Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tulishirikiana

Tulishirikiana

Simulizi la Maisha

Tulishirikiana

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MELBA BARRY

Mnamo Julai 2, 1999, mimi na mume wangu tulikuwa tumehudhuria kusanyiko kubwa la Mashahidi wa Yehova, kama tulivyokuwa tumefanya mara nyingi katika miaka 57 tangu tuoane. Ijumaa hiyo, Lloyd alikuwa akitoa hotuba ya mwisho kwenye mkusanyiko wa wilaya huko Hawaii. Kwa ghafula akaanguka. Licha ya jitihada nyingi za kumhuisha, akafa. *

NAWATHAMINI sana kama nini ndugu na dada hao Wakristo wa Hawaii ambao walinisaidia kukabiliana na msiba huo! Ndugu wengi wa Hawaii, hali kadhalika ndugu wengine wengi kutoka sehemu mbalimbali za ulimwengu, walivutiwa na Lloyd.

Katika miaka miwili hivi tangu afe, nimefikiria miaka yenye kupendeza sana tuliyoishi pamoja—mingi katika mgawo wa mishonari katika nchi za kigeni, na vilevile katika makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York. Ninakumbuka pia maisha yangu ya mapema huko Sydney, Australia, na magumu ambayo mimi na Lloyd tulikabili ili kuoana mwanzoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Pili. Hata hivyo, acheni kwanza niwaambie jinsi nilivyopata kuwa Shahidi na jinsi nilivyokutana na Lloyd mwaka wa 1939.

Jinsi Nilivyopata Kuwa Shahidi

Wazazi wangu, James na Henrietta Jones, walikuwa wenye upendo na wenye kujali. Nilimaliza shule mwaka wa 1932 nikiwa na umri wa miaka 14 tu. Wakati huo ulimwengu ulikuwa katikati ya Mshuko Mkubwa wa Kiuchumi. Nilianza kufanya kazi ili kusaidia familia yetu, iliyotia ndani dada zangu wachanga wawili. Baada ya miaka michache, nilipata kazi ya ofisi yenye mshahara mzuri na nilisimamia wanawake kadhaa vijana.

Wakati huohuo, mwaka wa 1935, Mama alichukua vichapo kutoka kwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na muda si muda akasadiki kwamba alikuwa amepata kweli. Wengine wetu katika familia tulifikiri alikuwa anarukwa na akili. Hata hivyo, siku moja niliona kijitabu chenye kichwa, Where Are the Dead? (Wafu Wako Wapi?) na kuvutiwa sana nacho. Nilikisoma kisiri na mambo yakabadilika! Nilianza mara moja kwenda pamoja na Mama kwenye mkutano wa katikati ya juma ulioitwa Funzo la Kigezo. Kijitabu chenye kichwa, Model Study (Funzo la Kigezo) kilikuwa na maswali na majibu na vilevile maandiko yaliyounga mkono majibu hayo. Hatimaye kukawa na vijitabu vingine viwili kama hicho.

Karibu na wakati huo, mnamo Aprili 1938, Joseph F. Rutherford, mwakilishi kutoka makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova, alizuru Sydney. Hotuba yake ya watu wote ndiyo iliyokuwa ya kwanza kuisikiliza. Ilipaswa kutolewa kwenye Jengo la Baraza la Mji la Sydney, lakini wapinzani wakafanikiwa kuzuia tusitumie jumba hilo. Badala yake, hotuba hiyo ilitolewa kwenye Uwanja wa Michezo wa Sydney, uliokuwa mkubwa zaidi. Kwa sababu ya upinzani wengi walipata kujua kuhusu hotuba hiyo, hivyo watu wapatao 10,000 wakahudhuria. Hiyo ilikuwa idadi yenye kustaajabisha hasa ikikumbukwa kwamba wakati huo kulikuwa na Mashahidi 1,300 pekee nchini Australia.

