Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kukabiliana na Kuvunjika Moyo

Jinsi ya Kukabiliana na Kuvunjika Moyo

Jinsi ya Kukabiliana na Kuvunjika Moyo

Asafu alilalamika hivi: “Hakika nimejisafisha moyo wangu bure, nimenawa mikono yangu kwa kutokukosa. Maana mchana kutwa nimepigwa, na kuadhibiwa kila asubuhi.”—Zaburi 73:13, 14.

● Baruku alipiga kite hivi: “Ole wangu! kwa maana BWANA ameongeza huzuni pamoja na maumivu yangu. Nimechoka kwa ajili ya kuugua kwangu, wala sioni raha.”—Yeremia 45:3.

● Naomi aliomboleza hivi: “Mwenyezi Mungu amenitenda mambo machungu sana. Mimi nalitoka hali nimejaa, naye BWANA amenirudisha sina kitu, kwani kuniita Naomi, ikiwa BWANA ameshuhudia juu yangu, na Mwenyezi Mungu amenitesa?”—Ruthu 1:20, 21.

BIBLIA yaeleza juu ya waabudu wengi waaminifu wa Yehova ambao mara kwa mara walikuwa wamevunjika moyo. Kwa kuwa sisi sote hatujakamilika, tunavunjika moyo mara kwa mara. Huenda baadhi yetu tunavunjika moyo kwa urahisi kuliko wengine—hata kujionea huruma kwa kiasi fulani—kwa sababu ya kupatwa na misiba maishani.

Hata hivyo, usipozishinda hisia hizo zinaweza kuharibu uhusiano wako pamoja na wengine na pamoja na Yehova Mungu. Mwanamke mmoja Mkristo ambaye hujionea huruma mara nyingi anakubali kwamba: “Nimekataa mialiko mingi ya kushirikiana na wengine kwa sababu nilihisi kwamba sikustahili kushirikiana na ndugu na dada kutanikoni.” Hisia hizo zinaweza kuharibu kabisa maisha ya mtu. Unaweza kufanya nini ili kushinda hisia hizo?

Mkaribie Yehova

Katika Zaburi 73, Asafu aliandika kinaganaga juu ya mfadhaiko wake. Alipolinganisha mafanikio ya waovu na hali yake mwenyewe, aliwaonea wivu. Aliona kwamba wasiomcha Mungu walikuwa wenye kiburi na wajeuri, lakini hawakuadhibiwa. Kisha, Asafu akatilia shaka faida ya kudumisha mwenendo wa haki maishani.—Zaburi 73:3-9, 13, 14.

Kama Asafu, je, umeona jinsi ambavyo waovu wanaojivunia uovu wao huonekana kufanikiwa maishani? Asafu alishindaje hali yake ya kuvunjika moyo? Anasema: “Nami nilifikiri jinsi ya kufahamu hayo; ikawa taabu machoni pangu; hata nilipoingia katika patakatifu pa Mungu, nikautafakari mwisho wao.” (Zaburi 73:16, 17) Asafu alichukua hatua zinazofaa kwa kumwendea Yehova katika sala. Kwa vile mtume Paulo alivyosema, Asafu alizuia “mtu wa kimwili” kwa kuamsha ndani yake mwenyewe “mtu wa kiroho.” Alipopata uelewevu mpya wa kiroho, alifahamu kwamba Yehova huchukia ubaya na katika wakati unaofaa waovu wataadhibiwa.—1 Wakorintho 2:14, 15.

Ni muhimu kama nini kuruhusu Biblia ikusaidie kuona maisha jinsi yalivyo! Yehova anatukumbusha kwamba anaona matendo ya waovu. Biblia yafundisha: “Msiongozwe vibaya: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia . . . Kwa hiyo acheni tusife moyo katika kufanya lililo bora.” (Wagalatia 6:7-9) Yehova atawaweka waovu “penye utelezi”; na kuwaangusha “mpaka palipoharibika.” (Zaburi 73:18) Mwishowe haki ya kimungu itashinda.

Kulishwa kiroho kunakoendelea kwenye meza ya Yehova na ushirika unaofaa pamoja na watu wa Mungu kutaimarisha imani yako na kukusaidia kushinda kuvunjika moyo na hisia nyingine zisizofaa. (Waebrania 10:25) Kama Asafu, ukikaa karibu na Mungu, utaweza kupata msaada wake wenye upendo. Asafu anaongeza: “Mimi ni pamoja nawe daima, umenishika mkono wa kuume. Utaniongoza kwa shauri lako, na baadaye utanikaribisha kwa utukufu.” (Zaburi 73:23, 24) Mkristo mmoja ambaye alitendwa vibaya alipokuwa mtoto alipata kuelewa hekima ya maneno hayo. Anasema: “Kushiriki kwa ukaribu na kutaniko kulinisaidia kuwa na maoni mapya juu ya maisha. Haikuwa vigumu kuona kwamba wazee Wakristo walikuwa wenye upendo, nao walikuwa wachungaji wala si askari.” Naam, wazee Wakristo wenye huruma wanaweza kusaidia sana kuondosha hisia zisizofaa.—Isaya 32:1, 2; 1 Wathesalonike 2:7, 8.

