu muhimu la kumweka rasmi Barnaba na Sauli (mtume Paulo) wawe mishonari na kuwaelekeza mahali walipopaswa kwenda na wasipopaswa kwenda. (Matendo 13:2, 4; 16:6, 7) Ilielekeza mitume na wanaume wazee waliokuwa Yerusalemu kufanya maamuzi. (Matendo 15:23, 28, 29) Roho takatifu iliongoza pia kuwekwa rasmi kwa waangalizi katika kutaniko la Kikristo.—Matendo 20:28.

18. Wakristo wa mapema walionyeshaje upendo?

18 Kwa kuongezea, roho takatifu ilijidhihirisha katika Wakristo wenyewe, na kutokeza sifa za kimungu, kama vile upendo. (Wagalatia 5:22, 23) Upendo uliwachochea Wakristo kushiriki vitu pamoja. Kwa mfano, baada ya Pentekoste ya 33 W.K., hazina ya pamoja ilianzishwa ili kushughulikia mahitaji ya kimwili ya wanafunzi waliokuwa Yerusalemu. Simulizi la Biblia lasema hivi: “Hapakuwa hata mmoja mwenye uhitaji miongoni mwao; kwa maana wote wale waliokuwa wenye kumiliki mashamba au nyumba walikuwa wakiviuza na kuleta thamani za vitu vilivyouzwa nao walikuwa wakiziweka kwenye miguu ya mitume. Nao ugawanyaji ulikuwa ukifanywa kwa kila mmoja, kama vile alivyokuwa na uhitaji.” (Matendo 4:34, 35) Walionyesha upendo kwa Wakristo wenzao na pia watu wengineo kwa kuwaeleza habari njema na kwa kuwaonyesha fadhili kwa njia mbalimbali. (Matendo 28:8, 9) Yesu alisema kwamba upendo wa kujidhabihu ungewatambulisha wafuasi wake. (Yohana 13:34, 35) Bila shaka sifa muhimu ya upendo iliwavuta watu kwa Mungu na kuchangia ukuzi katika karne ya kwanza sawa na inavyochangia ukuzi leo.—Mathayo 5:14, 16.

19. (a) Ni katika njia gani tatu neno la Yehova lilikua katika karne ya kwanza? (b) Tutachunguza nini katika makala ifuatayo?

19 Kwa ujumla, usemi “roho takatifu” wapatikana mara 41 katika kitabu cha Matendo. Kwa wazi, ukuzi halisi wa Kikristo katika karne ya kwanza ulihusiana sana na nguvu na mwongozo wa roho takatifu. Idadi ya wanafunzi iliongezeka, neno la Mungu likasambaa katika sehemu kubwa, na kushinda dini na falsafa za pindi hiyo. Ukuzi huo wa karne ya kwanza walingana na kazi ya Mashahidi wa Yehova leo. Katika makala ifuatayo, tutachunguza ukuzi wa neno la Mungu unaofanana na huo na wenye kuvutia siku za leo.

Je, Unakumbuka?

• Idadi ya wanafunzi wa mapema iliongezekaje?

• Ni katika njia gani neno la Mungu lilikua katika maeneo mbalimbali?

• Neno la Mungu lilishindaje katika karne ya kwanza?

• Roho takatifu ilitimiza fungu gani kuhusiana na ukuzi wa neno la Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Filipo alimhubiria Mwethiopia, na kusambaza habari njema katika maeneo mbalimbali

[Picha katika ukurasa wa 13]

Roho takatifu ilielekeza mitume na wanaume wazee waliokuwa Yerusalemu

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]

Juu kulia: Reproduction of the City of Jerusalem at the time of the Second Temple - located on the grounds of the Holyland Hotel, Jerusalem