Muda mfupi baadaye, nilishiriki katika huduma ya shambani kwa mara ya kwanza—bila hata kuzoezwa. Kikundi chetu kilipofika kwenye eneo ambalo tungehubiri, mwenye kutuongoza aliniambia, “Utahubiri nyumba ile.” Nilikuwa na wasiwasi mwingi sana hivi kwamba wakati mwanamke aliyekuwa ndani ya nyumba hiyo alipofungua mlango, nilisema, “Tafadhali, unaweza kuniambia ni saa ngapi?” Aliingia ndani, akaangalia saa, kisha akatoka na kuniambia. Sikusema chochote. Nilirudi kwenye gari.

Hata hivyo, sikuacha kuhubiri, na punde si punde nikaanza kujulisha wengine ujumbe wa Ufalme kwa ukawaida. (Mathayo 24:14) Mnamo Machi mwaka wa 1939, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa kubatizwa kwenye beseni ya kuogea ya jirani yetu wa karibu, Dorothy Hutchings. Kwa sababu hakukuwa na ndugu, punde baada ya kubatizwa, nilipewa majukumu kutanikoni ambayo kwa kawaida hupewa wanaume Wakristo.

Kwa kawaida tulifanya mikutano yetu katika nyumba za faragha, lakini mara nyingine tulikodisha jumba kwa ajili ya hotuba za watu wote. Ndugu kijana mwenye kuvutia kutoka Betheli, ofisi yetu ya tawi, alikuja kwenye kutaniko letu dogo kutoa hotuba. Sikujua kwamba alikuwa na sababu nyingine ya kuja—kunichunguza. Naam, hivyo ndivyo nilivyokutana na Lloyd.

Kukutana na Familia ya Lloyd

Punde si punde nikatamani kumtumikia Yehova wakati wote. Hata hivyo, nilipoomba kufanya upainia (kushiriki katika kazi ya kuhubiri wakati wote), niliulizwa kama ningependa kutumikia kwenye Betheli. Kwa hiyo, mnamo Septemba 1939, mwezi ambao Vita ya Ulimwengu ya Pili ilianza, nikawa mshiriki wa familia ya Betheli huko, Strathfield, kitongoji cha Sydney.

Mnamo Desemba 1939, nilisafiri hadi New Zealand ili kuhudhuria mkusanyiko. Kwa kuwa Lloyd alikuwa mzaliwa wa New Zealand, yeye pia alikuwa anaenda huko. Tulisafiri kwenye meli moja na kupata kujuana vema zaidi. Lloyd alipanga nikutane na mamake na babake na pia dada zake kwenye mkusanyiko huko Wellington na baadaye tukaenda nyumbani kwao huko Christchurch.

Kazi Yetu Yapigwa Marufuku

Jumamosi, Januari 18, 1941, wenye mamlaka katika serikali walikuja kwenye ofisi ya tawi kwa magari sita hivi meusi ili kunyakua ofisi hiyo. Kwa kuwa nilikuwa nikifanya kazi katika nyumba ndogo ya kupokelea wageni kwenye lango la Betheli, mimi ndiye niliyewaona kwanza. Muda wa saa 18 awali, tulikuwa tumearifiwa kuhusu marufuku hayo, kwa hiyo karibu vichapo vyote na faili zilikuwa zimeondolewa kwenye ofisi ya tawi. Juma lililofuata, washiriki watano wa familia ya Betheli, pamoja na Lloyd, walitiwa gerezani.

Nilijua kwamba kile ambacho ndugu waliokuwa gerezani walihitaji zaidi ni chakula cha kiroho. Ili kumtia moyo Lloyd, niliamua kumwandikia “barua za mapenzi.” Nilianza barua zangu kwa maneno ambayo kwa kawaida hutumiwa katika barua ya mapenzi, lakini nilinukuu makala nzima za Mnara wa Mlinzi na kumalizia barua hiyo kwa maneno ya mapenzi. Baada ya miezi minne na nusu, Lloyd aliachiliwa.

Kufunga Ndoa na Kuendelea na Utumishi

Katika mwaka wa 1940, mama ya Lloyd alikuja kutembea Australia, na Lloyd akamwambia kwamba tulikuwa tunafikiria kufunga ndoa. Alimshauri asifunge ndoa kwa kuwa ilionekana mwisho wa mfumo wa mambo ulikuwa karibu. (Mathayo 24:3-14) Aliwaambia marafiki wake pia kuhusu nia yake ya kufunga ndoa, lakini wakamshauri asifanye hivyo. Hatimaye, siku moja Februari 1942, Lloyd alinipeleka kimyakimya—pamoja na Mashahidi wanne ambao walikuwa wameahidi kutomwambia mtu yeyote kuhusu jambo hilo—kwenye ofisi ya usajili ambapo tulifunga ndoa. Wakati huo Mashahidi wa Yehova hawakuruhusiwa kufunganisha ndoa nchini Australia.