Kubali Ushauri wa Yehova

Baruku, mwandishi wa nabii Yeremia, alilalamika kwa sababu ya mikazo iliyosababishwa na kazi yake. Hata hivyo, kwa fadhili Yehova alimsaidia Baruku aone tatizo lake. “Je, unajitafutia mambo makuu? usiyatafute; kwa maana tazama, nitaleta mabaya juu ya wote wenye mwili, asema BWANA; lakini roho yako nitakupa iwe nyara, katika mahali pote utakapokwenda.”—Yeremia 45:2-5.

Yehova alieleza wazi kwamba kuvunjika moyo kwa Baruku kulisababishwa na ubinafsi wake mwenyewe. Baruku hakuweza kufurahia kazi ambayo alipewa na Mungu, huku akijitafutia mambo makuu. Yamkini hata wewe utapata kwamba njia bora ya kushinda kuvunjika moyo ni kuepuka kuvutiwa na mambo mengi. Na badala yake kujipatia amani ya akili ambayo hutokana na uradhi wa kimungu.—Wafilipi 4:6, 7.

Naomi aliyefiwa hakuruhusu msiba kumzuia asishiriki na watu wengine huko Moabu baada ya kifo cha mume na wana wake wawili. Hata hivyo, yaelekea alikuwa na roho chungu kujihusu na kuhusiana na wake wawili wa wana wake. Alipowahimiza warudi kwao, Naomi alisema hivi: “Maana ni vigumu kwangu kuliko kwenu, kwa sababu mkono wa BWANA umetoka juu yangu.” Alipowasili Bethlehemu, alisisitiza hivi tena: “Msiniite Naomi [“Kupendeza”], niiteni Mara [“Uchungu”], kwa sababu Mwenyezi Mungu amenitenda mambo machungu sana.”—Ruthu 1:13, 20.

Hata hivyo, Naomi hakujitenga na Yehova na watu wake kwa kuendelea kuomboleza kwa muda mrefu. Alipokuwa Moabu alikuwa amesikia kwamba “BWANA amewajilia watu wake na kuwapa chakula.” (Ruthu 1:6) Alielewa kwamba kuishi miongoni mwa watu wa Yehova kulikuwa kwema kwake. Baada ya hapo, Naomi alirejea Yuda pamoja na Ruthu, mke wa mwana wake na kumwelekeza Ruthu kwa busara jinsi alivyopaswa kutenda kuhusiana na mkombozi wake, Boazi.

Vivyo hivyo leo, watu waaminifu ambao wamefiwa na wenzi wao hukabili mikazo ya kihisia kwa mafanikio wakiwa na shughuli nyingi katika kutaniko la Kikristo. Kama vile Naomi, wao wanaendelea kuzingatia mambo ya kiroho kwa kusoma Neno la Mungu kila siku.

Manufaa za Kutenda Kupatana na Hekima ya Kimungu

Masimulizi hayo yaBiblia hutusaidia kuelewa jinsi mtu anavyoweza kukabiliana na kuvunjika moyo. Asafu alikwenda kwenye patakatifu pa Yehova ili kupata msaada na kungoja kwa subira ili Yehova atende. Baruku alikubali ushauri, naye akaepuka kuvutiwa na mali. Naomi alikuwa mwenye shughuli miongoni mwa watu wa Yehova. Alimtayarisha mwanamke kijana, Ruthu, kwa ajili ya mapendeleo yake kuhusiana na ibada ya Mungu wa kweli.—1 Wakorintho 4:7; Wagalatia 5:26; 6:4.

Unaweza kushinda kuvunjika moyo na hisia nyingine zisizofaa kwa kutafakari ushindi mbalimbali ambao Yehova amewapa watu wake, kama mtu mmoja-mmoja na kama kikundi. Tafakari juu ya tendo kuu la upendo la Yehova la kuandaa ukombozi kwa ajili yako. Thamini upendo wa kweli wa udugu wa Kikristo. Zingatia maisha yako katika ulimwengu mpya wa Mungu unaokaribia. Na useme kama Asafu: “Nami kumkaribia Mungu ni kwema kwangu; nimefanya kimbilio kwa Bwana MUNGU, niyahubiri matendo yako yote.”—Zaburi 73:28.