Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mababa wa Kanisa Walikuwa Watetezi wa Kweli ya Biblia?

Je, Mababa wa Kanisa Walikuwa Watetezi wa Kweli ya Biblia?

Je, Mababa wa Kanisa Walikuwa Watetezi wa Kweli ya Biblia?

Uwe unadai kuwa Mkristo au la, ufahamu wako kuhusu Mungu wa Biblia, Yesu, na Ukristo huenda uliathiriwa na watu hao. Mmoja wao aliitwa Mwenye Mdomo wa Dhahabu; mwingine, Mkuu. Wakiwa pamoja, wamefafanuliwa kuwa ‘watu walioiga maisha ya Kristo kwa ukaribu zaidi.’ Ni nani hao? Ni watu wa dini wa kale wenye kufikiri sana, waandishi, wanatheolojia, na wanafalsafa ambao wameathiri sana kufikiri kwa “Kikristo” leo—Mababa wa Kanisa.

“NENO la Mungu halipatikani tu katika Biblia,” adai profesa Mgiriki wa Othodoksi anayechunguza masuala ya kidini, Demetrios J. Constantelos. “Roho Takatifu haifunui tu neno la Mungu inafunua pia vitabu vingine.’ Kuna chanzo gani kingine chenye kutegemeka cha ufunuo wa kimungu? Katika kitabu chake Understanding the Greek Orthodox Church, Constantelos asisitiza hivi: ‘Mapokeo Matakatifu na Maandiko Matakatifu [huonwa] kuwa vyanzo vyenye kutegemeka vya ufunuo wa kimungu.’

Msingi wa hayo “Mapokeo Matakatifu” watia ndani mafundisho na maandishi ya Mababa wa Kanisa. Walikuwa wanatheolojia mashuhuri na wanafalsafa “Wakristo” ambao waliishi kati ya karne ya pili na ya tano W.K. Maandishi yao yameathirije mafundisho ya “Kikristo” leo? Je, mafundisho yao yalipatana na Biblia? Ni nini ambayo yapasa kuwa msingi wa kweli ya Kikristo kwa mfuasi wa Yesu Kristo?

Historia Yao

Katikati ya karne ya pili W.K., watu waliodai kuwa Wakristo walikuwa wakitetea imani yao dhidi ya wanyanyasi Waroma na vilevile waasi. Hata hivyo, pindi hiyo ilikuwa na watu wenye maoni mengi sana ya kitheolojia. Mijadala ya kidini kuhusu “uungu” wa Yesu na asili na matendo ya roho takatifu ilitokeza migawanyiko na mambo mengi sana. Kutoafikiana kabisa na kutokea kwa migawanyiko isiyoweza kurekebika kuhusu fundisho la “Kikristo” kulienea katika siasa na utamaduni, nyakati nyingine kukisababisha ghasia, maasi, zogo, hata vita. Mwanahistoria Paul Johnson aandika hivi: “Ukristo [wa uasi-imani] ulianza kwa vurugu, ubishi na mgawanyiko na kuendelea hivyo. . . . Katika karne ya kwanza na ya pili W.K. sehemu ya kati na ya mashariki mwa Mediterania ilisitawi ikiwa na dini nyingi sana, zilizokuwa zikipigania kujieneza. . . . Tokea mwanzo, kumekuwa na Ukristo wa namna mbalimbali uliotofautiana.”

Katika pindi hiyo, waandishi na watu wenye kufikiri sana waliohisi kwamba ilikuwa lazima kufasiri mafundisho ya “Kikristo” kwa kutumia semi za kifalsafa walianza kuongezeka. Ili kuridhisha wapagani walioelimika ambao walikuwa wageuzwa-imani wapya wa “Kikristo,” waandishi hao wa kidini walitegemea sana vichapo vya mapema vya Kigiriki na Kiyahudi. Kuanzia na mwandishi Justin Martyr (karibu 100-165 W.K.), aliyeandika kwa Kigiriki, watu waliodai kuwa Wakristo walizidi kuwa wazoefu katika kuchanganya maoni na mafundisho ya wanafalsafa Wagiriki na yale ya Kikristo.