Ingawa hatukuruhusiwa kuendelea na utumishi wetu Betheli tukiwa wenzi wa ndoa, tuliulizwa kama tungependa kufanya upainia wa pekee. Tulikubali kwa furaha mgawo wa kwenda kwenye mji wa mashambani ulioitwa Wagga Wagga. Kazi yetu ya kuhubiri bado ilikuwa imepigwa marufuku, na hatukuwa na usaidizi wowote wa kifedha, kwa hiyo ilitubidi kumtwika Yehova mzigo wetu.—Zaburi 55:22.

Tulitumia baiskeli ya kubebea watu wawili kwenda mashambani ambako tulikutana na watu wazuri na kuzungumza nao kirefu. Wengi hawakukubali funzo la Biblia. Hata hivyo, muuza-duka mmoja alithamini sana kazi tuliyokuwa tukifanya hivi kwamba alitupa matunda na mboga kila juma. Baada ya kukaa Wagga Wagga kwa miezi sita, tulialikwa tena Betheli.

Mnamo Mei 1942, familia ya Betheli ilikuwa imehama ofisi ya Strathfield na kwenda katika nyumba za watu binafsi. Walihama kutoka nyumba moja hadi nyingine kila baada ya majuma kadhaa ili wasigunduliwe. Wakati mimi na Lloyd tuliporudi Betheli mwezi wa Agosti, tulijiunga na familia hiyo katika mojawapo ya nyumba hizo. Mgawo wetu mchana ulikuwa kufanya kazi kwenye mojawapo ya matbaa iliyokuwa imeanzishwa kisiri. Hatimaye, mnamo Juni 1943, marufuku dhidi ya kazi yetu yakaondolewa.

Kujiandaa kwa Ajili ya Utumishi wa Mishonari

Mnamo Aprili 1947 tulipewa fomu za kwanza za maombi ya kuhudhuria Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower iliyokuwa South Lansing, New York, Marekani. Wakati huohuo, tulipewa mgawo wa kuzuru makutaniko huko Australia ili kuyaimarisha kiroho. Baada ya miezi michache, tulipata mwaliko wa kuhudhuria darasa la 11 la Gileadi. Tulikuwa na muda wa majuma matatu tu kushughulikia mambo muhimu na kufungasha mizigo yetu. Tuliacha familia na marafiki mnamo Desemba na kwenda New York pamoja na watu wengine 15 kutoka Australia ambao walialikwa kuhudhuria darasa hilohilo.

Miezi michache tuliyokaa Gileadi ilipita haraka na tulipewa mgawo wa mishonari kwenda nchini Japani. Kwa kuwa ilichukua muda kupata hati za kuturuhusu kwenda Japani, Lloyd alipewa tena mgawo wa kuwa mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova. Tulipewa mgawo wa kuzuru makutaniko kutoka jiji la Los Angeles hadi mpaka wa Mexico. Hatukuwa na gari, hivyo kila juma Mashahidi walitusafirisha kwa upendo kutoka kutaniko moja kwenda jingine. Mzunguko huo ambao ulikuwa mkubwa sana sasa umegawanywa kuwa mizunguko mitatu ya wilaya ya Kiingereza na mitatu ya Kihispania, kila wilaya ikiwa na mizunguko 10 hivi!

Oktoba 1949 ilifika ghafula na tulikuwa njiani kwenda Japani kwa meli ambayo hapo awali ilibeba majeshi. Sehemu moja ya meli hiyo ilikuwa imetengwa kwa ajili ya wanaume na ile nyingine kwa ajili ya wanawake na watoto. Siku moja tu kabla ya kufika Yokohama, tulikabili kimbunga. Ni dhahiri kwamba kimbunga hicho kiliondoa mawingu, kwa kuwa jua lilipochomoza siku iliyofuata, Oktoba 31, tungeweza kuona Mlima maridadi wa Fuji. Tulikaribishwa kwenye mgawo wetu na mandhari nzuri kama nini!

