Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kufanikiwa Licha ya Malezi Yako

Unaweza Kufanikiwa Licha ya Malezi Yako

Unaweza Kufanikiwa Licha ya Malezi Yako

NICHOLAS alikuwa mkaidi tangu utotoni. * Hatimaye mvurugo wake wa akili ukafanya aanze kutumia dawa za kulevya na kunywa kupindukia. Nicholas anaeleza hivi: “Baba yangu alikuwa mlevi, naye alifanya dada yangu nami tuteseke sana.”

Wazazi wa Malinda walionekana kuwa watu wema katika jumuiya yao, nao walikuwa washiriki wa kanisa. Lakini pia walikuwa wafuasi wa madhehebu fulani. “Baadhi ya mazoea yao ya kimadhehebu yalinidhuru na kuharibu mtazamo wangu nilipokuwa mtoto,” Malinda aliye na umri wa miaka 30 na kitu alalamika. Anaongeza kusema: “Kwa sababu hiyo, hisia za kukata tamaa na kujihisi duni zimeniathiri tangu utotoni.”

Ni nani awezaye kukataa kwamba tangu utotoni wengi wamekuwa na maisha yenye ujeuri, kutendwa vibaya, kupuuzwa na wazazi, na hali nyingine mbaya? Maisha ya utotoni yasiyo na furaha yanaweza kusababisha uchungu mwingi wa akili na moyo. Lakini je, uchungu huo utamzuia mtu asiweze kamwe kukubali ukweli wa Neno la Mungu na kuishi maisha yenye furaha? Licha ya malezi yao mabaya, je, Nicholas na Malinda wanaweza kufanikiwa kudumisha uaminifu-maadili maishani? Fikiria kwanza mfano wa Mfalme Yosia wa Yuda.

Mfano wa Kimaandiko

Yosia alitawala Yuda kwa miaka 31 katika karne ya saba K.W.K. (659-629 K.W.K.) Yosia alipotawazwa baada ya babaye kuuawa, hali nchini Yuda zilikuwa mbaya sana. Yuda na Yerusalemu zilijaa waabudu wa Baali na wale walioapa kwa mungu mkuu wa Amoni, Malkamu. Sefania aliyekuwa nabii wa Mungu katika kipindi hicho alisema kwamba wakuu wa Yuda walikuwa “simba wangurumao” na waamuzi walikuwa “mbwa-mwitu wa jioni.” Kwa hiyo, ujeuri na udanganyifu ulienea sana nchini. Wengi walikuwa wakisema mioyoni mwao hivi: “BWANA hatatenda mema, wala hatatenda mabaya.”—Sefania 1:3–2:3; 3:1-5.

Yosia akawa mtawala wa aina gani? Ezra, aliyeandika matukio ya Biblia kwa kupatana na wakati yalipotukia, aliandika hivi: “[Yosia] akafanya yaliyo mema machoni pa BWANA, akaziendea njia za Daudi babaye, asigeuke kwa kuume wala kwa kushoto.” (2 Mambo ya Nyakati 34:1, 2) Bila shaka Yosia alifanikiwa kufanya mema machoni pa Mungu. Lakini watu wa jamaa yake walikuwa watu wa aina gani?

Kutunzwa au Kutendwa Vibaya Utotoni?

Yosia alipozaliwa mwaka wa 667 K.W.K., Amoni, baba yake, alikuwa na umri wa miaka 16 tu. Na babu ya Yosia, Manase, alikuwa akitawala taifa la Yuda. Manase alikuwa mmojawapo wa wafalme waovu kabisa waliopata kutawala Yuda. Kwa kumjengea Baali madhabahu, “akafanya mabaya mengi machoni pa BWANA.” Baadhi ya wanawe aliwapitisha motoni. Alizoea uchawi na uaguzi, na kuendeleza uwasiliani-roho. Na alimwaga damu nyingi isiyo na hatia. Pia, Manase alileta kwenye nyumba ya Yehova sanamu ya kuchonga, nguzo takatifu, ambayo alikuwa ameagiza itengenezwe. Alipotosha Yuda na Yerusalemu “hata wakazidi kufanya mabaya kuliko mataifa, aliowaharibu BWANA mbele ya wana wa Israeli.”—2 Mambo ya Nyakati 33:1-9.

