Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utii Je, Ni Somo Muhimu Utotoni?

Utii Je, Ni Somo Muhimu Utotoni?

Utii Je, Ni Somo Muhimu Utotoni?

“WAZAZI Hutaka Watoto Wenye Maoni Yao Wenyewe, Si Utii Tu.” Hivyo ndivyo kichwa kikuu cha gazeti moja kilivyosema. Ripoti hiyo fupi ilitegemea matokeo ya uchunguzi uliofanywa huko New Zealand, ambao ulionyesha kwamba “asilimia 22 [tu] kati ya watu waliohojiwa ndio walioonelea kwamba watoto wapaswa kufunzwa utii nyumbani.” Uchunguzi huo pia ulionyesha kwamba leo wazazi wanaamini kwamba ni muhimu sana kuwafundisha watoto mambo kama vile tabia njema, uwezo wa kujiamulia mambo, na uwajibikaji.

Katika kipindi hiki cha ubinafsi na kujipenda, si ajabu kwamba watu wengi wana maoni yasiyofaa kuhusu utii nao hawafundishi watoto wao kuuhusu. Hata hivyo, je, kufunza watoto utii ni jambo la kizamani? Au je, utii ni mojawapo ya mambo muhimu zaidi ambayo watoto wanaweza kujifunza na kunufaika kutokana nayo? La muhimu hata zaidi, Yehova Mungu, aliye Mwanzilishi wa familia, huonaje utii kwa wazazi, na kuna manufaa gani zinazotokana na utii huo?—Matendo 17:28; Waefeso 3:14, 15.

“Hili Ni Lenye Uadilifu”

Paulo aliliandikia hivi kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza huko Efeso: “Watoto, iweni watiifu kwa wazazi wenu katika muungano na Bwana, kwa maana hili ni lenye uadilifu.” (Waefeso 6:1) Kwa hiyo, sababu kuu ya kutii wazazi ni kwamba jambo hilo linapatana na kiwango cha Mungu cha uadilifu. Kama Paulo alivyoandika, “hili ni lenye uadilifu.”

Kwa kupatana na hilo, twaona kwamba Neno la Mungu lafafanua nidhamu ya wazazi yenye upendo kuwa pambo lenye kuvutia, “kilemba cha neema kichwani pako, na mikufu shingoni mwako,” na kama kitu ‘chenye kupendeza vema katika Bwana.’ (Mithali 1:8, 9; Wakolosai 3:20) Kinyume cha hilo, kutotii wazazi hufanya mtu akataliwe na Mungu.—Waroma 1:30, 32.

“Ili Ipate Kuwa Vema Kwako”

Paulo alionyesha manufaa nyingine ya utii alipoandika: “‘Heshimu baba yako na mama yako’; ambayo ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi: ‘Ili ipate kuwa vema kwako nawe upate kudumu muda mrefu juu ya dunia.’” (Waefeso 6:2, 3; Kutoka 20:12) Ni katika njia zipi ambazo kutii wazazi hufanya hali ya mtu iwe njema?

Kwanza, si kweli kwamba wazazi wana umri mkubwa na uzoefu mwingi kuliko sisi? Ingawa huenda wasijue mengi kuhusu kompyuta au masomo mengine yanayofundishwa shuleni, wazazi wanajua mengi kuhusu maisha na jinsi ya kukabiliana na matatizo ya maisha. Kwa upande mwingine, vijana hawafikiri kwa njia yenye usawaziko nao hufanya hivyo kwa sababu ya kukosa ukomavu. Hivyo, wao hupata madhara kwa kufanya maamuzi harakaharaka, mara nyingi kwa sababu ya msongo wenye kudhuru wa marika. Kwa kufaa, Biblia yasema: “Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto.” Suluhisho ni nini? “Lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali.”—Mithali 22:15.

Utii hauleti manufaa tu katika uhusiano wa mzazi na mtoto. Ili jamii ya wanadamu iweze kutenda vizuri na kwa matokeo, lazima kuwe na ushirikiano, ambao pia wataka kiasi fulani cha utii. Kwa mfano, amani, upatano, na furaha katika ndoa hutokana na kuwa tayari kufikiria haki na hisia za yule mwingine wala si kutokana na kuwa mwenye kudai mno. Ili biashara au kazi yoyote ifanikiwe ni lazima waajiriwa wajitiishe kazini. Kutii sheria na kanuni za serikali huepusha mtu na adhabu na vilevile humletea angalau kadiri fulani ya usalama na ulinzi.—Waroma 13:1-7; Waefeso 5:21-25; 6:5-8.

Mara nyingi vijana wasiotii mamlaka wanakuwa watu wasiofaa katika jamii. Kinyume cha hilo, utii ambao mtu hujifunza utotoni waweza kumnufaisha katika maisha yake yote. Inafaa kama nini kujifunza utii tangu utotoni!

Manufaa Kubwa za Utii

Utii hutokeza mahusiano yenye furaha katika familia na manufaa nyingine zenye kudumu na hutuwezesha kujenga uhusiano muhimu kushinda yote—uhusiano kati yetu na Muumba wetu. Akiwa “Muumba” ambaye ndiye “chemchemi ya uzima,” kwa haki Yehova Mungu anastahili utii kamili kutoka kwetu.—Mhubiri 12:1; Zaburi 36:9.

Neno “-tii” limetumiwa sana na kwa njia mbalimbali katika Biblia. Isitoshe, sheria, maagizo, amri, maamuzi ya kihukumu, na kanuni za Mungu, ambazo zahitaji ujitiisho, zimerejezewa mara nyingi sana. Hatuna shaka kwamba Mungu huona utii kuwa takwa la kupata kibali chake. Naam, utii ni jambo la lazima ili kujenga uhusiano pamoja na Yehova. (1 Samweli 15:22) Inasikitisha kwamba kwa kawaida wanadamu hawana mwelekeo wa kutii bali wa kutotii. “Mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake,” yasema Biblia. (Mwanzo 8:21) Kwa hiyo ni lazima mtu ajifunze utii tangu utotoni na katika maisha yake yote. Kufanya hivyo hunufaisha sana.

Kumbuka kwamba kama mtume Paulo alivyosema, amri ya kutii wazazi ina ahadi mbili, yaani, ili “ipate kuwa vema kwako nawe upate kudumu muda mrefu juu ya dunia.” (Italiki ni zetu.) Uthibitisho wa kutimizwa kwa ahadi hiyo wapatikana kwenye Mithali 3:1, 2: “Mwanangu, usiisahau sheria yangu, bali moyo wako uzishike amri, zangu. Maana zitakuongezea wingi wa siku. Na miaka ya uzima, na amani.” Uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova sasa na uhai udumuo milele katika ulimwengu mpya wenye amani ndio manufaa kubwa ambayo wale wanaotii watapata.—Ufunuo 21:3, 4.

[Picha katika ukurasa wa 30, 31]

Utii hutokeza mahusiano yenye furaha katika familia, kazini, na pamoja na Yehova