Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ushirika wa Ulimwenguni Pote Unaosaidiana

Ushirika wa Ulimwenguni Pote Unaosaidiana

Ushirika wa Ulimwenguni Pote Unaosaidiana

WATU wamejaa kila mahali. Wengi ni wazee-wazee, baadhi yao ni walemavu na wanatembea kwa shida sana. Kuna wanawake wajawazito na wenzi wa ndoa wachanga walio na daraka la kuwalinda watoto. Wote—wanaume, wanawake, na watoto—ni wakimbizi ambao wamelazimika kukimbia makao yao na kutafuta hifadhi katika nchi jirani kwa sababu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe, misiba ya asili, au hali nyinginezo. Wengine wamelazimika kukimbia makao yao mara kadhaa. Waonapo tu zogo la wenyewe kwa wenyewe au msiba fulani wa asili, wanakusanya vitu vichache vya nyumbani, wanachukua watoto wao, na kuelekea mahali salama. Kisha, mambo yanapotulia, wakimbizi wengi hurudi ili kujenga upya nyumba zao na kuanza maisha upya.

Kwa miaka mingi, Jamhuri ya Afrika ya Kati imewakubali wakimbizi kutoka nchi kadhaa. Hivi karibuni, maelfu ya watu, kutia ndani Mashahidi wengi wa Yehova, walilazimika kukimbia Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo iliyokumbwa na vita na kwenda mahali salama katika Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Ndugu Wasaidia

Mashahidi katika Jamhuri ya Afrika ya Kati waliiona kazi ya kutoa msaada kuwa pendeleo. Makao yalipatikana kwa ajili ya ndugu Wakristo waliokuwa wakiwasili. Mwanzoni, vyumba vilipatikana katika nyumba za faragha, lakini kadiri idadi ya wakimbizi ilivyozidi kuongezeka, ikawa dhahiri kwamba mipango zaidi ilipasa kufanywa. Majumba fulani ya Ufalme yaligeuzwa kuwa mabweni. Mashahidi wa hapo walileta taa zaidi, wakaweka mifereji ya maji, na kuweka sakafu ya saruji ili kustarehesha wale ambao wangeishi hapo. Wakimbizi walisaidiana na ndugu wa mahali hapo kutayarisha mabweni hayo ya muda. Programu kamili ya mikutano ya Kikristo ilipangwa katika Kilingala ili watu waliokuwa wakiwasili wapate chakula cha kiroho kinachotegemeza uhai. Ushirikiano wa karibu kati ya Mashahidi wa hapo na wageni wao ulidhihirisha kwamba kuna udugu wa ulimwenguni pote.

Wakimbizi hawakuwasili pamoja wakiwa familia sikuzote. Nyakati fulani, washiriki wa familia waliokuwa wametenganishwa waliungana tena mwishoni mwa safari yao. Katika kila Jumba la Ufalme kulikuwa na orodha ya wale waliowasili salama. Mipango ilifanywa ya kutafuta wale waliokuwa wamepotea. Ofisi ya tawi inayosimamia kazi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi hiyo ilituma magari matatu kila siku ili kusaidia Mashahidi waliokuwa safarini bado na kutafuta wowote ambao huenda walikuwa wamepotea. Magari hayo yalitambulishwa kwa ishara kubwa, iliyosema “MNARA WA MLINZI—Mashahidi wa Yehova.”

Hebu wazia jinsi kikundi cha watoto saba waliokuwa wakimbizi na ambao walikuwa wametenganishwa na wazazi wao walivyoshangilia walipoona gari la kubebea mizigo la Mashahidi wa Yehova. Walikimbia mara moja hadi kwenye gari hilo na kujitambulisha kuwa ni Mashahidi. Ndugu waliwapandisha katika gari na kuwapeleka kwenye Jumba la Ufalme, ambapo hatimaye waliungana tena na familia zao.

Ni nini ambacho kimewawezesha Wakristo hao wa kweli kukabiliana na hali hizo, si mara moja tu bali mara kadhaa? Wanasadiki kabisa kwamba tunaishi katika siku za mwisho kama ilivyotabiriwa katika Maandiko Matakatifu.—2 Timotheo 3:1-5; Ufunuo 6:3-8.

Kwa hiyo, wanajua kwamba hivi karibuni Yehova Mungu atakomesha vita, chuki, jeuri, na zogo. Tatizo la wakimbizi litakomeshwa. Kwa sasa, kupatana na shauri la mtume Paulo kwenye 1 Wakorintho 12:14-26, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kusaidiana. Ingawa wametenganishwa na mito, mipaka, lugha, na umbali, wao husaidiana, kwa hiyo wanatenda mara moja mtu fulani anapohitaji msaada.—Yakobo 1:22-27.

[Ramani katika ukurasa wa 30]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

AFRIKA

Jamhuri ya Afrika ya Kati

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo

[Hisani]

Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Majumba matatu ya Ufalme yalitumiwa kama vituo vya kupokea wageni

[Picha katika ukurasa wa 31]

Mahali pa kupikia palijengwa mara moja

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wengi walizidi kuwasili

[Picha katika ukurasa wa 31]

Watoto waliozaliwa hivi karibuni ambao tayari ni wakimbizi