Manase alikuwa mbaya hivi kwamba Yehova aliamuru afungwe pingu na kupelekwa hadi Babiloni, mojawapo ya majiji ya kifalme ya mfalme wa Ashuru. Alipokuwa utekwani Manase alitubu, akanyenyekea, akaomba Yehova amsamehe. Mungu alisikia ombi lake la kupata ukubali wake, akamrudisha kuwa mfalme huko Yerusalemu. Kisha, Manase akaanzisha marekebisho nchini yaliyofanikiwa kadiri fulani.—2 Mambo ya Nyakati 33:10-17.

Uovu wa Manase na toba yake ilikuwa na matokeo gani juu ya mwanawe, Amoni? Alikuwa mwovu kabisa. Amoni hakumwunga Manase mkono alipotubu na kujitahidi kuondoa unajisi ambao yeye mwenyewe alikuwa ameingiza nchini. Amoni alikuwa na umri wa miaka 22 alipoanza kutawala, naye “akafanya yaliyo maovu machoni pa BWANA, kama alivyofanya Manase babaye.” Badala ya kujinyenyekeza mbele za Yehova, “Amoni akaongeza makosa juu ya makosa.” (2 Mambo ya Nyakati 33:21-23) Yosia alikuwa na umri wa miaka sita tu Amoni alipotawazwa kuwa mfalme wa Yuda. Bila shaka malezi ya utotoni ya Yosia yalikuwa mabaya sana!

Utawala mwovu wa Amoni ulikoma baada ya miaka miwili, watumishi wake walipofanya njama dhidi yake na kumwua. Hata hivyo, watu nchini waliwaua wale waliofanya njama dhidi ya Amoni, wakamtawaza mwanawe Yosia kuwa mfalme.—2 Mambo ya Nyakati 33:24, 25.

Licha ya hali zenye kudhuru za maisha ya utotoni, Yosia alifanya yaliyo mema machoni pa Yehova. Utawala wake ulikuwa wenye mafanikio hivi kwamba Biblia yasema: “Kabla ya huyo hapakuwa na mfalme mfano wake, aliyemwelekea BWANA kwa moyo wake wote, na kwa roho yake yote, na kwa nguvu zake zote, sawasawa na sheria zote za Musa; wala baada yake hakuinuka mmoja mfano wake yeye.”—2 Wafalme 23:19-25.

Mfano wa Yosia huwatia moyo kwelikweli wale ambao huenda walikuwa na maisha mabaya ya utotoni! Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wake? Ni nini kilichomsaidia Yosia kuchagua mwenendo wa maisha unaofaa na kuushikilia?

Jitahidi Kumjua Yehova

Manase, babu ya Yosia aliyetubu, alikuwa na uvutano mzuri katika maisha ya utotoni ya Yosia. Biblia haitaji umri wa Yosia wakati Manase aliporekebisha mwenendo wake, wala uhusiano baina ya Yosia na babu yake. Hata hivyo kwa kuwa washiriki wa jamaa za Wayahudi walikuwa na uhusiano wa karibu inawezekana kwamba Manase alijaribu kumsaidia mjukuu wake asipotoshwe na ufisadi ulioenea kotekote kwa kumfundisha kumcha Mungu wa kweli, Yehova, na kustahi neno lake. Mbegu zozote za ukweli ambazo Manase aliweza kuzipanda katika moyo wa Yosia, hatimaye zilitokeza matunda. Huenda kulikuwapo pia uvutano mwingine mzuri. Katika mwaka wake wa nane kama mfalme wa Yuda, Yosia mwenye umri wa miaka 15 alijitahidi kujua na kufanya mapenzi ya Yehova.—2 Mambo ya Nyakati 34:1-3.

