Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Hatari Ambayo Haijatambuliwa Kuhusu Afya ya Umma”

“Hatari Ambayo Haijatambuliwa Kuhusu Afya ya Umma”

“Hatari Ambayo Haijatambuliwa Kuhusu Afya ya Umma”

INASHANGAZA kwamba thuluthi ya watu wazima wanaotumia Internet nchini Marekani hutazama ngono katika vituo fulani vya Internet, kulingana na uchunguzi wa hivi majuzi kuhusu ngono katika Internet. Watu wengi sasa hutosheleza hamu yao ya ngono kwa kutazama vituo hivyo. ‘Jambo hilo huhatarisha afya ya umma kwa sababu kwa kadiri fulani watu wengi hawatambui au kuchukua kwa uzito hatari hiyo,’ akasema Dakt. Al Cooper, mwanasaikolojia aliyefanya uchunguzi huo.

Ni nani hasa wanaoelekea kudhuriwa kwa kutazama ngono katika Internet? ‘Ni wale ambao hawajajihusisha katika ngono kisha pasipo kutarajia wanapata habari chungu nzima zinazohusu ngono kwenye Internet,’ asema Dakt. Cooper.

Hata hivyo, wengi ambao hutazama ngono katika vituo hivyo, huona zoea hilo kuwa lisilodhuru. Je, ni salama? Kama vile mraibu wa dawa za kulevya huwa sugu kwa dawa ambayo amezoea, ndivyo waraibu wengi wa kutazama ngono katika Internet hutafuta habari zaidi zinazohusu ngono ili kutosheleza tamaa zao. Huenda hata wakahatarisha kazi yao na uhusiano wao pamoja na mwenzi wa ndoa!

Hata hivyo, wale wanaotaka kumpendeza Mungu wana sababu nyingine ya kuepuka kutazama ngono katika vituo hivyo vya Internet. Neno la Mungu lashauri hivi: “Kwa hiyo, fisheni viungo vya mwili wenu vilivyo juu ya dunia kwa habari ya uasherati, ukosefu wa usafi, hamu ya ngono, tamaa yenye kuumiza, na tamaa, ambako ni ibada ya sanamu. Kwa sababu ya mambo hayo hasira ya kisasi ya Mungu inakuja.” (Wakolosai 3:5, 6) Mtu anahitaji kusitawisha upendo mwingi sana kwa Yehova Mungu ili ‘afishe viungo vya mwili wake’ kuhusiana na hamu isiyo safi ya ngono. (Zaburi 97:10) Ikiwa mtu anashawishiwa kutazama ngono katika Internet jambo ambalo linahatarisha afya ya umma, anapaswa kuimarisha upendo wake kwa Yehova kwa kujifunza Neno la Mungu, Biblia. Ushirika wenye kujenga pamoja na Mashahidi wa Yehova kwenye Jumba la Ufalme waweza kumsaidia mtu aimarishe azimio lake la kumpendeza Mungu.