Kufanya Kazi Pamoja na Wajapani

Tulipokaribia kwenye gati, tuliona watu wengi sana wenye nywele nyeusi. ‘Ni wenye makelele mengi kama nini!’ tukawaza tuliposikia makelele mengi. Wote walivaa viatu vya magongo ambavyo vilifanya makelele kwenye gati. Baada ya kupisha usiku mmoja Yokohama, tulipanda gari la moshi kwenda kwenye mgawo wetu wa mishonari huko Kobe. Don Haslett, mwanafunzi mwenzangu huko Gileadi, alikuwa amefika Japani miezi kadhaa awali, na kukodisha makao ya mishonari. Ilikuwa nyumba kubwa nzuri, yenye orofa mbili, iliyokuwa imejengwa kwa mtindo wa Magharibi lakini haikuwa na fanicha yoyote!

Ili kupata magodoro ya kulalia, tulikata nyasi ndefu zilizokuwa nje ya nyumba hiyo na kuiweka sakafuni. Hivyo ndivyo tulivyoanza maisha yetu ya mishonari, bila chochote isipokuwa mizigo tuliyobeba. Tulipata meko madogo ya makaa, yaitwayo hibachi na kuyatumia kupasha nyumba joto na kupikia. Usiku mmoja, Lloyd alikuta mishonari wenzetu wawili, Percy na Ilma Iszlaub, wamezimia. Aliweza kuwahuisha kwa kufungua dirisha ili kupisha hewa baridi na safi. Mimi pia nilizimia wakati mmoja nilipokuwa nikipika kwenye meko ya makaa. Ilichukua muda kuzoea mambo fulani.

Lilikuwa jambo muhimu sana kujifunza Kijapani, na tulijifunza lugha hiyo kwa muda wa saa 11 kwa siku kwa mwezi mmoja. Baadaye, tulianza huduma kwa kutumia sentensi moja au mbili tulizokuwa tumeandika. Siku ya kwanza kabisa kwenye huduma, nilikutana na Miyo Takagi, mwanamke mwenye kuvutia, aliyenikaribisha kwa fadhili. Nilipomrudia, tulijitahidi kutumia kamusi za Kijapani-Kiingereza na kuanzisha funzo la Biblia lenye maendeleo. Mwaka wa 1999, tulipohudhuria programu ya kuwekwa wakfu kwa majengo ya ofisi ya tawi yaliyokuwa yamepanuliwa huko Japani, nilionana na Miyo tena, na vilevile watu kadhaa wapendwa ambao nilijifunza nao. Miaka 50 imepita, lakini bado wao ni watangazaji wenye bidii wa Ufalme, wakifanya yote wawezayo kumtumikia Yehova.

Huko Kobe, watu wapatao 180 waliadhimisha pamoja nasi Ukumbusho wa kifo cha Kristo, Aprili 1, 1950. Asubuhi iliyofuata, tulishangaa kuona watu 35 ambao walikuja kushiriki katika huduma ya shambani. Kila mishonari aliandamana kwenye utumishi na watu watatu au wanne miongoni mwa watu hao wapya. Wenye nyumba hawakuongea nami—mgeni asiyeelewa Kijapani—badala yake waliongea na Wajapani waliohudhuria Ukumbusho ambao waliambatana nami. Waliongea kwa muda mrefu lakini sikuelewa walikuwa wanazungumzia nini. Ninafurahi kusema kwamba baadhi ya watu hao wapya waliendelea kupata ujuzi na wameendelea katika kazi ya kuhubiri hadi leo.

Mapendeleo na Migawo Mingi

Tuliendelea na kazi yetu ya mishonari huko Kobe hadi mwaka wa 1952, wakati ambapo tulipewa mgawo wa kwenda Tokyo, ambako Lloyd alipewa kazi ya kusimamia ofisi ya tawi. Baada ya muda, mgawo huo ulimwezesha kusafiri kotekote nchini Japani, kutia ndani nchi nyingine. Baadaye, alipokuwa akizuru Tokyo, Nathan H. Knorr, kutoka makao makuu ya ulimwengu aliniuliza: “Je, unajua mume wako atazuru sehemu gani ya dunia katika ziara yake inayokuja? Australia na New Zealand.” Akaongezea kusema: “Unaweza kwenda ukijilipia nauli.” Nilisisimuka kama nini! Kwa kuwa miaka tisa ilikuwa imepita tangu tuondoke nyumbani.