Mwelekeo huo ulijitokeza sana katika maandishi ya Origen (karibu 185-254 W.K.), aliyekuwa mwandishi Mgiriki wa Alexandria. Simulizi la Origen katika kichapo On First Principles lilikuwa hatua ya kwanza iliyofanywa kwa utaratibu kueleza mafundisho makuu ya theolojia ya “Kikristo” kwa kutumia falsafa ya Kigiriki. Baraza la Nisea (325 W.K.), lililojaribu kueleza na kuthibitisha “uungu” wa Kristo, lilichochea sana kufasiriwa kwa fundisho la “Kikristo.” Baraza hilo liliashiria kipindi cha kufafanuliwa kwa fundisho kwa usahihi zaidi na mabaraza mengine ya kanisa.

Waandishi na Wasemaji

Eusebius wa Kaisaria, aliyekuwa mwandishi wakati wa Baraza la Nisea la kwanza, alishirikiana na Maliki Konstantino. Miaka mia moja na kitu baada ya Baraza la Nisea, wanatheolojia ambao wengi wao waliandika kwa Kigiriki, walijadiliana vikali na kwa muda mrefu kisha wakakuza fundisho la Utatu ambalo lingetambulisha Jumuiya ya Wakristo. Miongoni mwao kulikuwemo hasa Athanasius, kasisi mwenye kushikilia kauli wa Alexandria, na viongozi watatu wa kanisa wa Kapadokia, Asia Ndogo—Basil Mkuu, ndugu yake Gregory wa Nyssa, na rafiki yao Gregory wa Nazianzus.

Waandishi na wahubiri walioishi pindi hiyo walikuwa wafasaha sana. Gregory wa Nazianzus na John Chrysostom (linalomaanisha “mwenye Mdomo wa Dhahabu”) katika Kigiriki na vilevile Ambrose wa Milan na Augustine wa Hippo walikuwa wasemaji stadi sana wa Kilatini, lugha iliyopendwa sana wakati wao. Augustine ndiye aliyekuwa mwandishi mwenye uvutano mkubwa zaidi wakati huo. Makala yake ya kitheolojia imeathiri sana maoni ya watu wengi kuhusu “Ukristo” wakati wetu. Jerome, aliyekuwa msomi mashuhuri na mwenye ujuzi, alihusika hasa katika kutafsiri Biblia ya Kilatini ya Vulgate kutoka lugha za awali.

Hata hivyo, kuna maswali haya muhimu: Je, Mababa hao wa Kanisa walishikamana kwa ukaribu na Biblia? Je, mafundisho yao yalipatana kabisa na Maandiko yaliyopuliziwa? Je, maandishi yao ni mwongozo wenye kutegemeka wa kupata ujuzi sahihi juu ya Mungu?

Je, Ni Mafundisho ya Mungu au Ni Mafundisho ya Wanadamu?

Hivi karibuni, Kasisi wa Othodoksi ya Ugiriki, Methodius wa Pisidia aliandika kitabu The Hellenic Pedestal of Christianity ili kuonyesha kwamba utamaduni na falsafa ya Kigiriki ndio msingi wa “Ukristo” wa leo. Katika kitabu hicho, akiri hivi pasipo kusita: ‘Karibu Mababa wote wa Kanisa waliona falsafa za Kigiriki cha kale kuwa muhimu sana, na kuzitumia ili kuelewa na kufafanua kwa usahihi kweli za Kikristo.’

Kwa mfano, fikiria wazo la kwamba Baba, Mwana, na roho takatifu hufanyiza Utatu. Baada ya Baraza la Nisea Mababa wengi wa Kanisa walikuwa watetezi thabiti wa fundisho la Utatu. Maandishi na hotuba zao zilichangia sana kufanya Utatu uwe fundisho kuu la Jumuiya ya Wakristo. Hata hivyo, je, fundisho la Utatu linapatikana katika Biblia? La. Kwa hiyo Mababa wa Kanisa walitoa wapi fundisho hilo? Kichapo A Dictionary of Religious Knowledge chasema kwamba wengi husema kuwa Utatu “ni upotovu uliotokana na dini za kipagani, na kufanywa kuwa imani ya Kikristo.” Nacho kichapo The Paganism in Our Christianity chathibitisha hivi: “Asili ya [Utatu] ni ya kipagani kabisa.” *Yohana 3:16; 14:28.