Katika maisha yao ya utotoni, baadhi ya watu hawakuwa na uhusiano wa kiroho pamoja na mtu yeyote isipokuwa mtu wa ukoo wa mbali, mtu ambaye walifahamiana naye kidogo tu, au jirani. Hata hivyo, mbegu ambazo hupandwa kwa njia hiyo, zinaweza kutokeza matunda mazuri baadaye. Malinda, aliyetajwa mapema, alikuwa na jirani mzee mwenye fadhili aliyeleta magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni kwa ukawaida nyumbani kwao! Anapomfikiria jirani huyo kwa upendo, anasema hivi: “Jambo ambalo lilinivutia sana kuhusu jirani yangu lilikuwa kwamba hakusherehekea sikukuu. Jambo hilo lilikuwa muhimu kwangu kwa kuwa sikukuu ya Halloween (sherehe ya usiku wa tarehe 30 ya Oktoba) na baadhi ya sikukuu nyingine zilikuwa vipindi vya kufuatia desturi za madhehebu ya wazazi wangu.” Miaka kumi baadaye, rafiki ya Malinda alipomwalika kuhudhuria mkutano wa Kikristo kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, alimkumbuka jirani huyo, naye akakubali mwaliko huo bila kusita. Jambo hilo lilimsaidia kupata ukweli.

Jinyenyekeze Mbele za Mungu

Yosia alipotawala, marekebisho makubwa ya dini yalifanywa katika nchi ya Yuda. Yosia alianza kurekebisha nyumba ya Yehova baada ya kupambana na ibada ya sanamu na kutakasa nchi ya Yuda kwa muda wa miaka sita. Kazi ilipokuwa ikiendelea Kuhani Mkuu Hilkia aligundua kitu chenye maana sana! Alipata nakala ya awali ya “kitabu cha torati ya BWANA.” Hilkia alimkabidhi Shafani kitabu hicho muhimu sana, naye akamjulisha mfalme kuhusu jambo hilo. Je, Yosia, mwenye umri wa miaka 25, alijivunia mafanikio hayo?—2 Mambo ya Nyakati 34:3-18.

“Mfalme alipoyasikia maneno ya torati, [mara] aliyararua mavazi yake,” Ezra aandika. Alifanya hivyo kwa sababu ya kuhuzunika moyoni alipotambua kwamba babu zao hawakuwa wamefuata amri zote za Mungu. Jambo hilo lilikuwa dalili ya unyenyekevu. Upesi mfalme alituma msafara wa wajumbe watano kumwendea nabii wa kike Hulda ili kupata mwelekezo wa Yehova. Wakarudi na habari hii: ‘Mabaya yataletwa kwa sababu ya kutotii Sheria ya Yehova. Lakini kwa kuwa wewe, Mfalme Yosia, umejinyenyekeza, utawekwa kaburini mwako kwa amani, wala macho yako hayataona mabaya.’ (2 Mambo ya Nyakati 34:19-28) Yehova alipendezwa na mwelekeo wa Yosia.

Hata ingawa malezi yetu yalikuwa mabaya tunaweza pia kujinyenyekeza mbele za Mungu, Yehova, na kumstahi yeye na Neno lake, Biblia. Nicholas aliyetajwa mapema, alifanya hivyo. Anasema hivi: “Maisha yangu yalijaa matatizo na taabu kwa sababu nilikuwa mlevi na nilitumia dawa za kulevya, hata hivyo nilipendezwa na Biblia na kutaka kuwa na kusudi maishani. Hatimaye, nilikutana na Mashahidi wa Yehova, nikabadili mwenendo wangu wa maisha, nikakubali ukweli.” Naam, tunaweza kumstahi Mungu na Neno lake, hata hali yetu ya maisha iweje.