Tuliwasiliana haraka na familia zetu. Mama yangu alinisaidia kupata tiketi ya ndege. Mimi na Lloyd tulikuwa na shughuli nyingi kwenye migawo yetu, na hatukuwa na pesa za kutembelea familia zetu. Kwa hiyo sala zangu zilikuwa zimejibiwa. Kama uwezavyo kuwazia, Mama alifurahi sana kuniona. Alisema, “Nitaweka pesa akiba ili upate tiketi ya kuja tena baada ya miaka mitatu.” Tulipanga hivyo tulipoachana, lakini yasikitisha kusema kwamba alikufa mwezi wa Julai uliofuata. Ninatumaini kumwona tena katika ulimwengu mpya!

Hadi mwaka wa 1960 nilikuwa nikifanya kazi ya mishonari pekee, lakini nikapata barua iliyoeleza hivi: “Kuanzia leo utafua na kupiga pasi nguo za familia yote ya Betheli.” Wakati huo familia yetu ilikuwa na watu 12 hivi, kwa hiyo niliweza kufanya kazi hiyo mbali na mgawo wangu wa mishonari.

Katika mwaka wa 1962 nyumba yetu iliyojengwa kwa mtindo wa Kijapani ilibomolewa, na Makao mapya ya Betheli yenye orofa sita yakajengwa kwenye eneo hilo mwaka uliofuata. Nilipewa mgawo wa kusaidia ndugu wa Betheli, waliokuwa wapya na wachanga, kuweka vyumba vyao vikiwa safi na nadhifu. Kulingana na desturi ya Wajapani, wavulana hawakuwa wakifundishwa kufanya chochote nyumbani kwao. Elimu ya kilimwengu ndiyo iliyokaziwa zaidi, na mama zao walikuwa wakiwafanyia kila kitu. Muda si muda wakatambua kwamba singeweza kuwafanyia kila jambo kama mama zao walivyofanya. Baada ya muda, wengi walifanya maendeleo, wakapata migawo mipya yenye majukumu katika tengenezo.

Siku moja ya kiangazi yenye joto kali sana, mwanafunzi mmoja wa Biblia alizuru majengo yetu, akaniona nikisugua bafu. Alisema, “Tafadhali mwambie anayesimamia mahali hapa kwamba ningependa kukuajiria mtumishi mwanamke akufanyie kazi hii.” Nilimweleza kwamba ijapokuwa nilithamini wazo lake la fadhili, nilikuwa tayari kabisa kutekeleza mgawo wowote niliopewa katika tengenezo la Yehova.

Karibu na wakati huo, mimi na Lloyd tulipata mwaliko wa kuhudhuria darasa la 39 la Gileadi! Lilikuwa pendeleo lililoje kurudi shuleni mwaka wa 1964 nikiwa na umri wa miaka 46! Mtaala huo uliandaliwa hasa kusaidia wale waliokuwa wakitumikia katika ofisi za tawi ili washughulikie majukumu yao. Baada ya mtaala huo wa miezi kumi, tulipewa mgawo wa kurudi Japani. Kufikia wakati huo, Japani ilikuwa na watangazaji wa Ufalme zaidi ya 3,000.

Ukuzi ulishika kasi hivi kwamba kufikia mwaka wa 1972 kulikuwa na Mashahidi zaidi ya 14,000, na ofisi mpya ya tawi yenye orofa tano ikajengwa Numazu, kusini ya Tokyo. Tukiwa Betheli, tungeweza kuona Mlima maridadi wa Fuji. Zaidi ya magazeti milioni moja kwa mwezi katika Kijapani yalianza kuchapishwa kwa kutumia matbaa mpya kubwa. Lakini mgawo wetu ulikuwa unakaribia kubadilishwa.