Au fikiria fundisho la kutokufa kwa nafsi—imani ya kwamba sehemu fulani ya mwanadamu huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Mababa wa Kanisa walichangia sana kuanzishwa kwa wazo hilo katika dini ambayo haikuamini fundisho hilo. Biblia huonyesha waziwazi kwamba nafsi inaweza kufa: “Nafsi inayofanya zambi, itakufa.” (Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible) Mababa wa Kanisa walikuwa na msingi gani wa kuamini katika nafsi isiyoweza kufa? “Dhana ya Kikristo kuhusu nafsi ya kiroho iliyoumbwa na Mungu na kuingizwa ndani ya mwili wakati wa kutungwa kwa mimba yatokana na falsafa ya Kikristo iliyochukua muda mrefu kusitawi. Origen aliyeishi Mashariki na Mtakatifu Augustine aliyeishi Magharibi ndio waliofanya watu wengi wakubali kwamba nafsi ni kitu cha kiroho na dhana ya kifalsafa ikaanzishwa kuhusu asili ya nafsi. . . . [Fundisho la Augustine] . . . lilichangia sana (kutia ndani kasoro fulani) kuanzishwa kwa falsafa mpya ya Plato,” yasema New Catholic Encyclopedia. Gazeti Presbyterian Life lasema: “Kutokufa kwa nafsi ni dhana ya Kigiriki iliyoanzishwa katika madhehebu ya kifumbo ya kale na kufafanuliwa na mwanafalsafa Plato.” *

Msingi Thabiti wa Ukristo wa Kweli

Baada ya kuchunguza historia hii fupi ya Mababa wa Kanisa, na vilevile asili ya mafundisho yao, yafaa kujiuliza hivi, Je, imani ya Mkristo wa kweli yapasa kutegemea mafundisho ya Mababa wa Kanisa? Acha Biblia ijibu.

Kwanza kabisa, Yesu Kristo mwenyewe alipinga kutumia jina la cheo la kidini “Baba” aliposema: “Msiite yeyote baba yenu duniani, kwa maana mmoja ni Baba yenu, Aliye wa kimbingu.” (Mathayo 23:9) Kumwita mtu fulani wa dini “Baba” ni jambo lisilo la Kikristo na lisilopatana na Maandiko. Neno la Mungu lilikamilishwa yapata mwaka wa 98 W.K. vitabu vya mtume Yohana vilipoandikwa. Kwa hiyo, Wakristo wa kweli hawapaswi kumtegemea mtu yeyote ili kupata ufunuo uliopuliziwa. Wanajihadhari wasije ‘wakalibatilisha neno la Mungu’ kwa sababu ya mapokeo ya kibinadamu. Kuruhusu mapokeo ya kibinadamu yachukue mahali pa Neno la Mungu kwaweza kusababisha madhara ya kiroho. Yesu alitoa onyo hili: “Ikiwa kipofu aongoza kipofu, wote wawili wataanguka ndani ya shimo.”—Mathayo 15:6, 14.

Je, Mkristo ahitaji ufunuo wowote mbali na neno la Mungu Biblia? La. Kitabu cha Ufunuo chatoa onyo dhidi ya kuongeza jambo lolote katika maandishi yaliyopuliziwa: “Yeyote akiongezea mambo haya, Mungu atamwongezea tauni ambazo zimeandikwa katika hati-kunjo hii.”—Ufunuo 22:18.

Kweli ya Kikristo yapatikana katika Neno la Mungu, Biblia. (Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:16; 2 Yohana 1-4) Si lazima ujue falsafa ya kilimwengu ili kuielewa kweli hiyo. Yafaa kuuliza maswali ya mtume Paulo kuhusiana na watu waliojaribu kutumia hekima ya kibinadamu ili kueleza ufunuo wa kimungu: “Yuko wapi mtu mwenye hekima? Wapi mwandishi? Wapi mshindania-maneno wa mfumo huu wa mambo? Je, Mungu hakuifanya hekima ya ulimwengu iwe pumbavu?”—1 Wakorintho 1:20.

Isitoshe, kutaniko la Kikristo la kweli ni “nguzo na tegemezo la ile kweli.” (1 Timotheo 3:15) Waangalizi wa kutaniko huhakikisha kwamba wanafundisha mambo yasiyopotoka kutanikoni na kuzuia fundisho lolote potovu lisipenye. (2 Timotheo 2:15-18, 25) Wao hufukuza kutoka kwenye kutaniko ‘manabii wasio wa kweli, walimu wasio wa kweli, na mafarakano yenye kuangamiza.’ (2 Petro 2:1) Baada ya mitume kufa, Mababa wa Kanisa waliruhusu “matamko yaliyopuliziwa yenye kuongoza vibaya na mafundisho ya roho waovu” yasitawi katika kutaniko la Kikristo.—1 Timotheo 4:1.