Nufaika na Mpango wa Yehova

Pia, Yosia alistahi sana manabii wa Yehova. Mbali na kumwendea nabii wa kike Hulda kuomba ushauri, pia alitiwa moyo sana na manabii wengine wa siku zake. Kwa mfano, Yeremia na Sefania walikuwa wakishutumu ibada ya sanamu nchini Yuda. Bila shaka Yosia alitiwa nguvu kwa kusikiliza ujumbe wao alipopambana na ibada isiyo ya kweli!—Yeremia 1:1, 2; 3:6-10; Sefania 1:1-6.

“Bwana,” Yesu Kristo, ameweka kikundi cha wafuasi wake waliotiwa mafuta, ili watayarishe chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Wao ni “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Kupitia vichapo vya Biblia na mpango wa kutaniko, jamii ya mtumwa huyo, wanavuta fikira kwenye manufaa ya kutii ushauri wa Biblia na jinsi ya kuufuata maishani. Inafaa kama nini tutumie mpango wa Yehova utusaidie kushinda mielekeo isiyofaa ambayo inaweza kuwa vigumu kuishinda! Tangu utotoni, Nicholas alikuwa mkaidi. Hata alipojifunza ukweli wa Neno la Mungu, udhaifu huo ulimzuia asimtumikie Yehova kikamili. Kubadili mwelekeo huo hakukuwa jambo rahisi kwake. Hata hivyo, mwishowe akafaulu. Jinsi gani? “Wazee wawili wenye huruma walinisaidia,” Nicholas asema. “Nilikubali kwamba nilikuwa na tatizo, nikaanza kufuata ushauri wao wenye upendo wa Kimaandiko.” Aongeza hivi: “Ijapokuwa mara kwa mara ninaudhika kidogo, sasa nimeshinda ukaidi wangu.”

Malinda pia huwaendea wazee anapohitaji kufanya maamuzi muhimu maishani. Anapokabiliana na hisia ya kukata tamaa na kujihisi kuwa duni, hisia ambazo zilianza utotoni, kile ambacho humsaidia hasa ni makala mbalimbali za magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Anasema hivi: “Nyakati nyingine katika makala kuna fungu moja tu au sentensi—sehemu ndogo sana—ambayo hunisaidia. Yapata miaka tisa iliyopita nilianza kuweka makala hizo katika jalada, ili niweze kuzirejea kwa urahisi.” Kwa sasa, ana vitabu vitatu vyenye makala 400 hivi!

Kwa hiyo, si lazima uchungu ambao umesababishwa na maisha mabaya ya jamaa yawaathiri watu kwa kudumu. Kwa msaada wa Yehova wanaweza kufanikiwa kiroho. Kama vile malezi mazuri hayahakikishi kwamba mtu atakuwa mwaminifu, vivyo hivyo malezi mabaya hayawezi kumzuia mtu asiwe mwenye kumcha Mungu.

Baada ya kupata kitabu cha Sheria walipokuwa wakirekebisha hekalu, Yosia ‘akafanya agano mbele za BWANA, kumfuata BWANA, na kuzishika amri zake, kwa moyo wake wote, na kwa roho yake yote.’ (2 Mambo ya Nyakati 34:31) Naye hakuacha kufanya hivyo hadi kifo chake. Malinda na Nicholas pia, wameazimia kudumisha uaminifu wao kwa Yehova Mungu ili wafanikiwe kuwa watu wenye uaminifu-maadili. Nawe uazimie pia kudumisha uhusiano wa karibu na Mungu na kumtumikia kwa uaminifu. Uwe na uhakika kwamba utaweza kufanikiwa, kwa kuwa Yehova anaahidi hivi: “Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu.”—Isaya 41:10, 13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Licha ya kuwa na maisha ya utotoni yaliyokuwa mabaya kupindukia, Yosia alijitahidi kumjua Yehova, akafanikiwa maishani mwake

[Picha katika ukurasa wa 28]

Wazee wanaweza kukusaidia kushinda mwelekeo ambao si rahisi kushinda

[Picha katika ukurasa wa 28]

Magazeti ya “Mnara wa Mlinzi” na “Amkeni!” yaweza kukusaidia kudumisha uaminifu-maadili