Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wakumbuka?

Je, Wakumbuka?

Je, Wakumbuka?

Je, umethamini kusoma matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ebu ona kama unaweza kujibu maswali yafuatayo:

Kwenye Waroma 5:3-5, kwa nini mtume Paulo aliorodhesha tumaini mwisho baada ya kutaja mambo mbalimbali?

Paulo alitaja mambo mbalimbali ambayo huwapata Wakristo—dhiki, uvumilivu, hali yenye kukubaliwa, na tumaini. Hili “tumaini” si lile tumaini la kwanza ambalo mtu hupata kutoka kwa Biblia, bali ni tumaini lililoimarishwa, lililoongezwa kina, linalohusisha kila upande wa maisha na ambalo Mkristo anaweza kuwa nalo baada ya muda.—12/15, ukurasa wa 22-23.

Kwa nini huenda Mkristo leo akapendezwa na michezo ya riadha iliyofanywa katika Ugiriki ya kale?

Kuelewa asili na desturi ya michezo hiyo kwaweza kumsaidia mtu aelewe mistari kadhaa ya Biblia. Baadhi ya mistari hiyo inarejezea ‘kushindana kulingana na kanuni,’ ‘kuondoa kila uzito na kutazama kielelezo cha Yesu,’ ‘kukimbia hadi mwisho’ na kupokea taji, au tuzo. (2 Timotheo 2:5; 4:7, 8; Waebrania 12:1, 2; 1 Wakorintho 9:24, 25; 1 Petro 5:4)—1/1, ukurasa wa 28-30.

Ni njia gani mpya ya kutangaza habari njema iliyoanzishwa Januari 1914?

Sinema ya “Photo-Drama of Creation” ilitolewa wakati huo. Ilitolewa katika sehemu nne zilizotia ndani sinema yenyewe, na mamia ya slaidi za rangi, zilizoambatana na hotuba zilizorekodiwa katika rekodi za santuri. Seti 20 za Sinema hiyo zilitayarishwa na kutumiwa kufundisha watu ujumbe wa Biblia katika sehemu nyingi.—1/15, ukurasa wa 8-9.

Baraza Linaloongoza linatofautianaje na shirika la kisheria?

Ingawa wasimamizi wa shirika la kisheria huchaguliwa na washiriki wake, Baraza Linaloongoza haliwekwi rasmi na mtu yeyote bali huwekwa rasmi na Yesu Kristo. Si lazima wasimamizi wa mashirika mbalimbali yanayotumiwa na Mashahidi wa Yehova wawe washiriki wa Baraza Linaloongoza. Katika mkutano wa hivi majuzi ambao hufanywa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, washiriki wa Baraza Linaloongoza waliokuwa wakitumikia wakiwa wasimamizi na maofisa wake walijiuzulu nyadhifa zao. Nafasi zao zilichukuliwa na ndugu wakomavu wa “kondoo wengine.” (Yohana 10:16) Hivyo Baraza Linaloongoza linaweza kutumia muda mwingi zaidi kutayarisha chakula cha kiroho na kushughulikia mahitaji ya kiroho ya ndugu ulimwenguni pote.—1/15, ukurasa wa 29, 31.

Twaweza kuchunguza mifano gani miwili ya Biblia tunapojifunza jinsi ya kukabiliana na kivunja-moyo?

Mfano mmoja ni Hana, mamake Samweli. Angaliweza kuvunjika moyo alipoeleweka vibaya na Eli, kuhani wa cheo cha juu wa Israeli. Badala yake, alimweleza ukweli wa mambo kwa njia iliyo wazi lakini kwa heshima. Isitoshe, Hana hakumfungia Eli kinyongo. Kielelezo cha pili ni Marko, ambaye bila shaka alivunjika moyo wakati mtume Paulo alipokataa kwenda naye katika safari ya mishonari. Badala ya kuvunjika moyo kwa kupoteza pendeleo hilo, aliendelea kutumikia kwa bidii, akisafiri na Barnaba.—2/1, ukurasa wa 20-22.

Kwa nini Wakristo wawe waangalifu kuhusu kuwapa au kupokea kutoka kwa wengine, nakala za programu za kompyuta?

Programu nyingi za kompyuta (kutia ndani michezo ya kompyuta) zina leseni, ambayo humzuia mnunuzi/mtumiaji asiweke programu hiyo katika kompyuta nyingine. Kwa kawaida kuwatolea wengine nakala za programu hizo ni kuvunja sheria za haki za kumiliki, hata tunapozitoa bila malipo. Wakristo wanataka kutii sheria, ya ‘kumlipa Kaisari vitu vya Kaisari.’ (Marko 12:17)—2/15, ukurasa wa 28-29.

Cyril na Methodius walikuwa akina nani, nao walichangia jinsi gani funzo la Biblia?

Walikuwa ndugu wawili waliozaliwa Thesalonike, Ugiriki, katika karne ya tisa. Walianzisha alfabeti ya Kislavonia na kutafsiri sehemu kubwa ya Biblia katika lugha hiyo.—3/1, ukurasa wa 28-29.

Usemi “kuweka akili juu ya roho” wamaanisha nini?—Waroma 8:6.

Wamaanisha kuongozwa, kutawaliwa, na kuchochewa na kani ya utendaji ya Yehova. Tunaweza kuruhusu roho ya Mungu itutendeshe kwa kusoma na kujifunza Biblia, kwa kutii sheria ya Mungu kwa moyo wote, na kwa kusali ili kupata roho ya Mungu.—3/15, ukurasa wa 15.

Tufanyeje tunapohisi kwamba tumeeleweka vibaya?

Ni muhimu kujaribu kueleza mambo waziwazi kwa roho ya upendo. Njia hiyo isipofaulu, usikate tamaa. Omba uelewevu na msaada kutoka kwa Yehova, ambaye “huipima mioyo.” (Mithali 21:2; 1 Samweli 16:7)—4/1, ukurasa wa 21-23.