Mwishoni mwa mwaka wa 1974, Lloyd alipokea barua kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn iliyomwalika kutumikia kwenye Baraza Linaloongoza. Mwanzoni niliwaza: ‘Basi, sasa hatutaishi pamoja tena. Kwa kuwa Lloyd ana tumaini la kwenda mbinguni nami nina tumaini la kukaa duniani, siku moja tutaachana tu. Labda Lloyd apaswa kwenda Brooklyn peke yake.’ Lakini muda si muda nikarekebisha maoni yangu na kwa hiari nikaandamana na Lloyd mnamo Machi 1975.

Baraka Kwenye Makao Makuu

Hata akiwa Brooklyn, Lloyd alipenda sana Japani, na sikuzote alizungumzia yale tuliyoona huko. Lakini sasa tulikuwa na fursa za kupanuka. Kwa miaka 24 ya mwisho ya maisha yake, Lloyd alitumiwa sana akiwa mwangalizi wa eneo la dunia, kazi iliyohusisha kusafiri ulimwenguni pote. Nilisafiri pamoja naye mara kadhaa kuzunguka ulimwengu.

Kuzuru ndugu zetu Wakristo katika nchi nyingine kulinisaidia kufahamu hali ambazo wengi wao huishi na kufanya kazi. Sitasahau sura ya Entellia, msichana mwenye umri wa miaka 10, ambaye nilikutana naye huko kaskazini mwa Afrika. Alipenda jina la Mungu na alitembea kwa muda wa saa tatu kwenda na kurudi kutoka kwenye mikutano ya Kikristo. Licha ya upinzani mkali kutoka kwa familia yao, Entellia alijiweka wakfu kwa Yehova. Tulipotembelea kutaniko lao, kulikuwa na balbu moja tu, yenye mwangaza kidogo iliyoangaza maandishi ya msemaji—lakini sehemu nyinginezo za jengo hilo la mikutano zilikuwa na giza totoro. Hata katika giza hilo, ilivutia sana kusikia ndugu na dada wakiimba vizuri.

Kipindi chenye kuvutia zaidi katika maisha yetu kilitokea Desemba mwaka wa 1998 wakati mimi na Lloyd tulipojiunga na wajumbe waliohudhuria Mkusanyiko wa Wilaya wa “Njia ya Mungu ya Maisha” uliofanywa nchini Kuba. Tulivutiwa kama nini na shukrani na shangwe iliyoonyeshwa na ndugu na dada wa huko walipotembelewa na baadhi ya ndugu kutoka makao makuu ya Brooklyn! Ninakumbuka wapendwa wengi niliokutana nao ambao wanaendelea kumsifu Yehova kwa bidii.

Nyumbani Pamoja na Watu wa Mungu

Ingawa nilizaliwa nchini Australia, niliwapenda watu popote pale tengenezo la Yehova liliponituma. Ilikuwa hivyo nchini Japani, na kwa vile sasa nimekuwa Marekani kwa miaka zaidi ya 25, ninawapenda watu wa hapa pia. Mume wangu alipokufa, sikufikiria kurudi Australia, bali kukaa kwenye Betheli ya Brooklyn, ambapo Yehova amenipa mgawo.

Sasa nina umri wa miaka 80 na kitu. Baada ya miaka 61 ya huduma ya wakati wote, bado niko tayari kumtumikia Yehova popote anapoona panafaa. Yeye kwa kweli amenitunza vizuri. Ninathamini miaka zaidi ya 57 ambayo niliishi na mwenzi mpendwa ambaye alimpenda Yehova. Nina hakika kwamba Yehova ataendelea kutubariki, na najua kwamba Yeye hatasahau kazi yetu na upendo ambao tumeonyesha kwa ajili ya jina lake.—Waebrania 6:10.

[Maswali ya Funzo]

^ fu. 4 Ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1999, ukurasa wa 16 na 17.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa na mama mwaka wa 1956

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na Lloyd na kikundi cha wahubiri Wajapani mapema miaka ya 1950

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na Miyo Takagi, mwanafunzi wangu wa kwanza wa Biblia, huko Japani mapema miaka ya 1950 na mwaka wa 1999

[Picha katika ukurasa wa 28]

Nikiwa na Lloyd katika kazi ya kutoa ushahidi barabarani nchini Japani