Matokeo ya uasi-imani huo yanaonekana wazi katika Jumuiya ya Wakristo leo. Imani na mazoea yake hutofautiana kabisa na kweli ya Biblia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Habari zaidi kuhusu fundisho la Utatu yaweza kupatikana katika broshua Je, Uamini Utatu?, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 16 Kwa habari zaidi kuhusu fundisho la Biblia juu ya nafsi, ona ukurasa wa 100-106 na 232-236 katika kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]

MABABA WA KANISA WA KAPADOKIA

“Kanisa Othodoksi . . . huwastahi sana waandishi wa karne ya nne, na hasa wale inaowaita ‘Makasisi Wakuu watatu,’ Gregory wa Nazianzus, Basil Mkuu, na John Chrysostom,” asema mwandishi Kallistos, ambaye ni mtawa wa kiume. Je, maandishi ya Mababa hao wa Kanisa yalitegemea Maandiko yaliyopuliziwa? Kuhusu Basil Mkuu, kitabu The Fathers of the Greek Church chasema: ‘Maandishi yake yaonyesha kwamba alikuwa na uhusiano wa karibu na wa kudumu pamoja na Plato, Homer, wanahistoria na wasemaji wenye ufasaha, na bila shaka waliathiri mtindo wake wa kuandika . . . . Basil alidumisha mtazamo wa Kigiriki.’ Gregory wa Nazianzus alidumisha mtazamo huo pia. “Kwa maoni yake, ushindi na ubora wa Kanisa ungeonyeshwa ifaavyo kwa kukubali kabisa mapokeo ya utamaduni wa kale.”

Profesa Panagiotis K. Christou aandika hivi kuwahusu wote watatu: “Ingawa pindi kwa pindi wanaonya dhidi ya ‘falsafa na udanganyo mtupu’ [Wakolosai 2:8] —ili kutii amri ya Agano Ji-pya—wakati huohuo, wanajifunza kwa bidii falsafa na kanuni zinazohusiana nayo na hata kupendekeza kwamba wengine wajifunze mambo hayo.” Bila shaka, walimu hao wa kanisa walifikiri kwamba mbali na Biblia walihitaji maandishi mengine ya kuunga mkono maoni yao. Je, kutafuta utegemezo kutoka kwa watu wengine wenye mamlaka kulimaanisha kwamba mafundisho yao yalitofautiana na Biblia? Mtume Paulo aliwaonya hivi Wakristo Waebrania: “Msichukuliwe na mafundisho ya namna mbalimbali na yaliyo mageni.”—Waebrania 13:9.

[Hisani]

© Archivo Iconografico, S.A./CORBIS

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]

CYRIL WA ALEXANDRIA—BABA WA KANISA MBISHANI

Mmojawapo wa watu wabishani zaidi miongoni mwa Mababa wa Kanisa ni Cyril wa Alexandria (karibu 375-444 W.K.). Mwanahistoria wa masuala ya kanisa Hans von Campenhausen amfafanua kuwa “mwenye kushikilia kauli, mjeuri, tena mjanja, mwenye kujali sana sifa na adhama ya kazi yake,” na aongezea kwamba “hakuona jambo lolote kuwa sawa kamwe isipokuwa liwe lilimnufaisha au kufanya awe na nguvu na mamlaka zaidi . . . Hakujali kamwe kutumia njia za kikatili na zilizokiuka kanuni.” Alipokuwa kasisi wa Alexandria, Cyril alitoa hongo, aliandika mambo ya kukashifu, na uchongezi ili kumng’oa mamlakani kasisi wa Constantinople. Anadhaniwa kuwa alihusika katika mauaji ya kinyama ya mwanafalsafa mashuhuri Hypatia katika mwaka wa 415 W.K. Campenhausen asema hivi kuhusu maandishi ya kitheolojia ya Cyril: “Alianzisha zoea la kuamua masuala ya kidini si kwa kutegemea Biblia peke yake bali alinukuu mambo yaliyompendeza kutoka kwa waandishi mashuhuri.”

[Picha katika ukurasa wa 19]

Jerome

[Hisani]

Garo Nalbandian